MAAGIZO YA BWANA YESU NI BORA KULIKO MAAGIZO YA DAKTARI:

MAAGIZO YA BWANA YESU NI BORA KULIKO MAAGIZO YA DAKTARI:

Ukiwa mgonjwa, labda unaumwa TB, ukapewa dozi na Daktari ukaambiwa utumie hizo kwa muda wa miezi 6 bila kuruka siku hata moja!! Je! Utaacha baada ya mwezi mmoja kwasababu masharti ni magumu au kwasababu umepata unafuu??. Ni dhahiri kuwa hutaacha kwasababu unajua madhara yake, kwamba ukiacha hata kama unajihisi kama umepona, yatakuwa ni makubwa zaidi na badala ya kupona utajikuta utaleta ugonjwa sugu zaidi hivyo hali yako ya mwisho inakuwa mbaya kuliko ile ya kwanza. Ndio hapo utajua Daktari anayo sababu muhimu kwanini utumie dozi hiyo kwa miezi 6.

Vivyo hivyo na wanaokwenda kwa waganga wa kienyeji wanafahamu kuwa wasipofuata maagizo wanayopewa huko, kuna mawili aidha isilete matokeo yoyote au ilete madhara makubwa zaidi.

Kadhalika na Bwana wetu YESU KRISTO kama TABIBU wetu mkuu wa roho zetu atupendaye alitoa TIBA(damu yake) ya kuponya dhambi zetu. Na hii tiba iliambatana na MAAGIZO kuwa ni lazima yafuatwe, Na yasipofuatwa kisahihi au kuvunjwa kuna hatari ya matokeo kuwa hasi. Mungu huwa anatembea katika kanuni zake tu.

Bwana Yesu alisema maneno haya katika 

Marko 16:15 “Akawaambia, Enendeni ulimwenguni mwote, mkaihubiri Injili kwa kila kiumbe. AAMINIYE na KUBATIZWA ataokoka; asiyeamini, atahukumiwa.”

Unaona hapo tiba ya dhambi imekuja na maagizo, : Hatua ya kwanza ni kuamini; Ambayo hii inakuja pale mtu anapoiamini injili na kutubu na kukusudia kabisa kuacha dhambi kwa moyo wake wote,. Sasa baada ya mtu huyu kukusudia kufanya hivyo hapo ni sawa na amekutana na daktari akamweleza ugonjwa wake, na akaamini kwamba huyo daktari anao uwezo wa kumponya.

Hatua ya PILI inayofuata, ni KUBATIZWA: Haya ni maagizo Bwana Yesu aliyatoa kwa ajili ya ondoleo la dhambi zako, ni sawa na daktari amekupa dawa na kukuambia Katie kwenye maji na kuogea kwa muda wa wiki mbili kisha huo ugonjwa wa ngozi unaokusumbua utaisha. Lakini ukivunja maagizo, na kwenda kujinyunyuzia badala ya kuiogea je! Ugonjwa utatoka?. Ni wazi kuwa ugonjwa utabaki.

Vivyo hivyo katika ubatizo, Neno “Ubatizo” maana yake ni “kuzamishwa”, kwahiyo baada ya kuamini hatua inayofuata ni kubatizwa kwa ajili ya ondoleo la dhambi zako, kiashirio kuwa damu ya Yesu Kristo imefuta dhambi zako zote, Bwana Yesu alipokufa pale msalabani damu na maji vilitoka ubavuni mwake kuashiria kuwa hivi vitu viwili vinaenda pamoja. Na ndio maana siku ile ya Pentekoste baada ya watu kuiamini injili ya Petro ndipo walipomuuliza;

Matendo 2:37-38 “Walipoyasikia haya wakachomwa mioyo yao, wakamwambia Petro na mitume wengine, Tutendeje, ndugu zetu?

38 Petro akawaambia, TUBUNI, MKABATIZWE kila mmoja kwa jina lake YESU KRISTO, MPATE ONDOLEO LA DHAMBI ZENU, nanyi mtapokea kipawa cha Roho Mtakatifu.”

Umeona hapo maagizo yametolewa ili tuwe na uhakika kuwa dhambi zetu zimeondolewa ni lazima Tutubu kwanza kisha tubatizwe(Kwa kuzamishwa katika maji mengi na kwa jina la YESU) na dhambi zetu zitakuwa zimeondolewa.

Lakini kinachohuzunisha ni kwamba pale unaposikia mtu anapoambiwa juu ya umuhimu wa ubatizo sahihi na kuanza kutoa udhuru, na kusema hilo halijalishi, ni imani yako tu, iwe maji mengi au kidogo haijalishi!!! .. Ndugu inajalisha sana, Hivi daktari anapokuambia kaogee dawa hii mara tatu kwa siku, utamwambia hiyo haijalishi mimi nitainyunyuzia mwilini, ni imani yangu tu?? Kuna uhakika wa kupona kweli hapo?

Mgonjwa kweli aliyetayari kupona hatafikiria mara mbili mbili juu ya suala hilo hata aambiwe afanye hivyo mara kumi kwa siku atatii kwasababu yeye shida yake tu awe na uhakika wa kupona.

Maagizo mepesi kama haya yakitushinda tutaweza maagizo gani tena?.

