Category Archive Mafundisho

WATU WALIOINGIA  KAANANI, LAKINI SI NCHI YA AHADI.

Nuru ya UpendobibliayetuEdit Profile

Wana wa Israeli walitoka kweli Misri, na Mungu akawaahidia kuwa mbele yao wamewekewa nchi njema ibubujikayo maziwa na asali, nchi yenye raha, na ya kustarehe (Kutoka 3:8). Na kweli wakaifikia hiyo nchi, waliyoahidiwa lakini biblia inasema hawakuipata ile raha aliyoikusudia Mungu.

Waebrania 4:8-10

Maana kama Yoshua angaliwapa raha, asingaliinena siku nyingine baadaye.
Basi, imesalia raha ya sabato kwa watu wa Mungu.
10 Kwa maana yeye aliyeingia katika raha yake amestarehe mwenyewe katika kazi yake, kama vile Mungu alivyostarehe katika kazi zake.

Walidhani, wingi wa utajiri walioukuta, na ardhi yenye rutuba, na chakula kingi walichokutana nacho huko ndiyo raha yenyewe, lakini kumbe sio.  Mungu alikuwa amewawekea Raha yake maalumu, ambayo wao walikuwa hawaithamini.

Raha yenyewe ilikuwa ni YESU KRISTO.

Mathayo 11:28

28 Njoni kwangu, ninyi nyote msumbukao na wenye kulemewa na mizigo, nami nitawapumzisha.
29 Jitieni nira yangu, mjifunze kwangu; kwa kuwa mimi ni mpole na mnyenyekevu wa moyo; nanyi mtapata raha nafsini mwenu;

Mathayo 12:8

Kwa maana Mwana wa Adamu ndiye Bwana wa sabato.

Tangu wakiwa jangwani, Yesu alianza kujidhihirisha kwao kwa njia ya maumbo, na ishara,  lakini walimkataa, mfano ule mwamba waliounywea alikuwa ni Kristo (1Kor 10: 4:3), yule nyoka wa shaba  aliyeinuliwa (Yohana 3:14-17) alikuwa ni Kristo, ile Mana alikuwa ni Kristo (Yohana 6:48-58), Jinsi ile hema ya kukutania ilivyokuwa imepangiliwa, makabila yote kuzunguka hema, huchora umbo la msalaba, ilikuwa ni msalaba wa Kristo.

Hivyo Kristo alikuwa tayari ni raha yao, Hivyo hata walipokuwa wanaingia katika nchi ya Ahadi wamengemwona kwa maumbile mengi yaliyo bora kuliko yale, akiwaponya kimiujiza, akiwapa raha nafsini mwao, kwa kuwatiririshia  maji ya uzima mioyoni mwao, maziwa na asali yangeyaona halisi kabisa nafsini mwao, starehe wangeifikia, mpaka atakapotokea mwenyewe halisi katika mwili, ili kuubadilisha mfumo wa ulimwengu mzima kuwa milki ya Mungu.

Lakini baada ya kufika kwenye ile nchi walimpinga, sana, hata alipowatuma manabii wake bado hawakuwasikiliza, hatimaye, wakabakia tu Kaanani lakini sio rahani. Jambo hilo liliendelea kwa maelfu ya miaka, mpaka yeye mwenyewe Kristo alipochukua mwili na kuja katikati yetu,

Na tunaona wote waliompokea, waliingizwa kwenye Raha hii halisi, ambayo kwanza inaanza kwa kuwekwa huru mbali na utumwa wa dhambi, Lakini pia kujazwa Roho Mtakatifu, ndani yake ili kuruhusu badiliko kubwa kutokea ili kumfanya mtu aone kumpata Mungu ni raha zaidi ya fahari na mali zote za dunia.

Raha hii inaendelea ndani ya waamini, mpaka leo, na hadi Atakaporudi mara ya pili kuitimiza kwa ukamilifu wote wa macho kwa kutuingiza kwenye ile Mbingu mpya na nchi mpya, aliyotuandalia.

Hivyo kwasasa  tumekabidhiwa jukumu la kuitunza, kwasababu tusipodumu ndani ya Kristo haijalishi tumeingia Kaanani kwa kubarikiwa mwilini, kiasi gani, pengine kiafya, ki-makazi au vinginevyo, haitufaidii kitu, bado tupo matesoni na utumwani. Ni wajibu wetu kuhakikisha nyakati zote tunadumu ndani ya Kristo, ili tukifikishwe kwenye kilele cha raha hiyo atakaporudi.

Waebrania4:1-11

Basi, ikiwa ikaliko ahadi ya kuingia katika raha yake, na tuogope, mmoja wenu asije akaonekana ameikosa.
Maana ni kweli, sisi nasi tumehubiriwa habari njema vile vile kama hao. Lakini neno lile lililosikiwa halikuwafaa hao, kwa sababu halikuchanganyika na imani ndani yao waliosikia.
Maana sisi tulioamini tunaingia katika raha ile; kama vile alivyosema, Kama nilivyoapa kwa hasira yangu, Hawataingia rahani mwangu:
Kwa maana ameinena siku ya saba mahali fulani hivi, Mungu alistarehe siku ya saba, akaziacha kazi zake zote;
na hapa napo, Hawataingia rahani mwangu.
Basi, kwa kuwa neno hili limebaki kwamba wako watu watakaoingia humo, na wale waliohubiriwa habari ile zamani walikosa kuingia kwa sababu ya kuasi kwao,
aweka tena siku fulani, akisema katika Daudi baada ya muda mwingi namna hii, Leo; kama ilivyonenwa tangu zamani, Leo, kama mtaisikia sauti yake, Msifanye migumu mioyo yenu.
Maana kama Yoshua angaliwapa raha, asingaliinena siku nyingine baadaye.
Basi, imesalia raha ya sabato kwa watu wa Mungu.
10 Kwa maana yeye aliyeingia katika raha yake amestarehe mwenyewe katika kazi yake, kama vile Mungu alivyostarehe katika kazi zake.
11 Basi, na tufanye bidii kuingia katika raha ile, ili kwamba mtu ye yote asije akaanguka kwa mfano uo huo wa kuasi.

Hama Kaanani, zama rahani mwa Kristo.

Shalom.

Washirikishe na wengine habari hizi njema kwa kushea

Ikiwa utapenda kupata msaada wa kumpokea Yesu maishani mwako bure, Basi wasiliana nasi kwa namba uzionazo chini ya makala hii.

Pia kwa kupokea mafundisho ya kila siku kwa njia ya WHATSAPP, jiunge na channel yetu kwa kubofya link hii >> https://whatsapp.com/channel/0029VaBVhuA3WHTbKoz8jx10

Kwa mawasiliano: +255789001312 au +255693036618

Bwana akubariki.

