UNAMFAHAMU MUNGU WA KWELI?

UNAMFAHAMU MUNGU WA KWELI?

Mwanzo Bwana alipowatoa wana wa Israeli katika nchi ya Misri, hakuwakuta ni wakamilifu kwa asilimia zote kama anavyotaka yeye, kwasababu kule Misri walipokuwepo hakukuwa na utaratibu wowote wa kumwabudu Mungu wa kweli, na wala wana wa Israeli walikuwa hawamjui kwa kina Mungu wa Ibrahimu, walikuwa wanayo kama historia vichwani mwao kuwa kipindi Fulani nyuma Mungu alimtokea Baba yao Ibrahimu na kumpa maneno mengi ya Ahadi, walisikia tu kipindi Fulani Mungu, aliipiga dunia kwa njaa lakini alimfunulia Yusufu aliyekuwa mwisraeli kama wao juu ya majanga hayo  yatakayokuja..hawakumjua sana kwa undani, Mungu wao ni Mungu wa namna gani…Walimjua tu ni Mungu hodari na atakayekuja kuwaokoa katika matatizo yao basi.

Na kwa jinsi walivyokuwa wanaendelea kukaa katika nchi ya Misri, pasipo kumsikia kwa vizazi vingi,  kidogo kidogo walianza kumdhania Mungu wa Yakobo ni  kama miungu ya kimisri,  walidhani kwamba Mungu wa Yakobo baba yao anaweza akatengenezewa mfano wa kinyago Fulani kama wa-Misri wanavyoifanyia miungu yao. Waliona kwasababu wa-Misri wanatolea dhabihu sanamu zao huku wanaendelea na roho zao mbaya, na bado wanapata mvua nakufanikiwa wakajua na Mungu wa Yakobo yuko hivyo hivyo, wanaweza wakamtolea dhabihu, na sadaka lakini maisha yao yakaendelea kuwa vile vile, wakaendelea kuwa na kiburi chao, matusi yao, malalamiko yao, uuaji wao, n.k.

Hivyo kwasababu waliishi na Wa-Misri kwa muda mrefu, kwa zaidi ya miaka 400, ule utamaduni au ule mfumo wa kuabudu walioutumia wa-Misri, uliwaingia na wao pia kudhani kuwa Mungu wa Israeli naye anaabudiwa kama inavyoabudiwa miungu ya kimisri..

Hata katika maisha ni kawaida kuona mazingira Fulani yakiwaathiri watu Fulani na kudhani watu wote wako kama wao. Utakuta  kwamfano familia Fulani ina utaratifu wa kukaa pamoja, na kula pamoja mezani..lakini mmoja wa familia hiyo anatoka na kwenda kutembelea familia nyingine na kutazamia kuikuta familia ile ipo kama ya kwao, badala yake anakuta kila mtu yupo kivyake, baba na mama hawaongei, kila mtu na ratiba zake..lazima itamshangaza kidogo kwasababu amekuta kitu asichokitegemea..

Ndivyo ilivyokuwa kwa Wana wa Israeli, Bwana Mungu wakati anakuja kuwatoa ilikuwa ni shida sana wao kumwelewa na ndio maana tunaona Bwana Mungu aliwapitisha kwanza jangwani kabla ya kuwaingiza nchi ya Ahadi ili awafundishe yeye ni nani, na anataka nini kutoka kwao.

Utaona baada tu ya kutolewa nchi ya Misri, pamoja na kufanyiwa miujiza yote ile, wakaanza kunung’unika na kulalamika, ni kwasababu gani walikuwa wanafanya vile? Ni kwasababu walikuwa hawamjui bado Mungu wa Israeli kuwa hapendi watu wanaonungu’unika, wao walidhani Mungu wa Israeli ni kama miungu ya kimisri ambayo ukiinung’unikia tu haiwezi kufanya lolote, walidhani ni kama ile miungu ya kimisri ambayo ukiilalamikia na kuitukana haikufanyi chochote.

Na ukiendelea mbele zaidi utaona wana wa Israeli wanaanza kufikiria kutengeneza ndama ya kusubu ili iwarudishe Misri, ni kwanini walifanya vile? ni kwasababu walidhani Mungu wa Israeli ni kama miungu ya kimisri, kwamba inafika mahali inashindwa kufanya jambo Fulani, na hivyo kuitafutia njia mbadala.

Na mambo mengine mengi, waliyoyafanya wana wa Israeli yaliyomkasirisha Mungu yalitokana na kutomjua Mungu wa YAKOBO ni nani? Yalitokana na kumdhania Mungu wa Baba yao Ibrahimu ni mfano wa mmojawapo wa miungu ya Misri, isipokuwa yeye ana nguvu kidogo kipita yao.

Kwasababu hiyo basi iliwachukua muda mrefu sana kumjua Mungu wa Israeli ni nani..Mpaka Bwana alipoanza kuwapa sheria ndio kidogo kidogo ndipo Alipoanza kuwaambia yeye ni MUNGU  MMOJA, na hakuna mwingine zaidi yake wala wa kufananishwa na yeye, hivyo wasiwe na miungu mingine ya kando ila yeye peke yake. ALIPOANZA KUWAAMBIA YEYE NI MUNGU MTAKATIFU NA HIVYO ANAWATAKA NA WAO WAWE WATAKATIFU KAMA YEYE ALIVYO..

Walawi 11: 45 “Kwa kuwa mimi ni Bwana niliyewaleta kutoka nchi ya Misri, ili kwamba niwe Mungu wenu; BASI MTAKUWA WATAKATIFU, KWA KUWA MIMI NI MTAKATIFU”. 

