NI NANI ALIYEIDHARAU SIKU YA MAMBO MADOGO?.

NI NANI ALIYEIDHARAU SIKU YA MAMBO MADOGO?.

Ni nani aliyeidharau siku ya mambo madogo?…Ni swali Bwana alilouliza.

Jina la Bwana Yesu Kristo, libarikiwe, karibu katika kujifunza Neno la Mungu, Leo kwa Neema za Mungu, tutajifunza namna ya  kusimama imara siku ya mambo madogo?.

Najua unajiuliza SIKU YA MAMBO MADOGO NDIO NINI?...Lakini kabla ya kufikia huko kuelezea siku ya mambo madogo, hebu tujikumbushe kidogo historia fupi ya Taifa la Israeli, ambapo kwa kupitia hiyo tutaelewa kwa undani nini maana ya “siku ya mambo madogo”.

Kama wengi wetu tunavyojua Mungu aliwatoa wana wa Israeli kutoka katika nchi ya Misri, na kuwaingiza katika nchi ya ahadi, ambapo ndani ya nchi ile aliwaahidia kula mema yote endapo wataishi kwa kuzishika amri zake, na kama ni msomaji mzuri wa biblia utagundua kuwa vipo vizazi vilivyofanya vizuri kwa kwenda katika sheria za Mungu, ambavyo viliishi kwa raha na kwa amani, na vipo pia vizazi vya wana wa Israeli ambavyo havikufanya vizuri, vilikengeuka na kuacha kuyashika maagizo ya Mungu waliyopewa na badala yake  vikapitia vipindi vya tabu sana.

Na utaona pia baada tu ya Israeli kugawanyika na kuwa sehemu mbili yaani YUDA NA ISRAELI …ndio kipindi ambacho wana wa Israeli walipozidi  kukengengeuka kwa viwango vya hali ya juu. Kuanzia kipindi cha Mfalme Yeroboamu mpaka kipindi cha mfalme Hosea wa Israeli kulikuwa hakuna unafuu kabisa, watu waliabudu mabaali na sanamu wazi wazi na kuvukiza uvumba katika sehemu za juu. Na kwasababu ya maasi kuwa mengi, Bwana alituma idadi kubwa sana ya manabii wake katika kipindi hichi kuliko vipindi vyote vilivyotangulia ili kuwaonya wana wa Israeli wageuke na kuacha njia zao mbovu, hivyo kuanzia huo wakati manabii wengi sana walitokea kama wakina Eliya, Elisha, Nathani, Yona, Habakuki,Sefania, Hosea, Mika, Yeremia,Isaya, Obadia, Amosi,Nahumu,Ezekieli,Yoeli,Mika, Zekaria n.k Wote hawa walitokea ndani ya kipindi cha wafalme wa Israeli..Lakini hawakusikia, kinyume chake waliwaua wengine na kuwapiga kwa mawe.

Hivyo maovu yalipozidi hata kufikia kikombe cha ghadhabu ya Mungu kujaa, kukawa hakuna tena kusamehe, Mungu akaahidi kuwa watakwenda utumwani, na Miji yao yote itachomwa moto, na watu wengi sana watauawa kwa upanga, na wengine watakufa kwa njaa, na  wengine kwa Tauni. Na lile hekalu ambalo mfalme Sulemani alilitengeneza kwa gharama nyingi litavunjwa na kuteketezwa kabisa..Na kweli wakati ulipowadia Neno la Bwana lilitimia, Israeli ilichukuliwa utumwani Ashuru na wale waliosalia wa Yusa ,Wakaldayo(yaani watu wa Babeli)..walifika Yerusalemu wakauteketeza mji wao kwa moto, wakalivunja lile hekalu kama Ilivyotabiriwa wakawaua watu wengi kwa upanga; wanawake, kwa watoto na wachache waliobakia waliwachukua utumwani kwenda nao Babeli. Israeli Mji ambao ulipata sifa na kuogopeka na mataifa yote ulimwenguni ukageuka kuwa kama jalala.

Lakini Mungu ni wa rehema aliwaahidi kuwa hawatakaa huko utumwani milele, bali watakaa huko wakimtumikia Mfalme wa Babeli kwa miaka 70 tu! na baada ya hiyo miaka 70 kuisha watarejeshwa tena kwao.

Sasa ndio tunaelekea kwenye kiini cha somo letu, baada tu ya wana wa Israeli kutimiza ile miaka 70, wakiwa Babeli Mungu aliwafungulia mlango wa kurudi tena nchini mwao, lakini waliporudi kule walikuta tayari kuna watu wengine ambao walikuwa wanakaa pale, ambao sio waisraeli, ambao mfalme wa Uajemi aliwaweka wakae kule…Lakini Hao watu walipoona wana wa Israeli wamerudi tena nchini mwao wakaanza kuwapiga vita.

