MTOLEE BWANA KWA UFUNUO KAMA HANA

MTOLEE BWANA KWA UFUNUO KAMA HANA

Jina la Bwana YESU libarikiwe, karibu tujifunze Biblia, Neno la MUNGU wetu lililo Taa na Mwanga wa njia zetu (Zab. 119:105).

Katika Biblia tunajifunza jambo kubwa sana kwa mwanamke “Hana” ambaye alikuwa tasa lakini baadae Bwana alimfungua tumbo lake na kuzaa watoto.

Katika usomaji wa kitabu cha 1Samweli mlango wa kwanza na wa pili, ni rahisi kufikiri kuwa Hana alimwekea MUNGU nadhiri ya kumtoa mtoto wake wa kwanza atumike kwenye nyumba ya MUNGU daima, bila kuwa na ufunuo au sababu yoyote (ni rahisi kufikiri hilo).

Lakini tukijifunza kwa undani, tunaona wazi kuwa sababu kuu ya Hana kumtoa mtoto wake wa kwanza (Samweli) atumike kwenye nyumba ya MUNGU daima, ni matatizo aliyoyaona  ndani ya nyumba ya MUNGU, kwa wakati ule.

Kwani walikuwepo wana wawili wa kuhani Eli, walioitwa Hofni na Finehasi, vijana hawa hawakuwa waaminifu katika nyumba ya MUNGU,

Kwani walikuwa wanatumia vibaya dhabihu na sadaka zilizokuwa zinaletwa nyumbani mwa Bwana, na zaidi sana walikuwa wakizini na wanawake waliokuwa wakihudumu ndani ya nyumba ya MUNGU, na sifa zao hizo mbaya ziijulikana na watu wote, na hata mwanamke “Hana” aliwajua kwa sifa hiyo.

1 Samweli 2:22 “Basi Eli alikuwa mzee sana; naye alisikia habari za mambo yote ambayo wanawe waliwatenda Waisraeli; na jinsi walivyolala na wanawake waliokuwa wakitumika mlangoni pa hema ya kukutania.

23 Akawaambia, Mbona mnatenda mambo kama hayo? Maana nasikia habari za matendo yenu mabaya kwa watu hawa wote.

24 Sivyo hivyo, wanangu, kwa maana habari hii ninayoisikia si habari njema; mnawakosesha watu wa BWANA.

25 Mtu mmoja akimkosa mwenzake, Mungu atamhukumu; lakini mtu akimkosa BWANA, ni nani atakayemtetea? Lakini hawakuisikia sauti ya baba yao, kwa sababu BWANA amekusudia kuwaua”.

Kwasababu hiyo basi Hana, aliona shukrani pekee ambayo anaweza kumpa MUNGU endapo Mungu atamfungua tumbo lake si kutoa pesa, kwasababu hata akizipeleka madhabahuni  nyumbani mwa MUNGU zitatumiwa vibaya na wale vijana wawili wa Eli (Hofni na Fineasi), wala si dhabihu kwasababu pia zinatumika vibaya.

Ndipo alipotafakari na kuona nadhiri bora na sadaka maalumu itakuwa ya kumtoa mwanae wa kwanza kwa Bwana akawe Mtumishi wa madhabahuni,

Hiyo aliona inaweza kuwa sadaka njema kwake kwa BWANA, Kwani mtoto yule atakuwa katika misingi sahihi ya kiMungu, na atasimama katika kazi ya nyumba ya Bwana kwa uaminifu na kuwa baraka kwa Israeli yote.

Ndivyo Hana alivyofanya, na kupitia sadaka yake hiyo ya kiufunuo, Mungu alisikia maombi yake na kumpa mtoto Samweli, ambaye ndiye aliyekuja kuwaa nabii mkuu Israeli kwa wakati ule.

Ni hivyo hivyo kwa MUNGU wetu, aliona baraka kubwa atakayoibarikia dunia si kuleta mvua nyingi yenye kustawisha nafaka ili matatizo ya njaa yaishe duniani, wala si kumfanya kila mtu kuwa milionea, bali ni kwa kumtoa mwanae pekee YESU KRISTO, Kama dhabihu iliyo hai na sadaka kuu, na kupitia sadaka hiyo leo hii tunabarikiwa kwa baraka zote.

Na sisi tunajifunza mambo hayo hayo, kutazama katika roho ni nini cha kumtolea BWANA, si kila wakati fedha au mali zitakuwa ni sadaka sahihi kwa MUNGU au kwa Nyumba yake au kazi ya MUNGU, wakati mwingine wewe mwenyewe unaweza kuwa sadaka bora kwa kujitoa mwili wako na muda wako kutumika.

Warumi 12:1 “Basi, ndugu zangu, nawasihi, kwa huruma zake Mungu, itoeni miili yenu iwe dhabihu iliyo hai, takatifu, ya kumpendeza Mungu, ndiyo ibada yenu yenye maana.

Au si wewe bali mwanao anaweza kuwa bora zaidi na akawa sadaka yenye kumpendeza Bwana. (Kwa wewe kumuandaa kuwa mtumishi, kwa kumfundisha, kumwombea na kumtolea sadaka kwa MUNGU).

Kuna wakati ardhi inaweza kuwa sadaka nzuri kwa Bwana zaidi ya fedha, kuna wakati, kununua kitu na kukipeleka nyumbani mwa Bwana inaweza kuwa bora zaidi kuliko kutoa tu fedha, na kuna wakati fedha ni muhimu zaidi kuliko kitu utakachopeleka, hivyo ni muhimu kuwa na jicho la kiroho na kujua ni kipi kinafaa kutoa kwa wakati huo.

Na kumbuka siku zote, ni heri kutoa kuliko kupokea (Matendo 2:35).

Bwana YESU atusaidie katika  kumtolea yeye matoleo yenye kumpendeza.

Shalom.

Washirikishe na wengine habari hizi njema kwa kushea

Ikiwa utapenda kupata msaada wa kumpokea Yesu maishani mwako bure, Basi wasiliana nasi kwa namba uzionazo chini ya makala hii.

Pia kwa kupokea mafundisho ya kila siku kwa njia ya WHATSAPP, jiunge na channel yetu kwa kubofya link hii >> https://whatsapp.com/channel/0029VaBVhuA3WHTbKoz8jx10

Kwa mawasiliano: +255693036618 au +255789001312

Bwana akubariki.

Mafundisho mengine:

Print this post

MUNGU AUMBAYE TENA.

Biblia inatuonyesha Mungu ndiye muumba wa vitu vyote 

Mwanzo 1:1 Hapo mwanzo Mungu aliziumba mbingu na nchi.