 

KUSHURUTISHWA PIA NI SEHEMU YA HUDUMA YAKO.

Mungu anapotaka kumwinua mtu, si kila wakati atampa machaguzi fulani, au atamwagiza kiupendo, bali wakati mwingine atamshurutisha katika jambo ambalo halitaki kabisa, au hajawahi kulifanya, na hapa ndipo wengi hukimbia,

Simoni mkirene, alikuwa ni mkulima tu, akiendelea katika kazi zake za kilimo, lakini ghafla, alikamatwa na kutikwa msalaba ambao si wake,

Ni wazi kabisa hilo jambo halikumpendeza moyoni, na alionyesha ukinzani, ndio maana biblia inasema wakamshurutisha, lakini baadaye ilimbidi akubali tu, Bila kujua kuwa ndio heshima yake, ukuu wake, baraka zake zilipo.

Marko 15:21 Wakamshurutisha mtu aliyekuwa akipita, akitoka mashamba, Simoni Mkirene, baba yao Iskanda na Rufo, ili auchukue msalaba wake.

Shuruti maana yake ni kulazimishwa, kufanya matakwa magumu ya mtu mwingine.

Hakuna mtu anayependa shuruti, kulazimishwa kutenda, mambo ambayo hujajiandaa nayo, huna mapenzi nayo, huna nguvu nayo.  Lakini fahamu kuwa kwa Mungu shuruti ni sehemu ya kukuzwa kwako kiroho,

Wakati mwingine Mungu anapoweka shuruti kwa wazazi wako, viongozi wako, wachungaji wako, Maadamu ni jema, tii tu hata kama hujisikii, ukishurutishwa kufunga na kuomba, usiseme mimi sijisikii wakati huu, fungeni nyie, ukishurutishwa kutoa huduma fulani, usiseme mimi sijajiandaa, bado ni mchanga kiroho, ukishurutishwa kuhudhuria darasa fulani usiwe na udhuru mwingi, ukasema nina ratiba zangu. Tii tu hata kama utaathirika kwenye mambo mengine, kwasababu Mungu huwatumia wao bila kujua, kukuinua kiroho na kihuduma.

Kama Simoni mkirene angegoma kabisa, leo hii tungemjulia wapi, lakini mpaka sasa vizazi vyote vinamjua na kumwona heri kwa kutenda tu hiyo huduma ambayo haikuwa machaguzi yake.

Watumishi wengi makanisani, wanaokuwa kihuduma ukichunguza kwa ukaribu utaona  ni wale ambao wanapopewa majukumu yaliyo nje ya mipango yao, au zaidi ya uwezo na nafasi zao, huyapokea na kuyasimamia kikamilifu bila udhuru, bila kiburi.

Kubali shuruti za Bwana.

Shalom.

Washirikishe na wengine habari hizi njema kwa kushea

Ikiwa utapenda kupata msaada wa kumpokea Yesu maishani mwako bure, Basi wasiliana nasi kwa namba uzionazo chini ya makala hii.

Pia kwa kupokea mafundisho ya kila siku kwa njia ya WHATSAPP, jiunge na channel yetu kwa kubofya link hii >> https://whatsapp.com/channel/0029VaBVhuA3WHTbKoz8jx10

Kwa mawasiliano: +255789001312 au +255693036618

Bwana akubariki.

NABII ALIYEHUDUMIWA NA NYUNI MCHAFU

Eliya alipoagizwa na Mungu kuzifunga mbingu kwa miaka mitatu na miezi sita, aliagizwa aelekee, karibu na kijito cha kedroni, na huko Mungu atamuhudumia kupitia kunguru kumleta mkate na nyama, asubuhi na jioni.

1 Wafalme 17:2-6

[2]Neno la BWANA likamjia, kusema,

[3]Ondoka hapa, geuka, uende upande wa mashariki, ujifiche karibu na kijito cha Kerithi kinachokabili Yordani.

[4]Itakuwa utakunywa maji ya kile kijito; nami nimewaamuru kunguru wakulishe huko.

[5]Basi akaenda akafanya kama alivyosema BWANA; kwa kuwa akaenda akakaa karibu na kijito cha Kerithi, kinachokabili Yordani.

[6]Kunguru wakamletea mkate na nyama asubuhi, na mkate na nyama jioni, akanywa maji ya kile kijito.

Unaweza ukajiuliza kwanini hakumwagizia malaika wake kama alivyomfanyia wakati ule anaelekea mlima Herobu (1Wafalme 19:4-8), au kwanini asimwagizie mtumishi wake, au mnyama safi kama huwa (njiwa), kinyume chake anamuagizia kunguru mnyama mchafu na najisi.

Kwa wakati ule ndege hawa waliwekwa miongoni mwa ndege wachafu wa hali ya juu sana. Hivyo chochote kilichoguswa na wanyama hawa hakikuliwa..lakini Mungu alimwagiza Kunguru huyo huyo amletee Eliya chakula.

Mara nyingi njia na kanuni za Mungu hazichunguziki, Si kila wakati Mungu atatumia watu wema sana, kama tunavyodhani kutuhudumia kimahitaji.

Kunguru hajui kusoma, hakujui kuandika, lakini alisikia agizo la Mungu.

Watu hawa rohoni si lazima wajue theolojia, wajue kanisa, wajue njia za haki, lakini Mungu akiwaamuru, watafanya tu.

Kwanini Mungu anafanya hivi wakati mwingine, ni kutushusha kiburi chetu, na kumwachia hukumu yote yeye mwenyewe.

Mungu anaweza kumwagiza mtu wa dini nyingine, kuisapoti huduma yako. Lakini hilo lisimaanishe kwamba Mungu amemkubali..

Anaweza kutumia maskini, kukutoa mahali fulani na kukupeleka kwingine, anaweza tumia mtu nje ya duara lako, kutenda kitu kwako wewe mwana wa Mungu.

Huyo unayemdhania kwenye akili yako, anaweza asifanye, yule usiyekuingia akilini ndio akatumiwa kufanya.

Eliya angeweza kusema Aah! Bwana…umeshindwa kuniletea Gabrieli, mbona nisingenajisika, lakini Bwana anasema kunguru ndiye nimemwagiza kwako.

Swali, vipi kama kunguru ndiye anayekufadhili kwasasa…Je utamlaumu Bwana?

Kumbuka uumbaji wote bado unamtii Mungu, haijalishi umetengwa naye, kwa umbali mrefu kiasi gani. Bado ni milki ya Bwana.

