NITAJUAJE KUWA NIMEITWA ILI KUMTUMIKIA MUNGU?

by Admin | 3 August 2022 08:46 am08

SWALI: Bwana Yesu asifiwe, naomba kufahamu nitajuaje kama nimeitwa ili kumtumikia Mungu, ni viashiria gani vitanitambulisha?


JIBU: Shalom, Jina la Bwana wetu Yesu Kristo libarikiwe milele na milele.
Ni vizuri kufahamu kama vile ilivyokuwa ni mapenzi ya Mungu, watu wote waokolewe na kufikiwa na injili, sawasawa na;

1Timotheo 2:3 “Hili ni zuri, nalo lakubalika mbele za Mungu Mwokozi wetu;
4 ambaye hutaka watu wote waokolewe, na kupata kujua yaliyo kweli”.

Vivyo hivyo ni mapenzi ya Mungu watu wote wawe watumishi wake,wasimame kwa ajili ya kazi yake hapa duniani, tunalithibitisha hilo katika maneno ya Bwana Yesu mwenyewe alisema..

Marko 8:34 “Akawaita mkutano pamoja na wanafunzi wake, akawaambia, MTU YEYOTE, akitaka kunifuata na ajikane mwenyewe, ajitwike na msalaba wake, anifuate”.

Anasema mtu yeyote, akitaka kumfuata,…Kumfuata kuwa nani? Ni kumfuata kuwa mwanafunzi wake..Ni sharti ajikane mwenyewe maisha yake na kujitwika msalaba wake kila siku na kumfuata yeye.
Kumbuka si kila mtu anaweza kuwa mwanafunzi wa Yesu, Kipindi kile kulikuwa na makutano yaliyohitaji wokovu tu, na pia kulikuwa na wanafunzi wake, ambao ndio wale mitume wake, na wale wengine sabini, pamoja na lile kundi la wanawake wacha Mungu lililokuwa linaongozana naye..


Sasa hao wanafunzi wake ndio waliokuja kuwa watumishi wake, katika nyanja mbalimbali..
Hivyo, kilichoweza kuwatofautisha wanafunzi(watumishi) wa Yesu na wale wengine, ni kwamba wale wanafunzi walikubali kuingia gharama zote, alizoziorodhesha Yesu, za kiutumishi, wale wengine hawakuweza, ndio ilipotokea hapo.

Luka 14:25 “Makutano mengi walipokuwa wakifuatana naye, aligeuka, akawaambia,
26 Kama mtu akija kwangu naye hamchukii baba yake, na mama yake, na mke wake, na wanawe, na ndugu zake waume na wake; naam, na hata nafsi yake mwenyewe, hawezi kuwa mwanafunzi wangu.
27 Mtu ye yote asiyeuchukua msalaba wake na kuja nyuma yangu, hawezi kuwa mwanafunzi wangu.
28 Maana ni nani katika ninyi, kama akitaka kujenga mnara, asiyeketi kwanza na kuhesabu gharama, kwamba anavyo vya kuumalizia?
29 Asije akashindwa kuumaliza baada ya kuupiga msingi, watu wote waonao wakaanza kumdhihaki,
30 wakisema, Mtu huyu alianza kujenga, akawa hana nguvu za kumaliza.
31 Au kuna mfalme gani, akitaka kwenda kupigana na mfalme mwingine, asiyeketi kwanza na kufanya shauri, kwamba yeye pamoja na watu elfu kumi ataweza kukutana na yule anayekuja juu yake na watu elfu ishirini?
32 Na kama akiona hawezi, hutuma ujumbe kutaka sharti za amani, mtu yule akali mbali.
33 Basi, kadhalika kila mmoja wenu asiyeacha vyote alivyo navyo, hawezi kuwa mwanafunzi wangu”.

Hizo ndio gharama za utumishi.. Ikiwa wewe (Au mtu yeyote) utaweza kuzifuata, basi, tayari wewe ni mtumishi wa Yesu hapa duniani, kama utakuwa tayari kuacha kila kitu kwa ajili yake, wewe ni mtumishi wake, kuacha mambo yote ya kiulimwengu, kupoteza hata kazi yako, au elimu yako, Kukubali kutengwa na ndugu na wazazi pale inapobidi lakini usimwache Yesu, wewe ni mtumishi wake.


Tofauti na wengi wanavyodhani, kwamba ili ujue wewe ni mtumishi wa Yesu, ni lazima uoteshwe kwanza ndoto, au utokewe na Yesu kama mtume Paulo, au uwekewe mikono na askofu kanisani.. Ndugu hapo bado hujafanyika mwanafunzi wa Yesu, ikiwa ndani yako bado hakuna kujikana nafsi na kupoteza kila kitu kwa ajili yake. Yuda alikuwa ni mtume wa Yesu ambaye si kutokewa naye, bali aliishi naye akala naye kwa miaka mitatu, lakini mwisho wa siku akaishia kumsaliti Bwana wake..Hiyo yote ni kwasababu hakuwa tayari kuuacha ulimwengu kwa ajili ya Kristo.


Kwa kawaida ili mtu apewe dhamana ya kuwa askari wa kulinda raia, ni lazima mafunzo yake yawe tofauti kabisa na ya raia wengine, na ndivyo ilivyo kwa Bwana Yesu..Vigezo ndio hivyo ameshavitoa.
Hivyo kwa hitimisho ni kwamba, kila mmoja ameitwa kuwa mtumishi wa Mungu, isipokuwa ni wachache ndio wanaoweza kuingia gharama zake, Lakini ingetokea dunia nzima au wakristo wote wameingia hizo gharama basi wote ni watumishi bila kujali, jinsia, rangi, umri, au vyeo vyao.
Fanyika sasa mwanafunzi wa Yesu, naye atakuweka katika utumishi wake.


Bwana akubariki.

Tafadhali shea na wengine ujumbe huu;

Pia Kwa maombezi/ Ushauri/ Maswali/ Whatsapp:
Tuandikie katika BOXI la Maoni hapo chini au
Piga namba hizi: +255693036618 au +255789001312

Mada Nyinginezo:

Bwana alimaanisha nini kusema “Mwanafunzi hawi mkuu kuliko mwalimu wake”?

INJILI YA KRISTO HAITANGAZWI KWA HATI MILIKI.

SIKU YA MAONYESHO MAKUU YA BWANA YESU, IPO KARIBU.

MAPIGO YA VITASA SABA, NA SIKU YA BWANA.

MIHURI SABA

MKUMBUKE MKE WA LUTU.

Je ni kweli ilikuwa desturi ya Bwana kuishika sabato?(Luka 4:16)

Rudi nyumbani

DOWNLOAD PDF
WhatsApp

Source URL: https://wingulamashahidi.org/2022/08/03/nitajuaje-kuwa-nimeitwa-ili-kumtumikia-mungu/