Lakini hatujui ni nini kilitokea baadaye kikaifanya dunia kuwa ukiwa, mpaka akaanza kuirekebisha tena dunia aliyoiumba mwanzo.. 

Kwasababu mstari wa 2..unasema nayo nchi ilikuwa ukiwa, tena utupu na giza lilikuwa juu ya uso wa vilindi vya maji, 

Mungu akaanza tena kuifanya ikaliwe na watu, akaleta tena nuru kutoka kwenye giza, akayatenga maji, na kuyaweka sehemu stahiki,  akalitokeza anga..akamuumba mwanadamu.

Dunia ikawa nzuri tena, lakini baadaye mwanadamu akaasi, akaiharibu duniani, mpaka ikaangamia kwa maji. 

Bado Mungu hakuikatia tamaa dunia yake, akawaongeza,Nuhu na wazao wake, baadaye akamchagua Ibrahimu ili kumwandaa mkombozi atakayeikomboa dunia kikamilifu, akaja Kristo ulimwenguni ndio mwokozi wetu.

Watu wakaokolewa, ijapokuwa waliendelea kuiharibu dunia, bado Mungu akawa kwenye mwendelezo wa uumbaji wake unaoharibiwa .

Na kama tunavyojua Kristo aliahidi kurudi tena duniani mara ya pili, kuwanyakua watu wake, kisha kuukarabati huu ulimwenguni na kuufanya kuwa mbingu mpya na nchi mpya.(Ufunuo 21)

Hivyo kama ukichunguza asili ya tabia ya Mungu, si kufanya kitu mara moja, kisha pale kinapoharibika anakikatia tamaa ..

Hapana utaona hukiumba tena na tena na tena…kwa miaka na miaka na miaka..tena huanzia mbali sana mpango wake wa ukarabati..

Na sisi ni lazima tujue tumeumbwa kwa mfano wake na sura yake..ikiwa unaona hakuna mwenye hekima duniani  kumzidi Mungu, na kila lifanyalo ni bora, na kamilifu basi jifunze kuiga tabia zake ufanikiwe…

Mungu wetu alikuwa na siku moja katika juma ya kupumzika, wewe si ‘busy’ zaidi ya Mungu mpaka siku zote saba katika juma, mwaka mzima unafanya kazi mpaka unakosa muda wa kumwabudu Mungu wako.

Vivyo hivyo ni lazima kutambua kuwa kazi zake zimepitia changamoto nyingi sana za kuharibiwa zaidi ya zako lakini amekuwa katika uumbaji wake kila siku..Na wewe pia kuharibiwa kwa maono yako, si sababu ya kukata tamaa na kusema sitaendelea mbele…inuka anza tena na tena..

Unamtumikia Mungu, ile huduma iliyokaa ndani yako, ni kama imekufa, mwanzoni uliona hatua lakini sasa huoni, pengine ni kutokana na kuwa umedhulumiwa, umeibiwa, umefukuzwa..inuka tena na tena, anza upya..

Kuacha kazi uliyokwisha itaabikia na kuitolea jasho jingi, ni ishara ya kuwa bado tabia ya Mungu haijaumbika ndani yako.

Kumbuka mpaka leo hii Mungu anaendelea kufanya uumbaji wake, itapokuwa kazi hizo zingepeswa zikamilike tangu kule mwanzo…Wewe ni nani usifanye matengenezo yako yaliyokufa kila siku?

Anza sasa. Fanya kazi na Mungu.

Shalom.

 

Washirikishe na wengine habari hizi njema kwa kushea

Ikiwa utapenda kupata msaada wa kumpokea Yesu maishani mwako bure, Basi wasiliana nasi kwa namba uzionazo chini ya makala hii.

Pia kwa kupokea mafundisho ya kila siku kwa njia ya WHATSAPP, jiunge na channel yetu kwa kubofya link hii >> https://whatsapp.com/channel/0029VaBVhuA3WHTbKoz8jx10

Kwa mawasiliano: +255693036618 au +255789001312

Bwana akubariki.

Mafundisho mengine:

MBONA MMESIMAMA HAPA MCHANA KUTWA BILA KAZI?

USIMPE MWANAO VITU SASA.

Print this post

UPANGA USHIKAMANAO NA MKONO

2 Samweli 23:9-10

[9]Na baada yake kulikuwa na Eleazari, mwana wa Dodai, Mwahohi, mmojawapo wa wale mashujaa watatu waliokuwa pamoja na Daudi; walipowatukana Wafilisti waliokuwa wamekusanyika huko ili kupigana, na watu wa Israeli walikuwa wamekwenda zao; 

[10]huyo aliinuka, akawapiga Wafilisti hata mkono wake ukachoka, na mkono wake ukaambatana na upanga; naye BWANA akafanya wokovu mkuu siku ile; nao watu wakarudi nyuma yake ili kuteka nyara tu. 

Kibaolojia mwili wa mwanadamu unapokamata kitu, kwa muda mrefu sana, kwa nguvu, huwa unatabia ya kukakamaa katika hali hiyo hiyo hata kama mtu huyo hatakuwa na nia ya kuendelea kukishikilia kitu hicho.

Ndicho kilichomkuta huyu shujaa wa Daudi, alipokutana na jeshi la wafilisti angali yupo peke yake. Aligundua kitu pekee ambacho kingeweza kumtetea ni upanga wake. Hivyo aliukamata kwa nguvu sana bila kuuachia, akaanza kupambana na wafilisti wale kwa muda mrefu,  hakujua kuwa mkono wake utabakia katika hali ile ile…yeye aliendelea tu kupigana vita, mpaka  baadaye aliposhangaa  kuona hana jitihada yoyote tena ya kuushika upanga, ni kama vile ulikuwa ni sehemu ya kiungo chake…kazi yale ilikuwa ni kurusha tu mkono kuupeleka anapotaka, huku upanga ukiwa tu pale pale kiganjani hautoki…

Kikawaida hali ikishafikia hatua hiyo huwa inamgharimu mtu masaa mengi hata siku,  ili kung’atuka kutoka kwenye kitu kilichoshikamana naye..wakati mwingine ili kuharakisha uponyaji, wengine hutumia maji ya uvuguvugu na kuchua kiganja kwa muda baadaye kunyosha kidole kimoja baada ya kingine…

Sasa askari wa mwilini ni kivuli cha mtu wa rohoni. Yeye naye ana mikono na analazimika wakati wote kuwa na upanga…Lakini si upanga tu, wa kushika, bali ule Ugandao na mkono. 