Mjue sana Mungu ili uwe na amani!

SALA.

Bwana Yesu! Asante kwa kunifumbua macho yangu na kunijuza kuwa ulimwengu wote unakutii wewe, naomba niwe mwepesi kupokea neema zako mbalimbali kwa namna ambayo zinatimiza mapenzi yako, bila mimi kunajisika. Asante kwa hilo, nimeamini, nimepokea. Amen.

Shalom.

Washirikishe na wengine habari hizi njema kwa kushea

Ikiwa utapenda kupata msaada wa kumpokea Yesu maishani mwako bure, Basi wasiliana nasi kwa namba uzionazo chini ya makala hii.

Pia kwa kupokea mafundisho ya kila siku kwa njia ya WHATSAPP, jiunge na channel yetu kwa kubofya link hii >> https://whatsapp.com/channel/0029VaBVhuA3WHTbKoz8jx10

Kwa mawasiliano: +255789001312 au +255693036618

Bwana akubariki.

BWANA, UNATUACHAJE?

Kuna  kauli ambayo tunayo sana kwenye vinywa vyetu…Hususani pale boss au kiongozi wetu anapomalizana nasi katika mpango fulani na kutuaga..tunasema “bwana unaniachaje”?

Maana yake, baada ya kukaa chini yake muda mrefu, au kumtumikia, kuna namna anapaswa akuandalie mazingira ya kukufanya uendeleze lile jambo lake, au lako mwenyewe.. ndio hapo utaona wanawaachia watumwa wao aidha viinua mgongo, mitaji, au fedha za matumizi. 

Hili linaonekana ni jambo zuri kufanywa na bwana au kiongozi yeyote mwenye busara. 

Lakini kwa Yesu mambo yalikuwa tofauti, kwenye kauli yake ya mwisho alipokuwa anapaa.. Mitume hawakuachwa na lolote, na zaidi wanaambiwa wakashuhudie habari zake kutoka pale Yerusalemu walipo, waende uyahudi, Samaria na mpaka mwisho wa nchi.

Ukitafakari kwa ukaribu jambo hilo linahitaji rasilimali nyingi za kifedha, kiuchumi n.k. lakini hawakuachiwa hata senti kumi.

Ukiwa na mawazo kuwa kiongozi wako wa kiroho akuandalie rasilimali za kujikimu kimaisha, ndio ukamtumikie Bwana vizuri, ndugu utavunjika moyo..kwasababu yeye mwenyewe alipoitwa hakuandaliwa rasilimali, Na hilo halikuanzia kwake, lilianzia kwa mitume, hadi kwa wote waliofuata baadaye yao. Tena ungekuwepo nyakati za mitume ungevunjika moyo mara kumi zaidi.

Kumbuka Yesu anaonekana kama  “Bwana mgumu” kwa baadhi ya watumwa. Usipokuwa makini unaweza kumwona pia hivyo.

Kivipi?

Mkumbuke yule aliyepewa talanta moja aliona ameachwa bila màandalizi mazuri kimtaji…akabakia tu kulalamika na kusema huyu Bwana wangu ni mgumu sana.… hii talanta moja aliyoniachia  nitafanyia nini, Hata chakula cha siku moja tu hainitoshi, Bado anataka nimletee vingi, anataka kuvuna asipopanda… Ninakwenda kumwekea pesa yake. Nikafanye mambo yangu akirudi nimpe sitaki lawama.

Hakujua uamuzi huo ni kosa kubwa..

Luka 19:20-26

[20]Akaja mwingine akasema, Bwana, hili ndilo fungu lako, ambalo nililiweka akiba katika leso. 

[21]Kwa maana nilikuogopa kwa kuwa u mtu mgumu; waondoa usichoweka, wavuna usichopanda. 

[22]Akamwambia, Nitakuhukumu kwa kinywa chako, mtumwa mwovu wewe. Ulinijua kuwa ni mtu mgumu, niondoaye nisichoweka, na kuvuna nisichopanda; 

[23]basi, mbona hukuiweka fedha yangu kwa watoao riba, ili nijapo niipate pamoja na faida yake? 

[24]Akawaambia waliosimama karibu, Mnyang’anyeni hilo fungu, mkampe yule mwenye mafungu kumi. 

[25]Wakamwambia, Bwana, anayo mafungu kumi. 

[26]Nawaambia, Kila aliye na kitu atapewa, bali yule asiye na kitu atanyang’anywa hata alicho nacho. 

Ukiona unasubiri ufanyiwe na Yesu kwanza kitu fulani ndipo uwe na hamasa ya kuifanya kazi. 

Kuwa makini. ROHO MTAKATIFU TAYARI YUPO NDANI YAKO UMESHAPEWA. Hakuna kingine zaidi ya hiko.  Simama kwenye huduma yako, Timiza utume wako.

Shalom.

Washirikishe na wengine habari hizi njema kwa kushea

Ikiwa utapenda kupata msaada wa kumpokea Yesu maishani mwako bure, Basi wasiliana nasi kwa namba uzionazo chini ya makala hii.

Pia kwa kupokea mafundisho ya kila siku kwa njia ya WHATSAPP, jiunge na channel yetu kwa kubofya link hii >> https://whatsapp.com/channel/0029VaBVhuA3WHTbKoz8jx10

Kwa mawasiliano: +255789001312 au +255693036618

Bwana akubariki.

FUNDISHO, NI KUSEMA NENO USILOLIJUA

Ubora wa Kuhubiri au kufundisha haupimwi kwa elimu kubwa ya biblia, au mifano mizuri, au utashi fulani wa kupangilia maneno. Hapana, bali ni uwezo wa kupenya katika mioyo ya watu.

Haimaanishi kuwa na elimu ya biblia haichangii ubora wa fundisho au hubiri..inachangia sana lakini hiyo ni kama gamba la juu sana..ambalo linaweza lisitoe pia matokeo yoyote.

Pale fundisho linapoweza kuingia ndani ya moyo wa mtu, kupambanua, kuchoma, kulainisha, kupindua-pindua, kukarabati, kuponya hadi kumfanya mtu kuwa na mwitikio wa dhahiri wa nje. Hilo ndio linaitwa fundisho au hubiri kibiblia.

Sasa tendo hilo mpaka kufikiwa, si jambo rahisi hata kidogo, hakuna utashi wa kibinadamu unaweza kufanya hivyo.

Kwasababu hakuna anayejua ndani ya mtu mwingine kuna nini?

