Category Archive Kazi (Uchumi)

TENDA JAMBO LA ZIADA.

(Masomo maalumu yahusuyo kazi na uchumi).


Tunahitaji kujua kanuni chache ili tuweze kufungua milango yetu ya kiuchumi. Leo tutaangalia kanuni nyingine ambayo mkristo akiitumia basi anaweza kupata kibali mahali pale afanyiapo kazi.

Si wakati wote maombi tu pekee yanatosha kukuletea kibali katika maisha ya kazi/kuwajibika. Ni lazima pia uongeze na maarifa ili uweze kufungua milango hiyo ya Baraka.

Sasa ukitaka upate kibali kazini au kwa aliye juu yako, basi FANYA JAMBO LA ZIADA HAPO UFANYIAPO KAZI.

Kwa mfano Mshahara wako unaoupokea kwa siku, wiki au mwezi, ni kiasi Fulani…. baada ya kutoa sehemu ya Mungu (yaani sadaka pamoja na Zaka) kiasi kilichosalia  usikitumia chote katika mahitaji yako..bali toa sehemu kidogo ya hicho na ufanye jambo jipya na la kipekee hapo ufanyiapo kazi!.

Kwa mfano kama umeajiriwa na unafanya kazi ya usafi hapo kazini, badala ya kusubiri mwajiri wako akupe fedha ya kwenda kununua kifaa cha usafi, hebu wewe TENDA JAMBO LA ZIADA… toa kiasi kidogo cha pesa yako na nenda kununua kifaa hicho.

Kwa kufanya hivyo utaonekana mjinga mbele ya wafanyakazi wenzako na watu wengine walio karibu nawe pengine hata kwa mke wako/mume wako… lakini si kwa Mwajiri wako!, yeye atakusifu kama si kwa kinywa chake basi katika moyo wake, na hiyo itakuongezea kibali kikubwa sana katika maisha yako ya kazi… Utakuwa umepata nafasi katika moyo wake, na kiwango cha kukuamini na kukupenda kitaongezeka..

Au labda umeajiriwa katika mgahawa, hebu TENDA JAMBO LA ZIADA…badala ya kusubiri boss wako akupe fedha za kwenda kununua sahani za biashara, au akupe fedha za kwenda kununua sufuria, au sabuni.. hebu mara moja moja wewe toa kiasi chako kidogo cha mshahara kanunue zile sahani, au sufuria au kitu kingine chochote cha muhimu kinachohitajika pale..

Wala usianze kuangalia mahitaji uliyonayo (hayo yataendelea kuwepo tu)… wewe fanya hivyo kwasababu  unajua ni mbegu gani unayoipanda wakati huo!… wengine watakuona huna akili, au umechanganyikiwa, wewe usiangalie hayo bali angalia yanayokuja..

Pengine umeajiriwa kama mhasibu katika ofisi fulani, hebu TENDA JAMBO LA ZIADA, Toa kidogo katika mshahara wako kanunue kiti kingine cha ofisi au saa ya ofisi nzuri, au pamba kwa chochote kile pale ufanyiapo kazi.. weka mbali matatizo yako kwa muda, na mahitaji yako na ufanye hayo.. nakuhakikishia matokeo yake utakuja kuyaona baadaye.. Utapata kibali ambacho utakishangaa.

Wakati unafanya hayo, wengine watakuona ni mjinga, kwasababu hayo unayoyafanya yangepaswa kutekelezwa na boss wako au kampuni, na sio wewe…ndio maana watakuona umerukwa na akili, lakini Mwajiri wako atakuona ni shujaa..

Katika biblia Bwana YESU alitoa mfano wa wakili dhalimu, ambaye alitoa mali zake za wizi na kuwalipa wadeni wa Boss wake, na kupitia mali ile ya udhalimu alijipatanisha na boss wake pamoja na wadeni wa boss wake…na hivyo akasifiwa hata na yule yule aliyemwibia (yaani bosi wake). Soma Luka 16:1-12

Sasa huyu alijipatia kibali kwa mali ya udhalimu (maana yake mali ya wizi).. vipi wewe ambaye una mali ambayo sio ya wizi (halali), halafu ukaitumia katika kutafuta kibali?.. unadhani hutakipata??.

Lakini ukisema mimi nitaomba tu!, na kutumia kiasi chako kwa mahitaji yako tu…na huku hutaki kutenda jambo la ziada,  hapo unapofanyia kazi, utakuwa unajiwikwamishia Baraka zako tu!… kwasababu hayo uyafanyayo ni kila mtu anayafanya, na yameshazoeleka…lakini ukitenda TENDA TENDO LINGINE ZA ZIADA ambayo halifanywi na wengine wote, hapo utajipatia kibali.

Hata katika kumtumikia MUNGU, Bwana YESU alitufundisha kuwa ni lazima tujifunze kutenda tendo lingine la ziada ili tupokee kibali.

Mathayo 5:46 “Maana mkiwapenda wanaowapenda ninyi mwapata thawabu gani? Hata watoza ushuru, je! Nao hawafanyi yayo hayo?

47  Tena mkiwaamkia ndugu zenu tu, mnatenda tendo gani la ziada? Hata watu wa mataifa, je! Nao hawafanyi kama hayo?”

Hivyo pata maarifa na TENDA TENDO LA ZIADA, na utaona jinsi utakavyopokea kibali katika yote uyafanyayo!.

Bwana akubariki.

Tafadhali shea na wengine ujumbe huu;

Pia Kwa maombezi/ Ushauri/ Maswali/ Whatsapp:
Tuandikie katika BOXI la Maoni hapo chini au
Piga namba hizi: +255789001312 au +255693036618

Mafundisho mengine:

TENDA HAKI KWA FAIDA YAKO MWENYEWE.

Mfano wa wanawali kumi(Mathayo 25), unaelewekaje?

Mistari ya biblia kuhusu kibali.

NJIA NYINGINE YA KUPATA REHEMA NA KIBALI KUTOKA KWA MUNGU.

MAPAMBO YA WANAWAKE WALIOUKIRI UCHAJI WA MUNGU.

Rudi nyumbani

Print this post

UKITAKA KUFANIKIWA, FANANA NA MWANAMKE WA SAREPTA

Jina kuu la Bwana na Mwokozi wetu Yesu KRISTO libarikiwe, karibu tujifunze biblia.

Sarepta ulikuwa ni mji mdogo uliokuwepo nje kidogo mwa nchi ya Israeli, katika Taifa la Lebanoni.

Katika biblia tunasoma kipindi Nabii Eliya amefunga Mbingu miaka mitatu na nusu kwa Neno la Bwana,  aliongozwa aende mpaka mji huu wa Sarepta ambapo kulikuwepo na Mwanamke ambaye Bwana alikuwa amemwandaa ili amlishe.