Waefeso 6:11-14,17

[11]Vaeni silaha zote za Mungu, mpate kuweza kuzipinga hila za Shetani. 

[12]Kwa maana kushindana kwetu sisi si juu ya damu na nyama; bali ni juu ya falme na mamlaka, juu ya wakuu wa giza hili, juu ya majeshi ya pepo wabaya katika ulimwengu wa roho. 

[13]Kwa sababu hiyo twaeni silaha zote za Mungu, mpate kuweza kushindana siku ya uovu, na mkiisha kuyatimiza yote, kusimama. 

[14]Basi simameni, hali mmejifunga kweli viunoni, na kuvaa dirii ya haki kifuani,..

[17]Tena ipokeeni chapeo ya wokovu, na upanga wa Roho ambao ni neno la Mungu; 

Kama maandiko yanavyotuonyesha hapo Mtu wa rohoni, hulazimika kubeba upanga wake, ambao ni Neno la Mungu.

Tunapoonyesha nia ya kuling’ang’ania Neno la Mungu, mwanzoni ni kama tutatumia jitihada zetu, lakini haitakuwa hivyo mbeleni …baadaye litashikamana na sisi..maana yake haitakuwa jitihada tena kuliishi.

Jambo lolote la kiroho, mfano maombi ya masafa marefu, mwanzoni ukianza utaona kama ni jitihada zinatumika lakini ukiendelea mara mbili, mara tatu utaona ni kawaida..

Mambo yote ya rohoni iwe ni upendo, unyenyekevu, utaanza kwa jitihada fulani lakini Kwasababu umekusudia tu kung’ang’nia kwa nguvu, utagandamana navyo.

Kumbuka hakuna wepesi wowote utakuja bila mtu kutia nia kwanza. Anza sasa kutendea kazi Neno la Mungu.

Bwana akubariki.

 

Washirikishe na wengine habari hizi njema kwa kushea

Ikiwa utapenda kupata msaada wa kumpokea Yesu maishani mwako bure, Basi wasiliana nasi kwa namba uzionazo chini ya makala hii.

Pia kwa kupokea mafundisho ya kila siku kwa njia ya WHATSAPP, jiunge na channel yetu kwa kubofya link hii >> https://whatsapp.com/channel/0029VaBVhuA3WHTbKoz8jx10

Kwa mawasiliano: +255693036618 au +255789001312

Bwana akubariki.

Mafundisho mengine:


 

Print this post

ZIDI KUTAFUTA UJAZO WA ROHO MTAKATIFU.

Luka 11:13 “Basi, ikiwa ninyi mlio waovu mnajua kuwapa watoto wenu vipawa vyema, je! Baba aliye mbinguni HATAZIDI SANA KUWAPA ROHO MTAKATIFU HAO WAMWOMBAO?”.

Kufuatana na maandiko haya, ni wazi kuwa Biblia inatufundisha  ujazo wa Roho Mtakatifu ni jambo endelevu siku zote za maisha ya mtu.

Ikiwa na maana kuwa ni lazima kila siku tujazwe Roho Mtakatifu kila siku kwa kipimo kipya, kwani maandiko yasema yeye hamtoi Roho kwa kipimo (Yohana 3:34) na tena yanasema Tujazwe Roho..

Waefeso 5:18 “Tena msilewe kwa mvinyo, ambamo mna ufisadi; BALI MJAZWE ROHO”.

Sasa tunajazwaje Roho Mtakatifu?.

 Si kwa njia nyingine bali kwa kuomba.

Vifuatavyo ni vipengele muhimu katika maombi ya ujazo wa Roho Mtakatifu.

1.      OMBA KUFUNDISHWA NA ROHO MTAKATIFU.

Yohana 14:26 “Lakini huyo Msaidizi, huyo Roho Mtakatifu, ambaye Baba atampeleka kwa jina langu, ATAWAFUNDISHA YOTE…”

Unaposoma BIBLIA, Roho Mtakatifu akawe mwalimu wako katika kulielewa vizuri Neno, tenga muda wa kutosha kumwomba MUNGU akakujaze Roho wake wa ualimu.

Watu waliojaa Roho Mtakatifu kweli kweli, wanajifunza Biblia na kuielewa vizuri kwasababu ndani yao Roho Mtakatifu anawafundisha.

Pia wanakuwa ni watu wenye maisha yaliyostaarabika kwasababu ndani yao wanaye mwalimu anayewafundisha kanuni za maisha.

2.      OMBA KUKUMBUSHWA NA ROHO.

Yohana 14:26 “Lakini huyo Msaidizi, huyo Roho Mtakatifu, ambaye Baba atampeleka kwa jina langu, atawafundisha yote, na KUWAKUMBUSHA YOTE niliyowaambia”.

Kuna mambo uliyowahi pengine kufunuliwa na MUNGU zamani, kwa njia ya Neno au ndoto, na umesahau, unapojaa Roho Mtakatifu, basi atakukumbusha yote aliyekuambia au kukuonesha.

Na sio tu kukumbusha  maneno ya Mungu au maagizo yake bali hata mambo yako mengine ya kimaisha yaliyo ya muhimu, Roho Mtakatifu atakukumbusha na kukutahadharisha.

Hata katika elimu za Dunia, Wanafunzi waliojaa Roho Mtakatifu, ni ngumu kusahau kabisa waliyojifunza, kwani yupo msaidizi ndani yao anayewakumbusha waliyojifunza.

Hali kadhali watu wenye Roho Mtakatifu kweli kweli huwa hawasahau maelekezo au maneno ya Mungu kwani yupo Msaidizi, Roho Mtakatifu anayewakumbusha kila siku.

Kwahiyo tenga muda wa kutosha kuomba unazo wa Roho Mtakatifu ndani yako.

3.      KUONGOZWA NA ROHO.

Yohana 16:13 “Lakini yeye atakapokuja, huyo Roho wa kweli, ATAWAONGOZA awatie kwenye kweli yote….”.

Pia Roho Mtakatifu kazi yake nyingine ni kumwongoza Mtu, nini cha kusema, nini cha kufanya, au ni wakati gani wa kusema na wakati gani wa kunyamaza, ni wakati gani wa kutenda na wakati gani wa kutulia.

Zaidi sana Roho Mtakatifu pia anamwongoza mtu nini cha kusikiliza na nini ambacho hakifai kusikiliza au kufanya..

Na katika maombi pia, Roho Mtakatifu anamwongoza mtu nini cha kuomba na jinsi ya kuomba.

Warumi 8:26 “Kadhalika Roho naye hutusaidia udhaifu wetu, kwa maana hatujui kuomba jinsi itupasavyo…..”.