Ubatizo sahihi ndugu ni muhimu katika safari yako ya ukristo, ikiwa kweli umemaanisha kwenda mbinguni utatii maagizo yote uliyopewa na mkombozi wa roho yako, ukisoma biblia yote hakuna mahali popote mtu alibatizwa kwa kunyunyiziwa, wote walizamishwa tena wakabatizwa kwa jina la YESU na sio kwa jina la Baba na Mwana na Roho Mtakatifu kama wengi wao wafanyavyo kimakosa soma (Matendo 2:38. Mdo 8:16, Mdo 10:48, Mdo 19:5 utathibitisha jambo hilo), Unapaswa ufahamu jina la Baba, na Mwana na Roho Mtakatifu Bwana alilolizungumzia katika Mathayo 28:19 Ni lipi? Utakuja kugundua kuwa ni jina moja hilo na ndilo mitume walilitumia kubatizia, nalo ni JINA LA YESU.

Ukizidi kujifunza maandiko utaona pia hakuna ubatizo wa vichanga, kwasababua mtoto mchanga hajatubu bado, hafahamu jema wala baya, hivyo hawezi kubatizwa, watoto wachanga wanawekewa mikono tu kama Baraka juu ya maisha yao yamwishie Mungu basi na sio kubatizwa. Mambo ya wokovu yanahitaji uamuzi binafsi na sio kufanyiwa kwa niaba ya mtu mwingine. Pale wakishafikia umri wa kujua jema na baya ndipo kwa uamuzi wao wenyewe wanamwendea Yesu na kuoshwa dhambi zao kwa kubatizwa, Hivyo ndugu kama ulibatizwa utotoni unapaswa ukabatizwe tena, ili kuufanya wito wako na uteule wako imara.

Na pia ubatizo hauhitaji shule yoyote ya kupitia kama baadhi ya dini zinavyofanya, pale unapoamini tu na kukusudia kuishi maisha mapya katika Kristo haraka sana nenda kabatizwe, Filipo alipokutana na yule towashi mara tu alipoamini akabatizwa saa ile ile.

Matendo 8: 35-38 “Filipo akafunua kinywa chake, naye, akianza kwa andiko lilo hilo, akamhubiri habari njema za Yesu.

36 Wakawa wakiendelea njiani, wakafika mahali penye maji; yule towashi akasema, Tazama, maji haya; ni nini kinachonizuia nisibatizwe?

37 Filipo akasema, Ukiamini kwa moyo wako wote, inawezekana. Akajibu, akanena, Naamini ya kwamba Yesu Kristo ndiye Mwana wa Mungu.]

38 Akaamuru lile gari lisimame; wakatelemka wote wawili majini, Filipo na yule towashi; naye akambatiza.”

Hivyo kama ulishaamini na haujabatizwa, au ulibatizwa utotoni, au haujabatizwa kwa ubatizo sahihi kwa jina la YESU, ni vizuri ukafanya hivyo sasa kwa uhakika wa safari yako ya wokovu.

Na Hatua ya TATU na ya mwisho baada ya kubatizwa ni Roho Mtakatifu. Biblia inasema Roho Mtakatifu ni MUHURI wa Mungu(Waefeso 4:30, Waefeso 1:13, 2wakoritho 1:22), Unapopokea Roho Mtakatifu unakuwa umekamilishwa mpaka siku ya ukombozi wako.

Matendo 19:1-5

“1 Ikawa, Apolo alipokuwa Korintho, Paulo, akiisha kupita kati ya nchi za juu, akafika Efeso; akakutana na wanafunzi kadha wa kadha huko;

2 akawauliza, Je! MLIPOKEA ROHO MTAKATIFU MLIPOAMINI? Wakamjibu, La, hata kusikia kwamba kuna Roho Mtakatifu hatukusikia.

3 Akawauliza, Basi mlibatizwa kwa ubatizo gani? Wakasema, Kwa ubatizo wa Yohana. 

4 Paulo akasema, Yohana alibatiza kwa ubatizo wa toba, akiwaambia watu wamwamini yeye atakayekuja nyuma yake, yaani, Yesu.

5 Waliposikia haya WAKABATIZWA kwa JINA LA BWANA YESU.

6 Na Paulo, alipokwisha kuweka mikono yake juu yao, ROHO MTAKATIFU akaja juu yao; wakaanza kunena kwa lugha, na kutabiri.

7 Na jumla yao walipata wanaume kumi na wawili.”

Hivyo hatua hizi TATU ni muhimu sana kwa mkristo aliyemaanisha kuokolewa, kwa kufanya hivyo atakuwa “ameufanya wito wake na uteule wake imara 2 petro 1:10”.

Kama haujabatizwa ipasavyo tafuta mahali wanapobatiza ubatizo sahihi, au wasiliana na mimi, uwe ni wa kuzamishwa mwili wako wote na kwa jina la YESU.

Mungu akubariki.

Pia unaweza ukapata mafundisho haya Kwa njia ya Whatsapp yako, jiunge na channel yetu Kwa kubofya hapa >> WHATSAPP


Mada Nyinginezo:

UBATIZO SAHIHI

MVUTO WA TATU!

ROHO YA MPINGA KRISTO IKITENDA KAZI SIKU HIZI ZA MWISHO

NINI MAANA YA “TAMAA YAKO ITAKUWA KWA MUMEO”?

JE, KAMA HAUNA UBATIZO SAHIHI HAUWEZI KUWA NA ROHO MTAKATIFU?


Rudi Nyumbani

Print this post

About the author

Admin administrator

Subscribe
Notify of
guest
1 Comment
Newest
Oldest Most Voted
Inline Feedbacks
View all comments
M
M
1 year ago

Amen