TUKAZE MWENDO KWA TULIYOANDALIWA.

by Admin | 2 January 2019 08:46 am01

Luka 10:22 “Akasema, NIMEKABIDHIWA VYOTE NA BABA YANGU, wala hakuna amjuaye Mwana ila Baba; wala hakuna amjuaye Baba ila Mwana, na ye yote ambaye Mwana apenda kumfunulia.”


Yohana 13:3 “Yesu, hali akijua ya kuwa Baba amempa vyote mikononi mwake, na ya kuwa alitoka kwa Mungu naye anakwenda kwa Mungu”


Ufunuo wa Yohana 5 : 1-14 

1 Kisha nikaona katika mkono wa kuume wake yeye aliyeketi juu ya kile kiti cha enzi kitabu kilichoandikwa ndani na nyuma, kimetiwa muhuri saba. 

2 Nikaona malaika mwenye nguvu akihubiri kwa sauti kuu, N’nani astahiliye kukifungua kitabu, na kuzivunja muhuri zake? 

3 Wala hapakuwa na mtu mbinguni, wala juu ya nchi, wala chini ya nchi, aliyeweza kukifungua hicho kitabu, wala kukitazama. 

4 Nami nikalia sana kwa kuwa hapakuonekana mtu astahiliye kukifungua hicho kitabu, wala kukitazama. 

5 Na mmojawapo wa wale wazee akaniambia, Usilie; tazama, Simba aliye wa kabila ya Yuda, Shina la Daudi, yeye ameshinda apate kukifungua kile kitabu, na zile muhuri zake saba. 

6 Nikaona katikati ya kile kiti cha enzi na wale wenye uhai wanne, na katikati ya wale wazee, Mwana-Kondoo amesimama, alikuwa kana kwamba amechinjwa, mwenye pembe saba na macho saba, ambazo ni Roho saba za Mungu zilizotumwa katika dunia yote. 

7 Akaja, akakitwaa kile kitabu katika mkono wa kuume wake yeye aliyeketi juu ya kile kiti cha enzi. 

8 Hata alipokitwaa kile kitabu, hao wenye uhai wanne na wale wazee ishirini na wanne wakaanguka mbele za Mwana-Kondoo, kila mmoja wao ana kinubi, na vitasa vya dhahabu vilivyojaa manukato, ambayo ni maombi ya watakatifu. 

9 Nao waimba wimbo mpya wakisema, Wastahili wewe kukitwaa hicho kitabu na kuzifungua muhuri zake; kwa kuwa ulichinjwa, ukamnunulia Mungu kwa damu yako watu wa kila kabila na lugha na jamaa na taifa, 

10 ukawafanya kuwa ufalme na makuhani kwa Mungu wetu; nao wanamiliki juu ya nchi. 

11 Nikaona nikasikia sauti ya malaika wengi pande zote za kile kiti cha enzi, na za wale wenye uhai, na za wale wazee, na hesabu yao ilikuwa elfu kumi mara elfu kumi na elfu mara elfu, 

12 wakisema kwa sauti kuu, Astahili Mwana-Kondoo aliyechinjwa, kuupokea uweza na utajiri na hekima na nguvu na heshima na utukufu na baraka.”

Shalom! Umewahi kujiuliza wafu leo wapo wapi?, je! mtu akifa leo katika dhambi au katika haki anakwenda wapi?…Ni wazi kuwa mtu akifa katika haki, roho yake inakwenda mahali panapojulikana kama Paradiso au peponi, ni mahali pa zuri na pa raha, ambapo roho ya mtu huyo itapumzishwa huko kwa kitambo kidogo pamoja na wenzake wa imani moja naye ambao nao walikufa katika haki..Huko wanakusanyika pamoja, mpaka siku Kristo atakapokuja mawinguni ambapo wataamshwa(au kufufuliwa) na kuvaa miili ya utukufu, na kisha kwenda mbinguni kwa Baba.


Kumbuka mbinguni Bwana Yesu alipo hakuna mtu aliyefika sasa, ni mahali pa zuri ambapo hapana mfano huko hata Eliya hayupo, wala Musa, wala Henoko, wala Ibrahimu, huko ni sehemu mpya kabisa ambayo jicho halijawahi kuona wala sikio kusikia mambo yaliyopo kule…Eliya na Henoko ambao hawakuonja mauti hawakupelekwa huko mbinguni Bwana aliko sasa,bali walipelekwa Paradiso.


Yohana 3: 13 WALA HAKUNA MTU ALIYEPAA MBINGUNI, ila yeye aliyeshuka kutoka mbinguni, yaani, Mwana wa Adamu”.


Bwana Yesu alisema “Nyumbani mwa Baba yangu mna makao mengi; kama sivyo, ningaliwaambia; maana naenda kuwaandalia mahali. Basi mimi nikienda na kuwaandalia mahali, nitakuja tena niwakaribishe kwangu; ili nilipo mimi, nanyi mwepo. Yohana (14:2-3)


Umeona Bwana anasema anakweda kutuandalia makao, ikiwa na maana kuwa, ni mahali kupya kabisa panapokwenda kuandaliwa…na akishamaliza atatukaribisha kwake, ili alipo nasi tuwepo.