Wakati wana wa Israeli wanapanga kumjengea tena Mungu Hekalu lingine jipya baada ya lile la kwanza kuharibiwa na Mfalme wa Babeli miaka 70 iliyopita, wanakutana tena na changamoto nyingine ya kusumbuliwa…hivyo kwasababu ya hao watu iliwafanya waishiwe nguvu kabisa ya kuijenga tena nyumba ya Mungu, kwasababu pia kwa idadi yao waliorudi Israeli walikuwa ni wachache sana.

Lakini ulipofika wakati Mungu aliwanyanyua manabii wake wawili HAGAI na ZEKARIA kuwatabiria wana wa Israeli kwamba wasimame imara waijenge nyumba ya Mungu wasiogope changamoto zilizopo mbele yao, ijapokuwa hawana fedha wala utajiri lakini Bwana atakuwa nao katika UDOGO WAO. Bwana akamwambia Hagai maneno haya awaambie wana wa Israeli.

Hegai 2: 1 “Katika mwezi wa saba, siku ya ishirini na moja ya mwezi, neno la Bwana lilikuja kwa kinywa cha Hagai nabii, kusema,

2 Sema sasa na Zerubabeli, mwana wa Shealtieli, liwali wa Yuda, na Yoshua, mwana wa Yehosadaki, kuhani mkuu, na hayo mabaki ya watu, ukisema,

3 Miongoni mwenu amebaki nani aliyeiona nyumba hii katika utukufu wake wa kwanza? Nanyi mnaionaje sasa? Je! Mbele ya macho yenu, siyo kama si kitu?

4 Lakini sasa uwe hodari, Ee Zerubabeli, asema Bwana; nawe uwe hodari, Ee Yoshua, mwana wa Yehosadaki, kuhani mkuu, nanyi iweni hodari, enyi watu wote wa nchi hii, asema Bwana; MKAFANYE KAZI, kwa kuwa mimi ni pamoja nanyi, asema Bwana wa majeshi;

5 KAMA NENO LILE NILILOAGANA NANYI MLIPOTOKA KATIKA NCHI YA MISRI; NA ROHO YANGU INAKAA KATI YENU; MSIOGOPE.

6 Kwa maana Bwana wa majeshi asema hivi, Mara moja tena, ni kitambo kidogo tu, nami nitazitikisa hizo mbingu, na hii nchi, na bahari, na nchi kavu;

7 nami nitatikisa mataifa yote, na vitu vinavyotamaniwa na mataifa yote vitakuja; nami nitaijaza nyumba hii utukufu, asema Bwana wa majeshi.

8 FEDHA NI MALI YANGU, NA DHAHABU NI MALI YANGU, asema Bwana wa majeshi.

9 Utukufu wa mwisho wa nyumba hii utakuwa mkuu kuliko utukufu wake wa kwanza, asema Bwana wa majeshi; na katika mahali hapa nitawapa amani, asema Bwana wa majeshi”.

Unaona maneno hayo?..Bwana anawatia moyo wana wa Israeli kuwa WASIOGOPE! Utukufu wa hekalu la pili utakuwa mkubwa kuliko utukufu wa lile Hekalu la Kwanza. Hivyo wasonge mbele, wakafanye kazi, wasiangalie umaskini walio nao, wala shida waliyo nayo wasonge mbele kwasababu utukufu wa nyumba ya pili utakuwa ni mkubwa kuliko utukufu wa nyumba ya kwanza, na FEDHA NA DHAHABU NI MALI ya Bwana.. haleluya!! Haleluya!!.

Zaidi ya hayo wakati wana waisraeli wakiongozwa na kiongozi wao aliyeitwa ZERUBABELI wanatazama kuwa kujenga nyumba na uchache wao, na umaskini wao, pamoja na wingi wa maadui uliowazunguka ni jambo lisilowezekana, ni kama mlima mkubwa umewekwa mbele yao halafu uusawazishe kwa beleshi..Lakini jicho la Mungu lilikuwa linaona tofauti..Na ndio Bwana akampa nabii Zekaria maono mengine miezi miwili baada ya yale maono ya Hagai na kusema..

Zekaria 4: 5 “Ndipo malaika aliyesema nami akajibu, akaniambia, Hujui vitu hivi ni nini? Nikasema, La, Bwana wangu.

6 Akajibu akaniambia, akisema, Hili ndilo neno la Bwana kwa Zerubabeli, kusema, SI KWA UWEZO, WALA SI KWA NGUVU, BALI NI KWA ROHO YANGU, ASEMA BWANA WA MAJESHI.