Mungu angeweza kumshushia Nabii Eliya mana kutoka mbinguni na akala akashiba, lakini hakufanya hivyo, bali alitumia watu na viumbe kumlisha wakati dunia nzima inapitia njaa. Mara ya kwanza alitumia kunguru (1Wafalme 17:4), na mara ya pili akatumia Mtu (ambaye ndiye huyu mwanamke wa Sarepta).

Sasa huyu mwanamke wa Sarepta alikuwa na tabia ya kipekee ambayo kupitia hiyo tunaweza kuvuna hekima ya mafanikio ya kimwili na kiroho.

Inawezekana mambo yako hayaendi sawa, inawezekana unapitia kipindi kigumu sana cha mbingu kufungwa juu yako, kila mahali unapogusa hapaendi, kila unalojaribu halifanikiwi, kila mahali ni ukame!!

Kama unapitia hii hali, basi usiende kutafuta kuombewa! Bali fanya kama alivyofanya huyu mwanamke wa Sarepta.

Ukifanya kama alivyofanya huyu mwanamke wa Sarepta, basi kipindi ambacho wengine watakuwa wanalia matatizo na dhiki, wewe hutakuwa katika hayo matatizo wala hizo dhiki..

Sasa ni kitu gani alichokifanya huyu mwanamke mpaka kufikia hatua ya yeye kuishi vizuri katikati ya vipindi vya shida na njaa na mauti?

Hebu tusome habari yake kwa ufupi kisha tujifunze tabia aliyokuwa nayo.

1Wafalme 17:7 “Ikawa, baada ya siku kupita, kile kijito kikakatika, kwa sababu mvua haikunyesha katika nchi. 

8 Neno la Bwana likamjia, kusema,

9 Ondoka, uende Sarepta, ulio mji wa Sidoni, ukae huko. Tazama, nimemwagiza mwanamke mjane wa huko akulishe

10 Basi, akaondoka, akaenda Sarepta; hata alipofika langoni pa mji, kumbe! Mwanamke mjane alikuwako akiokota kuni; akamwita, akamwambia, Niletee, nakuomba, maji kidogo chomboni nipate kunywa.

11 Alipokuwa akienda kuleta, akamwita akasema, Niletee, nakuomba, kipande cha mkate mkononi mwako.

12 Naye akasema, Kama Bwana, Mungu wako, aishivyo, sina mkate, ila konzi ya unga katika pipa, na mafuta kidogo katika chupa; nami ninaokota kuni mbili ili niingie nijipikie nafsi yangu na mwanangu, tuule tukafe.

13 Eliya akamwambia, Usiogope; enenda ukafanye kama ulivyosema; lakini unifanyie kwanza mkate mdogo ukaniletee; kisha ujifanyie nafsi yako na mwanao. 

14 Kwa kuwa Bwana, Mungu wa Israeli, asema hivi, Lile pipa la unga halitapunguka, wala ile chupa ya mafuta haitaisha, hata siku ile Bwana atakapoleta mvua juu ya nchi.

15 Basi akaenda, akafanya kama alivyosema Eliya; na yeye mwenyewe, na Eliya, na nyumba yake, wakala siku nyingi. 

16 Lile pipa la unga halikupunguka, wala ile chupa ya mafuta haikuisha, sawasawa na neno la Bwana alilolinena kwa kinywa cha Eliya”.

Umeona tabia ya huyu mwanamke?.. alikubali kutoa chakula chake kipindi ambacho amebakiwa nacho kidogo!!.. kipindi ambacho hajui kesho itakuwaje.. Alikubali kuweka sababu zake kando ilimradi tu aone Neno la Mungu linazidi kusambaa kupitia mtumishi wake,  aliona mtu wa Mungu,au kazi ya Mungu ina thamani mara nyingi zaidi ya kazi zake yeye au uwepo wake yeye na mwanae.  

Hivyo akajitoa sadaka maisha yake.. akijua kuwa hata kama atakufa na njaa yeye na mwanae lakini atakuwa na thawabu kubwa mbinguni, atakuwa hajaifanya kazi ya Mungu isimame… Hicho ndicho kilichomfanya Mungu ayaangalie matatizo yake, na kumfungulia Mbingu wakati wengine bado mbingu zimefungwa.

Na Mungu ni yeye Yule jana, leo na hata milele hajabadilika (Waebrania 13:8)..  Ukitaka Bwana ayaangalie mambo yako, basi wewe weka kando mambo yako na shida zako, na anza kujishughulisha na mambo yake..

Hii ndio shida kubwa inayowakabili wakristo wengi, huwa wanatanguliza matatizo yao mbele za Mungu na huku hawataki kumjali Mungu katika maisha yao.. wanatafuta kuombewa mambo yao yakae sawa, lakini kutafuta kuyaweka sawa mambo ya Mungu hawataki..

Watamwambia Mungu, tazama mwanangu hajala, mwanangu hana ada ya shule, mwanangu yuko hivi yuko vile, mimi sina chakula, mimi sina kazi, mimi sina hiki au kile..(wanakuwa ni watu wa kujijali wao) na hawana habari na mambo ya Mungu au kazi ya Mungu, wakidhani kuwa kwasababu Mungu ni muweza wa mambo yote, hivyo hahitaji kupewa chochote au kufanyiwa chochote.

Ni kweli yeye ni mweza wa yote, na hahitaji kufanyiwa chochote, lakini wakati mwingine anafanya hivyo kutujaribu upendo wetu kwake,.. angeweza kumshushia Eliya Mana kama alivyowashushiwa wana wa Israeli jangwani lakini hakufanya hivyo kwa Eliya, bali alimpeleka Eliya kwa huyu mwanamke, ili aujaribu upendo wake kwake.

Wengi wetu hatujui kuwa Mungu anafurahiwa sana na matoleo yetu kipindi ambacho hatuna kitu zaidi ya kipindi ambacho tuna kila kitu. Utasema hilo tunalithibitisha vipi kimaandiko?… Rejea ile habari ya Yule mwanamke mjane aliyetoa riziki yake yote katika sanduku la hazina…Utaona baada ya kutoa Bwana Yesu anamsifia, na tena anasema katoa zaidi ya wote, kwasababu hao wengine walitoa katika sehemu zilizowazidi…

Marko 12:41  “Naye akaketi kulielekea sanduku la hazina, akatazama jinsi mkutano watiavyo mapesa katika sanduku. Matajiri wengi wakatia mengi.

42  Akaja mwanamke mmoja, mjane, maskini, akatia senti mbili, kiasi cha nusu pesa.

43  Akawaita wanafunzi wake, akawaambia, Amin, nawaambia, Huyu mjane maskini ametia zaidi kuliko wote wanaotia katika sanduku la hazina;

44  maana hao wote walitia baadhi ya mali iliyowazidi; bali huyu katika umaskini wake ametia vyote alivyokuwa navyo, ndiyo riziki yake yote pia”

Kwaufupi huyu mjane, hakubakiwa na kitu, huenda alijua baada ya kutoa vile atakaa siku kadhaa na njaa… lakini akiwa katika hiyo hali, Bwana Yesu alimsifia.. huenda baada ya pale, alishangaa kwa milango ya Baraka iliyofululiza mbele yake.

