LIVUNJENI HEKALU HILI, NAMI KATIKA SIKU TATU NITALISIMAMISHA.

by Admin | 5 March 2020 08:46 pm03

Livunjeni hekalu hili nami katika siku tatu nitalisimamisha..

Mara nyingine Bwana Yesu alipotaka kufikisha ujumbe Fulani, alikuwa anatumia mfano wa mahali husika ili kuchanganya mada mbili kwa wakati mmoja …Kwamfano utaona wakati ule mitume wa Bwana Yesu waliposahau kuchukua ile mkate ambayo ilibaki wakaanza kugombana wao kwa wao kwa kulaumiana kwanini hawakuibeba, …lakini Bwana Yesu alipowasikia, mabishanao yao alitumia mfano mwingine kuzungumza nao kana kwamba alikuwa hamaanisha hicho walichokuwa wanakibishania kwa wakati huo..

Marko 8:13 “Akawaacha, akapanda tena chomboni, akaenda zake hata ng’ambo.

14 Wakasahau kuchukua mikate, wala chomboni hawana ila mkate mmoja tu.

15 Akawaagiza, akasema, Angalieni, jihadharini na chachu ya Mafarisayo na chachu ya Herode.

16 Wakabishana wao kwa wao, kwa kuwa hawana mikate.

17 Naye Yesu akatambua, akawaambia, Mbona mnabishana kwa sababu hamna mikate? Hamfahamu bado, wala hamjaelewa? Je! Mioyo yenu ni mizito?

18 Mna macho, hamwoni; mna masikio, hamsikii? Wala hamkumbuki?

19 Nilipoivunja ile mikate mitano na kuwapa wale elfu tano, mlichukua vikapu vingapi vimejaa vipande? Wakamwambia, Kumi na viwili.

20 Na ile saba kuwapa wale elfu nne, mlichukua makanda mangapi yamejaa vipande? Wakamwambia, Saba.

21 Akawaambia, Hamjafahamu bado?”

Unaona hapo? Bwana Yesu alitumia mfano wa chachu, na kusema, jilindeni na chachu ya mafarisayo…Lakini mitume wakadhani anazungumzia chachu ya mikate ya mafarisayo, hiyo ikiwafanya wazidi kugombana zaidi ili apate kuwanasa vizuri,..Hapo ndipo Bwana akapata nafasi ya kuwakemea kwa kukosa kwao ufahamu, akawaambia hamjafahamu bado?, mimi sizungumzii habari za mikate, mmesahau ni mikate mingapi mlikusanya kama masalia wakati ule?, hamjafahamu bado, hamjaelewa, mioyo yenu ni mizito, hamna imani kwa Mungu bado kuwa hata sasa anaweza kuwafanyia muujiza kama ule ule wa mikate mengine mkala mkashiba, pasipo kuwa na chochote?…lakini bado mnamtilia shaka Mungu?…Mimi sizungumzii habari za mikate ninaachomaanisha ni jilindeni na mafundisho ya mafarisayo..

Sasa utaona hapo mitume walipata mafundisho mawili, la kwanza ni kutokana na kile walichokuwa wanakifiria juu ya tumbo, kuwa Mungu bado anaweza kuwahudumia hata kama kunaonekana hakuna mlango wa kupata chakula, na cha pili ni kuhusu mafundisho ya mafarisayo (ambayo yanafananishwa na chachu/hamira) ambayo kazi yake ni kuumua na kupindua uhalisia wa Neno la Mungu…Lakini waliupata ule ujumbe uliokuwa unawahusu kwa wakati wao.

Ndivyo hivyo hata wakati ule Bwana Yesu alipokwenda hekaluni, akaona jinsi watu walivyoweka tumaini lao lote katika lile hekalu, jinsi lilivyokuwa limepambwa kwa namna ya ajabu, jinsi lilivyokuwa kubwa, na kukarabatiwa kwa muda mrefu wa miaka 46 na Herode..jinsi watu wengi walivyokuwa wanatoa sadaka zao kwa ajili ya hekalu lile.. Lakini jicho la Bwana Yesu lilikuwa linaona mbali zaidi yao, lilikuwa linaona muda si mrefu hekalu lile halitakuwepo, litakuwa limebomolewa, mahali pale patakuwa pamechomwa moto, watu watauawa na kuchinjwa kama kuku..lakini wale watu hawakuliona hilo, walikuwa wanajisifia tu majengo yake, hawaoni wakati umekaribia mji huo waliokuwepo ambao wanaupenda utateketezwa kwa moto…

Ndipo sasa wakati Bwana akiwa pale hekaluni anavuruga vuruga bishara zao.. wayahudi wakamfuata na kumuuliza, Ni ishara gani utuonyeshayo, kwamba unafanya haya?