7 NANI WEWE, EE MLIMA MKUBWA? MBELE YA ZERUBABELI UTAKUWA NCHI TAMBARARE; NAYE ATALILETA LILE JIWE LA KUWEKWA JUU KABISA PAMOJA NA VIGELEGELE VYA, NEEMA, NEEMA, ILIKALIE.

8 Tena neno la Bwana likanijia, kusema,

9 Mikono yake Zerubabeli imeiweka misingi ya nyumba hii, na mikono yake ndiyo itakayoimaliza; nawe utajua ya kuwa Bwana wa majeshi amenituma kwenu

10 MAANA NI NANI ALIYEIDHARAU SIKU YA MAMBO MADOGO? Kwa kuwa watafurahi, nao wataiona timazi katika mkono wa Zerubabeli…..”

Unaona hapo anasema NANI WEWE, EE MLIMA MKUBWA? MBELE YA ZERUBABELI UTAKUWA NCHI TAMBARARE, Mbele ya changamoto zote zinazoonekana kama ni milima, mbele za masihi wa Bwana zitakuwa ni nchi tambarare…na sio kwa uwezo wa Zerubabeli wala kwa nguvu zao bali kwa roho yake Bwana ndio watausawazisha huo mlima.

Na zaidi ya yote Bwana anamwambia Zerubabeli.. “MAANA NI NANI ALIYEIDHARAU SIKU YA MAMBO MADOGO”…

Sasa siku ya mambo madogo ndio ipi?..Ndio hiyo siku ambayo walikuwa hawana chochote, siku ambayo walikuwa wanaona hakuna chochote kinachoweza kufanyika, siku ambayo walikuwa wanaona ndio kwanza mambo bado hata hayajaanza, siku ambazo nguvu zao ni chache, hizo ndio siku za mambo madogo?..Na Bwana anawauliza ni nani anayezidharau siku hizo??…Ni nani anayesema kwamba jambo hilo la kuisimamisha nyumba yenye utukufu mwingi halitafanikiwa?..Ni nani anayesema kuwa katika udhaifu huo hakuna chochote kinachoweza kufanyika?!…sentensi hiyo huwa inamuhuzunisha Mungu sana.

Ndugu somo hili ni la kukutia moyo tu! wewe ambaye upo katika safari ya kwenda mbinguni, kuwa USIIDHARAU SIKU YA MAMBO MADOGO.

Kama ndio kwanza unaanza kumtafuta Mungu, usizidharau siku hizi ambazo unajiona huwezi kuitenda kazi ya Mungu, siku inafika utakayoleta matunda mengi kwa Kristo, endapo hutazimia unachopaswa kufanya ni kuendelea kusonga mbele kwa bidii zote bila kukata tamaa,…Mtaji ulionao moyoni mwako uzalishe, kwasababu ni kama mbegu ndogo, na itakapokuwa itakuletea faida nyingi sana mbeleni. Mwingine aliniambia jana siwezi kumgeukia Mungu kwasasa sina kazi,..ndugu hata ukipata bilioni 100 leo bado utajiona tu hujafika, anza leo na Bwana.

Na pia katika maisha ya kawaida ya kujitafutia riziki, ikiwa wewe ni mkristo na kwanza ndio shughuli  uzifanyazo zinaanza kuchipuka, upo  kama fukara tu! au una mtaji kidogo, au kazi yako ni ya hadhi ya chini sana, na ukiangalia mbele unaona milima mikubwa, hiyo milima isikuogopeshe, ITAKUWA NCHI TAMBARARE…. Usidharau siku ya mambo madogo nenda kakifanyie kazi hicho kidogo, kakizalishe!! Usimvunjie Mungu heshima kwa kutomwamini endelea kutenda haki katika utakatifu wote kwa sababu fedha na dhahabu ni mali yake, mwisho wa siku atakunyanyua tu! kama alivyomnyanyua Zerubabeli na haitakuwa kwa nguvu zako wala kwa uwezo wako bali kwa ROHO WA MUNGU,…NI NANI WEWE UNAYEIDHARAU SIKU YA MAMBO MADOGO! Mungu mwenyewe haidharau wewe ni nani uidharau na mtu mwingine yoyote yeye ni nani hata aidharau siku ya mambo yako madogo!!..Hata kama unauza mchicha usizidharau hizo siku.

Na mwisho kabisa tunaona baada ya Zerubabeli kupata unabii ule kutoka kwa Bwana, kwa vinywa vya Hagai na Zekaria Manabii wa Bwana, alipata nguvu mpya yeye pamoja na Yoshua na wana wa Israeli wote na kwenda kuijenga nyumba ya Mungu, na baada tu ya kutia nia ya kwenda kuijenga nyumba, wakati huo huo vibali vikaanza kufunguka, mara mfalme anatoa amri wapewe ruhusa ya kujenga pasipo kusumbuliwa, mara mfalme anasema wapewe fedha na wasilipishwe kodi yoyote na fursa nyingi na upendeleo mwingi waliupata kutoka kwa watu na mfalme, nyumba ya Mungu ilipatikana na dhahabu nyingi na fedha nyingi, na ikamalizika chini ya mikono ya Zerubabeli salama sawasawa na unabii Bwana alioutoa.

