Nini maana ya mstari huu: (Mtu ambarikiye mwenzake kwa sauti kuu asubuhi na mapema; Itahesabiwa kuwa ni laana kwake.Mithali 27:14 )?

by Admin | 2 September 2019 08:46 pm09

SWALI: Maana unanipa utata je! Ni kwamba Nisiwabariki watu asubuhi?.


JIBU: Kumbuka Neno kubariki katika biblia ni Neno pana, licha tu ya kuwa na maana ya kutoa Baraka kwa mtu lakini pia linaweza kumaanisha kushukuru, kutukuza, kusifia, kusujudia, au kuhimidi..inategemea na mahali lilipotumika.   Kwamfano mstari kama huu

Zaburi 96:2 “Mwimbieni Bwana, libarikini jina lake, Tangazeni wokovu wake siku kwa siku”

Haimaanishi tu tulibariki (kwa kulitakia mema jina lake), hapana bali pia linamaanisha litukuzeni, lihimidini jina lake takatifu.   Sasa tukirudi kwenye huo mstari hapo juu, Tunaweza kuona kuna mambo mawili ambayo yamesababisha Baraka za huyu mtu zibadilishwa na kuwa laana. Jambo la kwanza ni kitendo cha yeye kumbariki mwenzake kwa SAUTI KUU. Na jambo la pili ni kufanya hilo tukio ASUBUHI NA MAPEMA.

  Mpaka mtu amsifie mwenzake kwa sauti kuu, kumbuka sio sauti tu ya kawaida hapana bali kwa sauti KUU ni wazi kuwa mtu huyo lengo lake ni asikiwe au aonekane na watu kitu anachokifanya na siku zote sifa za namna hiyo huwa zinakuwa si za kweli bali ni za kinafki. Na ndio hapo zinageuzwa na kuwa laana, mfano wake ndio ule Bwana Yesu alioutoa katika..  

Mathayo 6:5 “Tena msalipo, msiwe kama wanafiki; kwa maana wao wapenda kusali hali wamesimama katika masinagogi na katika pembe za njia, ili waonekane na watu. Amin, nawaambia, Wamekwisha kupata thawabu yao.6 Bali wewe usalipo, ingia katika chumba chako cha ndani, na ukiisha kufunga mlango wako, usali mbele za Baba yako aliye sirini; na Baba yako aonaye sirini atakujazi.”

Unaona mtu huyu, kama angekuwa na nia kweli ya kubariki angemwombea yeye mwenyewe kwa siri au kwenda kuzungumza naye kawaida tu, na sio mpaka apige panda mbele.  

Pili kitendo cha mtu huyu kufanya hivyo asubuhi na mpema katika roho kuna maana kubwa sana. Sikuzote asubuhi na mapema ni wakati mtulivu ndio mwanzo wa siku, ambao mtu analazima kukatiza usingizi wake kwa ajili ya mambo ya muhimu sana. Na jambo la kwanza kabisa mtu akiamka asubuhi anachopaswa kufanya ni Kumbariki Mungu wake (kwa kumshukuru, kumwimbia na kumsifu). Ndege wakiamka asubuhi jambo la kwanza wanalolifanya ni kumsifu Mungu kwa sauti kuu ya shangwe, utawasikia kila mahali kwenye viota vyao kabla hata hawajaenda popote huko ndani wanamsifu Mungu.   Daudi aliamka ALFAJIRI na kumbariki Mungu kwa vinanda na vinubi kwa sauti Kuu sana.  

Zaburi 57:7 “Ee Mungu, moyo wangu u thabiti, Moyo wangu u thabiti. Nitaimba, nitaimba zaburi, 8 Amka, utukufu wangu. Amka, kinanda na kinubi, NITAAMKA ALFAJIRI. 9 Ee Bwana, nitakushukuru kati ya watu, Nitakuimbia zaburi kati ya mataifa. 10 Maana fadhili zako ni kubwa hata mbinguni, Na uaminifu wako hata mawinguni. 11 Ee Mungu, utukuzwe juu ya mbingu, Na juu ya nchi yote uwe utukufu wako”.  

Halikadhalika Mungu aliwaamsha Manabii wake, asubuhi na mapema wawpeleke habari njema za wokovu kwa watu wake(Yeremia 44:4)

Unaona Alfajiri siku zote ni ya Mungu..Ukiamka na Bwana, basi siku yako yote itakuwa ni ya Baraka.   Lakini huyu anaamka asubuhi na mpema jambo la kwanza ni kumpa mwanadamu utukufu, tena kwa sauti kubwa kana kwamba yeye ndio aliyemfanya aamke asubuhi. Hivyo mbele za Mungu kwake inakuwa ni laana. Mambo kama hayo yanajirudia hata sasa hivi ikiwa utamka asubuhi jambo la kwanza ni kukimbila SMARTPHONE yako uangalie message zote jana zilizotumwa whatsapp na facebook. Jambo la kwanza ni kuchati na kupiga simu za biashara zako, jambo la kwanza ni kuamka na kuwatukuza wanadamu badala ya muumba wake, Jambo la kwanza ni kuongea na mpenzi wako ambaye hata si mke wako/mume wako.Basi fahamu kuwa hata siku yako nzima umeiharibu mwenyewe.

Mika 1: 1 “Ole wao wakusudiao mambo maovu, na kutenda mabaya vitandani mwao! Kunapopambazuka asubuhi huyafanya, kwa sababu ya katika uwezo wa mikono yao”.  

Isaya 5:11 “Ole wao waamkao asubuhi na mapema, wapate kufuata kileo; wakishinda sana hata usiku wa manane mpaka mvinyo imewaka kama moto ndani yao!”.

Hivyo Ujumbe mkuu hapo tuopaswa kuufahamu ni kuwa kitendo cha kusumbukia kitu kingine asubuhi na mapema tena kwa sauti kubwa kabisa, basi hicho kitu ni wazi kabisa kimekuwa ni KINGA yako, na biblia imeweka wazi kuwa amelaaniwa mtu Yule amfanyaye mwanadamu kuwa kinga yake. (Yeremia 17:5).   Alfajiri ikiwa ni ya Bwana, basi yaliyosalia nayo yatabarikiwa.

Warumi 11:16 “Tena malimbuko yakiwa matakatifu, kadhalika na donge lote; na shina likiwa takatifu, matawi nayo kadhalika”

Ubarikiwe.

DOWNLOAD PDF
WhatsApp

Source URL: https://wingulamashahidi.org/2019/09/02/nini-maana-ya-mstari-huu-mtu-ambarikiye-mwenzake-kwa-sauti-kuu-asubuhi-na-mapema-itahesabiwa-kuwa-ni-laana-kwake-mithali-2714/