Kwahiyo tenga muda wa kutosha kuomba Ujazo wa Roho Mtakatifu, ili uweze kunufaika na tunda hili la kuongozwa na Roho.

4.      OMBA KUFUNULIWA NA ROHO MAMBO YAJAYO.

Yohana 16:13 “Lakini yeye atakapokuja, huyo Roho wa kweli, atawaongoza awatie kwenye kweli yote; kwa maana hatanena kwa shauri lake mwenyewe, lakini yote atakayoyasikia atayanena, NA MAMBO YAJAYO ATAWAPASHA HABARI YAKE”.

  Ni muhimu sana kuyajua mambo yajayo yahusuyo maisha yako, kanisa, familia…kwani uishivyo sasa ni kutokana na kile unachokiona mbele yako, na Roho Mtakatifu pekee ndiye awezaye kufunua mambo yajayo ya mtu au watu kwa usahihi.

Kwa mambo haya manne, tutaimarisha  ile safari yetu ya kuenenda kwa Roho.

Wagalatia 5:16 “Basi nasema, Enendeni kwa Roho, wala hamtazitimiza kamwe tamaa za mwili”.

Bwana atusaidie.

 

Washirikishe na wengine habari hizi njema kwa kushea

Ikiwa utapenda kupata msaada wa kumpokea Yesu maishani mwako bure, Basi wasiliana nasi kwa namba uzionazo chini ya makala hii.

Pia kwa kupokea mafundisho ya kila siku kwa njia ya WHATSAPP, jiunge na channel yetu kwa kubofya link hii >> https://whatsapp.com/channel/0029VaBVhuA3WHTbKoz8jx10

Kwa mawasiliano: +255693036618 au +255789001312

Bwana akubariki.

Mafundisho mengine:

Print this post

Kauli ya Bwana ya “Heri kutoa kuliko kupokea” tunaisoma wapi?

Swali: Katika Matendo 20:15, tunasoma Mtume Paulo akirejea kauli ya Bwana kwamba akisema “Heri kutoa kuliko kupokea”.. Je ni wapi katika Injili nne, Bwana YESU alisema maneno hayo?

Jibu: Tuanzie kusoma ule mstari wa 33..

Matendo 20:33 “Sikutamani fedha wala dhahabu, wala mavazi ya mtu.

34 Ninyi wenyewe mnajua ya kuwa mikono yangu hii imetumika kwa mahitaji yangu na ya wale waliokuwa pamoja nami.

35 Katika mambo yote nimewaonyesha ya kuwa kwa kushika kazi hivi imewapasa kuwasaidia wanyonge, NA KUYAKUMBUKA MANENO YA BWANA YESU, JINSI ALIVYOSEMA MWENYEWE, NI HERI KUTOA KULIKO KUPOKEA”.

Katika vitabu vyote vinne vya injili (yaani kitabu cha Mathayo, Marko, Luka na Yohana) hakuna mahali popote pameandikwa  maneno hayo ya Bwana kama yalivyo kwamba “heri kutoa kuliko kupokea”. Lakini ni wazi kuwa aliyasema mahali fulani ila hayakuandikwa katika vitabu vinne vya injili.

Tunalithibitisha vipi hilo?.. Turejee kitabu cha Yohana 21:24..

Yohana 21:24 “Kuna na mambo mengi aliyoyafanya Yesu; ambayo yakiandikwa moja moja, nadhani hata ulimwengu usingetosha kwa vile vitabu vitakavyoandikwa”.

Hapa Mtume Yohana anasema, yapo mambo mengi aliyoyafanya Bwana YESU ambayo hayakuandikwa katika vitabu hivyo..maana yake yapo maneno mengi aliyoyafundisha na mifano mingi na ishara nyingi alizozifanya ambazo laiti kama zingeandikwa moja baada ya nyingine, dunia isingetoshea kwa vitabu..

Kwa mantiki hiyo basi tunaanza kuelewa kuwa maneno hayo ya “heri kutoa kuliko kupokea” ni kweli Bwana YESU aliwahi kuyasema mahali fulani, isipokuwa tu hayakunukuliwa na waandishi wa vitabu vinne vya injili.

Lakini pamoja na hayo, yapo maneno aliyoyasema yenye mlengo huo huo wa “uheri wa kutoa kuliko kupokea”

Luka 6:38 “Wapeni watu vitu, nanyi mtapewa; kipimo cha kujaa na kushindiliwa, na kusukwa-sukwa hata kumwagika, ndicho watu watakachowapa vifuani mwenu. Kwa kuwa kipimo kile kile mpimacho ndicho mtakachopimiwa”.

Hii ni kauli ya Bwana YESU akitufundisha faida za kuwapa watu vitu, kwani tunapotoa ndivyo tutakavyopokea, na si tupokee kwanza na ndipo tutoe.. hiyo ikithibitisha kuwa ni kweli Bwana alifundisha uheri wa kutoa kuliko kupokea, na pia alituonya tujilinde na “uchoyo”.

Luka 12:15  “Akawaambia, Angalieni, jilindeni na choyo, maana uzima wa mtu haumo katika wingi wa vitu vyake alivyo navyo”.

Je umempokea YESU?.. Je una uhakika akirudi leo utakwenda naye?

Kama bado tengeneza maisha yako kwani majira tunayoishi ni ya hatari na parapanda ya mwisho imekaribia sana kulia.

Bwana atusaidie.

 

Washirikishe na wengine habari hizi njema kwa kushea

Ikiwa utapenda kupata msaada wa kumpokea Yesu maishani mwako bure, Basi wasiliana nasi kwa namba uzionazo chini ya makala hii.

Pia kwa kupokea mafundisho ya kila siku kwa njia ya WHATSAPP, jiunge na channel yetu kwa kubofya link hii >> https://whatsapp.com/channel/0029VaBVhuA3WHTbKoz8jx10

Kwa mawasiliano: +255693036618 au +255789001312

Bwana akubariki.

Mafundisho mengine:

Print this post

MAISHA YA IMANI NI KAMA SIFA YA MTI.

Mti una sifa moja, hautembei kutoka sehemu moja Kwenda nyingine, Utaupanda eneo fulani, utaridhika kubakia hapo hapo, haijalishi ni pabaya kiasi gani, utaenda utarudi miaka na miaka utaukuta pale pale, tofauti na viumbe hai vingine, ambavyo vyenyewe, vikiona hali si nzuri ya mahali, huama na Kwenda kutafuta makazi pengine. Lakini Mti hauna sifa hiyo, na bado utaendelea kustawi na kuwepo kwa miaka mingi zaidi ya viumbe hai vingine,  haijalishi ni kipindi gani kitapita.

