JE! KARAMA NI UTHIBITISHO WA KUWA NA MUNGU?

by Admin | 14 June 2019 08:46 pm06

Jina la Bwana wetu Yesu Kristo libarikiwe…Karibu tujifunze Neno la Mungu,.

Mojawapo ya jambo linalochanganya watu wengi wa Mungu..Na hata mimi lilikuwa linanichanganya mwanzoni sana wakati nampa Bwana maisha yangu…Ni jinsi ya “kuwatambua watumishi wa uongo”. Nilikuwa nachanganyikiwa kuona mtu anafanya miujiza kwa jina la Yesu, anatoa pepo, anamwombea mtu anapona, anaona maono, anatoa unabii n.k lakini bado mtu huyo huyo ni mkorofi, ni mtu mzinzi, mtukanaji, ni mtu wa majivuno n.k…Nilikuwa nipo njia panda sana inawezekanikaje mtu akawa hivyo na Mungu bado yupo naye. Nilipojaribu kuwashirikisha baadhi ya watu kwanini jambo hilo linatokea, wengi wakaniambia wanatumia nguvu za giza. Wanakwenda kwa waganga kupokea nguvu za kichawi kisha wanakuja madhabahuni kufanya wanayoyafanya.

Lakini baada ya kujifunza zaidi, nilikuja kufahamu kuwa wengi wao hawatumii nguvu za giza hata kidogo. Leo tutajinza kwa kutumia Biblia ni kwanini hawatumii nguvu za giza.

Ni kweli wapo ambao wanatumia nguvu za giza kufanya miujiza, lakini hao hatutawazungumzia kwasasa kwasababu si wengi sana kama wale ambao hawatumii nguvu za giza.

Tukisoma biblia tunamwona Nabii mmoja ambaye alikwenda kinyume na maagizo ya Mungu, kwani aliambiwa baada ya kutoa unabii kwa mfalme Yeroboamu aondoke na asirudie njia aliyoipitia, na pia asizungumze na mtu njiani. Lakini ukisoma habari ile utaona alidanganywa na nabii mwenzake akayaacha maagizo ya Mungu na hivyo ikawa mauti kwake. Hebu tenga muda usome hichi kisa kwa utulivu kisha tutaendelea.

1 Wafalme 13: 6 “Mfalme akajibu, akamwambia yule mtu wa Mungu, Umsihi sasa Bwana, Mungu wako, ukaniombee, ili nirudishiwe mkono wangu tena. Yule mtu wa Mungu akamwomba Bwana mkono wa mfalme ukarudishwa tena, ukawa kama ulivyokuwa kwanza.

7 Mfalme akamwambia mtu wa Mungu, Karibu nyumbani kwangu ujiburudishe, nami nitakupa thawabu.

8 Mtu wa Mungu akamwambia mfalme, Ujaponipa nusu ya nyumba yako, sitaingia pamoja nawe, wala sitakula chakula, wala sitakunywa maji mahali hapa;

9 maana ndivyo nilivyoagizwa kwa neno la Bwana, kusema, Usile chakula cho chote wala usinywe maji, wala usirudi kwa njia ile uliyoijia.

10 Basi akaenda zake kwa njia nyingine, wala hakurudi kwa njia ile aliyoijia Betheli.

11 BASI NABII MMOJA MZEE alikuwa akikaa katika Betheli; na wanawe wakamwendea wakamwambia kila neno alilolitenda yule mtu wa Mungu siku ile katika Betheli; na maneno aliyomwambia mfalme, hayo nayo walimwambia baba yao.

12 Baba yao akawaambia, Amekwenda zake kwa njia ipi? Kwa maana wanawe walikuwa wameiona njia ile aliyoiendea yule mtu wa Mungu aliyetoka katika Yuda.

13 Akawaambia wanawe, Nitandikieni punda. Wakamtandikia punda, naye akampanda.

14 Akamfuata mtu wa Mungu, akamkuta ameketi chini ya mwaloni, akamwambia, Je! Wewe ndiwe yule mtu wa Mungu aliyetoka katika Yuda? Akamwambia, Mimi ndiye.

15 Akamwambia, Karibu kwangu nyumbani, ule chakula.

16 Naye akamwambia, Siwezi kurudi pamoja nawe, wala kuingia pamoja nawe; wala sili chakula wala sinywi maji pamoja nawe hapa;

17 kwani nimeambiwa kwa neno la Bwana, Usile chakula wala usinywe maji huko, wala usirudi kwa njia ile uliyoijia.

18 Akamwambia, Mimi nami ni nabii kama wewe, na malaika akaniambia kwa neno la Bwana, kusema, Mrudishe pamoja nawe nyumbani kwako, ale chakula, akanywe maji. Lakini alisema uongo.

19 Basi mtu yule akarudi pamoja naye, akala chakula, akanywa maji nyumbani mwake.

20 Hata ikawa, walipokuwa wameketi mezani, neno la Bwana likamjia nabii yule aliyemrudisha;

21 akamlilia yule mtu wa Mungu aliyetoka katika Yuda, akinena, Bwana asema hivi, Kwa sababu umeiasi kauli ya Bwana, wala hukuishika amri ile aliyokuamuru Bwana, Mungu wako,

22 bali umerudi, ukala chakula ukanywa maji, hapo alipokuambia, Usile chakula, wala usinywe maji; maiti yako haitaliingia kaburi la baba zako.