Na wewe ukitaka Mbingu zifunguke juu yako, usianze kutoa visababu katika kumtolea Mungu, usianze kusema sijalipa kodi, usianze kusema sina chakula, sijalipa ada, sijafanya hiki, sijafanya kile, ngoja nikusanye kidogo nitakapopata nitatoa.. Ni kweli siku ukipata na kutoa basi Bwana atakubariki, hataacha kukubariki!!!… lakini  hujui tarehe wala siku mambo yako yatakapokuwa sawa..

Walikuwepo wanawake wengi sana kipindi cha Eliya wenye matatizo ya chakula kama huyu wa Sarepta, ambao na wenyewe pengine walikuwa wanafunga na kuomba Mungu awape riziki kwasababu ya ukame…lakini Eliya hakutumwa kwao kwasababu hizo hizo, huenda angeenda kwao na kuwaambia wampe yeye kwanza mkate, wangemfukuza kwa mawe, tena wangemtukana…

Wangesema hatuwezi kuona watoto wetu wanakufa njaa halafu tukupe wewe mzee chakula chao, wangetumia hata na maandiko kuthibitisha hilo.. Kwaufupi kila mmoja angeeleza shida zake na sababu zake kwanini asingempa Eliya mkate.. Ndicho Bwana Yesu alichokisema katika Luka 4:25.

Luka 4:25 “Lakini, kwa hakika nawaambia, Palikuwa na wajane wengi katika nchi ya Israeli zamani za Eliya, wakati mbingu zilipofungwa miaka mitatu na miezi sita, njaa kuu ikaingia nchi nzima;

26  wala Eliya hakutumwa kwa mmojawapo, ila kwa mjane mmoja wa Sarepta katika nchi ya Sidoni”.

Na sisi pia tukitaka mbingu zifunguke juu yetu kabla ya wakati wake, hatuna budi kumjali Mungu zaidi ya kujijali sisi, hatuna budi kuyatazama mambo ya Mungu zaidi kuliko mambo yetu. Hii ni moja ya kanuni za Mafanikio.

Bwana Yesu atubariki.

Maran atha.

Tafadhali shea na wengine ujumbe huu;

Pia Kwa maombezi/ Ushauri/ Maswali/ Whatsapp:
Tuandikie katika BOXI la Maoni hapo chini au
Piga namba hizi: +255693036618 au +255789001312

Mada Nyinginezo:

Je Eliya aliandika waraka baada ya kupaa mbinguni?

Kwanini wajane vijana hawakupaswa kuandikwa?

NYAKATI SABA ZA KANISA NA WAJUMBE WAKE.

MWANAMKE, BINTI, MAMA. (Sehemu ya 3)

Nini maana ya kumpenda Bwana kwa moyo,roho, akili na nguvu zetu zote?

Rudi nyumbani

Print this post

Biblia inasemaje kuhusu Kazi?

Jibu: Biblia imetuelekeza kufanya kazi za Mikono, ambayo kupitia hiyo Mungu atatupa riziki zetu za kila siku.

1Wathesalonike 4:11  “Tena mjitahidi kutulia, na kutenda shughuli zenu, na kufanya kazi kwa mikono yenu wenyewe, kama tulivyowaagiza;

12  ili mwenende kwa adabu mbele yao walio nje, wala msiwe na haja ya kitu cho chote”

Hivyo ni wajibu wa kila mmoja mwenye uwezo wa kufanya kazi, afanye kazi, aidha za Mikono au za kiutumishi.

Kazi za mikono ni zile zote zinazohusisha kuajiriwa au kujiajiri, na kazi za kiutumishi ni zile zote za Madhabahuni au za kiinjilisti. Mkristo yoyote ni lazima awepo katika kundi mojawapo ya hayo mawili, akikosekana katika yote (na ilihali ni mzima, au hana tatizo lolote lile) basi mtu huyo yupo kinyume na Neno la Mungu, aidha kwa kujua au kutokujua.

Mtume Paulo alisema kwa uongozo wa Roho, kuwa mtu yeyote asiye na shughuli yoyote katika Mwili wa Kristo, yaani asiyefanya kazi yoyote ya Madhabahuni  kama Uchungaji, Uinjilisti, au Shemasi, au Mzee wa kanisa au ya Uinjilisti, au mfanya kazi wa kanisani (inayomfanya muda wake mwingi atumie kuhubiri) mtu huyo basi asipewe fungu lolote kutoka kanisani..

1Wathesalonike 3:10 “ Kwa kuwa hata wakati ule tulipokuwapo kwenu tuliwaagiza neno hili, kwamba ikiwa mtu hataki kufanya kazi, basi, asile chakula.

11  Maana twasikia kwamba wako watu kwenu waendao bila utaratibu, hawana shughuli zao wenyewe, lakini wanajishughulisha na mambo ya wengine.

12  Basi twawaagiza hao, na kuwaonya katika Bwana Yesu Kristo, watende kazi kwa utulivu na kula chakula chao wenyewe”

Kumbuka pia unapoamua kufanya kazi za Mikono, basi huwezi kuwa Mchungaji kwa wakati huo huo, kwasababu huwezi kushikilia mambo mawili kwa wakati mmoja.. Ni aidha ushikilia moja uache lingine! Huwezi kuwa mchungaji na huku ni Mbunge, huwezi kuwa Mchungaji na huku ni Mfanya biashara mashuhuri.. jambo hilo haliwezekani!, haijalishi mtu atalilazimisha kiasi gani?.

Mathayo 6:24  “Hakuna mtu awezaye kutumikia mabwana wawili; kwa maana atamchukia huyu, na kumpenda huyu; ama atashikamana na huyu, na kumdharau huyu. Hamwezi kumtumikia Mungu na mali”

Tofauti na inavyodhaniwa na wengi kwamba Mtume Paulo alikuwa anafanya kazi muda wote!, kwamba alikuwa anashona Mahema kila wakati ili kujipatia riziki, nataka nikuambie kuwa haikuwa hivyo, ni sehemu chache sana ndizo alizokuwa anashona mahema, lakini sehemu kubwa ya maisha ya Paulo ilikuwa ni kuhubiri injili, na Mungu alikuwa anamfungulia milango ya riziki kupitia injili hiyo, na alikuwa haombi kwa watu fedha wala mali, (ili awe kielelezo) bali watu walikuwa wanampa kwa kadiri wanavyoguswa.

