YESU NDIYE ATAKAYEKURUSHIA MAWE, USIPOTUBU.

by Admin | 3 February 2022 08:46 am02

Tunaishi katika ulimwengu ambao, ukisimama tu kuhubiri, au kukemea dhambi, moja kwa moja utaambiwa UNAHUKUMU, Ukimweleza mtu madhara ya dhambi ya uzinzi kuwa mwisho wake, ni motoni, atakuambia, wewe ni nani mpaka utoe hukumu hiyo.

Wakati Fulani nilizungumza na watu Fulani ambao walikuwa wanatetea dhambi ya ushoga, nikawaambia watu wanaofanya matendo kama hayo, mwisho wao ni jehanamu walinishambulia, kisha wakanipa andiko, lile, ambalo linamzungumzia yule mwanamke aliyefumaniwa katika uzinzi, ambapo mafarisayo walimpeleka kwa Yesu, kwa lengo la kumjaribu, kama na yeye ataridhia kupigwa mawe, lakini mambo yakawa tofauti badala ya kuwaruhusu wampige mawe akawaambia, “Yeye asiye na dhambi miongoni mwenu na awe wa kwanza wa kumtupia jiwe”. Basi wote wakatawanyika wakamwacha yule mwanamke akiwa na Bwana peke yake.( Yohana 8:1-11)

Hivyo kwa Habari hiyo hawa watu nao wakaniambia, kama wale watu hawakumtupia yule mwanamke mawe, wewe ni nani utuhukumu sisi kwa tunachokifanya, humwogopi Yesu?.

Nikawaambia mimi  siwezi kuwatupia ninyi mawe, lakini Yesu mwenyewe atawatupia ninyi mawe, wakati wenu ukifika.

Watu wanadhani Kristo atakuwa katika kiti chake cha rehema milele, kuchukuliana na dhambi zetu,, hawajui kuwa atasimama kama hakimu siku moja kuwahukumu na kuwaadhibu waovu wote,..Wanadhani, Bwana anafurahia uasherati wa mtu, au uzinzi wa mtu, wanadhani alifurahia pia Uzinzi wa yule mwanamke, ndio maana hakufanya chochote.

Nataka nikuambie ikiwa yule mwanamke angeendelea katika uzinzi wake, ni kweli angekwepa mawe ya wanadamu kwa wakati ule, lakini angekutana na mawe ya Kristo siku ile ya hukumu.

Wakati huo hakutakuwa na huruma yoyote katika macho ya Bwana Yesu, haijalishi wewe ni mtoto au mlemavu, au mzee, kama ulikufa katika dhambi, utahukumiwa na kutupwa motoni milele.

Hata kabla ya siku ya hukumu yenyewe kufika, siku ile ambayo atakuwa anarudi katika mawingu kuja kutawala kama mfalme, biblia inasema, ulimwengu mzima utamwombolezea (Ufunuo 1:7).. Na utamwombolezea kwasababu gani, kwasababu ya hayo mapigo atakayokuwa anawamwagia waasi wote katika huuu ulimwengu.

Inatisha sana kwasababu, Bwana Yesu atawaua watu wengi sana, wasiokuwa na idadi. Soma hapa;

Isaya 66:15 “Maana Bwana atakuja na moto, na magari yake ya vita kama upepo wa kisulisuli; ili atoe malipo ya ghadhabu yake kwa moto uwakao, na maonyo yake kwa miali ya moto.

16 Kwa maana Bwana atateta na wote wenye mwili, kwa moto na kwa upanga wake; NAO WATAKAOUAWA NA BWANA WATAKUWA WENGI”.

Siku hiyo Wazinzi, mashoga, wafiraji, walevi, washirikina, watatamani milima iwaangukie, ili tu waiepuke hiyo ghadhabu ya Bwana Yesu, lakini haitakuwa hivyo; watashiriki tu mapigo yake.

Ufunuo 6:15 “Na wafalme wa dunia, na wakuu, na majemadari, na matajiri, na wenye nguvu, na kila mtumwa, na mwungwana, wakajificha katika pango na chini ya miamba ya milima,

16 wakiiambia milima na miamba, Tuangukieni, tusitirini, mbele za uso wake yeye aketiye juu ya kiti cha enzi, na hasira ya Mwana-Kondoo.

17 Kwa maana siku iliyo kuu, ya hasira yao, imekuja; naye ni nani awezaye kusimama”?

Ndugu, yangu, huu wakati usitamani ukukute, kwasababu hata baada ya kupokea mapigo hayo makali kutoka kwa Bwana Yesu, bado utasimama katika kiti chake cha hukumu na kutoa hesabu ya mambo yote uliyokuwa unayafanya hapa duniani yasiyompendeza Mungu, na baada ya hapo utatupwa katika lile ziwa la moto uangamie milele na milele.

Tukiyatafakari haya kwa umakini, ndio tutajua ni kwa namna gani Bwana Yesu hapendezwi na dhambi hata kidogo, Kuona leo hii unatoa mimba hafanyi chochote, unatazama picha za ngono, hachukui hatua yoyote, unaiba hakuadhibu, unazini, unalewa, unaabudu sanamu, bado hajishughulishi na wewe..usipumbazike ukadhani, hali hiyo itaendelea hivyo hivyo milele, hata baada ya kufa.

Waebrania 10:31 “Ni jambo la kutisha kuanguka katika mikono ya Mungu aliye hai”.

Ni heri ukayasalimisha Maisha yako leo kwa Bwana Yesu maadamu neema ipo, Wakati umekaribia, mambo yatabadilika ghafla, parapanda italia, kisha watakatifu wataondoka..Wewe ambaye utabakia katika huu ulimwengu, ndio utakayekutana na huo upande wa pili wa shilingi wa Bwana Yesu, ni kilio na kusaga meno!. Hutaamini kama huyu ndio yule Bwana aliyekuwa ananililia kila siku niache dhambi kwa sura ya upole, nikawa namdharau. Atakuuwa mwili na roho.

Mathayo 10:28b “… afadhali mwogopeni yule awezaye kuangamiza mwili na roho pia katika jehanum”.

Bwana atusaidie sana, ikiwa hujaokoka, embu anza Maisha yako upya na Kristo leo. Tubu dhambi zako kwa kumaanisha kuziacha, kisha tafuta ubatizo sahihi wa kuzamishwa katika maji mengi na uwe katika jina la Bwana Yesu Kristo, ili upokee ondoleo la dhambi zako, na baada ya hapo Bwana atakusaidia. Hatuna muda tena, Yesu anarudi wakati wowote.

Kwa msaada ya kumpokea Yesu, basi wasiliana nasi kwa namba hizi; +255789001312 /+255693036618

Tafadhali washirikishe na wengine habari hizi njema,

pia kama utapenda uyapate mafundisho haya kwa njia ya Whatsapp au email basi tutumie ujumbe kwenye namba hizo hizo.

Mada Nyinginezo:

MAPIGO YA VITASA SABA, NA SIKU YA BWANA.

UNYAKUO.

KIKOMBE CHA GHADHABU YA MUNGU KINAJAA…TUBU UMGEUKIE MUNGU

UPENDO WA MUNGU.

Rudi nyumbani

DOWNLOAD PDF
WhatsApp

Source URL: https://wingulamashahidi.org/2022/02/03/yesu-ndiye-atakayekurushia-mawe-usipotubu/