UFUNUO: Mlango wa 17

UFUNUO: Mlango wa 17

Karibu tujifunze kitabu cha Ufunuo leo tukiwa katika mwendelezo wetu wa sura ya 17, Biblia inasema…

Ufunuo 17:1-6″
1 Akaja mmoja wa wale malaika saba, wenye vile vitasa saba, akanena nami, akisema, Njoo huku, nitakuonyesha hukumu ya yule kahaba mkuu aketiye juu ya maji mengi;

2 ambaye wafalme wa nchi wamezini naye, nao wakaao katika nchi wamelevywa kwa mvinyo ya uasherati wake.

3 Akanichukua katika Roho hata jangwani, nikaona mwanamke, ameketi juu ya mnyama mwekundu sana, mwenye kujaa majina ya makufuru, mwenye vichwa saba na pembe kumi.

4 Na mwanamke yule alikuwa amevikwa nguo ya rangi ya zambarau, na nyekundu, amepambwa kwa dhahabu, na kito cha thamani, na lulu, naye alikuwa na kikombe cha dhahabu mkononi mwake, kilichojawa na machukizo, na machafu ya uasherati wake.

5 Na katika kipaji cha uso wake alikuwa na jina limeandikwa, la siri, BABELI MKUU, MAMA WA MAKAHABA NA MACHUKIZO YA NCHI.

6 Nikamwona yule mwanamke amelewa kwa damu ya watakatifu, na kwa damu ya mashahidi wa Yesu. Nami nilipomwona nikastaajabu ajabu kuu.

Tukirudi nyuma kidogo kwenye ile sura ya 13, tunamwona yule mnyama aliyetoka baharini mwenye vichwa saba na pembe 10, akielezewa, jambo hilo hilo tunaliona tena katika hii sura ya 17 mnyama yule yule mwenye vichwa 7 na pembe 10 na majina ya makufuru ametokea tena, isipokuwa hapa katika sura hii ya 17 tunaona kuna jambo lingine limeongezeka; anaonekana MWANAMKE  AKIWA AMEKETI JUU YAKE.

 Kwahiyo msisitizo mkubwa katika sura hii ni juu ya huyo mwanamke aliyepambwa kwa dhahabu, lulu na vito vya thamani aliyeketi juu ya huyo mnyama.

Sasa mwanamke huyu ni nani?

Mwanamke katika biblia anawakilisha KANISA, Sisi wakristo tunatambulika kama BIBI-ARUSI wa KRISTO,(2Wakoritho 11:2 Paulo anasema “..Maana nawaonea wivu, wivu wa Mungu; kwa kuwa naliwaposea mume mmoja, ili nimletee Kristo BIKIRA SAFI. “) Na pia..

Ufunuo 19:7 inasema..” Na tufurahi, tukashangilie, tukampe utukufu wake; kwa kuwa arusi ya Mwana-Kondoo imekuja, na MKEWE amejiweka tayari. Naye amepewa kuvikwa kitani nzuri, ing’arayo, safi; kwa maana kitani nzuri hiyo ni matendo ya haki ya watakatifu.  Pia Taifa la Israeli Bwana alilitambua kama MKE WAKE” [soma ezekieli16:1-63, ezekieli 23] utaona jambo hilo. Hivyo mahali popote Mungu anapozungumza juu ya kundi la watu wake huwa analifananisha na mwanamke.

Lakini hapa tunaona mwanamke mwingine ametokea ambaye anaonekana ni KAHABA,  amelewa kwa DAMU za watakatifu na za mashahidi wa YESU, na tena wafalme wa nchi wamezini naye, nao wakaao katika nchi wamelevywa kwa mvinyo ya uasherati wake.  Na katika kipaji cha uso wake ana jina limeandikwa, la SIRI, BABELI MKUU, MAMA WA MAKAHABA NA MACHUKIZO YA NCHI.

Hivyo tunaona tabia ya huyu mwanamke (ambaye anawakilisha KANISA fulani) kuwa ni KAHABA, Na kama tunavyofahamu kanisa la KRISTO haliwezi kuwa kahaba, kwasababu ni BIKIRA SAFI, na haliwezi kuua watakatifu wa Mungu, kwasababu lenyewe ni TAKATIFU, Hivyo hili Kanisa haliwezi kuwa lingine zaidi ya KANISA KATOLIKI chini ya uongozi wa PAPA.

Kwanini ni Kanisa  KATOLIKI na si kitu kingine?