Tunalithibitisha hilo katika kitabu cha Wafilipi, 4:1-19, (Zingatia Mistari iliyoainishwa kwa herufi kubwa)

Wafilipi 4:14  “Lakini mlifanya vema, mliposhiriki nami katika dhiki yangu.

15  Nanyi pia, ninyi wenyewe mnajua, enyi Wafilipi, ya kuwa katika mwanzo wa Injili, nilipotoka Makedonia, hakuna kanisa lingine lililoshirikiana nami katika HABARI HII YA KUTOA NA KUPOKEA, ila ninyi peke yenu.

16  KWA KUWA HATA HUKO THESALONIKE MLINILETEA MSAADA KWA MAHITAJI YANGU, WALA SI MARA MOJA.

17  Si kwamba nakitamani kile kipawa, bali nayatamani mazao yanayozidi kuwa mengi, katika hesabu yenu.

18  Lakini ninavyo vitu vyote na kuzidi, tena nimejaa tele; NIMEPOKEA KWA MKONO WA EPAFRODITO VITU VILE VILIVYOTOKA KWENU, HARUFU YA MANUKATO, SADAKA YENYE KIBALI, IMPENDEZAYO MUNGU.

19  Na Mungu wangu atawajazeni kila mnachokihitaji kwa kadiri ya utajiri wake, katika utukufu, ndani ya Kristo Yesu”

Umeona hapo ? Sio wakati wote Paulo alikuwa anafanya kazi ya kushona, Soma pia 2Wakorintho 8:1-5..

Lakini biblia inatufundisha nini katika hali tulizopo (yaani ya kufanya kazi ya Mikono au ya Madhabahuni)?

Biblia imetufundisha kutumika kwa uaminifu popote pale tunapopatumikia, maana yake kama ni Mtumwa basi tumika ipasavyo kwa Bwana wako (maana yake Boss wako, au Mkubwa wako) kana kwamba unamtumikia Kristo.

Waefeso 6:5  “Enyi watumwa, watiini wao walio bwana zenu kwa jinsi ya mwili, kwa hofu na kutetemeka, kwa unyofu wa moyo, kana kwamba ni kumtii Kristo;

6  wala si kwa utumwa wa macho tu kama wajipendekazao kwa wanadamu bali kama watumwa wa Kristo, mkitenda yampendezayo Mungu kwa moyo;

7  kwa nia njema kama kumtumikia Bwana wala si mwanadamu;

8  mkijua ya kuwa kila neno jema alitendalo mtu atapewa lilo hilo na Bwana kwamba ni mtumwa au kwamba ni huru”.

Vile vile kama tunatumika katika utumishi wowote ule.. Maandiko yanatufundisha  KURIDHIKA, Maana yake TUSIJISIKIE VIBAYA kutumika pale tulipopachagua sisi, kwasababu ni mapenzi ya Mungu. Kama ni Mfanyakazi wa kuajiriwa maana yake wewe ni Huru kwa kazi ya Bwana ya madhabahuni, hivyo usijisikie vibaya kuifanya kazi hiyo, kilicho kikubwa na cha muhimu ni wewe kuwa Mwaminifu katika kazi unayoifanya na pia katika kumtolea Bwana, na mwisho wa siku utapokea thawabu kutoka kwa Mungu, vile vile kama wewe ni mtumishi wa Madhabahuni au wa Injili, maana yake wewe ni Huru katika utumishi wa kazi za kidunia, hivyo basi usijisikie vibaya kutumika hivyo, maana ni Mungu kakuita katika hali hiyo, wala usiitamani kazi nyingine zaidi ya hiyo uliyopewa!.  

1Wakorintho 7:21  “Je! Uliitwa u mtumwa? Usione ni vibaya lakini kama ukiweza kuwa na uhuru, afadhali kuutumia.

22  Kwa maana yeye aliyeitwa katika Bwana hali ya utumwa, ni huru wa Bwana. Vivyo hivyo yeye naye aliyeitwa hali ya uhuru, ni mtumwa wa Kristo.

23  Mlinunuliwa kwa thamani; msiwe watumwa wa wanadamu”

Maran atha!

Tafadhali shea na wengine ujumbe huu;

Pia Kwa maombezi/ Ushauri/ Maswali/ Whatsapp:
Tuandikie katika BOXI la Maoni hapo chini au
Piga namba hizi: +255693036618 au +255789001312

Mada Nyinginezo:

REKEBISHA YAFUATAYO ILI UCHUMI WAKO UKAE SAWA.

MAOMBI YA KUFUNGULIWA KIUCHUMI.

Orodha ya mistari ya biblia kuhusu watoto.

Kwanini iwe ni nchi ibubujikayo maziwa na asali?

Biblia inapotumia neno “Bila kazi ya mikono”, ina maana gani?

Rudi nyumbani

Print this post

IJUE HEKIMA YA MUNGU KATIKA KUKUINUA KIMAISHA.

Ipo hekima ambayo Mungu anaitumia, pindi anapotaka kututoa katika hatua moja ya kimaisha kwenda nyingine.

Kiasili, nafsi zetu sisi wanadamu zinapenda kupokea majibu ya maombi pale tu tunapoomba… Lakini hekima ya Mungu wakati mwingine si kutupa kile tunachokiomba wakati ule ule tunapoomba… Wakati mwingine inaweza kuchukua muda mrefu kupokea majibu, na bado ikawa ni mapenzi ya Mungu.

Yapo mambo ambayo tukimwomba Mungu, ni rahisi kupokea majibu papo kwa hapo, lakini yapo ambayo yatachukua muda kujibiwa!..Sasa si kwasababu Mungu hawezi kujibu papo hapo! La!, anaweza kwasababu hakuna kinachomshinda yeye, lakini anapoyachelewesha wakati mwingine kwa faida yetu.

Hebu tengeneza picha, mtoto wa miaka 6 ambaye hajui hata kusoma, anamwomba Baba yake ambaye ni tajiri sana, ampe gari!.. Ni kweli Baba yake anao uwezo wa kumpa gari pale pale alipoomba, lakini hawezi kumpa kwasababu bado hajajua hata kusoma, atawezaje kuendesha hilo gari?..kwasababu aendapo akipewa gari katika akili hiyo aliyonayo, kitakachofuata ni Ajali!.. na mzazi atakuwa amemwua mtoto wake, badala ya kumpa uzima!..

Kwahivyo Ni sharti kwanza aende darasani akafundishwe kusoma na kuandika, na hesabu.. halafu akishajua hayo yote, ndipo aende kwenye shule ya udereva, akajifunze kanuni za uendeshaji magari, na baada ya kuhitimu na kupata leseni, ndipo baba yake ampe gari!..

Hivyo zoezi zima hilo la kusoma mpaka kupata leseni mpaka siku ya kukabidhiwa gari, linaweza kuchukua miaka hata 10. Kwahiyo ni sawa na kusema kwamba, mtoto kajibiwa ombi lake la kupewa gari baada ya miaka 10.