23 Basi ikawa, alipokwisha kula chakula na kunywa maji, yule nabii aliyemrudisha akamtandikia punda.

24 Na alipokuwa amekwenda zake, simba alimkuta njiani, akamwua. Maiti yake ikatupwa njiani, na yule punda akasimama karibu naye; na yule simba naye akasimama karibu na maiti”.

Sasa kama umeelewa habari hiyo utaona kuwa huyo Nabii Mzee alimdanganya huyo nabii mwingine…lakini baadaye Mungu akampa maono huyo nabii mzee amwambie huyo nabii mwingine aliyedanganywa kuwa atakufa kwa kulikaidi Neno la Mungu.

Sasa hapo unaweza ukajiuliza kwanini Mungu aendelee kumpa maono Yule nabii mzee aliyemwambia uwongo mwenzake na kumsababishia mauti..Hiyo inadhihirisha kuwa MTU ANAWEZA KUONA MAONO na Bado akawa mtenda dhambi..mtu anaweza kuwa mwongo au mwasherati na bado Mungu akaendelea kumpa maono. Unaona?..inaogopesha sana!. Huyu nabii Mzee hapa hakutumia nguvu za giza kumtabiria kuwa atakufa. Hapana bali alitabiri kwa uweza wa Mungu. Alifanya dhambi kuzungumza uwongo, lakini Mungu hakumpokonya karama aliyokuwanayo ya kinabii. Na kama hakutubia dhambi hiyo mpaka kufa basi siku ya hukumu atakwenda kwenye ziwa la moto.

Ndio maana Bwana Yesu alisema..

Mathayo 7: 22 “Wengi wataniambia siku ile, Bwana, Bwana, hatukufanya unabii kwa jina lako, na kwa jina lako kutoa pepo, na kwa jina lako kufanya miujiza mingi?

23 Ndipo nitawaambia dhahiri, Sikuwajua ninyi kamwe; ondokeni kwangu, ninyi mtendao maovu”.

Hapo anasema “hatukufanya unabii kwa jina lako?”… ikiwa na maana kuwa sio kwa nguvu za mapepo bali kwa jina lake…Mfano wa huyo nabii aliyemdanganya mwenzake na baadaye akamtolea unabii kwa jina la Bwana…Lakini Bwana Yesu anasema watu wengi wa namna hiyo siku ile atawafukuza na kuwaambia siwajui kamwe…ondokeni kwangu ninyi mtendao maovu.

Hivyo ndugu hapo tunajifunza kuwa, usiangalia karama uliyonayo au mtu mwingine anayejiita mtumishi aliyonayo…bali jiangalie matendo yako ndipo ujihukumu kuwa upo sawa na Mungu au la! Usijiangalie karama yako ya kuimba ukadhani hichi ndicho kinachompendeza Mungu, au karama yako ya kiualimu, au karama yako ya kunena kwa lugha, au karama yako ya kinabii, unaona maono mengi mpaka ya kitaifa ukadhani wewe ni spesheli sana kwa Mungu…badala yake jiangalie ndani yako je! Unayatenda mapenzi ya Mungu je! Kuna utakatifu ndani yako??.

Unaweza ukawa kila anayekuja kwako ukimwombea anapona au tatizo lake linaondoka…au kila anayekuja kwako Bwana anakufunulia tatizo lake kwenye maono…lakini bado ukawa mbali na Mungu…Unaweza ukawa umetokewa na malaika au Bwana Yesu mwenyewe lakini siku ile akakwambia sikujui…Mungu anaweza akawa anaongea na wewe kila siku na kukupa maagizo ya kufanya hichi na kufanya kile kama alivyompa huyu Nabii Mzee, lakini siku ile bado akakukataa..Balaamu alikuwa ni nabii anayezungumza na Mungu na kupokea maagizo kutoka kwa Mungu lakini bado alikuwa ni mchawi.

Biblia inasema wazi katika Waebrania 12:14 kwamba PASIPO UTAKATIFU HAKUNA MTU ATAKAYEMWONA MUNGU.

Hivyo ni wakati wa kutafuta kuyatenda mapenzi ya Mungu ambao ndio utakatifu, Na si kuangalia upako wala karama kama uthibitisho wa kuwa Mungu yupo pamoja na sisi.Ikiwa karama itafuata baada ya utakatifu hiyo ni vizuri sana. Vile vile si wakati wa kumhukumu mtumishi wa ukweli au wa uwongo kwa karama anazozidhihirisha..bali tutawatambua kwa matunda yao biblia inatuambia hivyo (Mathayo 7:16)…na Matunda yanayozungumziwa hapo ni matendo yao…

Bwana akubariki.jiunge na channel yetu Kwa kubofya hapa >> WHATSAPP


Mada Zinazoendana:

NITAIFAHAMU VIPI KARAMA YANGU?

 KARAMA YA ILIYO KUU NI IPI?

KARAMA YA MUNGU NI IPI?

JE KUNENA KWA LUGHA MPYA KUKOJE? NA HIZI LUGHA NI ZIPI, NA JE! NI LAZIMA KILA MKRISTO ALIYEPOKEA ROHO MTAKATIFU ANENE KWA LUGHA MPYA?.


Rudi Nyumbani

 

DOWNLOAD PDF
WhatsApp

Source URL: https://wingulamashahidi.org/2019/06/14/je-karama-ni-uthibitisho-wa-kuwa-na-mungu/