Tunajua siku zote shetani anatabia ya kuunda “copy” inayofanana na ya Mungu ili aabudiwe kirahisi, au kudanganya watu kirahisi, vinginevyo asingeweza kupata wengi, ili noti feki iweze kufanya kazi ni lazima ifanane sana na orijino, shetani anataka kuabudiwa kama Mungu hivyo atatumia njia zote zinazofanana na za Mungu  ili apate wafuasi wengi. Na ndio maana Mungu alikataza Mtu kutengeneza mfano wa Kitu chochote kama Mungu ili kukiabudu kwasababu mtu anaweza akadhani anamwabudu Mungu kumbe anamwabudu shetani mwenyewe kwa kivuli cha ile sanamu pasipo kujua.ZIKIMBIE IBADA ZA SANAMU. Mimi sipo kinyume na wakatoliki, wala siwahukumu ndugu zangu wakatoliki, bali nipo kinyume na mifumo ya kanisa Katoliki kwasababu Mungu alishaihukumu, na kupiga mbiu watu wake watoke huko wasishiriki mapigo yake!.

Sasa mpango wa Mungu aliouunda tangu awali ni kumleta “MTU” atakayesimama kwa niaba yake ili kuwakomboa wanadamu (VICAR) katika dhambi zao hivyo akamleta mwanae anayeitwa YESU KRISTO, ambaye kwetu sisi ni Mungu mwenyewe katika mwili..shetani kuona hivyo akaanza kuiga kwa kumtengeneza mtu wake (VICAR), ambaye naye atasimama kwa niaba yake hapa duniani, na akampa jina lililo maarufu (VICARIUS FILII DEI) yaani tafsiri yake,  ni “Badala ya mwana wa Mungu duniani”, hivyo huyu mtu wake anasimama hapa duniani badala ya mwana wa Mungu (yaani YESU KRISTO), na  shetani akamvika uwezo wake bandia kwamba na yeye anaweza kusamehe dhambi duniani kama vile BWANA WETU YESU KRISTO alivyo na uwezo wa kusamehe dhambi.

Na kama vile Mungu alivyounda kanisa lake takatifu kwa kupitia BWANA YESU KRISTO, ambalo ndilo linaloitwa BIBI-ARUSI safi, vivyo hivyo shetani naye alilitengeneza Kanisa lake kwa kupitia huyu (VICARIUS FILII DEII) yaani PAPA, Kutimiza kusudi lake la kutaka kuabudiwa na kupeleka watu kuzimu na hilo KANISA  ndilo KAHABA, Na si lingine zaidi ya KANISA KATOLIKI. 

Na tunajua Kanisa la Kristo safi linaongozwa na ROHO MTAKATIFU kwa kupitia zile huduma na karama za roho, yaani mitume, manabii,wachungaji, wainjilisti na waalimu lakini hili kanisa kahaba na lenyewe limevuviwa vyeo vya uongozi  kama Upapa, Ukadinali, upadre, paroko, ukasisi n.k.

Kwahiyo unaweza ukaona ni jinsi gani cha uongo kinavyofanana na cha ukweli, na watu wengi wamepofushwa macho na shetani wakidhani kuwa wanamwabudu Mungu hapo kumbe ni shetani.

Na ni kwasababu gani ni kahaba?

Ni kahaba kwasababu biblia inasema wafalme wa nchi wamezini naye nao wakaao katika nchi wamelevywa kwa mvinyo wa usherati wake, si ajabu Kanisa hili lina nguvu nyingi katika mataifa mengi kwa utajiri wake kwa jinsi linavyotoa misaada na miradi mingi ya kimaendeleo na ya kijamii, linajenga mashule na mahospitali linatoa misaada ya majanga na kusapoti siasa za nchi, linafanya hivi kwa lengo moja tu! kupumbaza mataifa na wafalme wa nchi ili kuwalewesha kwa kupenyeza mafundisho na itikadi zake za uongo kwa watu ambazo zipo nje ya MANENO MATAKATIFU YA MUNGU.

Na ndio maana tunaona mwanamke huyu ana jina limeandikwa kwa SIRI katika kipaji cha uso wake “BABELI MKUU MAMA WA MAKAHABA, NA MACHUKIZO YA NCHI”..Umeona hapo, jina lake lipo katika SIRI, hivyo inahitaji HEKIMA kumtambua, kwasababu shetani huwa hafanyi vitu vyake kwa wazi wazi, anatumia kivuli cha “orijino” ili kuwadanganya watu.