Siri ya mti ipo wapi?

Jibu ni kwenye mizizi yake. Ijapokuwa hautembei kwa juu, lakini chini unatembea. Kwa juu utauna upo pale pale, lakini kwa chini mizizi yake ina mwendo, kila siku inaendelea katika safari ya huku na huko kutafutia virutubisho na maji.

Ni nini Bwana anatufundisha katika maisha ya mti.

Yeye hutupanda apendako.

Leo hii ni rahisi kulalamika, kwanini nimezaliwa hili taifa, kwanini hili kabila, kwanini hii familia, kwanini hii jinsia, kama ningezaliwa kwenye nchi ile, kabila lile, familia ile yenye Uchumi mkubwa ningekuwa mbali sana, ningestawi vizuri sana, ningeimarika kiroho kwa kasi kubwa mno… Kama umekuwa na Mawazo hayo, basi kuna tatizo la kiufahamu.

Mafanikio ya mwanadamu hayapo katika mazingira yake sasa. Mafanikio yake yapo katika mizizi yake rohoni. Mti ukikosa mizizi, hata uwe kwenye udongo mzuri kiasi gani hauwezi kukua popote.

Kama mwamini fahamu mzizi uliyopewa inauwezo wa kukustawisha popote, isipokuwa sifa yake ni ile ile yaani huwa haionekani kwa juu, hukaa matopeni, na huzidi Kwenda chini kila siku sio kurudi juu. Vivyo hivyo na sisi tujue nguvu yetu ipo rohoni, (pasipoonekana), Na katika unyenyekevu kwa Mungu wetu kila siku, ndivyo tutakavyoleta ustawi mema wa maisha yetu.

Kunyenyekea kiroho ni mjumuiko wa mambo : kumkubali Kristo, kutii maagizo yake (ikiwemo maombi, ushirika), kuliishi Neno, na kumtumikia yeye.

Huko ndiko kurefusha mizizi.

2 Wafalme 19:30

[30]Na mabaki yaliyookoka ya nyumba ya Yuda yatatia mizizi chini, na kuzaa matunda juu. 

Kristo alipaswa aishi Yerusalemu, mji  wenye sifa za kiroho na kisomi, lakini alipelekwa Nazareti , mji mnyonge, lakini huko huko alimzalia Mungu matunda, kwasababu mizizi yake ilienea sana.

Yusufu aliuuzwa utumwani, akawa msikwao, asiye na makazi kule Misri, lakini aliendea kuiimarisha mizizi yake, ijapokuwa kwa nje, hakukuonekana dalili ya badiliko lolote, lakini hatimaye, Mungu akamwinua akawa, mkuu kule kule Misri, Ndivyo ilivyokuwa kwa Danieli, Ayubu na watumishi wa Mungu.

Kabla ya kulalamikia mazingira, jiuliza kwanza je! Mizizi yangu, ipo sawa? Kwasababu haiwezekani mizizi ikawa sawa, mti ukafa. Haiwezekani ukawa mtakatifu halafu ukamezwa na mazingira.

Imarisha kiroho chako.

Shalom.

Ikiwa utapenda kupata msaada wa kumpokea Yesu maishani mwako bure, Basi wasiliana nasi kwa namba uzionazo chini ya makala hii.

Pia kwa kupokea mafundisho ya kila siku kwa njia ya WHATSAPP, jiunge na channel yetu kwa kubofya link hii >> https://whatsapp.com/channel/0029VaBVhuA3WHTbKoz8jx10

Kwa mawasiliano: +255693036618 au +255789001312

Bwana akubariki.

Print this post

MIINGILIANO MINGINE, IPOKEE KAMA MWITO WA KI-MUNGU.

Ni kawaida Mtu mwenye malengo yake au mpangilio wa ratiba zake, mfano  kukatokea mvurugano fulani mambo mengine yakaingilia ratiba zake huwa anakereka sana, na kujiona ameshindwa,  kusimamia maono yake.

Lakini kama mwana wa Mungu, si kila wakati mwingiliano wa vitu, ni kutoka kwa adui. Wakati mwingine ni kwa Mungu, hivyo kuliko kulaumu, kuvunjika moyo au kuchukia embu tulia kisha litazame kama mwito wa ki-Mungu, kutimiza kusudi fulani.

Kwamfano kuna wakati Petro alialikwa kwenye nyumba ya Kornelio, katikati ya somo lake, pengine hata watu hawajaelewa vizuri, Roho Mtakatifu akawashukia watu waliokuwa pale wakaanza kunena kwa lugha kabla hata ya kubatizwa, au kuhubiriwa toba, na kuwekewa mikono.

Kama mhubiri angeweza  kusema, “Naomba kuwe na utulivu” tusikilize Neno, …lakini Petro alibakia tu kushangaa jambo lile, liliwezekanikaje kwa haraka vile kwa mataifa wasiomjua Mungu kujazwa Roho.,Akaendelea kumwacha Mungu afanye kazi zake.

Bwana Yesu hakuwa mtu wa kulaumu au kukatiza kila mvurugano uliokuja mbele yake, bali alijifunza kutulia na kumsikia Mungu, wenda yupo nyuma ya mwingiliano huo.

Kwa mfano Wakati fulani alikuwa anaelekea Tiro na Sidoni kuwatafuta kondoo  waliopotea wa Israelitu, lakini mwanamke mmoja ambaye si mwisraeli aliingilia ziara yake, na kutaka kuhudumiwa…Mwanzoni Yesu hakumsemesha kitu, watu wakasema..achana naye anatupigia kilele, lakini Yeye akatulia kwa muda na kuanza kuhojiana naye..mwishowe akamtendea muujiza ambao mpaka leo tunausoma kama fundisho la imani. Kama angesema achana na mimi, ni marufuku kukusikiliza akaendelea na safari yake…kusudi la Mungu la siku hiyo lisingetimia.

Mathayo 15:22-28

[22]Na tazama, mwanamke Mkananayo wa mipaka ile akatokea, akampazia sauti akisema, Unirehemu, Bwana, Mwana wa Daudi; binti yangu amepagawa sana na pepo. 

[23]Wala yeye hakumjibu neno. Nao wanafunzi wake wakamwendea, wakamwomba, wakisema, Mwache aende zake; kwa maana anapiga kelele nyuma yetu. 

[24]Akajibu, akasema, Sikutumwa ila kwa kondoo waliopotea wa nyumba ya Israeli. 

[25]Naye akaja akamsujudia, akisema Bwana, unisaidie. 