Yesu akawajibu…

Yohana 2:19 “…..Livunjeni hekalu hili, nami katika siku tatu nitalisimamisha.

20 Basi Wayahudi wakasema, Hekalu hili lilijengwa katika muda wa miaka arobaini na sita, nawe utalisimamisha katika siku tatu?

21 Lakini yeye alinena habari za hekalu la mwili wake.

22 Basi alipofufuka katika wafu, wanafunzi wake wakakumbuka ya kuwa alisema hivi, wakaliamini lile andiko na lile neno alilolinena Yesu”.

Unaona, Bwana Yesu alimaanisha kweli juu ya hekalu la mwili wake kuwa atakufa na siku ya tatu atafufuka, lakini pia alitaka wafikirie vile vile juu ya habari za kubomolewa kwa hekalu, ili awafundishe jambo..lakini wengi wao hawakuwa tayari kutaka kujua zaidi, wakamwona kama karukwa na akili..anazungumza ujinga.

Lakini baadaye wanafunzi wake wanyenyekevu waliliweka hilo akilini…wakaanza tena kumwonyesha majengo ya hekalu lile ambalo yeye alisema watu walibomoe,..jinsi lilivyojengwa vizuri kwa mawe ya thamani…

Mathayo 24:1 “Yesu akaenda zake, akatoka hekaluni; wanafunzi wake wakamwendea ili kumwonyesha majengo ya hekalu

2.Hamyaoni haya yote? Amin, nawaambieni, Halitasalia hapa jiwe juu ya jiwe ambalo halitabomoshwa”.

Lakini wanafunzi walivyosikia vile, hawakuishia pale, walizidi kuendelea kutaka kujua hatma ya hayo mambo itakuwaje, wakamfuata sasa faraghani, wakiwa peke yao tu Bwana, ndipo wakamuuliza..mambo hayo yatakuwa lini? Nayo ni nini dalili ya kuja kwako? Na ya Mwisho wa dunia? Maswali matatu.

Hapo sasa ndipo Bwana Yesu akaanza kuwafunulia hatua kwa hatua, mambo yatakayotendeka kuanzia ule wakati, mpaka siku mji ule utakapozingirwa na majeshi, na hekalu kubomolewa, mpaka siku za mwisho..ambayo maneno haya hata sisi wa kizazi hiki tunayatumia kama dira ya kutambua majira ya kuja kwa Bwana Yesu..Soma Mathayo 24, Marko 13, na Luka 21. Utaona habari zote za siku za mwisho zitakavyokuwa.

Lakini mafunuo hayo yote yalitoka katika Neno moja tu la Kubomolewa kwa hekalu..Kama mtume wasingetaka kujua zaidi, basi habari za kuteketezwa kwa Yerusalemu na warumi mwaka 70W.K, ambapo watu waliuawa kikatili, wasingekaa wajue pia habari za manabii wa uongo, na kusimama kwa chukizo la uharibifu wasingekaa wajue..

Vivyo hivyo hata sasa, tukiwa tayari kutaka kujua zaidi juu ya maneno ya Bwana wetu Yesu Kristo katika Neno lake, kwa kumaanisha kujifunza Neno lake na sio kusoma tu kama gazeti, ndipo tunapojijengea nafasi nzuri ya kupokea mafunuo zaidi yamuhusuyo yeye.

Lakini kama tutasoma biblia juu juu tu, na kusema aa hii haiwezekani, au tunasema kile Bwana alimaanisha vile sio hivi..Tutabakia, kuujua upande mmoja tu wa maandiko..Na kufanana na wale watu waliomsulubisha pale msalabani na kumdhihaki…walisikia tu upande mmoja (livunjeni hekalu hili)

Zaburi 25:14 “Siri ya Bwana iko kwao wamchao, Naye atawajulisha agano lake”.

Hivyo Bwana atusaidie tuzidi kumjua Zaidi yeye, mpaka tutakapofikia ukamilifu.

Bwana akubariki.

Tafadhali washirikishe na wengine habari hizi njema, na pia kama utapenda tuwe tunakutumia masomo haya kwa njia ya email yako au Whatsapp tutumie ujumbe kwenye box la maoni chini au piga namba hii +255 789001312


Mada Nyinginezo:

Rudi Nyumbani:

DOWNLOAD PDF
WhatsApp

Source URL: https://wingulamashahidi.org/2020/03/05/livunjeni-hekalu-hili-nami-katika-siku-tatu-nitalisimamisha/