KANUNI JUU YA KANUNI.

KANUNI JUU YA KANUNI.

Isaya 28:13 “Kwa sababu hiyo neno la Bwana kwao litakuwa hivi, amri juu ya amri, amri juu ya amri; kanuni juu ya kanuni, kanuni juu ya kanuni; huku kidogo na huku kidogo; ili waende na kuanguka nyuma, na kuvunjwa, na kunaswa, na kuchukuliwa.”

Yapo madhara makubwa sana ya kufungwa katika vifungo vya kidini kwa muda mrefu, au kanuni Fulani za kidhehebu kwa muda mrefu kwasababu hiyo inapelekea kuridhika na kubakia katika hali hiyo hiyo, na mwisho wa siku Roho Mtakatifu anakuwa hana nafasi tena ya kumwongoza mtu wa namna hiyo kwasababu tayari kanuni za dini yake zimeshamfunga, na hivyo haoni haja tena ya kumtaka Roho Mtakatifu awe kiongozi wake. Na hilo ndilo lililokuwa pia katika kipindi cha Bwana wetu YESU.

Wakati ule wayahudi walikuwa chini ya dini zao kongwe (Mafarisayo na Masadukayo), ni kweli baadhi ya mambo waliyokuwa wanaamini chanzo chake ni Mungu lakini hawakuweza kuufikia utimilifu wote wa kukubaliwa na Mungu kwasababu tayari walishajifunga, walikwama sehemu Fulani kwa muda mrefu.

Lakini wakati ulipofika wa Mungu kuona sasa kuna haja ya kuleta utimilifu wote duniani ndipo alipomtuma mwanae mpendwa YESU aje duniani kutueleza yote. Lakini wale watu kwa kuwa kanuni za dini zao zilikuwa zimewakaa sana walijiona tayari ni wakamilifu, hivyo hawakuona kuna haja ya mtu kuwaletea ukamilifu mwingine zaidi ya huo walionao, waliona kuwa sheria ya Musa inatosha tu! mtu akiishika hiyo inamtosha kumfanya awe mkamilifu.

Torati inasema usizini, hivyo mtu akishiishi bila kuzini hata kama anawakata tamaa kila siku ndani ya moyo wake basi inatosha yeye kuonekana kuwa mkamilifu maadamu hajawahi kuzini katika maisha yake, na ndio maana hata Bwana Yesu alipokuja kutilia mkazo amri hiyo hiyo pale alipowaambia mtu amtazamaye mwanamke kwa kumtamani amekwisha zini naye, wakaona kuwa kama huyu anavunja maagizo ya Mungu. Hawakujua kuwa ni kile kile Bwana anakisisitiza isipokuwa katika ukamilifu wote,..Ni amri juu ya amri, kanuni juu ya kanuni. Lakini wao kwakuwa walikariri maandiko walimpinga vikali.

Kadhalika na mambo mengine yote Yesu aliyokuwa anayasema wao walidhani kuwa wanaletewa mambo mapya, walipoombiwa mtu amwoneaye ndugu yake hasira ni sawa na muaji, walidhani Kristo kajitungia mwenyewe maneno yale, lakini Kristo alikuwa anawafanya kuwa wakamilifu zaidi katika sheria zao. Ni sawa mwalimu amwambie mwanafunzi wake kuwa licha tu ya kuandika majibu ya mtihani wake, apange kazi yake vizuri na aandike vizuri pia… Lakini kwa kuwa walijizoelea kuenenda hivyo katika kanuni zao kwa muda mrefu, basi hata kutafari tena ni kwanini yale maneno yalisemwa vile kukafa ndani yao.

Wanakuwa wanayafuata tu kama desturi au mila, na sio kama vile Roho anawaongoza, au anawataka wao wawe watakatifu.