[26]Akajibu, akasema, Si vema kukitwaa chakula cha watoto na kuwatupia mbwa. 

[27]Akasema, Ndiyo, Bwana, lakini hata mbwa hula makombo yaangukayo mezani pa bwana zao. 

[28]Ndipo Yesu akajibu, akamwambia, Mama, imani yako ni kubwa; na iwe kwako kama utakavyo. Akapona binti yake tangu saa ile. 

Miujiza mingi ya Yesu ilifanyika nje ya ratiba alipokuwa njiani kuelekea katika ziara zake, mafundisho mengine aliyafundisha kulingana na matukio aliyopishana nayo, si yale aliyokusudia kuwaambia watu.

Hii ni kuonyesha kuwa na sisi, sehemu kubwa ya mwito wa Mungu unaweza kuwa katika mambo yanayotuingilia kila siku..

Unaweza kupangilia fedha yako, kwa wiki nzima au mwaka mzima ufanyie hivi au vile…lakini ikatokea tu mtoto wa mjomba ni mgonjwa inahitaji fedha ya matibabu, na ukalazimika kuitoa karibu yote, sasa ni rahisi kulalamika mbona nikiweka malengo sifikii…mbona nikipata tu kinatoka…mbona nikipata kitu kinang’ang’aniwa  na wengine, mimi sivitumii.

Kabla hujahuzunika Jifunze kuusikia mwito wa Mungu nyuma ya mivurugano hiyo, kwasababu sehemu kubwa ya maisha yetu ni mivurugano, Na huko huko Mungu hutimiza makusudi yake.

Bwana akubariki.

 

Ikiwa utapenda kupata msaada wa kumpokea Yesu maishani mwako bure, Basi wasiliana nasi kwa namba uzionazo chini ya makala hii.

Pia kwa kupokea mafundisho ya kila siku kwa njia ya WHATSAPP, jiunge na channel yetu kwa kubofya link hii >> https://whatsapp.com/channel/0029VaBVhuA3WHTbKoz8jx10

Kwa mawasiliano: +255693036618 au +255789001312

Bwana akubariki.

Mafundisho mengine:

Print this post

JINA LAKO LIMEANDIKWA WAPI?

Je jina lako limeandikwa wapi?, kwenye nyaraka za umma?, kwenye vitabu vya simulizi?, kwenye vitambulisho vya umma?, kwenye orodha ya wafungwa?, kwenye orodha ya wahalifu?, kwenye vilinge vya wachawi?, kwenye vitabu vya washirika wa kanisa?, kwenye vitabu vya walipa kodi na watoaji zaka?.. au limeandikwa wapi?.

Ni muhimu kujitathmini ni wapi jina lako lipo wapi?.. Kama jina lako litakuwepo kila mahali pa heshima duniani na likakosekana mbinguni, heshima yako ni bure, hadhi yako ni bure, uzuri wako ni bure, umaarufu wako ni bure na nguvu zako ni bure.

Hata kama jina lako litakuwa limeandikwa Kanisani, kama mtoaji mzuri, au mshirika mzuri bado kama halipo mbinguni wewe au mimi si kitu kabisa.

Kama kanisa lina washirikia efu, na hakuna hata mmoja aliyeandikwa mbinguni bado hilo kanisa ni bure, ndivyo Biblia inavyotufundisha kuwa kanisa halisi ni la watu waliondikwa majina yao mbinguni.

Waebrania 12:23 “Mkutano mkuu na KANISA LA WAZALIWA WA KWANZA WALIOANDIKWA MBINGUNI, na MUNGU MWAMUZI WA WATU WOTE, na roho za watu wenye haki waliokamilika”.

Hata mtu akitenda miujiza mingi na miujiza  na akafanikiwa sana na akafurahi na kushangilia kama jina lake halipo mbinguni bado ni kazi bure..

Luka 10:20 “Lakini, msifurahi kwa vile pepo wanavyowatii; bali furahini KWA SABABU MAJINA YENU YAMEANDIKWA MBINGUNI”.

Je jina lako limeandikwa mbinguni?.. Utauliza je jina la mtu linaandikwaje mbinguni?

Ndio jina la mtu linaandikwa mbinguni baada ya kuzaliwa mara ya pili, maana yake kuokoka na kuacha dhambi na kuishi maisha matakatifu yanayompendeza MUNGU, lakini pia jina la mtu linaweza kufutwa mbinguni ikiwa mtu huyo atarudi nyuma na kuiacha ile njia nyoofu ya usafi na utakatifu.

Kutoka 32:33 “Bwana akamwambia Musa, Mtu ye yote aliyenitenda DHAMBI NDIYE NITAKAYEMFUTA KATIKA KITABU CHANGU”.

Je umeokoka na kusimama?.. au maisha yako ni ya uvuguvugu?, leo upo kanisani kesho kwenye vijiwe vya usengenyaji?.. leo unaomba kesho unakula rushwa?, leo unamwimbia Mungu kesho unamwimbia ibilisi, simu yako imejaa uchafu na wakati huo huo ina nyimbo za injili.

Fahamu maisha ya uvuguvugu yanaondoa jina lako kwenye kile kitabu cha uzima, maisha ya kusita sita kumtafuta MUNGU yanalifuta jina lako mbinguni, na siku ya mwisho ni majina yetu ndiyo yatakayotafutwa ndani ya kile kitabu cha uzima, na si picha zetu, wala sifa zetu, wala umaarufu wetu…na majina yakikosekana hakuna nafasi ya kuingia malango ya mbinguni.

Ufunuo 20:15 “Na iwapo mtu ye yote hakuonekana ameandikwa katika kitabu cha uzima, alitupwa katika lile ziwa la moto”.

Bwana atusaidie tuweze kusimama na kuishi maisha ya kumpendeza yeye daima.

Shalom.

 

Washirikishe na wengine habari hizi njema kwa kushea

Ikiwa utapenda kupata msaada wa kumpokea Yesu maishani mwako bure, Basi wasiliana nasi kwa namba uzionazo chini ya makala hii.

Pia kwa kupokea mafundisho ya kila siku kwa njia ya WHATSAPP, jiunge na channel yetu kwa kubofya link hii >> https://whatsapp.com/channel/0029VaBVhuA3WHTbKoz8jx10

Kwa mawasiliano: +255693036618 au +255789001312

Bwana akubariki.

Mafundisho mengine:

Print this post

JINSI MWANADAMU ANAVYOUHARIBU USO WAKE.

Zawadi kubwa na ya kipee alipewa  mwanadamu na Mungu, iliyomtofautisha na viumbe vingine vyote, (vya mbinguni na duniani) basi ni Uso wa Mungu.