Lakini endapo mtoto Yule angeomba “peremende” kwa Baba yake, ni dhahiri kuwa “angepatiwa muda ule ule alioomba”.

Na kwa Mungu wetu ni hivyo hivyo, yapo mambo ambayo tukiomba tutajibiwa wakati huo huo, lakini yapo mambo mengine yatachukua muda mrefu sana, hata miaka kadhaa kujibiwa!!…

Hivyo kama umezoea kumwomba Mungu jambo na kupokea majibu yake saa hiyo hiyo, na ukamwomba jambo lingine ukaona hujajibiwa muda huo huo kama unavyotaka wewe!!.. Fahamu kuwa sio kwamba Mungu kakunyima hilo jambo, au kwamba hajasikia maombi yako!.. Amesikia maombi yako, na tayari majibu kashayaachia, lakini yatakuja kudhihirika siku nyingi za mbeleni endapo ukidumu katika kuishikilia ahadi hiyo.

Hebu tujifunze mfano mmoja juu ya wana wa Israeli, kipindi wanatoka Misri..

Tunasoma katika maandiko kuwa, kipindi wanaingia Kaanani, Mungu hakuwatoa wakaanani katika ile nchi ndani ya siku moja, au ndani ya mwaka mmoja, biblia inasema ilichukua miaka kadhaa, Mungu kuwaondoa Wakaanani na wengineo waliokuwa wanaikalia ile nchi ya Ahadi.

Sasa ni kwasababu gani Mungu hakuwaondoa Wakaanani wote na wahivi wote ndani ya siku moja??..Jibu: Si kwasababu hakuwa na uwezo huo, alikuwa nao tele, lakini kwafaida ya watoto wake Israeli, ilikuwa hana budi kuwapa urithi huo kidogo kidogo!…kwasababu angewapa siku ile ile, basi yangezuka matatizo mengine, ambayo tunayasoma katika mistari ifuatayo…

Tusome,

Kutoka 23: 27 “Nitatuma utisho wangu utangulie mbele yako, nami nitawafadhaisha watu wote utakaowafikilia, nami nitawafanya hao adui zako wote wakuonyeshe maungo yao. 

28 Nami nitapeleka mavu mbele yako, watakaomfukuza Mhivi, na Mkanaani, na Mhiti, watoke mbele yako. 

29 SITAWAFUKUZA MBELE YAKO KATIKA MWAKA MMOJA; NCHI ISIWE UKIWA, NA WANYAMA WA BARA WAKAONGEZEKA KUKUSUMBUA. 

30 NITAWAFUKUZA KIDOGO KIDOGO MBELE YAKO, HATA UTAKAPOONGEZEKA WEWE, NA KUIRITHI HIYO NCHI” 

Umeona hapo?..Sababu ya wao kutopewa Nchi yote ndani ya siku moja, ni lli wanyama wasiongezeke juu ya nchi, na kuwaletea madhara.. Kwasababu kipindi wanatoka Misri, walikuwa wachache.. halafu wanakwenda kupewa nchi kubwa!.. ni lazima sehemu kubwa ya nchi hiyo itakuwa MAPORI!.. Kwasababu hakuna watu wa kuijenga wala kukaa juu yake..na hivyo Nyoka wataongezeka, chatu na fisi wataongezeka, watakaokula mifugo yao..hali kadhalika samba na mbu!, watakuwa wengi kwasababu ya wingi wa mapori, na hivyo itanyanyuka shida nyingine..

Kwahiyo hekima ya Mungu, ikaamua maadui wa Israeli wasifukuzwe wote, bali waachwe kwanza kwa kitambo kifupi, waendelee kufyeka mapori, mpaka idadi ya Israeli itakapoongezeka, kufikia kiwango cha kuweza kuitawala nchi nzima, ndipo maadui wote waondolewe!.

Na sisi ni nini tunajifunza hapo?…tunajifunza kuwa wavumilivu, na kuwa na Subira katika ahadi za Mungu na kwamba si kila ombi litajibiwa siku tunayoitaka sisi.

Ikiwa wewe ni binti au kijana, na umemwomba Mungu akupe mwenza wa maisha, na unaona hujibiwi kwa wakati unaotaka wewe, huenda ni kwasababu wakati wake haujafika! Aidha Umri wako ni mdogo, au pengine akili yako bado haijakuwa vya kutosha, bado haijafundishwa vya kutosha maisha ya ndoa,.. Na ili Mungu asikupoteze ndio maana hakupi unachotaka kwa wakati huo huo.

Vile vile Ukimwomba Mungu mali na huku akili yako inawaza kwenda kujionyesha mbele za watu, fahamu kuwa Mungu ameshasikia maombi yako, lakini hutapokea saa hiyo hiyo, ulipopmba…badala yake utakwenda kwanza kwenye madarasa yake ambayo atakufundisha maisha ukiwa na mali, (huenda yakachukua hata miaka 20), inategemea na akili yako, na ukifaulu madarasa yake! basi atakupatia!..kwasababu utakuwa umeshajengeka vya kutosha, kiasi kwamba mali haziwezi kukuangusha wala kukurudisha nyuma kiroho, wala kuwaharibu wengine.

Na maombi mengine yote ni hivyo hivyo..yanayo hatua mpaka tuone matokeo, hivyo tuwe wavumilivu na watu wa subira..

Bwana Yesu atubariki.

Maran atha!

Tafadhali shea na wengine ujumbe huu;

Pia Kwa maombezi/ Ushauri/ Maswali/ Whatsapp:
Tuandikie katika BOXI la Maoni hapo chini au
Piga namba hizi: +255693036618 au +255789001312

Mada Nyinginezo:

IJUE SIRI YA UTAUWA.

HEKIMA NI NINI? NA UFAHAMU UNAPATIKANA WAPI?

Tofauti kati ya lijamu na hatamu ni ipi kibiblia?

Kigao ni nini? Na Je kinafunua nini kwa agano jipya?

Tofauti kati ya Hekima, ufahamu na maarifa, ni ipi?

Rudi nyumbani

Print this post

MAOMBI YA KUFUNGULIWA KIUCHUMI.

Kabla ya kwenda katika maombi Awali ya yote ni vizuri ukafahamu kuwa mafanikio ya kiuchumi yanaweza kuletwa na vitu vikuu vitatu

  1. Mwanadamu mwenyewe.
  2. Shetani.
  3. Mungu.

Na kila mmoja anayo kanuni yake ya kuyafikia hayo mafanikio.