Lakini lililo gumu zaidi ni kuwa hata yeye mwenyewe hajijui vema, kama anahitaji matengenezo katika eneo fulani la moyo wake. Anaweza akawa ana hofu akadhani huwenda chanzo cha hofu hiyo ni ule ugonjwa uliomshika, kumbe chanzo ni kingine kabisa.

Kwasababu mwanadamu mwenyewe moyo wake ni fumbo kubwa.

Yeremia 17:9

[9]Moyo huwa mdanganyifu kuliko vitu vyote, una ugonjwa wa kufisha; nani awezaye kuujua?

Umeona jinsi ilivyo ngumu sana. Ikiwa yeye mwenyewe hajijui, wewe mtu wa tatu utayajulia wapi yaliyomo moyoni mwake? Lakini Mungu anataka uyahubiri yahusuyo moyo wake.

Usifikiri unapomwona mtu, labda ana huzuni, au furaha au ana tabia za ulevi, wizi, , ukadhani anahitaji fundisho linaloendana na hiyo tabia unayoiona kwa nje.

Unaweza ukakosa shabaha kwa maili nyingi sana, ukifikiri tu hivyo.

Utamwona analia, pengine ni mgonjwa, amefiwa, amepoteza kila kitu kama ilivyokuwa kwa Ayubu na wewe unamfuata na fundisho la faraja, ukadhani kuwa ndio uponyaji wake utakapotokea.

Kumbe Mungu anajua anataka makemeo, na makaripio ili aponywe.

Wakati mwingine utasimama kwenye mkusanyiko wa watu wengi labda mia. Huko huko wapo wanaohitaji faraja, wanaohitaji unabii, wanaohitaji maonyo, wanaohitaji maarifa, wanaohitaji kufunguliwa. Sasa wewe unasimama na fundisho lako lenye mlengo mmoja wa makemeo, unadhani wote watahudumiwa na hilo. Kama ukikosa namna ya ki-ungu, unaweza ukawa unazungumza maneno yako.

Na lengo la Mungu ni watu wote wahudumiwe na Neno.

Hapo ndio linakuja suala la hakuna mbobezi wa fundisho au hubiri. Inahitaji hekima nyingine itokayo juu, ya kuhubiri usichokuwa na ufahamu nacho, au ujuzi nacho.

Siku ile ya Pentekoste, kilichotendeka mpaka ikapelekea watu wale kuchomwa mioyo, na hatimaye kuamini kwa idadi ile kubwa ya watu.

Haikuwa kwasababu walipaza sauti sana, au walihubiri kwa ujasiri sana, au maneno yao yalikuwa na elimu kubwa ya theolojia..

Hapana angalia utaona yalikuwa ni maneno ya kawaida kabisa… lakini yaliyoundwa na Roho Mtakatifu kwa namna ambayo yalipenya katika moyo wa kila mmoja.

Utaona, hatua ya kwanza walinena kwa lugha ambazo hata wao wenyewe hawakuzijua, lugha hizo zilikuwa zinawahubiria wengine.. zinanena mambo yao ya sirini, zinawakemea, zinawafariji, zinawaponya, zinawashuhudia Kristo.

Mpaka baadaye wanamaliza kunena tayari injili imeshahubiriwa wasijue ni kitu gani kimehubiriwa.

Petro aliposimama kumalizia maneno yake, wote wamenywea wanasubiri tu kupewa maelekezo ni nini cha kufanya baada ya pale..

Matendo ya Mitume 2:37

[37]Walipoyasikia haya wakachomwa mioyo yao, wakamwambia Petro na mitume wengine, Tutendeje, ndugu zetu?

Hao ni watu wasio na elimu yoyote, walikuwapo waandishi, na mafarisayo wenye elimu lakini hakuna matokeo yoyote ya mafundisho yao.

Hata leo hii mimi na wewe.. Tujue kuwa kuhubiri na kufundisha hakutegemei sana ujuzi, au utashi, bali kunategemea zaidi Roho Mtakatifu.

Kwanini Roho Mtakatifu?

Kwasababu yeye ndiye anayeweza kuzama ndani ya mioyo ya watu na kujua shida zao, na kuwaponya.

Ni nini tunapaswa kufanya, ili fundisho likazame moyoni, lisitoke kwa makisio yetu?

Jambo kuu ni Kuwa na maandalizi ya kutosha.

Maandalizi hayo yapo kwa namna mbili.

1) Kumwandalia Roho Mtakatifu njia ya kuanzia..Ndio hapo unahitaji kwanza kusoma na kuandaa somo / fundisho. Kumbuka Ni lazama utenge muda kuandaa fundisho ambalo utalihubiri. Andika, na ujue pa kuanzia, bila kuwa na maandalizi hayo, unasema nitaenda tu kuzungumza. Ujue tayari umeizuia njia ya Roho Mtakatifu kufundisha.

2) Lakini hilo peke yake halitoshi, hatua nyingine ni kuomba maingilio ya Roho Mtakatifu yawe makubwa. Hapo ndipo unatenga muda mrefu wa kuomba, ili Roho Mtakatifu akatembee kwenye vyumba vya ndani kabisa ambavyo wewe hujui, wakati utakaposimama na kufundisha, kushuhudia.

Sasa ukimaliza hapo. Jiandae kwenda kusema ulichokusudia.. kumbuka mhubiri anayetumia dakika kumi kufundisha lakini amekuwa na maandalizi ya masaa matano kwenye kusoma na maombi. Ana nguvu zaidi ya yule atakayefundisha masaa matano, halafu alijiandaa kwa dakika tano.

Mwisho Ukienda kufundisha na kuona mazungumzo yako yanasogea nje ya mada, au taarifa nyingine zinakuja kichwani mwako tofauti na zile ulizoziandika kwenye daftari ujue ni kazi za Roho Mtakatifu usizizuie.

Baadaye utakuja kusikia tu shuhuda, na hata kama hazitasemwa, ujue Neno lako halijakwenda bure.

Tukiwa wahubiri na waalimu wa namna hii. Roho nyingi za watu zitaokolewa.

Kuhubiri ni kusema tusichokijua, cha wengine.

Shalom

Washirikishe na wengine habari hizi njema kwa kushea

Ikiwa utapenda kupata msaada wa kumpokea Yesu maishani mwako bure, Basi wasiliana nasi kwa namba uzionazo chini ya makala hii.

Pia kwa kupokea mafundisho ya kila siku kwa njia ya WHATSAPP, jiunge na channel yetu kwa kubofya link hii >> https://whatsapp.com/channel/0029VaBVhuA3WHTbKoz8jx10

Kwa mawasiliano: +255789001312 au +255693036618

Bwana akubariki.

Mafundisho mengine:

MWANAMKE ALIYEONGOZWA NYIKANI.