Ni mwanadamu pekee ndiye aliyeumbwa kwa mfano na sura ya Mungu (Mwanzo 1:27-28).

Biblia inaposema sura, inafananisha na mfano wa kioo,  pale mtu anapojitazama kwenye kioo, anaiona taswira yake vilevile kama yeye alivyo, ikiwa ni mwenye chunusi, basi ataiona chunusi yake kwenye kile kioo, ikiwa ni mweupe vivyo hivyo ndivyo atakavyojiona.

Kwahiyo sisi ni taswira ya Mungu kabisa, lakini ifahamike kuwa taswira hiyo sio hii ya nje, yaani pua, mdogo, masikio, hapana bali ile ya ndani, yaani tabia na sifa alizonazo Mungu, sisi pia tunazo.

Sasa kazi kubwa ya shetani, aliyokuwa nayo kwa Mwanadamu ni kumbadilisha SURA yake. Ili ifanane na kitu kingine tofauti na Mungu.

Na alijua njia pekee na kubwa ambayo hubadili taswira ya mtu, ni IBADA.

Yaani kile ambacho mwanadamu anakiabudu basi moja kwa moja hufanana nacho, wala si kile anachokitazama, au anachokishika, au anachokiangalia Hapana bali kile akifanyiacho ibada, moja kwa moja kinambadilisha taswira yake.

Ndio maana amri ya kwanza na ya pili ambayo Mungu aliwapa watu wake (Kutoka 20), ni kuhakikisha hawajifanyii sanamu ya kuchonga ya aina yoyote na kuiabudu, wala hawawi na miungu mingine, ila yeye.

Kwanini? Kwasababu wamwabudupo yeye, hudumisha tabia zake, na mwonekano wake ndani yao.Lakini wanadamu walipoanza kuabudu miungu, mfano wa Baali, Arishtoreth, n.k. hawakujua kwamba moja kwa moja wanafanana nazo.

Zaburi 115: 4-8

4 Sanamu zao ni fedha na dhahabu, Kazi ya mikono ya wanadamu.
5 Zina vinywa lakini hazisemi, Zina macho lakini hazioni,
6 Zina masikio lakini hazisikii, Zina pua lakini hazisikii harufu,
7 Mikono lakini hazishiki, miguu lakini haziendi, Wala hazitoi sauti kwa koo zake.
8 WAZIFANYAO WATAFANANA NAZO, Kila mmoja anayezitumainia

Maandiko yanasema hapo, wazifanyao, hufanana nazo, maana yake Walikuwa vipofu rohoni, viziwi rohoni, wamepooza, kabisa, hawana uhai, ndio maana hata walipokuwa wakihubiriwa Habari za hukumu na manabii hawakuelewa wala kuona ni kitu, hata Kristo alipokuja duniani bado hawakutambua wakati wa kujiliwa kwao, sio kwamba walikuwa wanafanya makusudi, lakini ni kwasababu waliabudu miungu isiyo hai, waliabudu mashetani yasiyojua kesho yao itakuwaje, mizimu isiyojua amani ya kweli ina Ladha gani, mapepo yasiyoweza kuganga mioyo ya watu, mwishowe wakafanana nao, wakawa wakatili, wauaji, wenye wivu .

Lakini tunaposoma biblia tunadhani sanamu ziliabudiwa zamani tu, Hapana, hata sasa sanamu zipo, ambapo zinawakilishwa na vitu vyote vinavyochukua nafasi ya Mungu katika mioyo ya wanadamu.

Fedha, ni sanamu, ukiiabudu ujue utafanana nayo, simu/TV yaweza kuwa sanamu, inapochukua muda wako mwingi, kutazama maudhui zake, na kuacha kabisa kumtafuta Mungu, umeshakuwa mfu hata kama unatembea,  mtu anaweza kuwa sanamu, unapomtegemea yeye zaidi ya Mungu, hapo hesabu umelaaniwa.

Lakini unapomwabudu Mungu, yaani unapomtegemea, unapomtii, unapomtumikia, unapomsujudia, ufahamu kuwa ndivyo unavyofanana na yeye, na hatimaye utakuwa hai kama yeye alivyo hai, sikuzote. Mungu anaishi milele, na wewe vivyo hivyo, Mungu ni mweza, na wewe utakuwa vivyo hivyo, Mungu ni mwenye upendo na wewe utakuwa kama yeye. Mungu ni mtakatifu, ni wa rehema, ndivyo na wewe utakuwa kama yeye. Ibada yako kwa Mungu isiibiwe na kitu chochote.

Bwana akubariki.

 

Washirikishe na wengine habari hizi njema kwa kushea

Ikiwa utapenda kupata msaada wa kumpokea Yesu maishani mwako bure, Basi wasiliana nasi kwa namba uzionazo chini ya makala hii.

Pia kwa kupokea mafundisho ya kila siku kwa njia ya WHATSAPP, jiunge na channel yetu kwa kubofya link hii >> https://whatsapp.com/channel/0029VaBVhuA3WHTbKoz8jx10

Kwa mawasiliano: +255693036618 au +255789001312

Bwana akubariki.

Mafundisho mengine:

KUSUDI LA MUNGU NYUMA YA SAFARI.

AINA ZA FARAJA BWANA AZIACHILIAZO KWA WATUMISHI WAKE.

MTU WA NNE, ANADHIHIRISHWA KWA MOTO

Print this post

WATAKATIFU BABELI.

Moja ya ombi kubwa la watu wa Mungu, pale wanapojikuta wameokoka, ni kubadilishwa mazingira waliyopo, wapelekwe kwenye mazingira mengine yenye uwepo wa karibu zaidi na Mungu, Kwasababu wakiangalia kwa sehemu kubwa mambo ambayo yanawakosesha huchangiwa na mazingira yao. Mazingira husika yanaweza kuwa mitaa wanayoishi, shule wanazosoma, maeneo ya kazi/ biashara walipo, watu wanaowazunguka, hata nchi yanayotokea.

Hii ni hali ya kawaida, na hufikia hatua wengi kuwaza mioyoni mwao, “Kama ningekuwa eneo Fulani, basi ningekuwa na mahusiano ya karibu na Mungu, ningekuwa mwombaji sana, ”

Lakini Je! Kuwaza hivyo ni sahihi?

Ndio kuwaza kubadilishwa mazingira yanayokosesha, ni vema, lakini kuwaza kuwa Hapo ulipo huwezi kumpendeza Mungu kwa viwango vyote ni uongo,. Kwasababu maandiko yanatuonyesha Mungu amewaweka watumishi wake katika mazingira yote, yaani mazingira rafiki na yale yasiyo rafiki, kwa mapenzi yake, na kuthibitisha kuwa kote kote, kumpendeza Mungu kunawezekana. Kwasababu dunia moja.