Ni BABELI mkuu kwasababu tafsiri yenyewe ya neno BABELI ni “MACHAFUKO”, Hivyo Mji wa Babeli ndio ulikuwa chimbuko la machafuko yote, ibada za kipagani za kuabudu miungu mingi na uchawi ndipo zilipozaliwa, Nimrodi akiwa muasisi wa mji ule na mke wake Semiramis pamoja na mtoto wao Tamuzi, waliabudiwa kama miungu, ndipo baadaye Waroma wakaja kutohoa mfumo huo wa kuabudu miungi mingi, na sio ajabu tunaona baadaye wakaja kumweka Yosefu kama Nimrodi, Semiramis kama Mariam na Tamuz kama mtoto YESU ili kutimiza matakwa yao ya ibada zao za sanamu ambazo walikuwa nazo tangu zamani, kwakweli haya ni machafuko makubwa sana katika KANISA LA KRISTO.

Na mji huu huu wa Babeli baadaye ndio uliohusika kuutesa na kuuchukua uzao wa Mungu (ISRAELI) mateka, sasa hii ilikuwa ni Babeli ya mwilini iliyolichukuwa Taifa la Israeli mateka sasa hii iliyopo leo ni  BABELI YA ROHONI(ambayo ni kanisa Katoliki ) inawachukua wakristo wengi mateka kwa kuwafanya waabudu miungu mingine mbali na YAHWE  YESU KRISTO MUNGU WETU. 

Lakini Biblia inasema hakika BABELI HII ya sasa itaangushwa tu! kama ilivyoangushwa ile ya kwanza ya mwilini. Nadhani kuanzia hapo utakuwa umeanza kupata picha ni kwanini mwanamke yule anajulikana kama BABELI MKUU. Sasa tuone ni kwa nini anaitwa “MAMA WA MAKAHABA”.

Ni Mama wa makahaba kwasababu amezaa wabinti ambao nao pia ni makahaba kama yeye na si mengine zaidi ya madhehebu yote yanayoshirikiana naye, wale waliokuwa wanajiita ma-protestants mwanzo  sasa hivi hawapo hivyo tena, wanashirikiana naye kwa namna zote. Kanisa Katoliki limefanikiwa kuwalewesha na kuwavuta tena kwake, lutheran imeshaungana na katoliki rasmi, pamoja na madhehebu mengine mengi,na ndio maana linaitwa “KANISA MAMA”. Sasa ni rahisi kuelewa hapo kwanini ni “MAMA WA MAKAHABA”..Kwasababu yeye ameshakuwa kanisa mama, na mabinti wake wameshafuata mifumo yake ya ibada zisizotokana na NENO la Mungu.

Na ni kwanini ni “Mama wa Machukizo ya nchi”?.

Hili kanisa lenyewe ndio linalohusika na machukizo yote ya nchi yanayovuta ghadhabu yote ya Mungu juu ya nchi, kama ya kuwauwa watakatifu wa Mungu, kimwili na kiroho, kwa ibada zake za sanamu, kanisa hili limeua zaidi ya wakristo milioni 68 katika historia hiyo ni idadi kubwa sana, hata Bwana YESU  alishatabiri juu yao alisema..Yohana 16:1-3″Maneno hayo nimewaambia, msije mkachukizwa. Watawatenga na masinagogi; naam, saa yaja atakapodhania KILA MTU AWAUAYE YA KUWA ANAMTOLEA MUNGU IBADA. Na hayo watawatenda kwa sababu hawakumjua Baba wala mimi. ” 

Hiyo ndio sababu ya yule mwanamke kuonekana amelewa kwa damu za watakatifu ..Haya yote ni machukizo makuu mbele za Mungu, na yule  mpinga-kristo atakayetokea huko ndiye atakayelisimamisha lile CHUKIZO LA UHARIBIFU lililotabiriwa na nabii Daneli na BWANA wetu YESU KRISTO, ndio  maana anajulikana kama “MAMA WA MACHUKIZO YA NCHI”.

SIRI YA YULE MNYAMA.

Tukiendelea Ufunuo 17:7-18 “7 Na yule malaika akaniambia, Kwani kustaajabu? Nitakuambia siri ya mwanamke huyu, na ya mnyama huyu amchukuaye, mwenye vile vichwa saba na zile pembe kumi.