Ulishawahi kutafakari kwanini yule mwanamke aliyemzaa yule mtoto wa kiume, kupewa uwezo wa kukimbilia nyikani, kama njia ya kuepushwa na joka lile?

Kwanini asichuliwe mashambani, au mjini, au milimani, kinyume chake iwe nyikani.

Ufunuo 12:13-14

[13]Na joka yule alipoona ya kuwa ametupwa katika nchi, alimwudhi mwanamke yule aliyemzaa mtoto mwanamume.

[14]Mwanamke yule akapewa mabawa mawili ya tai yule mkubwa, ili aruke, aende zake nyikani hata mahali pake, hapo alishwapo kwa wakati na nyakati na nusu ya wakati, mbali na nyoka huyo.

Nyikani ni mahali ambapo hapana uzuri wowote, hapana mahitaji yoyote ya msingi, mahali pasipovutia, kwasasa tunaweza kusema ni nyakati za ukame, ambazo huoni, jambo lolote, huoni hatua yoyote dhahiri,ijapokuwa unajitahidi sana..huoni mafanikio yoyote, huoni mazingira rafiki..

Wakati mwingine ni kipindi cha kupungukiwa kwa muda mrefu, upo pale pale.

Tunapofikia hatua hii, mara nyingi tunamlilia Mungu atuondoe huko, tunahuzunika, tunanyong’onyea, tunasinyaa kiroho, tunamlilia Mungu kwa juhudi nyingi atuvushe..

Ni kweli kabisa jangwa si zuri, lakini wakati mwingine Bwana hulitumia kutuepusha na yule mwovu. Njia pekee iliyompasa huyu mwanamke kuepushwa na joka lile, ilikuwa ni kukimbilia jangwani, na si vinginevyo.

Hivyo ujikutapo katika nyakati mbalimbali ngumu, maadamu upo ndani ya Kristo na unaendelea vema katika imani, fahamu pia huko ulipo Mungu anakuandaa na unatimiza kusudi la Mungu.

Tuwapo katika mazingira yoyote, suluhisho si kulalamika bali ni kuomba, kushukuru na kuitafuta hekima.

Bwana akubariki.

Shalom

Washirikishe na wengine habari hizi njema kwa kushea

Ikiwa utapenda kupata msaada wa kumpokea Yesu maishani mwako bure, Basi wasiliana nasi kwa namba uzionazo chini ya makala hii.

Pia kwa kupokea mafundisho ya kila siku kwa njia ya WHATSAPP, jiunge na channel yetu kwa kubofya link hii >> https://whatsapp.com/channel/0029VaBVhuA3WHTbKoz8jx10

Kwa mawasiliano: +255789001312 au +255693036618

Bwana akubariki.

KIJAKAZI ALIYEJUA UPONYAJI ULIPO.

Hauhitaji nafasi kubwa kuzijua siri za Mungu.

Naamani alikuwa ni mtu mkuu, jemedari wa vita, lakini alikaa na ukoma uliomtesa kwa muda mrefu, bila ufumbuzi wowote wala tumaini lolote la kupona.

Katika ushujaa wake, na cheo chake hakuwahi kujua siri za uponyaji zipo wapi, isipokuwa kijakazi wake ambaye hajatajwa hata jina lake, aliuona uzima wa Bwana wake, mahali ulipo, mbali sana na taifa lake, kwa mtu wa Mungu aliyeitwa Elisha.

Kijakazi huyu ndiye aliyefungua njia ya Naamani  kupokea uponyaji wake mkamilifu

2 Wafalme 5:1-4

[1]Basi Naamani, jemadari wa jeshi la mfalme wa Shamu, alikuwa mtu mkubwa mbele ya bwana wake, na mwenye kuheshimiwa, kwa sababu kwa mkono wake BWANA alikuwa amewapa Washami kushinda; tena alikuwa mtu hodari wa vita; lakini alikuwa mwenye ukoma. 

[2]Na Washami walikuwa wametoka vikosi, wakachukua mfungwa mmoja kijana mwanamke kutoka nchi ya Israeli; naye akamhudumia mkewe Naamani. 

[3]Akamwambia bibi yake, Laiti bwana wangu angekuwa pamoja na yule nabii aliyeko Samaria! Maana angemponya ukoma wake. 

[4]Mtu mmoja akaingia, akamwambia bwana wake, akasema, Yule kijana mwanamke aliyetoka nchi ya Israeli asema hivi na hivi. 

Huhitaji kuwa mtu fulani, wala huhitaji kuwa hodari duniani, kuwa msomi sana, jasiri sana, kuzidhihirisha nguvu za Mungu, au kuwahudumia watu wake, au kuwaponya na kuwafundisha,  unahitaji tu, unyenyekevu ambao unadhihirishwa kwa kumcha Bwana. Kisha yeye mwenyewe Mungu kwa hekima yake ataitengeneza njia yake anayoijua mwenyewe kuwasaidia wengine kupitia wewe.

Ndio maana Neno la Mungu linasema;

1 Wakorintho 1:26-29

[26]Maana, ndugu zangu, angalieni mwito wenu, ya kwamba si wengi wenye hekima ya mwilini, si wengi wenye nguvu, si wengi wenye cheo walioitwa; 

[27]bali Mungu aliyachagua mambo mapumbavu ya dunia awaaibishe wenye hekima; tena Mungu alivichagua vitu dhaifu vya dunia ili aviaibishe vyenye nguvu; 

[28]tena Mungu alivichagua vitu vinyonge vya dunia na vilivyodharauliwa, naam, vitu ambavyo haviko, ili avibatilishe vile vilivyoko; 

[29]mwenye mwili awaye yote asije akajisifu mbele za Mungu. 

Wekeza zaidi kwenye kumcha Mungu, zaidi ya juhudi za kibinadamu kwasababu hekima yake ni mbali sana na mavumbuzi ya wanadamu.

Bwana akubariki.

Washirikishe na wengine habari hizi njema kwa kushea

Ikiwa utapenda kupata msaada wa kumpokea Yesu maishani mwako bure, Basi wasiliana nasi kwa namba uzionazo chini ya makala hii.

Pia kwa kupokea mafundisho ya kila siku kwa njia ya WHATSAPP, jiunge na channel yetu kwa kubofya link hii >> https://whatsapp.com/channel/0029VaBVhuA3WHTbKoz8jx10

Kwa mawasiliano: +255789001312 au +255693036618

Bwana akubariki.

MATUKIO KATIKA MAANDIKO YANAYOISHI HATA LEO.

Katika maandiko ukikutana na kisa kinaishia kwa kusema ‘hata leo’. Basi kuwa makini hapo kwasababu  lipo la kukusaidia.