Ndipo walipoanza kumwelewa Mungu kuwa sio kama miungu ya Misri waliyoizoea kwamba unaweza ukaitumikia na bado ukaendelea kuwa mwizi, unaweza ukaitolea dhabihu na bado ukaendelea kuwa mnung’unikaji, unaweza ukaitumikia na bado ukaendelea kuwa muuaji au mwizi unaweza ukaiabudu na  kuiimbia na bado ukaendelea kuilalamikia, unaweza ukaifuata na bado ukaendelea kuwa mzinzi, au mlaji rushwa, au mtu mwenye chuki, kwamba unaweza ukawa na miungu mingine midogo midogo mingi ya pembeni ya kukusaidia pale Mungu mkubwa anapokwama,   n.k ndipo walipojua kuwa Mungu wa Israeli sio kama walivyokuwa wanamdhania kama miungu ya Misri waliyoizoea Ndipo walipomwelewa vizuri Mungu wa Israeli ni Mungu mtakatifu sana  na hana msaidizi na yupo mmoja,Iliwachukua miaka zaidi ya 40 kumwelewa vizuri Mungu wa Israeli..

Na baada akili zao kubadilishwa kumjua Mungu wa kweli ni Mungu wa namna gani, ndipo wakaweza kutembea na Mungu.

Kaka/Dada unayesoma haya..swali ni lile lile   “Je! Unamjua Mungu wa kweli??” Kumbuka unaposema umetoka kwenye dhambi ni sawa na Bwana kakutoa nchi ya Misri ambayo ulikuwa ni mtumwa wa dhambi? Lakini je! Baada ya kutoka huko umemfahamu Mungu unayemtumikia?? Au unamchukulia Mungu, kama ile miungu uliyokuwa unaiabudu kabla ya kumpokea yeye??…

Biblia inasema katika agano jipya pia..

1 PERTO 1: 13 “kwa hiyo vifungeni viuno vya nia zenu, na kuwa na kiasi; mkiitumainia kwa utimilifu ile neema mtakayoletewa katika ufunuo wake yesu kristo.

14 kama watoto wa kutii msijifananishe NA TAMAA ZENU ZA KWANZA ZA UJINGA WENU;

15 bali kama yeye ALIYEWAITA ALIVYO MTAKATIFU, NINYI NANYI IWENI WATAKATIFU KATIKA MWENENDO WENU WOTE;

16 kwa maana imeandikwa, MTAKUWA WATAKATIFU KWA KUWA MIMI NI MTAKATIFU.

17 na ikiwa mnamwita baba, yeye ahukumuye kila mtu pasipo upendeleo, kwa kadiri ya kazi yake, enendeni kwa hofu katika wakati wenu wa kukaa hapa kama wageni”.

Huwezi ukasema umetolewa katika utumwa wa dhambi na bado unasujudia sanamu, huwezi ukasema umetolewa katika utumwa wa dhambi na bado ukawa mwasherati, au mlevi, au mtukanaji…Huwezi ukasema umeokolewa kutoka katika utumwa wa dhambi na bado unavaa nguo zinazoonyesha maungo yako, unavaa nguzo zinazo kubana, unavalia vimini, suruali na kupaka wanja..Hizo zote ni tamaduni za miungu ya ki-Misri na huwezi kumtumikia Mungu wa kweli kwa tamaduni za ki-Misri.

Ndugu yangu kama unataka kwenda na Bwana, mtii anayokuambia leo, Geuka upate ufahamu, usidanganyike kwamba Mungu anaangalia roho haangalii mwili, usidanganyike kwamba wanaopaka lipstick,na wanja na wanaovaa hereni, na wigi wataingia mbinguni..Usidanganyike kuwa wanaofanya masturbation, na wanaotazama pornography, na wanaoishi na wanawake/wanaume ambao hawajaoana kuwa wataingia mbinguni, usidanganyike kuwa ukiwa vuguvugu, nusu Mungu nusu ulimwengu, utaingia mbinguni.. Bwana anasema mwenyewe kuwa ATAKUTAPIKA!!  Kwasababu yeye ni mtakatifu na hivyo tutakuwa watakatifu kama yeye alivyo..

Waebrania 12:14 “Tafuteni kwa bidii kuwa na amani na watu wote, NA HUO UTAKATIFU, AMBAO HAPANA MTU ATAKAYEMWONA BWANA ASIPOKUWA NAO;”

Ni maombi yangu kuwa utamjua Mungu wa kweli ni nani, kama hujamjua na utachukua uamuzi thabiti wa kumfuata yeye kwa viwango anavyotaka yeye vya UTAKATIFU. Na kama hujabatizwa nakushauri ufanye hivyo mapema, kwasababu ubatizo sahihi wa kuzamishwa katika maji mengi, na kwa Jina la Yesu  ni wa muhimu sana, katika kuikamilisha safari yako ya wokovu.

Bwana akubariki.

Pia unaweza ukapata mafundisho haya Kwa njia ya Whatsapp yako, jiunge na channel yetu Kwa kubofya hapa >> WHATSAPP

Tafadhali “Share” ujumbe huu kwa wengine na Bwana atakubariki.


Mada Nyinginezo:

TAWI LIZAALO HULISAFISHA ILI LIZIDI KUZAA.

NGUVU YA MUNGU YA UUMBAJI

IKO NJIA IONEKANAYO KUWA SAWA MACHONI PA MTU.

MNGOJEE BWANA


Rudi Nyumbani

Print this post

About the author

Admin administrator

Subscribe
Notify of
guest
0 Comments
Inline Feedbacks
View all comments