Kwahiyo kwa muhtasari huo unaweza ukaona kwamba Kristo Yesu pekee ndiye aliyeko mbinguni sasa, akituandalia sisi makao, na Makao hayo si mengine zaidi ya nafasi zetu sisi tutakazukuwa nazo kule, pamoja na miili yetu ya utukufu tutakayoivaa siku atakayokuja kutuchukua.


Sasa unaweza ukauliza mbona kuna watu wengi wanasema wamepelekwa mbinguni wakaona hiki na kile?..Jibu rahisi ya swali hilo ni kwamba hawakupelekwa mbinguni bali walionyeshwa maono ya mbinguni..Na kumbuka maono ni lugha ya picha…Mtu anaweza akapewa maono ya mbinguni, katika maono yale akaona barabara za dhahabu, akaona na milima na mabonde mazuri, akaona na maua mazuri na chemchemi nzuri, lakini mtu huyo hajapelekwa mbinguni…bali amepewa tu maono ya mahali ambapo pangeweza pakafananishwa na Mbinguni…Ni sawa leo, mtu aoneshwe clip ya Taifa la Urusi akiwa hapa Tanzania, je! mtu huyo atakuwa amefika Urusi? Ni dhahiri kuwa bado hajafika, ni kaonyeshwa tu kipande cha video ya Urusi, Ndivyo ilivyo kwa watu wengi wanaopewa maono ya Mbinguni, wanakuwa tu wanapewa vipengele vidogo vidogo vya jinsi mbingu ilivyo uzuri wake kwa lugha ya kibinadamu. Lakini kiuhalisia kabisa ni mambo ambayo hayatamkiki kibinadamu.


mbinguni Bwana Yesu alipo hakuna mtu yoyote anayejua yanayoendelea huko..Ni siri, mpaka siku Kanisa litakaponyakuliwa ndipo watakatifu watakapoenda kuona mambo mazuri na mapya walioandaliwa. Ni mambo ambayo jicho halijawahi kuona wala sikio kusikia.


Biblia inasema..

Waebrania 11: 36 “wengine walijaribiwa kwa dhihaka na mapigo, naam, kwa mafungo, na kwa kutiwa gerezani;  

37 walipigwa kwa mawe, walikatwa kwa misumeno, walijaribiwa, waliuawa kwa upanga; walizunguka-zunguka wakivaa ngozi za kondoo na ngozi za mbuzi; walikuwa wahitaji, wakiteswa, wakitendwa mabaya;  

38 (watu ambao ulimwengu haukustahili kuwa nao), walikuwa wakizunguka-zunguka katika nyika na katika milima na katika mapango na katika mashimo ya nchi.  

39 Na watu hao wote wakiisha kushuhudiwa kwa sababu ya imani yao, hawakuipokea ahadi;  

40 kwa kuwa Mungu alikuwa ametangulia kutuwekea sisi kitu kilicho bora, ILI WAO WASIKAMILISHWE PASIPO SISI.


Unaona hapo, watakatifu wote waliotutangulia, ukisoma Waebrania 11&12 yote utaona wingu kubwa la mashahidi linazungumziwa pale, utaona akina Ibrahimu, Henoko, Musa, Gideoni, n.k. fahamu tu wote hao mpaka sasa hawajaipokea ile ahadi walioahidiwa kwasababu yetu sisi, na ndio maana hapo biblia inasema ILI WAO WASIKAMILISHWE PASIPO SISI. Hii ikiwa na maana wingu hilo la mashahidi waaminifu wa Kristo waliojitoa maisha yao kikamilifu kwa ajili ya Bwana wote bado hawajakamilishwa wote wapo mahali wamehifadhiwa wakitusubiria sisi nasi tukamilishe ili kwa pamoja siku ile ya Bwana wote tuende mbinguni YESU wetu alipo kwenye makao aliyokwenda kutuandalia.


Ni raha iliyoje tukifahamu hilo. Hivyo mimi na wewe tukazane tufike sehemu hiyo, ambayo imeandaliwa kwa ajili yetu. Kwasababu itakuwa ni majuto makubwa sana na vilio kwa wale ambao watakosa unyakuo,.Wakati huo ukifiria wenzako wapo mbinguni wanang’aa kama jua na wewe unasubiria ziwa la moto, itakuwa ni majuto kiasi gani, kibaya zaidi ukijua kabisa ulikuwa na muda wa kutubu lakini uliupuuzia..Fanya uamuzi leo, yatengeneze maisha yako upya tena, naye Bwana atakurehemu.


Ubarikiwe sana.

Pia unaweza ukapata mafundisho haya Kwa njia ya Whatsapp yako, jiunge na channel yetu Kwa kubofya hapa >> WHATSAPP

DOWNLOAD PDF
WhatsApp

Source URL: https://wingulamashahidi.org/2019/01/02/tukaze-mwendo-kwa-tuliyoandaliwa/