Kwamfano kwa mwanadamu, ili aweze kujikomboa kiuchumi, kanuni ni moja nayo ni “kuwa na bidii katika kufanya kazi”..haijalishi kazi hiyo itakuwa ni ya kuuza pipi, maadamu unatia bidii ndani yake, utafanikiwa kwasababu  katika bidii hiyo, huko huko ndio unazalika ubunifu  na mikakati, ya kupiga hatua, na kuwekeza,n.k. na mwisho wa siku utafanikiwa, Hata kama hatofikia utajiri ule, lakini mwisho wa siku utajikomboa kiuchumi, haijalishi atafanya hivyo kwa muda gani. Na hapo atakuwa tayari kashajikomboa kiuchumi.

Lakini kanuni za ibilisi ni tofauti na zile za kibinadamu. Pengine kwake si lazima ujishughulishe sana, lakini akakupa mafanikio tu, Kwasababu ndicho alichojaribu kufanya kwa Bwana Yesu, kwa kumwambia  tu amsujudie ndipo atakapompa mali zote.

Mathayo 4:9 “akamwambia, Haya yote nitakupa, ukianguka kunisujudia.”

Unapokwenda kwa waganga watakupa mafanikio, lakini wakiwa na masharti yao kwamba ni lazima ufanye kitu fulani kwa shetani n.k..

Lakini tunaporudi kwa Mungu, napo pia kuna kanuni zake, za kufanikiwa. Ukienda nje ya hizo, na huku unahitaji mafanikio, au kukombolewa kiuchumi usijidanganye, unapoteza muda. Nenda tu kajibidiishe huko kama wanadamu wengine, utafanikiwa pia kwa njia hizo.

Lakini Kanuni za Mungu za kumkomboa mtu kiuchumi  ni zipi?;

Kabla ya kuombewa ni lazima uwe mwana wake. Na mtu anakuwa mwana wake kwa kutubu dhambi zake zote, na kubatizwa, kisha kupokea Roho Mtakatifu. Na baada ya hapo kuanzia huo wakati na kuendelea kuishi maisha yampendezayo Mungu.

Biblia inasema..

Mathayo 6:31 “Msisumbuke, basi, mkisema, Tule nini? Au Tunywe nini? Au Tuvae nini?

32 Kwa maana hayo yote Mataifa huyatafuta; kwa sababu Baba yenu wa mbinguni anajua ya kuwa mnahitaji hayo yote.

33 Bali utafuteni kwanza ufalme wake, na haki yake; na hayo yote mtazidishiwa”.

Unaona? Ukishautafuta kwanza ufalme wake na haki yake, kuanzia huo wakati unakuwa tayari sasa, kushiriki Baraka zote kutoka kwa Mungu, kiwepesi  pale unapomwomba.

Neno la Mungu linasema hivi..

2Wakorintho 8:9 “Maana mmejua neema ya Bwana wetu Yesu Kristo, jinsi alivyokuwa maskini kwa ajili yenu, ingawa alikuwa tajiri, ili kwamba ninyi mpate kuwa matajiri kwa umaskini wake”.

Na pia Yesu mwenyewe alisema..

Mathayo 19:28 “Yesu akawaambia, Amin, nawaambia ya kwamba ninyi mlionifuata mimi, katika ulimwengu mpya, atakapoketi Mwana wa Adamu katika kiti cha utukufu wake, ninyi nanyi mtaketi katika viti kumi na viwili, mkiwahukumu kabila kumi na mbili za Israeli.

29 Na kila mtu aliyeacha nyumba, au ndugu wa kiume au wa kike, au baba, au mama, au watoto, au mashamba, kwa ajili ya jina langu, atapokea mara mia, na kuurithi uzima wa milele.

30 Lakini wengi walio wa kwanza watakuwa wa mwisho, na walio wa mwisho watakuwa wa kwanza”.

Hivyo kabla ya kwenda kukuombea Baraka zako kutoka kwa Mungu.. ni sharti kwanza uwe  tayari leo kumkabidhi Bwana Yesu maisha yako, kwa kumaanisha kabisa. Kama upo tayari basi hapo ulipo tafuta sehemu yenye utulivu, kisha piga magoti, kisha sema sala hii kwa imani, kwa kumaanisha kabisa, na Mungu atakuokoa siku ya leo.

EE MUNGU BABA, NAJA MBELE ZAKO, NIKIWA NINAJITAMBUA KUWA MIMI NI MKOSAJI NA NIMEKUTENDA DHAMBI NYINGI, NA KWAMBA NIMESTAHILI HUKUMU. LAKINI WEWE MUNGU WANGU ULISEMA KATIKA NENO LAKO KUWA WEWE NI MUNGU WA REHEMA UNAYEWAREHEMU  MAELFU ELFU YA WATU WANAOKUPENDA WEWE. NA LEO HII NINAKUJA MBELE ZAKO NAHITAJI MSAMAHA WAKO NA MSAADA WAKO MUNGU WANGU, NINATUBU DHAMBI ZANGU ZOTE KWA KUMAANISHA NA KWA MOYO WANGU WOTE, NINAKIRI KUWA YESU KRISTO NI BWANA, NA YEYE NDIYE MWOKOZI WA HUU ULIMWENGUNI. HIVYO NAOMBA DAMU YA MWANAO TAKATIFU INISAFISHE UOVU WANGU WOTE SASA NIFANYIKE KUWA KIUMBE KIPYA KUANZIA LEO NA HATA MILELE.

ASANTE BWANA YESU KWA KUNIPOKEA NA KUNISAMEHE.

AMEN.

Sasa kwa sala hiyo fupi, amini kuwa Bwana Yesu ameshakusamehe, Na kuanzia sasa unakuwa tayari kushiriki, Baraka zote kutoka kwa Mungu.

Yeye mwenyewe alisema maneno haya;

Kumbukumbu: MLANGO 28

1 Itakuwa utakaposikia sauti ya Bwana, Mungu wako, kwa bidii, kutunza kuyafanya maagizo yake yote nikuagizayo leo, ndipo Bwana, Mungu wako, atakapokutukuza juu ya mataifa yote ya duniani;

2 na baraka hizi zote zitakujilia na kukupata usikiapo sauti ya Bwana, Mungu wako.

3 Utabarikiwa mjini, utabarikiwa na mashambani.

4 Utabarikiwa uzao wa tumbo lako, na uzao wa nchi yako, na uzao wa wanyama wako wa mifugo, maongeo ya ng’ombe wako, na wadogo wa kondoo zako.

5 Litabarikiwa kapu lako, na chombo chako cha kukandia unga.

6 Utabarikiwa uingiapo, utabarikiwa na utokapo.

7 Bwana atawafanya adui zako wainukao juu yako kupigwa mbele yako; watakutokea kwa njia moja, lakini watakimbia mbele yako kwa njia saba.

8 Bwana ataiamuru baraka ije juu yako katika ghala zako, na mambo yote utakayotia mkono wako; naye atakubarikia katika nchi akupayo Bwana, Mungu wako.

