Kama ndege aendaye huko na huko mbali na kitundu chake;

by Admin | 22 March 2023 08:46 am03

SWALI: Nini maana ya huu mstari?

Mithali 27:8 “Kama ndege aendaye huko na huko mbali na kitundu chake; Ndivyo alivyo mtu aendaye huko na huko mbali na mahali pake”

JIBU: Hapa Sulemani alikuwa anajaribu kueleza jinsi tabia ya ndege inavyoweza kufananishwa na tabia ya mkristo katika maisha yake hapa duniani. Kwa kawaida ndege anapotoka katika kiota chake, huwa na lengo la aidha kutafuta chakula, au kukiendeleza kiota chake, au kujipumzisha mahali Fulani kwa muda. Hivyo huwa anaenda na kurudi, anaenda na kurudi kwa siku hata mara 10 na zaidi, anaweza kufanya hivyo.

 Lakini wakati huo huo, awapo katika mazingira ya kuzunguka huko na huko, hukutana na hatari nyingi sana. Aidha Maadui au mitego. Hivyo asipokuwa makini anaweza asirudi, kabisa nyumbani kwake.

Hivyo ndivyo alivyo mkristo, ambaye misingi yake ni “biblia na Kanisa”. Ukweli ni kwamba si kila wakati atakuwa katikati ya watakatifu, au atakuwa uweponi akimsifu Mungu na kumwimbia, au akilitafakari Neno la Mungu. Zipo nyakati atatoka kwa muda ataenda kazini, atatoka kwa muda ataenda shambani pengine kujitafutia riziki, ataenda shuleni masomoni na kama si hivyo basi kwa namna moja au nyingine atajihusisha na mambo ya kijamii, kama kutembelea jamaa, na ndugu, majirani n.k.

Sasa awapo katika mazingira haya anafananishwa na ndege atokaye katika kiota chake na kuzunguka huko na huko. Hivyo anapaswa awe na busara kwa sababu huko nje, zipo hatari nyingi sana za yeye kunaswa na adui asipokuwa makini.

Ni lazima ajiwekee mipaka, si kila biashara afanye, si kila jambo la kidunia analoletewa mbele yake ajihusishe nalo, si kila mazungumzo ayaongee. Bali muda wote awapo nje, atambue kuwa makao yake ni KANISANI awezapo kufanya ibada, na kujumuika na watakatifu wenzake. Muda wote atambue usalama  wake ni katika Neno la Mungu basi. Alale katika hilo na aamke katika hilo.

Akitafutacho huko nje ajue ni kwa lengo la kuendeleza tu kiota chake (kazi ya Mungu), na sio vinginevyo. Mtu huyo akizingatia vigezo hivyo atakuwa salama. Lakini watu wengi wamenaswa na ulimwengu. Hata Kanisani hawaonekani tena baada ya kupata kazi, Upendo wao kwa Mungu umepoa pale walipokutana na marafiki Fulani wapya, muda wa maombi wanakosa kisa wapo buzy na mihangaiko ya maisha. Kauli zao zimebadilika, kwasababu muda mwingi wamekaa na watu wenye mizaha, na matusi, hadi na wao wakajifunza lugha zao.

Biblia inatuambia,

Waefeso 5:15  “Basi angalieni sana jinsi mnavyoenenda; si kama watu wasio na hekima bali kama watu wenye hekima; 16  mkiukomboa wakati kwa maana zamani hizi ni za uovu. 17  Kwa sababu hiyo msiwe wajinga, bali mfahamu ni nini yaliyo mapenzi ya Bwana.

Anasema tena..

Wakolosai 4:5  “Enendeni kwa hekima mbele yao walio nje, mkiukomboa wakati. 6  Maneno yenu yawe na neema siku zote, yakikolea munyu, mpate kujua jinsi iwapasavyo kumjibu kila mtu”.

Hivyo tuwapo nje ya uwepo wa Bwana, tujichunge, tujizuie, tuwe na kiasi, tutakuwa salama. Ili tusijikute tunanaswa katika mitego ya ibilisi.(Mithali 1:17,  7:22)

Bwana akubariki.

Shalom.

Tafadhali shea na wengine ujumbe huu;

Pia Kwa maombezi/ Ushauri/ Maswali/ Whatsapp:
Tuandikie katika BOXI la Maoni hapo chini au
Piga namba hizi: +255693036618 au +255789001312

Jiunge na kundi letu la mafundisho ya Biblia whatsapp kwa kubofya hapa >> WHATSAPP-GROUP

Mada Nyinginezo:

Mambo yale yaliyo mbali, na yale yaendayo chini sana,

Dia ni nini katika biblia? (Mithali 13:8)

Mithali 24:17 inamaana gani kusema Tengeneza kazi yako huko nje?

Nini maana ya “Atamwangamiza kwa ufunuo wa kuwapo kwake”. (2Wathesalonike 2:8).

Aibusu midomo atoaye jawabu la haki (Mithali 24:26)

Kuwaogopa wanadamu huleta mtego,(Mithali 29:25)

Marijani ni nini katika biblia(Ayubu 28:18,Mithali 8:11)?

Rudi nyumbani

DOWNLOAD PDF
WhatsApp

Source URL: https://wingulamashahidi.org/2023/03/22/kama-ndege-aendaye-huko-na-huko-mbali-na-kitundu-chake/