MOJA YA HIZI SIKU TUTAONA MABADILIKO MAKUBWA SANA.

by Admin | 13 April 2020 08:46 am04

Kama kuna majira ambayo si ya kufanya mchezo na masuala ya wokovu wetu hata kidogo basi ni haya. Kwani moja ya hizi siku tutashuhudia mabadiliko makubwa sana na ya ghafla katika kanisa la Kristo,..wakati ambao Bwana Yesu anakwenda kuchukua hatua ambayo hakuwahi kuichukua tangu aondoke hapa duniani.. Na hatua yenyewe ni Kuingia na kuufunga mlango wa hekalu lake.

Hayo mambo pengine utayashuhudia kwa macho yako siku si nyingi,..Kumbuka biblia inalifananisha kanisa la Kristo na hekalu lake (Waefeso 2:19-22)..Sasa ukisoma kitabu cha Ezekieli utaona anaonyeshwa matukio yanayoambata na hakalu la Mungu, Na utaona akionyeshwa malango mengi ya hekalu yakiwa wazi, lakini ukisoma ile sura ya 44 utaona Ezekieli anaonyeshwa ghafla lango la mashariki likiwa limefungwa..Na anaambiwa halitafunguliwa tena, wala mtu awaye yote hataingia kwa kupitia lango hilo.

Ndipo Ezekieli akaambiwa sababu ya lango hilo kufungwa, na sababu yenyewe ilikuwa ni hii..tusome..

Ezekieli 44:1 “Kisha akanirudisha kwa njia ya lango lile la nje, la mahali patakatifu lililoelekea upande wa mashariki; nalo lilikuwa limefungwa.

2 Bwana akaniambia, Lango hili litafungwa, halitafunguliwa, wala mtu awaye yote hataingia kwa lango hili, kwa maana Bwana, Mungu wa Israeli, ameingia kwa hilo; basi kwa sababu hiyo litafungwa”.

Unaona, sababu ni kuwa Bwana, Mungu wa Israeli (KRISTO), ameingia kwa lango hilo.. Hii ni kuonyesha kuwa mlango huo uliwekwa mahususi kwa ajili yake na si mwingine, yeye ndiye aliyekuwa amewekewa wazi mlango huo mpaka atakapofika,. Hivyo wale waliokuwa wanaingia kabla ya hapo ni neema tu, lakini haukuwekwa wazi kwa ajili yao..

Hivyo Habari hiyo jambo kwa sehemu limetimia lakini ni unabii wa siku za mwisho, wakati ambao Mlango wa Neema utafungwa.

Ndugu, huu mlango ambao tunauita wa neema tulio nao leo hii, Mungu kauacha wazi si kwasababu yetu, bali kwasababu ya Yesu Kristo, Ni mlango wa Kristo Yesu mwenyewe na sio wetu, na moja ya siku hizi, hivi karibuni atasimama, kisha ataupita, na akishaingia, basi utafungwa na ukishafungwa, Habari imeishia hapo hautafunguliwa tena milele..

Mambo yatakayokuwa yanaendelea humo ndani ni siri yake na wale watakaokuwa humo.. Kwahiyo usione unahubiriwa injili, usione unapigiwa kilele utubu dhambi ukadhani Mungu anakuangalia wewe sana, hilo jambo halipo! Mungu anamtazama Kristo tu!, achukue hatua yake, na akishaichukua, hapo ndipo kutakuwa na kilio na kusaga meno kama alivyosema, hakutania alimaanisha kweli wapo watu watalia kweli kweli wakitamani hata nusu saa nyuma lirudi watengeneze mambo yao lakini watakuwa wameshachelewa.

Luka 13:24 “Jitahidini kuingia katika mlango ulio mwembamba, kwa maana nawaambia ya kwamba wengi watataka kuingia, wasiweze.

25 Wakati mwenye nyumba atakaposimama na kuufunga mlango, nanyi mkaanza kusimama nje na kuubisha mlango, mkisema, Ee Bwana, tufungulie; yeye atajibu na kuwaambia, Siwajui mtokako;

26 ndipo mtakapoanza kusema, Tulikula na kunywa mbele yako, nawe ulifundisha katika njia zetu. 27 Naye atasema, Nawaambia, Siwajui mtokako; ondokeni kwangu ninyi nyote mlio wafanyaji wa udhalimu.