Bwana aliwaweka watakatifu Babeli, alikuwepo Shedraka, Meshaki, Abednego na Danieli.

Hawa waliishi katika taifa la kipagani usiokuwa wa kawaida,ni taifa lenye shinikizo kubwa la mtu kuabudu miungu hata kama hapendi, lenye mikorogo ya kila namna ya maovu. Lakini watu hawa walisimama vema na Bwana.

Waliwezaje?

Yafuatayo ni mambo ambayo yaliyatenda mpaka ufanikiwa kuishi katika viwango vyote vya ukamilifu.

1) Waliitangaza Imani yao mapema.

Mwanzoni kabisa akina Danieli walipochukuliwa Babeli, na kusomeshwa elimu ya wakaldayo,tunaona walipewa vyakula ambavyo ni najisi, lakini Danieli alisimama mapema na kumwomba msimamizi, kulishwa vyakula vingine visivyo najisi. Na Mungu akawa Pamoja nao. Wakatambulika tangu mapema kuwa wao ni watumishi wa wayahudi wasiojichangamana na desturi za kimataifa.

Hawakungoja, miaka ipite baadaye..bali mezani tu, wanaanza kutangaza misimamo yao.

Danieli 1:8-9

[8]Lakini Danieli aliazimu moyoni mwake ya kuwa hatajitia unajisi kwa chakula cha mfalme, wala kwa divai aliyokunywa; basi akamwomba yule mkuu wa matowashi ampe ruhusa asijitie unajisi. 

[9]Basi Mungu alimjalia Danieli kupata kibali na huruma machoni pa huyo mkuu wa matowashi. 

Hii ni desturi ambayo na sisi, kama watoto wa Mungu babeli, tuwapo katikati ya wasioamini, tujitambulishe mapema. Hiyo itasaidia sana wao kutokukuhusisha katika matendo yao ya giza wakijua kuwa wewe ni mwamini.

Wengi wameshindwa kung’atuka katika mazingira mabovu kwasababu ya kushindwa kujitambulisha wao ni akina nani, kwa wanaowazunguka.

2) Walikuwa waombaji

Danieli akiwa Babeli, alijijengea desturi na kutwa mara tatu, kupiga magoti na kuomba, akijua kuwa nguvu ya kusimama na kuendelea mbele ilitegemea sana maombi…

Ijapokuwa alikuwa na majukumu makubwa kama waziri katika taifa lakini hakuruhusu muda wake mahususi wa maombi kuibwa.

Danieli 6:10

[10]Hata Danieli, alipojua ya kuwa yale maandiko yamekwisha kutiwa sahihi, akaingia nyumbani mwake, (na madirisha katika chumba chake yalikuwa yamefunguliwa kukabili Yerusalemu;) akapiga magoti mara tatu kila siku, akasali, akashukuru mbele za Mungu wake, kama alivyokuwa akifanya tokea hapo. 

Vivyo hivyo na sisi tuwapo popote pasipofaa, hatuwezi sema hatuna muda wa sala. Ikiwa umebanwa upo muda wa chakula cha mchana kazini unaweza tumika nafasi kusogea mahali tulivu na kuomba.

3) Walikubali kujitwika misalaba yao.

Kujitwika msalaba maana yake ni kukubali kuipokea imani kwa gharama yoyote ile, yaani kama ikitokea nitatengwa kwasababu ya imani yangu, nitafungwa, nitauawa..Je nipo tayari?

Ndivyo ilivyokuwa kwa Meshaki, shedraka, Abednego, Danieli, Yusufu.

Wote hawa walikubali kutupwa kwenye matanuru ya moto, kwenye magereza, matanuru ya simba, walipojaribiwa.

Vivyo hivyo na sisi, lazima tufahamu mapema kuwa, imani haipendwi, ulimwengu sio rafiki kwetu, kama ikitokea tunalazimishwa kuikana imani je! Tutachukua hatua gani?

Wengine wameshindwa na majaribu mbalimbali ya Babeli, wameanguka katika uzinzi,wizi, upagani kwa sababu tu ya kuhofia kupoteza kazi zao, familia zao, heshima zao, mali zao, uhai wao.

Ili uweza kuishi vema Babeli, ufahamu huu wa kujitwika msalaba ni lazima uwe nao tangu mwanzo kabisa wa kuamini kwako. Kumbuka sikuzote nguvu ya kuushinda ulimwengu upo katika msalaba.

4) Waliwajibika kwa bidii na uaminifu.

Utaona hawakuwa wavivu, au walegevu, au watu wasiokuwa na shughuli zao maalumu, bali waliwajibika..Danieli pamoja na wenzake walisoma ili kupata elimu na kuwajibika katika shughuli za kifalme mpaka wakaonekana hakuna wa kufanana na wao kwa hekima na ujuzi, 

Yusufu naye alisimama kwenye majukumu yake, wala hakuna mahali alionekana mlegevu. Na wote hawa walitanguliza uaminifu.

Walijua kabisa kutowajibika ni mlango mwingine wa shetani, kuinua majaribu.

Waefeso 4:27-28

[27]wala msimpe Ibilisi nafasi. 

[28]Mwibaji asiibe tena; bali afadhali afanye juhudi, akitenda kazi iliyo nzuri kwa mikono yake mwenyewe, apate kuwa na kitu cha kumgawia mhitaji. 

Hivyo na sisi pia tuwapo kwenye Babeli zetu, tuwe makini kuwajibika kwa bidii na uaminifu, tuepuke uvivu, kama watoto wa Mungu ni wajibu kujishughulisha.

Tukifanikiwa kuwa na uwiano huo mzuri, Neema ya Mungu itatusaidia.

Bwana akubariki.

Ikiwa utapenda kupata msaada wa kumpokea Yesu maishani mwako bure, Basi wasiliana nasi kwa namba uzionazo chini ya makala hii.

Pia kwa kupokea mafundisho ya kila siku kwa njia ya WHATSAPP, jiunge na channel yetu kwa kubofya link hii >> https://whatsapp.com/channel/0029VaBVhuA3WHTbKoz8jx10

Kwa mawasiliano: +255693036618 au +255789001312

Bwana akubariki.

Mafundisho mengine:

MNARA WA BABELI

Ipi tofauti ya Falme, Mamlaka na Wakuu wa giza (Waefeso 6:12)

KWA KUWA FURAHA YA BWANA NI NGUVU ZENU. 

Print this post