Hivyo ndugu, Bwana ndiye anayenyanyua na ndiye anayeshusha, kama alikushusha chini wakati mwingine ni kwasababu ya maovu yako (ingawa sio kila kushushwa chini ni kwasababu ya maovu, nyingine ni kwa utukufu wa Mungu kama Ayubu), kama ilivyo tu kufanikiwa, sio mafanikio yanatoka kwa Mungu…lakini kama maisha yako yalikuwa hayampendezi Mungu huko nyuma na akakushusha ni kwasababu anakupenda anataka akupe tumaini tena, kama alivyowashusha wana wa Israeli kukaa Babeli miaka 70, na walipotubu aliwarudisha tena katika nchi yao na kuwapa faraja kubwa kama hiyo, na kuwanyanyua tena! Kwanini na wewe asikufanyie hivyo endapo utatubu kabisa kwa kumaanisha kuziacha dhambi zako na kumgeukia yeye. Na kumbuka USITUBU! Kwasababu tu unataka KUPATA UTAJIRI WA ULIMWENGU HUU, tubu kwasababu unataka kwanza kupata UTAJIRI WA ULIMWENGU UNAOKUJA!…..Huo ukiupata hata huu wa ulimwengu hauhitaji kuuhangaikia, Bwana alisema TUTAZIDISHIWA, kuzidishiwa sio kusumbukia, kitu cha kutafuta ni Ufalme wa Mungu, huo ndio tumeambiwa tuutafute kwa bidii zote …“ Mathayo 6:33..utafute kwanza ufalme wake na haki yake, na hayo mengine mtazidishiwa”.

Hivyo Kama hujampa Bwana maisha yako, huu ndio wakati wako wa kufanya hivyo, kabla mlango wa Neema haujafungwa, Roho wa Mungu anataka utii thabiti kutoka ndani ya moyo wako na sio kulazimishwa, anataka utubu kabisa kwa kudhamiria KUACHA, sio KUPUMZIKA, hapana bali kuacha dhambi, unakusudia kuacha kwa vitendo usengenyaji, uasherati, rushwa, utukanaji, ulevi, uvaaji usio na heshima(vimini na suruali kwa wanawake), unakusudia kuacha anasa zote za ulimwengu, na ukisha tubu hatua inayofuata ni ubatizo sahihi, na ubatizo sahihi ni wa maji Mengi na kwa Jina la Yesu Kristo, kulingana na Matendo 2:38, na kisha baada ya ubatizo Bwana mwenyewe atakupa kipawa cha Roho wake Mtakatifu atakayekusaidia kushinda dhambi. Na hapo utakuwa umezaliwa mara ya pili kwa maji na kwa Roho.

Mungu akubariki sana.

Pia unaweza ukapata mafundisho haya Kwa njia ya Whatsapp yako, jiunge na channel yetu Kwa kubofya hapa >> WHATSAPP


Mada Zinazoendana:

SHETANI ANATOLEA WAPI FEDHA, ANGALI TUNAJUA FEDHA NA DHAHABU NI MALI YA BWANA?.

TOA HUDUMA ILIYO BORA.

JE! KUBET NI DHAMBI?


Rudi Nyumbani

Print this post

About the author

Admin administrator

Subscribe
Notify of
guest
2 Comments
Newest
Oldest Most Voted
Inline Feedbacks
View all comments
Hosea kateko
Hosea kateko
1 year ago

Amina barikiwa kwa ujumbe mzuri,ninaswali kwa habari ya ubatizo ukisoma matendo ya mitume 1:5 Yesu aliwaambia wanafunzi wake yohana aliwabatiza kwa maji lakin ninyi sasa mtabatizwa kwa Roho mtakatifu pia Yesu alipokuwa kasurubiwa msalaban alikuwa yupo na waalifu wawili ambapo mmoja alimwamini katika dakika za mwisho na Yesu akamwambia tutakuwa wote peponi japo hakubatizwa ivyo suala la maji mengi na macheche ni mambo ya mwilini yakiashilia kuamini kwa mtu ila ubatizo ni jambo la rohoni kwa sababu kuna watu mazingira yao sio rahic kupata maji mengi, wengine wapo magerezan, wagonjwa nk nao pia wananeema ya wokovu maji sio kifungo cha mtu kumwamini Yesu kama kweli kamaanisha.

Flaviani
Flaviani
2 years ago

Barikiwa kwa ujumbe wenye tafsiri inayoeleweka