28 Ndipo kutakapokuwa na kilio na kusaga meno…”

Kumbuka hatua hiyo sio ya unyakuo, hapo unyakuo bado, mambo hayo yatatendeka hapa hapa duniani, kwasababu wakati huo utatamani umjue Kristo, lakini hutaweza tena, kwasababu anayewavuta watu kwa Kristo sasa ni Roho Mtakatifu na sio mtu mwenyewe..Hivyo Roho Mtakatifu akishaondoka juu yako huwezi tena kumfuata Mungu hata iweje..(Yohana 6:44)

Sasa muda mfupi baada ya huo wakati, Unyakuo ndio utapita, na wewe ambaye humtaki Kristo sasa…utaendelea kubaki hapa hapa duniani ambacho kitakachofuata ni dhiki kuu kabla hujafa na kuingia katika jehanamu ya moto. Kama tunavyoona mambo yalivyo sasa, ni tunaishi katika muda wa nyiongeza tu.., hii dunia ingepaswa iwe imeshaisha tangu zamani kulingana na unabii wa kibiblia, lakini dalili zote zinaonyesha sasa wakati wowote, mambo yatabadilika kwa ghafla sana. Na Mlango utafungwa na watu watatamani kuingia watashindwa..

Soma Habari hii kulithibitisha hilo tena..uone jinsi wanawali wale wapumbavu waliporudi na kukuta mlango umefungwa, ufananishe na hali itakavyokuwa wa wakristo wengi vuguvugu waliopo leo duniani..

Mathayo 25 : 1-13 “Ndipo ufalme wa mbinguni utakapofanana na wanawali kumi, waliotwaa taa zao, wakatoka kwenda kumlaki bwana arusi.

2 Watano wao walikuwa wapumbavu, na watano wenye busara.

3 Wale waliokuwa wapumbavu walizitwaa taa zao, wasitwae na mafuta pamoja nao; 4 bali wale wenye busara walitwaa mafuta katika vyombo vyao pamoja na taa zao.

5 Hata bwana arusi alipokawia, wote wakasinzia wakalala usingizi.

6 Lakini usiku wa manane, pakawa na kelele, Haya, bwana arusi; tokeni mwende kumlaki.

7 Mara wakaondoka wanawali wale wote, wakazitengeneza taa zao.

8 Wale wapumbavu wakawaambia wenye busara, Tupeni mafuta yenu kidogo; maana taa zetu zinazimika. 9 Lakini wale wenye busara wakawajibu, wakisema, Sivyo; hayatatutosha sisi na ninyi; afadhali shikeni njia mwende kwa wauzao, mkajinunulie.

10 Na hao walipokuwa wakienda kununua, bwana arusi akaja, nao waliokuwa tayari wakaingia pamoja naye arusini; mlango ukafungwa.

11 Halafu wakaja na wale wanawali wengine, wakasema, Bwana, Bwana, utufungulie.

12 Akajibu akasema, Amin, nawaambia, siwajui ninyi.

13 Basi kesheni, kwa sababu hamwijui siku wala saa”.

Je! Na wewe bado nje ya mlango huo hujaingia tu ndani mpaka sasa?..Kumbuka tena jambo hili lango hilo likishafungwa mara moja, halitafunguliwa tena milele..(Na Yesu ndiye lango) Ni heri ukatubu dhambi zako leo ikiwa hujafanya hivyo..Ili Mungu atakusamehe na kukupa uzima wa milele bure.

Ufunuo 22:17 “Naye mwenye kiu na aje; na yeye atakaye, na ayatwae maji ya uzima bure.”

Bwana akubariki.

Tafadhali washirikishe na wengine habari hizi njema, na pia kama utapenda tuwe tunakutumia masomo haya kwa njia ya email yako au Whatsapp tutumie ujumbe kwenye box la maoni chini au piga namba hii +255 789001312


Mada Nyinginezo:

MAMBO 5 AMBAYO KILA MKRISTO ANAPASWA KUFAHAMU.

JE! WATOTO WACHANGA WANAWEZA KUHUKUMIWA NA KUTUPWA MOTONI.

Biblia inamaanisha nini inaposema “Tusitweze unabii”?

TUMAINI NI NINI?

Je! Adamu aliwasaliana na Mungu kwa lugha ipi pale bustanini?

JE ADAMU ALIKUWA NA KITOVU?

Rudi Nyumbani:

DOWNLOAD PDF
WhatsApp

Source URL: https://wingulamashahidi.org/2020/04/13/moja-ya-hizi-siku-tutaona-mabadiliko-makubwa-sana/