Kwamfano Ibrahimu alipopanda kule mlimani kumtolea Mungu sadaka kwa Isaka, Mungu alimpa kondoo badala yake,  Kwa tukio hilo Ibrahimu akapaita mahali pale Yehova-yire. (Maana yake Mungu-mpaji). Hivyo jambo  lile maandiko yanasema liliendelea kutamkwa na watu kwa wakati mwingine mwingi sana  kama usemi uliohai ‘Yehova-yire’, Mungu atupaye.

Mwanzo 22:13-14

[13]Ibrahimu akainua macho yake, akaangalia, na tazama, kondoo mume yuko nyuma yake, amenaswa pembe zake katika kichaka. Basi Ibrahimu akaenda akamtwaa huyo kondoo, akamtoa awe sadaka ya kuteketezwa badala ya mwanawe. 

[14]Ibrahimu akapaita mahali hapo Yehova-yire,

kama watu wasemavyo hata leo, Katika mlima wa BWANA itapatikana. 

Mfano mwingi ni wakati wa Yoshua alipoiangamiza nyumba ya Akani, msaliti, biblia inasema;

Yoshua 7:26

[26]Kisha wakakusanya juu yake chungu kubwa ya mawe hata leo; naye BWANA akauacha ukali wa hasira yake. Kwa sababu hiyo jina la mahali pale likaitwa, Bonde la Akori, hata hivi leo. 

Ikiwa na maana bonde hilo liliendelea kuitwa vile vile hadi wakati wa mwandishi. ‘Ipo sababu’.

Mfano mwingine ni kipindi cha Yehu alipoyavunja mahekalu ya Baali..

2 Wafalme 10:27

[27]Wakaibomoa nguzo ya Baali, na kuiangusha nyumba ya Baali, wakaifanya choo hata leo. 

Ikiwa na maana  mpaka wakati mwandishi anaandika hicho kitabu eneo hilo lilikuwa ni choo.

Mahali pengine ni hapa..

Israeli kuwa hatarini kuvamiwa na wamoabu, wakamlilia Mungu, kisha kawaambia hawatapigana vita bali watakwenda kuokota nyara,  kazi yao iwe ni kusifu na kuimba tu. Maadui zao wakauana wao kwa wao Na eneo lile wakaliita bonde la baraka hata leo.

2 Mambo ya Nyakati 20:25-26

[25]Nao Yehoshafati na watu wake walipokuja kuchukua nyara zao, wakaona kati yao wingi wa mali, na mavazi, na johari za thamani, walivyojivulia, zaidi kuliko wawezavyo kuchukua; wakawa siku tatu katika kuteka nyara, maana zilikuwa nyingi sana. 

[26]Hata siku ya nne wakakusanyika katika bonde la Baraka; maana ndipo walipombarikia BWANA; kwa hiyo jina lake mahali pale pakaitwa Bonde la Baraka hata leo. 

Mahali pengine ni wakati wa kifo cha Yuda, lile shamba lililonunuliwa liliitwa konde la damu mpaka nyakati za mwandishi..

Mathayo 27:8

[8]Kwa hiyo konde lile huitwa konde la damu hata leo. 

Sasa biblia kusema ‘hata leo’ sio tu kutoa uthibitisho wa tukio kwamba kweli lilitokea ..lakini ni vema kujua tafsiri yake rohoni…kwamba kuna minyororo aidha ya baraka au laana inatembea mpaka leo.

Kwamfano watu waliposema Yehova-yire walijua Mungu ni mpaji wakati wote…hivyo wakamwona katika mazingira hayo..ndio maana wakasema ‘hata sasa’ si tu wakati wa Ibrahimu.

Neno hilo lipo hai hata leo rohoni. Ukiamini Mungu aliyomtendea Ibrahimu anakwenda kukutendea na wewe, utapokea…kwasababu lipo hivyo hata leo.

Anaposema mahali pale pakaitwa bonde la baraka hata leo. Ni kweli rohoni hata leo bonde hilo lipo.

Ukiamini kwamba katika kumwimbia Mungu unaingia katika bonde la baraka. Utapokea vingi kwa Mungu, sawasawa na walivyopokea Israeli kipindi cha Yehoshafati vitani.

Hivyo mambo mengi na matukio mengi yanaendelea kutembea katika roho hata sasa…Je! Macho yako yanaona?

Ukiwa mwovu kama Akani, kumbuka bonde la Akori lipo mpaka leo, ikiwa utakuwa msaliti kama Yuda konde la damu lipo hata leo utazikiwa huko.

Chagua mema, yaishi mema, upokee mema

Shalom.

Washirikishe na wengine habari hizi njema kwa kushea

Ikiwa utapenda kupata msaada wa kumpokea Yesu maishani mwako bure, Basi wasiliana nasi kwa namba uzionazo chini ya makala hii.

Pia kwa kupokea mafundisho ya kila siku kwa njia ya WHATSAPP, jiunge na channel yetu kwa kubofya link hii >> https://whatsapp.com/channel/0029VaBVhuA3WHTbKoz8jx10

Kwa mawasiliano: +255693036618 au +255789001312

Bwana akubariki.

Mafundisho mengine:

NIFANYE NINI PALE NINAPOSAHAU NDOTO NILIZOOTA?

Moja la lango ambalo Mungu hulitumia sana, kutufikishia  sisi taarifa zake, ni ndoto. Na kama ni lango la Mungu basi ni vema tufahamu kuwa ibilisi hatalipenda. Hivyo atahakikisha taarifa hizo anazivuruga au hazitufikii vema, kama tu vile anavyohakikisha watu hawalielewi Neno, au mahubiri, Ndivyo anavyofanya na kwenye ndoto pia.

Taarifa zitokazo kwa Mungu zinaangukia katika makundi matatu;

  1. Tahadhari
  2. Unabii
  3. Baraka

1) Tahadhari

Hizi ni taarifa za maonyo, au hatari zinazokuja mbeleni. Mfano wa taarifa hizi ni kama zile zilizomfikia Yusufu, alipokuwa Israeli, akaambiwa akimbilie Misri, kwasababu Herode anataka kumuua mtoto, na aliporudi baadaye, akaonywa tena asikae Yerusalemu, bali aende Nazareti.