9 Bwana atakuweka uwe taifa takatifu kwake, kama alivyokuapia; utakaposhika maagizo ya Bwana, Mungu wako, na kutembea katika njia zake.

10 Na mataifa yote ya duniani watakuona umeitwa kwa jina la Bwana, nao watakuwa na hofu kwako.

11 Bwana atakufanya uwe na wingi wa uheri, katika uzao wa tumbo lako, na uzao wa wanyama wako wa mifugo, na uzao wa nchi yako, katika nchi Bwana aliyowaapia baba zako kwamba atakupa.

12 Atakufunulia Bwana hazina yake nzuri, nayo ni mbingu, kwa kutoa mvua ya nchi yako kwa wakati wake, na kwa kubarikia kazi yote ya mkono wako; nawe utakopesha mataifa mengi, wala hutakopa wewe.

13 Bwana atakufanya kuwa kichwa, wala si mkia; nawe utakuwa juu tu, wala huwi chini; utakapoyasikiza maagizo ya Bwana, Mungu wako, nikuagizayo hivi leo, kuyaangalia na kufanya;

14 msipokengeuka katika maneno niwaamuruyo leo kwa lo lote, kwenda mkono wa kuume wala wa kushoto, kwa kuifuata miungu mingine na kuitumikia.

Baraka hizo zote, zitakufuata endapo utadumu tu katika WOKOVU.

Basi sasa, nitakuombea, ili milango hii ifunguke, katika maisha yako. Hapo ulipo Piga tena magoti, niombe kwa ajili yako. Fuatisha kwa sauti sala hii;

Baba Mwenyezi, Mungu wa milele, ahsante kwa kutupa zawadi ya kutuletea mkombozi duniani, Bwana wetu Yesu Kristo. Asante kwa kuwa alikuja kutukomboa kutoka katika dhambi zetu na laana zetu. Lakini hakuishia hapo tu, bali alitukomboa, mpaka na UCHUMI wetu.

Nami leo hii nimempokea na kumkiri kwa kumaanisha kabisa kumfuata tangu sasa hadi milele. Naomba Mungu wako zile Baraka zote ulizoziahidi katika Kumbukumbu la Torati 28:1-14, zinijilie juu yangu. Nami nikawe Baraka kwa jamii na kwa kanisa lako. Kuanzia sasa ikiwa kuna kazi zozote za ibilisi zilizotangulia nyuma yangu kunizuilia Baraka zangu, ninazikataa kwa jina la Yesu Kristo. Naiita Damu ya Yesu ikasafishe kapu langu, na mfuko wangu.

Asante Mungu wangu kwa kunikomboa.

Amen.

Basi, ikiwa umeyafuatilisha maombi hayo, ujue kuanzia sasa, Mungu atatembea na wewe katika uchumi wako, kwa kile unachokifanya, tenda mapenzi ya Mungu, utaona akikupigania. Lakini kumbuka Kama tulivyotangulia kusema, inahitaji Kutembea na Mungu ili akukamilishie ahadi hizo, sio tu kukiri kwa mdogo, unakwenda kuendelea na mambo yako..nikuambie ukweli tu, inahitaji maisha.

Mungu akubariki sana.

Ikiwa utahitaji msaada zaidi wa kumjua Mungu, au ubatizo, au unaswali lolote kuhusu biblia,  basi wasiliana nasi kwa namba zetu hizi Simu/Whatsapp: +255693036618 /  +255789001312

Mada Nyinginezo:

REKEBISHA YAFUATAYO ILI UCHUMI WAKO UKAE SAWA.

TWEKA MPAKA VILINDINI.

NI YESU YUPI UMEMPOKEA?, NI ROHO IPI UMEIPOKEA? NA INJILI IPI UMEIPOKEA?

HUTATAMBUA LOLOTE, SIKU YA UNYAKUO IKIFIKA.

Rudi nyumbani

Print this post

REKEBISHA YAFUATAYO ILI UCHUMI WAKO UKAE SAWA.

Jina la Bwana Yesu libarikiwe, karibu tujifunze biblia, Neno la Mungu wetu.
Leo tutajifunza, mambo Matatu ambayo, kama Mkristo ukiyarekebisha hayo basi uchumi wako utaimarika zaidi.

1. KUWA MWAMINIFU KWA MUNGU WAKO.

Dawa ya kwanza ya mafanikio yoyote yale, yawe ya kimwili au kiroho, ni kuwa MWAMINIFU KWA BWANA.

Mithali 3:7
“ Usiwe mwenye hekima machoni pako;
Mche BWANA, ukajiepushe na uovu.

8 Itakuwa afya mwilini pako,
Na mafuta mifupani mwako.

Kumcha Bwana ni kuishi maisha matakatifu na yanayompendeza yeye, ambayo Nuru yako inakuwa inaangaza kila mahali.
Jambo moja kubwa wakristo wengi wasilolijua ni kwamba, tumewekwa ulimwenguni ili tuhubiri injili, licha ya kwamba Mungu anataka sisi tupate faida katika mambo yetu kutoka kwake, lakini pia Mbingu inategemea kupata faida kutoka kwetu.. Na faida yenyewe ni sisi kuwavuta wengine waingie katika ufalme.

Kwahiyo maana yake ni kwamba kama wewe unafanya biashara, au kazi yoyote ya kuajiriwa au kujiajiri.. Mungu anategemea maisha yako yawe sababu ya kuwavuta wengine.

Hivyo Bwana akikuamini, atakuvutia watu wengi kwako, kama ni wateja au watu wa fursa wakujie, lengo si tu waje kununua bidhaa zako, au kukupa wewe fursa, bali Mungu anawasogeza kwako ili wapate kuiona nuru yako na wamgeukie Mungu na kutubu..Hivyo wewe unafanyika daraja la wao kumfikia Mungu zaidi.

Lakini kama wewe maisha yako hayana ushuhuda wowote,maana yake ni maisha ya uzinzi, ya wizi, ya ulevi, utukanaji, umbea, usengenyaji n.k.

maana yake Mungu akikuletea watu, ni sawa na kampelekea shetani kondoo..Hivyo ili awalinde watu wake wasizidi kupotea, anazuia wateja wasije kwako, kwasababu utawaharibu kwa tabia zako..na Mungu hapendi watu wake wapotee.

Atawazuia wasije kwako, na atawapeleka kwa watu wengine wenye staha zaidi..Huku nyuma wewe utabaki kufikiri umelogwa, kumbe ni wewe mwenyewe umejiharibu kwa kutokuwa mwaminifu kwa Mungu wako.

Mathayo 5:14
“Ninyi ni nuru ya ulimwengu. Mji hauwezi kusitirika ukiwa juu ya mlima.

15 Wala watu hawawashi taa na kuiweka chini ya pishi, bali juu ya kiango; nayo yawaangaza wote waliomo nyumbani.

16 Vivyo hivyo nuru yenu na iangaze mbele ya watu, wapate kuyaona matendo yenu mema, wamtukuze Baba yenu aliye mbinguni”.

