Title December 2021

Kutia mkono chini ya paja kama ishara ya kiapo, kulimaanisha nini?

Tofauti na desturi za mataifa mengi ya sasa zilivyo, kwamba mtu akitaka kuapa, huwa anashika kitabu Fulani cha dini kama vile biblia, au anaweka mkono wako kifuani ndipo anatamka kiapo chake..Zamani kulingana na desturi wa wayahudi ilikuwa ni mtu anaweka mkono wake, chini ya paja la anayemwapisha.

Pajani kibiblia ni sehemu ambayo ipo karibu sana na viungo vya uzazi.. Sehemu nyeti, ambapo hapawezi kufikiwa kama jambo lililopangwa halihitaji umakini sana. Ni sawa na leo watu wanavyotumia biblia mahakamani kuapa, ni kitabu nyeti sana, kiasi kwamba mpaka kimetumiwa hiko ni kuonyesha umakini wa kile unachotakiwa kukifanya.

Na ndivyo ilivyokuwa kwa Ibrahimu, na Yakobo. Kwamfano Ibrahimu alipotaka mwanawe Isaka apatiwe mke kutoka katika nyumba ya Ndugu yake, aliyekuwa mbali sana, alimwita mtumwa wake, akamwapisha kwamba akamletee binti sawasawa na alivyomwagiza, Hivyo ili kuthibitisha kuwa mtumwa wake atayatekeleza yale aliyoagizwa, akachukua mkono wake, na kuulia katika paja lake, kuonyesha pia kwamba yupo tayari kutii kila agizo lililoamriwa juu yake.

Mwanzo 24:2 “Ibrahimu akamwambia mtumishi wake, mzee wa nyumba yake, aliyetawala vitu vyake vyote, Tafadhali uutie mkono wako chini ya paja langu, 3 nami nitakuapisha kwa Bwana, Mungu wa mbingu, na Mungu wa nchi, kwamba hutamtwalia mwanangu mke katika binti za Wakanaani ambao nakaa kati yao;”…

9 Yule mtumishi akaweka mkono wake chini ya paja la Ibrahimu bwana wake, akamwapia katika neno hilo. 10 Kisha huyo mtumishi akatwaa ngamia kumi katika ngamia za bwana wake akaenda zake, maana mali zote za bwana wake zilikuwa mkononi mwake, akaondoka, akaja mpaka Mesopotamia, mpaka mji wa Nahori.

Jambo kama hilo tunaliona pia kwa Yakobo, siku ile alipokaribia kufa, alimwita Yusufu na kumwambia, aweke mkono wake chini ya paja lake, ali amwapie, kwamba hatamzika kule Misri bali, katika nchi ya Baba yake.

Mwanzo 47:29 “Siku za kufa kwake Israeli zikakaribia; akamwita mwanawe Yusufu, akamwambia, Kama nimeona kibali machoni pako, weka mkono wako chini ya paja langu, ukanifanyie rehema na kweli; nakusihi usinizike katika Misri.

30 Lakini nitakapolala pamoja na baba zangu, unichukue toka Misri, unizike katika kaburi lao. Akasema, Nitafanya kama ulivyosema.

31 Akanena, Niapie. Naye akamwapia. Israeli akajiinamisha kwenye mchago wa kitanda”.

Lakini sisi katika agano jipya, hatujapewa ruhusa ya kuapa bali Bwana Yesu alisema, maneno yetu yawe Ndio, ndio.. Au Sio,..sio..Na si zaidi. (Mathayo 5:33-37). Hakuna sababu ya kuapa, kwasababu hatuna mamlaka ya kutangua au kuthibitisha chochote katika maisha yetu kana kwamba vipo chini ya uwezo wetu.
Sisi si Mungu.

Bwana akubariki.

Tafadhali washirikishe na wengine habari hizi njema,

Kwa maombezi/Ratiba za ibada/ Ushauri/ Maswali.
Piga namba hizi: +255693036618 au +255789001312

pia kama utapenda uyapate mafundisho haya kwa njia ya Whatsapp au email basi tutumie ujumbe kwenye namba hizo hizo.

Mada Nyinginezo:

Naomba kujua nini maana ya kuteguka uvungu wa paja?

Je Bwana Yesu alikuwa na mchoro (tattoo) katika paja lake? (Ufunuo 19:16).

JE! NI KWELI UMEMFUATA YESU?

Kwanini Yesu aliwakataza mitume wake kumdhihirisha?

Rudi nyumbani

Print this post