Mathayo 2:19-22

19 Hata alipofariki Herode, tazama, malaika wa Bwana alimtokea Yusufu katika ndoto huko Misri,
20 akasema, Ondoka, umchukue mtoto na mamaye, ushike njia kwenda nchi ya Israeli; kwa maana wamekufa walioitafuta roho ya mtoto.
21 Akaondoka akamchukua mtoto na mamaye, akafika nchi ya Israeli.
22 Lakini aliposikia ya kwamba Arkelao anamiliki huko Uyahudi mahali pa Herode babaye, aliogopa kwenda huko; naye akiisha kuonywa katika ndoto, akasafiri pande za Galilaya,

Lengo la taarifa hizi ni mtu kuchukua hatua, aidha ya kivitendo au ya kimaombi.

Kwamfano Mungu anaweza kukuonyesha ajali, au msiba fulani. Hapo ujue hasaa unahitajika kuchukua hatua kimaombi kuharibu hizo roho za mauti, kwa kinywa chako.

2) Unabii

Hizi ni taarifa za mambo yajayo, Yale yatakayotokea baadaye, kwenye maisha yako, huduma, familia, nchi, au taifa. Mfano wa ndoto hizi, ni kama ile ya Farao juu ya miaka saba ya shibe na njaa, (Mwanzo 41) na Nebukadreza, juu ya ile sanamu kubwa, iliyowakilisha falme nne, zitakazokuja kusimama ulimwenguni (Danieli 2).

Halikadhalika Mungu anaweza kukuonyesha, maisha yako baadaye yatakuwaje, huduma yako baadaye, itasimamaje, maono yako baadaye yatafikia wapi, anaweza kukuonyesha mambo ya siku za mwisho, matukio yajayo, kuhusu nchi, watu, familia. Hatua unayopasa kuichukua ni kuomba, na kuandaa mazingira sasa. Mfano Farao aliposaidiwa tafsiri ya ndoto yake na Yusufu, alichukua hatua ya kuweka hazina ya vyakula kwasababu njaa ilikuwa inakuja mbele. Mungu akikuonyesha huduma yako itakuwa kubwa, anza leo kujiwekea hazina ya maarifa ya Neno la Mungu, anza kutendea kazi wito wako,. Akikuonyesha unawaombea watu wengi wanapona, anza leo kuwaombea watu hata kama hawaponi, omba hivyo hivyo kila siku, usikae tu ukasubiri ije kutimia na huonyeshi jitahada yoyote, akikuonyesha biashara yako imekuwa, ongeza juhudi kufanya kazi.

3) Baraka

Mungu anaweza kuachia Neno la Baraka kwako, kwamfano ukaota, ndoto njema, labda unatiwa mafuta na Kristo, au unaambiwa maneno ya mafanikio kama vile  Sulemani alipotokewa na Mungu na kuelezwa atapokea Hekima, na kuwa na mali nyingi. Uotapo ndoto ambazo ni za mafanikio kwako, uamkapo, hakikisha unazinenea kwa Imani. Unasema

“Na iwe kwangu kwa jina la Yesu Kristo”. Kama tu vile unavyobatilisha ndoto za maovu, labda mauti, vivyo hivyo hizi unazipokea kwa kinywa chako. Ni muhimu sana.

Ibrahimu aliota ndoto

Mwanzo 51:1-6

Baada ya mambo hayo neno la Bwana likamjia Abramu katika njozi, likinena, Usiogope, Abramu, Mimi ni ngao yako, na thawabu yako kubwa sana.
2 Abramu akasema, Ee Bwana MUNGU, utanipa nini, nami naenda zangu hali sina mtoto, na atakayeimiliki nyumba yangu ni huyu Eliezeri, Mdameski?
3 Abramu akasema, Tazama, hukunipa uzao, na mtu aliyezaliwa nyumbani mwangu ndiye mrithi wangu.
4 Nalo neno la Bwana likamjia likinena, Huyu hatakurithi, bali atakayetoka katika viuno vyako ndiye atakayekurithi.
5 Akamleta nje, akasema, Tazama sasa mbinguni, kazihesabu nyota, kama ukiweza kuzihesabu. Akamwambia, Ndivyo utakavyokuwa uzao wako.
6 Akamwamini Bwana, naye akamhesabia jambo hili kuwa haki.

Sasa kinachotokea ni kwamba ndoto nyingi sana, za taarifa mbalimbali  kutoka kwa Mungu zinapotea akilini mwetu, na tunaona kawaida,

Ndoto hupotea kwa aidha namna mbili;

  • Tunakumbuka kwamba tuliota ndoto, lakini hatujui ni ndoto gani
  • Hatukumbuki kabisa kama tuliota ndoto yoyote. Lakini ipo ndoto tuliyoota

Namna mojawapo inaweza kutokea kwa mtu. Usikae ukafikiria kisa hukumbuki chochote, ukadhani hukuota ndoto yoyote. Zipo ndoto ulizoota. Hivyo ni vema ukajifunza namna ya kukabiliana na lango lako la ndoto. Ndio maana utaona wengine tukio likishatokea ndio anakumbuka kuwa alishawahi onyeshwa tukio hilo. Hiyo haitakiwi.

Nifanye nini ili nikumbuke ndoto zangu?

Njia tatu zinazoweza kumfanya mtu akumbuke ndoto.

i) Kuomba:

Kila asubuhi uamkapo, katika maombi yako, hakikisha unashika Kichwa chako, kisha unasema maneno haya

‘Baba, nafungua lango la ndoto zangu, yote uliyosema nami usiku nilipolala, ninayoyakumbuka na nisiyoyakumbuka yakawe bayana sasa kwa jina la Yesu, ndoto zilizoibiwa na ibilisi, kumbukumbu zangu, na fikra zangu zilizofutika, navirejesha vyote ndani ya ufahamu wangu sasa kwa jina la Yesu Kristo’.

Ukijifunza kuomba namna hiyo, tayari umekaribisha msaada wa Mungu, mahususi katika eneo lako la ndoto na hivyo urahisi wa kukumbuka unakuja.

ii) Utulivu (Kutafakari)

Ukishaomba, pendelea kupata utulivu, kisha tafakari kwanza Neno la Mungu. Kila asubuhi hakikisha unapata kwanza mkate wa uzima ambao ni Neno, tafakari Neno kwa muda kidogo, jiulize vifungu hivi vinamaana gani, je! Siku ya leo nitaviwekaje katika maisha yangu? Fanya tu hivyo tembea maeneo mbalimbali ya kwenye biblia, kisha tafakari tena juu ya maisha yako ya rohoni, juu ya maono yako, juu ya familia yako utajiboreshaje, baadaye juu ya ratiba zako za siku..

Katika wingi wa kutafakari, mara nyingi Mungu hurejesha ndoto zilizosahaulika, utashangaa katika tafakari Fulani hapo hapo unakumbuka kuna jambo uliota, linaloendana na tukio hilo. Ujue huo ni ujumbe wa Mungu.