Kumbuka mpango wa Mungu juu ya maisha yetu sio tu kuokolewa halafu basi, hapana, Mungu anataka tufikie ukamilifu wote alioukusudia mwanadamu aufikie, ingekuwa tu ndio hivyo halafu basi siku ile ulipoyasalimisha maisha yako kwa Bwana basi ungepaswa ufe uende kwa Baba. Lakini haiko hivyo ni lazima tufikie ukamilifu wote Mungu anaoutaka ndio tuondoke, sasa basi ikiwa ndio hivyo ni wajibu wa Bwana kila siku kutupa amri juu ya amri, kanuni juu ya kanuni, huku kidogo na huku kidogo,.,na ndio maana biblia haina kitabu kimoja, bali 66, imekuwa hivyo ili tuweze kuvumbua utimilifu wote wa Mungu.

Ikiwa mtu ni mwamini wa kweli utakuta hapo mwanzoni alipomwamini Kristo, hakuona kuwa kuvaa vimini ni dhambi, lakini kwa kuwa Roho wa Mungu yupo ndani yake, anamfundisha na kumpa kanuni juu ya kanuni kila siku ili kumfanya kuwa mkamilifu, utaona baadaye anaona si sawa kuwa na zile nguo hivyo anachoma vile vimini, alivyokuwa anavaa kadhalika hapo mwanzo alikuwa anaona ni sawa tu kwa mwanamke wa kikristo kuvaa suruali lakini kwa kuwa Roho wa Mungu yupo ndani yake, Neno la Mungu likimjia kumwambia atupe hizo suruali, kwamba haimpasi mwanamke kuvaa mavazi yampasayao mwanamume, hatashangaa kwasababu atajua kuwa maagizo hayo yanalandana na utakatifu ambao ndio Mungu anautaka. Lakini utakuwa mtu mwingine ambaye yeye yupo chini ya kanuni za kidhehebu au za kidini, sasa kwa kuwa dini yake haisemi kuwa mwanamke kuvaa vimini na suruali pamoja na wanja na hereni ni machukizo mbele za Mungu, siku ambapo atasikia kwa mara ya kwanza Neno hilo utamwona anaanza kupinga pasipo hata kutafakari, atadai kwamba maadamu sizini mimi sina hatia, lakini hajui kuwa anaambiwa hivyo kwa faida yake mwenyewe ili aukamilishe utakatifu wake wa kutokuzini, kwasababu biblia inasema amtazamaye mwanamke kwa kumtamani amekwisha zini naye, sasa ni kweli yeye anaweza akawa hajatamani wala hajazini, lakini yupo mwingine kazini juu yake, kwasababu ya mavazi yake ya uchi uchi, Na Bwana Yesu alishasema mtu yeyote atakayemkosesha mmojawapo wa wadogo hawa ingemfaa zaidi mtu huyo jiwe la kusagia lifungwe shingoni mwake kisha akatupwe baharini. Je! hapo mtu kama huyo atakuwa na la kujitetea siku ile ya Hukumu?.

Kuna hatari kubwa sana ya kuongozwa na mapokeo yale yale tu yaliyo kwenye dini zetu, na kusahau Roho Mtakatifu anataka nini kwa mwaminio katika wakati anaoishi. Mungu hafanyi kazi ya kuokoa tu watu, anafanya kazi pia ya kuwafanya wawe wakamilifu. “Mathayo 5:48 “Basi ninyi mtakuwa wakamilifu, kama Baba yenu wa mbinguni alivyo mkamilifu.”

Umebatizwa ukiwa mchanga, na sasa unajua kabisa hakuna ubatizo wa watoto wachanga, wala wa kunyunyiziwa bali wa kuzamwishwa kwenye maji tele na kwa jina la YESU, lakini hapo kabla ulifanya kimakosa na hivyo haukukamilishwa, lakini sasa Bwana anakupa kanuni sawasawa na Neno lake katika (Mdo 2:38, 8:16, 10:48, 19:5) kwamba ukabatizwe tena kwa maji mengi na kwa jina la YESU KRISTO upate ondoleo la dhambi zako. Usifanye moyo wako mgumu, ukadhani kuwa ni dini mpya au mtu anataka kukutoa kwenye dhehebu lako. Tii tu kwasababu ni maagizo ya YESU BWANA WAKO.