8 Yule mnyama uliyemwona alikuwako, naye hayuko, naye yu tayari kupanda kutoka kuzimu na kwenda kwenye uharibifu. Na hao wakaao juu ya nchi, wasioandikwa majina yao katika kitabu cha uzima tangu kuwekwa misingi ya ulimwengu, watastaajabu wamwonapo yule mnyama, ya kwamba alikuwako, naye hayuko, naye atakuwako.

9 Hapo ndipo penye akili zenye hekima. Vile vichwa saba ni milima saba anayokalia mwanamke huyo.

10 Navyo ni wafalme saba. Watano wamekwisha kuanguka, na mmoja yupo, na mwingine hajaja bado. Naye atakapokuja imempasa kukaa muda mchache.

11 Na yule mnyama aliyekuwako naye hayuko, yeye ndiye wa nane, naye ni mmoja wa wale saba, naye aenenda kwenye uharibifu

12 Na zile pembe kumi ulizoziona ni wafalme kumi, ambao hawajapokea ufalme bado, lakini wapokea mamlaka kama wafalme muda wa saa moja pamoja na yule mnyama.

13 Hawa wana shauri moja, nao wampa yule mnyama nguvu zao na mamlaka yao.

14 Hawa watafanya vita na Mwana-Kondoo, na Mwana Kondoo atawashinda, kwa maana Yeye ni Bwana wa Mabwana, na Mfalme wa Wafalme, na hao walio pamoja naye ndio walioitwa, na wateule, na waaminifu.

15 Kisha akaniambia, Yale maji uliyoyaona, hapo aketipo yule kahaba, ni jamaa na makutano na mataifa na lugha.

16 Na zile pembe kumi ulizoziona, na huyo mnyama, hao watamchukia yule kahaba, nao watamfanya kuwa mkiwa na uchi, watamla nyama yake, watamteketeza kabisa kwa moto.

17 Maana Mungu ametia mioyoni mwao kufanya shauri lake, na kufanya shauri moja, na kumpa yule mnyama ufalme wao hata maneno ya Mungu yatimizwe.

18 Na yule mwanamke uliyemwona, ni mji ule mkubwa, wenye ufalme juu ya wafalme wa nchi. “

Hapa pia tunaona Yohana anaonyeshwa siri ya yule mnyama ambaye ndio yule yule aliyeonyeshwa katika ile sura ya 13 ambaye ana vichwa 7 na pembe 10, isipokuwa hapa zile pembe 10 zinaonanekana hazina vilemba ikiwa na maana hazijapokea ufalme bado, na ndio maana tukisoma mstari wa 12 inasema watakuja kupokea ufalme(yaani kuvikwa vilemba) saa moja na yule mnyama.

Kumbuka vile vichwa saba vya mnyama, ni FALME 7, ambazo shetani alizikalia kuutesa au kutaka kuungamiza kabisa uzao wa Mungu, ambazo ni 1) MISRI   2)ASHURU  3)BABELI   4)UMEDI & UAJEMI  5) UYUNANI   6)  RUMI-ya-KIPAGANI   7) RUMI-ya KIPAPA…

kwa maelezo marefu juu ya huyu mnyama kama anavyoonekana kwenye sura 13 fungua hapa >> UFUNUO: Mlango wa 13

Lakini tunaona hapo wakati Yohana anaonyeshwa maono hayo aliona watano wameshakwisha anguka, na mmoja yupo na mwingine hajaja bado. Kumbuka wakati ule Yohana anapewa haya maono  AD 90 ,utawala uliokuwa unaitawala dunia wakati ule  ni RUMI ya kipagani, kwahiyo zile tawala tano za kwanza zilikuwa  zimeshapita yaani Misri, Ashuru, Babeli, Umedi&uajemi pamoja na Uyunani. Hivyo ule wa Urumi ndio uliokuwepo na ndio ule uliomsulibisha KRISTO.

Na kama alivyoambiwa mmoja bado hajaja(ambaye ni wa 7), Na kwamba atakapokuja itampasa akae muda mchache, sasa  huo  si mwingine bali ni ule utawala wa RUMI ya kidini chini ya upapa ulioongoza dunia nzima kuanzia kile kipindi cha karne ya 4, ni ule ule tu wa RUMI sema hapa umegeuka ukawa wa kidini chini ya upapa.