Ukikosa muda wa kutosha asubuhi, Fanya hivyo muda wa usiku kabla ya kulala, Pata utulivu mwingi peke yako, Utakumbushwa ndoto nyingi.

iii) Mazungumzo

Njia nyingine ambayo humfanya Mungu arejeshe ndoto zetu kirahisi, ni katika mazungumzo, kumbuka kila eneo la maisha yako au wengine, yamkini Bwana alishawahi kusema na wewe, kwa njia ya ndoto, lakini hujui.

Kwamfano ukiwa na mwenzako, au wenzako, mnazungumza sana, Habari njema za kanisa, katika mazungumzo ya muda mrefu ikiwa lipo ambalo Bwana alikuonyesha, utaona kumbukumbu hiyo inakujia, au labda mnazungumza kwa kina Habari ya siku za mwisho, Kumbukumbu ya ndoto kama hiyo itakujia, au malengo ya maono yako.

Hivyo mazungumzo mazuri na yenye maana hurejesha fikra zilizopotea. Kwahiyo, jijengee desturi ya kuwa na mazungumzo mema.

Zingatia pia si kila ndoto hutoka kwa Mungu, ili kuweza kutofautisha ndoto za Mungu na za shetani, fungua link hii, uweze kupitia..>>>> https://wingulamashahidi.org/2019/09/03/nitajuaje-kama-ndoto-ni-ya-mungu-au-ya-shetani/

Mungu akubariki.

Washirikishe na wengine habari hizi njema kwa kushea

Ikiwa utapenda kupata msaada wa kumpokea Yesu maishani mwako bure, Basi wasiliana nasi kwa namba uzionazo chini ya makala hii.

Pia kwa kupokea mafundisho ya kila siku kwa njia ya WHATSAPP, jiunge na channel yetu kwa kubofya link hii >> https://whatsapp.com/channel/0029VaBVhuA3WHTbKoz8jx10

Kwa mawasiliano: +255693036618 au +255789001312

Bwana akubariki.

Mafundisho mengine:

SIFA NJEMA YA KIRUKA NJIA

Kuna ndege anaitwa kiruka njia, ambaye anatajwa kama mmoja wa ndege najisi, kwenye Kumbukumbu 14:15, lakini ndege huyu anasifa moja ambayo, huwa ina  funzo kubwa sana la kiroho.

Tofauti na ndege wengine, ambao huruka aidha mchana, au usiku, kujitafutia chakula, kwamfano mwewe, mbayuwayu, korongo, tai, ni ndege wa mchana, lakini pia bundi, popo, ni ndege wa usiku, wote hawa hufanya kazi aidha majira ya kutwa nzima ya mchana, au usiku kucha.

Lakini kiruka njia, huruka zaidi, majira ya alfajiri sana, na jioni sana. Majira haya huyapendelea kwasababu, ni wakati wa mageuko ya siku, ambayo ndege wote wawindaji hujiandaa Kwenda mapumziko, au kuamka. Kwamfano muda wa jioni kama vile saa 12, ndege wakali wawindaji kama vile tai, mwewe, kipanga, n.k. wanaacha uwindaji, na kutafuta makao yao kupumzika, lakini pia wakati huo huo ndege wakali wa usiku kama vile bundi, hujiandaa kutoka waende kwenye mawindo yao saa mbili, Kwahiyo huo muda hapo Katikati mazingira kwake huwa si ya upinzani mkubwa.

Kwasababu yeye ni ndege dhaifu, na anaweza kuwindwa na ndege wakubwa, majira hayo kwake ni salama zaidi. Vivyo hivyo ule muda wa alfajiri sana, miale ya jua inapoanza kuonekana kwa mbali sana, hutoka na Kwenda kuwinda, muda huo ndege wa usiku ndio wanakwenda kulala, huku ndege wa mchana wanajiandaa kutoka, mpaka inapofika saa 12 asubuhi, tayari ameshamaliza uwindaji wake.

Licha ya kuwa wakati huo, ndege wengi hawapo hewani, lakini wakati huo, wa alfajiri sana na jioni sana, ndio makundi ya wadudu wengi wa ardhini hutoka kuruka juu, ikiwemo mbu, kumbikumbi, mchwa, nondo, mende n.k. kwasababu yeye hula wadudu, anaweza kukamata wadudu hata elfu moja ndani ya saa moja tu. Hivyo kwa muda mfupi sana akawa ameshashiba, zaidi ya mihangaiko mingi ya kutwa nzima, kugombania vyakula, na masumbufu mengi.

Ndege huyu mchana hupumzika zake, kwenye miti, na usiku pia, lakini hutumia alfajiri yake na jioni yake vizuri. Ndio maana ni vigumu kujulikana, kwasababu shughuli zake anazifanya wakati anga ni tulivu.

Hutufundisha nini?

Bwana alituambia tuwatafakari ndege (Mathayo 6:26)

Ni lazima tuthamini mida hii miwili, kuitumia kuwa uweponi mwa Bwana, Bwana Yesu alipendelea sana, kuamka alfajiri kuomba,

Marko 1:35 Hata alfajiri na mapema sana akaondoka, akatoka akaenda zake mahali pasipokuwa na watu, akaomba huko.

 Ipo faida kubwa sana kuamka  mapema kuomba kwasababu, muda huo anga ni tulivu, wakati watu wamelala, wewe unapokea thawabu za siku kutoka kwa Bwana. Kuna usemi unaosema biashara ni asubuhi, kwasababu wameona  Riziki nyingi huwaga majira hayo, vivyo hivyo rohoni, ukijifunza kuomba majira hayo, na jioni pia kabla hujaimaliza siku, Basi utaona tofauti kubwa sana, na wepesi mwingi wa masumbufu ya siku.

Bwana akubariki.

Washirikishe na wengine habari hizi njema kwa kushea

Ikiwa utapenda kupata msaada wa kumpokea Yesu maishani mwako bure, Basi wasiliana nasi kwa namba uzionazo chini ya makala hii.

Pia kwa kupokea mafundisho ya kila siku kwa njia ya WHATSAPP, jiunge na channel yetu kwa kubofya link hii >> https://whatsapp.com/channel/0029VaBVhuA3WHTbKoz8jx10

Kwa mawasiliano: +255693036618 au +255789001312

Bwana akubariki.

Mafundisho mengine:

Hawa ndege katika Walawi 11:13-19 ndio ndege gani kwasasa?

MTEGO HUTEGWA BURE, MBELE YA MACHO YA NDEGE YE YOTE.

Je tamaa ni dhambi kulingana na Yakobo 1:15?