Hapo mwanzo ulikuwa unadhani kuna mpatanishi zaidi ya mmoja, kwamba hata bikira Maria anaweza akawa mpatanishi wa dhambi zako, na kukuombea,..haukuwa na nia mbaya kufahamu hivyo..Lakini sasa umejua ukweli kuwa mpatanishi wa dhambi zetu ni mmoja tu! biblia inasema “hakuna wokovu kwa mwingine awaye yote zaidi ya YESU (matendo 4:12)”. Hiyo ni kanuni ambayo ulikuwa hauijui, Bwana amekupa tena leo, usiipinge wala kuikataa kwasababu lengo lake Bwana ni kukufanya wewe uwe mkamilifu ili siku ile uweze kusimama mbele yake. Hakuna maagizo ya kwenda toharani kwenye biblia. Mtu ameandikiwa kufa mara moja baada ya kifo ni hukumu…elimu nyingine inayosema kuna nafasi ya pili baada ya kufa ni kutoka kwa Yule adui, akitaka ujitumainisha ya kwamba hata ukiendelea katika dhambi ipo nafasi ya pili huko unakokwenda…Biblia inasema mkumbuke Muumba wako kabla roho haijamrudia yeye aliyeiumba (Mhubiri 12:1-7).

Hivyo ndugu ikiwa ulishamwamini Bwana, ni wakati wa wewe kukua kutoka hatua moja ya utakatifu hadi nyingine, na hiyo lazima iendane na kanuni za Mungu pamoja na amri zake, kutoka kanuni moja hadi nyingine.. Angalia maisha yako ya leo je! ni sawa na ulivyokuwa jana na juzi?, je! kuna kitu chochote kimeongezeka ndani yako?. Umekaa ndani ya wokovu kwa miezi sasa, kwa miaka sasa, je! kuna mabadiliko ,mambo unayoyatenda unataka yafanane na mtu aliyemkabidhi Bwana maisha yake leo?. Kama hakuna badiliko basi fahamu kuwa uongozo wa Roho Mtakatifu ulishakufa ndani yako siku siku nyingi, ulishamzimisha Roho ndani yake asiendelee kukufundisha. Hivyo geuka urudi..naye Roho atarudi ndani yako kukuongoza.

Waefeso 4:13 “hata na sisi sote tutakapoufikia umoja wa imani na kumfahamu sana Mwana wa Mungu, HATA KUWA MTU MKAMILIFU, hata kufika kwenye cheo cha kimo cha utimilifu wa Kristo;

14 ili tusiwe tena watoto wachanga, tukitupwa huku na huku, na kuchukuliwa na kila upepo wa elimu, kwa hila ya watu, kwa ujanja, tukizifuata njia za udanganyifu”.

Hivyo ni maombi yangu Bwana atakujalia kukua na kutii maagizo yote Mungu anayokupa leo na kuyatendea kazi Na Maneno haya yawe akiba katika moyo wako, Mungu akubariki sana.

Tafadhali “share” ujumbe huu kwa ndugu zako na rafiki zako.

Mungu akubariki.

Pia unaweza ukapata mafundisho haya Kwa njia ya Whatsapp yako, jiunge na channel yetu Kwa kubofya hapa >> WHATSAPP


Mada Nyinginezo:

MUNGU MWENYE HAKI.

MANA ILIYOSHUSHWA KUTOKA MBINGUNI.

SAUTI NYUMA YA ISHARA.

MTI WA UZIMA NA MTI WA MAARIFA.


Rudi Nyumbani

Print this post

About the author

Admin administrator

Subscribe
Notify of
guest
0 Comments
Inline Feedbacks
View all comments