Tukiendelea kusoma mstari wa 11 inasema..” Na yule mnyama aliyekuwako naye hayuko, yeye ndiye wa nane, naye ni mmoja wa wale saba, naye aenenda kwenye uharibifu.”.Hivyo tunaona mnyama mwingine wa 8 anajitokeza hapo, lakini biblia inasema huyu wa 8 ndio yule yule wa 7, hii ikiwa na maana kuwa ni kile kile kichwa cha saba isipokuwa kimebadilisha taswira, kwasababu yule mnyama tayari anavyo vichwa saba hawezi akawa tena na vichwa nane,

Na huyu mnyama wa 8 biblia inasema ambaye alikuwako naye hayupo naye anaenda kwenye uharibifu, tukirudi kwenye historia tunamwona  huyu mnyama (ambaye ndio kile kichwa cha 7 -Rumi ya kidini chini ya Upapa wa Kanisa Katoliki) ulikuwa na nguvu kipindi kile cha utawala wake, lakini baadaye ulikuja kutiwa jeraha la mauti na wale wanamatengezo, hivyo nguvu zake za kutawala dunia nzima zilikufa, lakini tunaona lile jeraha lilianza kupona tena, kuanzia kile kipindi cha vita vya pili vya dunia mpaka leo linaendelea kupona, utakapofika wakati atakaporejeshewa nguvu zake tena alizopoteza ndipo atakapoingia katika UHARIBIFU, naye ataitawala dunia kwa kipindi kifupi cha miaka mitatu na nusu ndio kile kipindi cha dhiki kuu, ndio maana biblia inasema alikuwepo naye hayupo, naye anajiandaa kwenda kwenye uharibifu. Kwasababu hapo mwanzo alishawahi kutawala na atakuja kutawala tena.

Sasa Zile pembe 10 za yule mnyama ambayo ni yale mataifa 10 ya ULAYA(EU), Biblia inasema  yatakuja kupata nguvu wakati mmoja na yule mnyama. Na haya ndiyo mpinga-kristo PAPA atakayoyatumia kuwatesa wale ambao hawataipokea chapa ya mnyama katika kile kipindi cha dhiki kuu.

Lakini mstari 16 tunaona jambo lingine..” Na zile pembe kumi ulizoziona, na huyo mnyama, hao watamchukia yule kahaba, nao watamfanya kuwa mkiwa na uchi, watamla nyama yake, watamteketeza kabisa kwa moto.” 

Mwisho wa yote baada ya dhiki kuu kukaribia kuisha yale mataifa 10 ya Ulaya yatagundua kuwa utawala wa mpinga-kristo(PAPA) Chini ya kanisa katoliki hauna manufaa yoyote wala haujasaidia chochote kutimiza matakwa yao, na suluhu zao za AMANI, sasa kwa pamoja yatamchukia yule mwanamke(yaani PAPA) na Makao yake VATICAN  na kumwangamiza kabisa, hiyo ndio HUKUMU ya YULE KAHABA MKUU kama mstari wa kwanza unavyosema.

” Akaja mmoja wa wale malaika saba, wenye vile vitasa saba, akanena nami, akisema, Njoo huku, nitakuonyesha hukumu ya yule kahaba mkuu aketiye juu ya maji mengi;”

Huo utakuwa ndio mwisho wa Utawala wa Upapa na Kanisa Katoliki, kwasababu makao makuu yake VATICAN yatakuwa yameshateketezwa, hukumu hii imeelezewa kwa urefu kwenye SURA YA 18, jinsi Babeli ulivyoanguka na kuwa ukiwa mfano wa ile Babeli ya kwanza ilivyokuwa.

Baada ya huyu mwanamke Babeli mkuu kuhukumiwa, sasa mstari wa 14 unasema. zile pembe 10 (yaani yale mataifa ya ulaya)” ndio yatafanya vita na Mwana-Kondoo, na Mwana Kondoo atawashinda, kwa maana Yeye ni Bwana wa Mabwana, na Mfalme wa Wafalme, na hao walio pamoja naye ndio walioitwa, na wateule, na waaminifu.” Kumbuka hii itakuwa ndio ile vita ya MUNGU MWENYEZI yaani “HARMAGEDONI”  inayozungumziwa kwenye ufunuo 16:16.

Ufunuo 18:1-5″

1 Baada ya hayo naliona malaika mwingine, akishuka kutoka mbinguni, mwenye mamlaka kuu; na nchi ikaangazwa kwa utukufu wake.

