by Admin | 6 July 2021 08:46 am07

UNYAKUO.

Unyakuo ni kitendo ambacho Bwana Yesu atawahamisha watakatifu wake, kutoka katika huu ulimwengu na kuwapeleka mbinguni yeye alipo. Kwa mujibu wa biblia Tendo hilo litakuwa ni la ghafla sana, kama vile mtu anafumba macho na kufungua.

Siku hiyo paraparanda ya Mungu italia, ulimwenguni kote, lakini haitasikiwa na watu wote, bali wale watu waliomwamini Yesu hapa duniani, na wale watakatifu waliokufa katika yeye.

1Wakorintho 15:51 “Angalieni, nawaambia ninyi siri; hatutalala sote, lakini sote tutabadilika,

52 kwa dakika moja, kufumba na kufumbua, wakati wa parapanda ya mwisho; maana parapanda italia, na wafu watafufuliwa, wasiwe na uharibifu, nasi tutabadilika”.

Unaona? Siku hiyo, itakuwa ya kipekee sana, Bwana Yesu aliendelea kusema..

Mathayo 24:40 “Wakati ule watu wawili watakuwako kondeni; mmoja atwaliwa, mmoja aachwa;

41 wanawake wawili watakuwa wakisaga; mmoja atwaliwa, mmoja aachwa.

42 Kesheni basi; kwa maana hamjui ni siku ipi atakayokuja Bwana wenu”.

Sasa kulingana na majira tuliyopo sasa, dalili zote zinaonyesha Yesu yupo karibu sana kurudi, hatujui pengine ni leo usiku, au kesho au mwezi ujao, lakini kulingana na tabiri zote za kimaandiko, inatuonyesha kuwa siku yoyote Kristo anarudi. Haleluya.

Na kama ikitokea amerudi leo, wewe uliyempokea Yesu, Utaisikia paraparanda hiyo ya Mungu, ikilia. Na ghafla utayaona makaburi ya watakatifu yanafunguka, na wao wakitoka makaburini (Mathayo 27:51-53), kisha baada ya hapo mtakuwa kitu kimoja, na kwa pamoja, mtanyakuliwa mawinguni kumlaki Bwana Yesu ,.

Tendo hilo litakuwa ni la kufumba na kufumbua, na moja kwa moja mtaelekea mbinguni, kule ambapo Yesu alisema amekwenda kutuandalia makao (Yohana 14:1-3). Huko tutakutana na mambo ambayo jicho halijawahi kuona wala sikio kusikia, kutakuwa na furaha isiyo na kifani, tutakapoingia katika hiyo karamu ya mwanakondoo. Ni mahali ambapo hata mmoja wetu hapaswi kukosa.

Ufu 19:9 “Naye akaniambia, Andika, Heri walioalikwa karamu ya arusi ya Mwana-Kondoo. Akaniambia, Maneno haya ni maneno ya kweli ya Mungu”.

Lakini ikiwa wewe hujaokoka, parapanda hiyo ikilia, siku hiyo hutafahamu au kusikia chochote, kinyume chake, utashangaa tu, fulani ambaye aliyempokea Yesu ulikuwa naye sekunde chache tu nyuma, ametoweka, uliyekuwa  unalima naye shambani humuoni, mume/mke uliyekuwa umelala naye ameondoka na milango imefungwa. Hapo ndipo utakapojua Kristo amesharudi na kulinyakua kanisa lake.

Vilevile ikiwa utakufa leo katika hali ya dhambi na bado Bwana hajarudi. Siku ya unyakuo ikifika, hautafufuliwa badala yake utaendelea kubaki hapo makaburini mpaka siku ya hukumu ya mwisho ambayo utafufuliwa na kuhukumiwa kisha kutupwa katika lile ziwa la moto (Ufu 20:11-15).

Ndugu yangu, Ipo sababu kwanini leo umekutana na ujumbe huu, wakati tunaoishi ni wakati wa nyongeza tu, Yesu hajarudi bado ni kusudi kwamba wewe ambaye hujampokea, umpokee sasa, vinginevyo angekuwa amesharudi siku nyingi sana. Anakusubiria wewe ambaye pengine ni mmoja wa wale kondoo wa mwisho mwisho, utubu dhambi zako uokoke.

Hataki hata mmoja wetu aikose hiyo karamu aliyokwenda kutuandalia mbinguni kwa miaka 2000 sasa. Haijalishi wewe ni dini gani au dhehebu gani, Yesu anawapokea watu wote, anawapa tumaini jipya, kisha anawaandaa kwa ajili ya kuwakaribisha nyumbani kwake mbinguni.

Hivyo tubu leo, kisha uwe tayari kubatizwa kwa ajili ya kuukamilisha wokovu wako, Na baada ya hapo yeye mwenyewe atakupa kipawa cha Roho wake Mtakatifu. Hivyo kama utahitaji msaada wa kuokoka/kubatizwa, basi wasiliana nasi kwa namba hizo mwishoni mwa kipeperushi hichi, au tafuta kanisa la kiroho lililo hai, wakusaidie.

Bwana akubariki.

DOWNLOAD PDF
WhatsApp

Source URL: https://wingulamashahidi.org/2021/07/06/16273/