2 Akalia kwa sauti kuu, akisema, Umeanguka, umeanguka Babeli ule mkuu; umekuwa maskani ya mashetani, na ngome ya kila roho mchafu, na ngome ya kila ndege mchafu mwenye kuchukiza;

3 kwa kuwa mataifa yote wamekunywa mvinyo ya ghadhabu ya uasherati wake, na wafalme wa nchi wamezini naye, na wafanya biashara wa nchi wamepata mali kwa nguvu za kiburi chake.

4 Kisha nikasikia sauti nyingine kutoka mbinguni, ikisema, TOKENI KWAKE, ENYI WATU WANGU, MSISHIRIKI DHAMBI ZAKE, WALA MSIPOKEE MAPIGO YAKE.

5 Kwa maana dhambi zake zimefika hata mbinguni, na Mungu amekumbuka maovu yake.”

Hivyo ndugu unaona ni HATARI! gani  iliyo mbele yetu?, ni wazi kabisa muda umeshaisha Yule mnyama siku yoyote anaingia katika uharibifu, kumbuka wakati huo kanisa ambaye ni BIBI-ARUSI safi atakuwa ameshanyakuliwa, bibi-arusi asiyeabudu sanamu, bibi-arusi aliyebikira kwa NENO tu na sio pamoja na mapokeo mengine yaliyo nje na NENO LA MUNGU Kama kusali Rosari na ibada za wafu. Bibi-arusi Anayemwabudu Mungu katika Roho na kweli  sio katika mifumo ya ki-DINI  na ya-kimadhehebu, Bibi-arusi aliyepokea kweli ubatizo wa Roho Mtakatifu, na kama tunavyofahamu asili ya bibi-arusi ni kuvaa vazi refu la kujisitiri, je! na wewe mwanamke mavazi yako ni ya kujisitiri?, Utakuwa mkristo na bado uwe  kahaba kwa mavazi unayovaa? kumbuka fashion zote ni dhambi! lipstic,vimini, wigy,suruali, wanja nk. vitakupeleka kuzimu mwanamke.

BWANA YESU ANASEMA…

12 Tazama, naja upesi, na ujira wangu u pamoja nami, kumlipa kila mtu kama kazi yake ilivyo.

13 Mimi ni Alfa na Omega, mwanzo na mwisho, wa kwanza na wa mwisho.

14 Heri wazifuao nguo zao, wawe na amri kuuendea huo mti wa uzima, na kuingia mjini kwa milango yake.

15 Huko nje wako mbwa, na wachawi, na wazinzi, na wauaji, NA HAO WAABUDUO SANAMU, na kila mtu apendaye uongo na kuufanya.

16 Mimi Yesu nimemtuma malaika wangu kuwashuhudia ninyi mambo hayo katika makanisa. Mimi ndimi niliye Shina na Mzao wa Daudi, ile nyota yenye kung’aa ya asubuhi.

17 NA ROHO NA BIBI-ARUSI WASEMA, NJOO!  Naye asikiaye na aseme, Njoo! Naye mwenye kiu na aje; na yeye atakaye, na ayatwae maji ya uzima bure.

TUBU ANGALI MUDA UPO.

Mungu akubariki. Kwa mwendelezo >>UFUNUO: Mlango wa 18

Ikiwa utapenda tuwe tunakutumia mafundisho ya Neno la Mungu ya mara kwa mara,  kwa njia ya whatsapp basi tutumie ujumbe kwenye namba hii +255789001312. Na kama utapenda kwa njia ya E-mail basi tuandikie email yako katika boksi la maoni chini.


Mada zinazoendana…


MNARA WA BABELI

CHAPA YA MNYAMA

SIRI YA KUASI KATIKA KANISA LA MUNGU.

ROHO YA MPINGA KRISTO IKITENDA KAZI SIKU HIZI ZA MWISHO

NILIMWONA SHETANI, AKIANGUKA KUTOKA MBINGUNI.

UFUNUO: Mlango wa 18


Rudi Nyumbani

Print this post

About the author

Admin administrator

Subscribe
Notify of
guest
3 Comments
Newest
Oldest Most Voted
Inline Feedbacks
View all comments
Ntahondi Salvatory
Ntahondi Salvatory
3 years ago

Mungu akubariki. Naomba kuuliza, “umesema utawala wa kipapa wa kidini umeanza karne4 na kutiwa jeraha la mauti kipindi cha wanamatengenezo, ukatawala wake ukawa haupo, Sasa kwa muda mtawala ni yupi? Maana bado hajaja bado.

long'ida mollel
long'ida mollel
3 years ago

Tupe ishara/ vitu vinavyoonyesha kuwa kanisa katoliki wanakosea