Angaza Nuru yako ili milango ifunguke.

2. KUWA MWAMINIFU KATIKA KAZI UNAYOIFANYA.

Hili ni jambo la pili ambalo, ni muhimu kulijua.

Wengi wetu hatujui kuwa Mungu si Mungu wa kuwadhuru watu, bali wa kuwapatia watu mema.. Mteja yeyote Mungu anayemleta kwako, ni kwasababu Mungu anataka apate huduma bora ya viwango, ili aweze kumshukuru Mungu baada ya hapo, na Mungu apokee shukrani zake..

lakini hawezi kumleta kwako wewe unayeuza kitu kilichoisha muda wake wa matumizi (kime-expire). Hapo Mungu atakuwa muuaji na mkatili na si Mungu mwenye fadhili..

Alisema..

Mathayo 7:9
“9 Au kuna mtu yupi kwenu, ambaye, mwanawe akimwomba mkate, atampa jiwe?

10 Au akiomba samaki, atampa nyoka?

11 Basi ikiwa ninyi, mlio waovu, mnajua kuwapa watoto wenu vipawa vyema, je! Si zaidi sana Baba yenu aliye mbinguni atawapa mema wao wamwombao?”

Hiyo ndio maana watu wateja hawawezi kuja kwako, kwasababu Mungu hawezi kuwaongoza watoto wake kwenda kula sumu, au vitu vilivyo chini ya ubora..vinginevyo atakuwa mwongo hapo aliposema.. “Basi ikiwa ninyi, mlio waovu, mnajua kuwapa watoto wenu vipawa vyema, je! Si zaidi sana Baba yenu aliye mbinguni atawapa mema wao wamwombao?”.

Hebu tengeneza picha wewe umeamka asubuhi, na kumwomba Baba akulinde na yule mwovu na pia akupe riziki njema..halafu unatoka hapo Mungu anakuongoza kwenda kununua Soda iliyo-expire! Kwenye duka la mtu fulani…huyoo Mungu si atakuwa mkatili sana?..

Hivyo ili Mungu kumpa mtoto wake kipawa chema sawasawa na Neno lake hilo, atamwepusha kuja kwenye duka lako, au kukupa wewe ajira..badala yake anampeleka kwenye duka lingine au kumpa mtu mwingine ajira ambaye atatoa huduma iliyo bora na kuleta faida katika ufalme wa mbinguni.

Hiyo ndio sababu wakristo wengi Mungu anaifunga milango ya riziki katika biashara zao, au katika mambo yao mengine na kuishia kudhani wamelogwa, na kuzunguka huku na huko kutafuta maombezi kumbe ni kwasababu wao wenyewe sio waaminifu katika kazi zao na hawatoi huduma iliyo bora!.

Na vile vile kuwa mwaminifu katika kumtolea Mungu, maandiko yanasema wote wasiomtolea Mungu zaka ni wezi, wanamwibia Mungu..hivyo Mungu hawezi kuwabariki wezi.

Malaki 3:8 “Je! Mwanadamu atamwibia Mungu? Lakini ninyi mnaniibia mimi. Lakini ninyi mwasema, Tumekuibia kwa namna gani? Mmeniibia zaka na dhabihu.

9 Ninyi mmelaaniwa kwa laana; maana mnaniibia mimi, naam, taifa hili lote”

Mithali 3:9 “Mheshimu BWANA kwa mali yako,Na kwa malimbuko ya mazao yako yote.

10 Ndipo ghala zako zitakapojazwa kwa wingi, Na mashinikizo yako yatafurika divai mpya”.

3. IMARISHA KAZI YAKO, AU UJUZI WAKO.

Hili ni jambo lingine pia la muhimu kujua.
Wengi wetu hatupendi kuziimarisha kazi zetu, au ni walegevu katika kuziimarisha, wakati mwingine tukidhani si mpango wa Mungu.

Lakini leo nataka nikuambie kuwa kuiimarisha kazi yako, ni jambo la muhimu sana na la kimaandiko.

Kila siku buni na tafuta mbinu mpya na ongeza ujuzi katika shughuli unayojishughulisha nayo au unayoifanya..hayo ni mapenzi ya Mungu pia!

Bwana Mungu baada ya kuimaliza kazi yake ya uumbaji pale Edeni, alipumzika, lakini baada ya kipindi fulani alinyanyuka tena na kusema..”Si vyema mtu huyu awe peke yake nitamfanyizia msaidizi wa kufanana naye”.Ndipo akamletea Hawa kama msaidizi.

Kadhalika na sisi hatuna budi kusema siku zote “si vyema kazi hii ikabaki yenyewe, basi niongeze nyingine kama hii, na nyingine na nyingine”.

Si vyema kazi hii iwe kama ilivyokuwepo mwaka jana, basi nitaiimarisha hivi na hivi..si vyema ujuzi huu nilionao nikaendelea nao, basi nitauongeza tena na tena..

Kwa kufanya hivyo, Bwana atakubariki kwasababu na yeye pia anafanya matengenez kila siku katika maisha yetu.
Haya ndiyo mambo makuu matatu yanayozuia uchumi wetu kusonga mbele.

Na yaliyo ya muhimu zadi ni hayo mawili ya kwanza.

Tofauti na wengi wanaofikiri kwamba matatizo mengi yanasababishwa na uchawi.

Uchawi wa kwanza shetani anaologa nao mtu sio kuifanya biashara yake isifanikiwe..anachokifanya cha kwanza, na tena anakifanya kwa bidii ni kumfanya MTU AWE MTENDA DHAMBI!.

Kwasababu anajua Dhambi ndio mzizi na chanzo chaatatizo yote na shida na dhiki.

Mtu aliyejitenga na dhambi kamwe shetani hamwezi, na wala hakuna uchawi mwingine wowote utakaoweza kufanya kazi juu yake.

Lakini kama mtu hajajitenga na dhambi, basi uchawi mwingine wowote utafanya kazi juu yake na kumletea madhara.

Swali ni je?

WEWE NI MWAMINIFU KWA MUNGU?…NA JE! NI MWAMINIFU KATIKA KAZI YAKO?..NA JE UMEJITENGA NA DHAMBI?

Kumbuka hakuna mtu yeyote kwa nguvu zake anaweza kuishinda dhambi, Bali tunaishinda dhambi kwa Kumwamini kwanza Bwana Yesu, kwamba yeye ni Bwana na Mwokozi na anaweza kutusamehe dhambi zetu na kutuosha..

Kwa kumwamini huko, na kubatizwa basi yeye mwenyewe anaingia ndani yetu, na kutupa huo UWEZO WA KIPEKEE WA KUSHINDA DHAMBI, ambao unatufanya kuwa Wana wa Mungu.

Yohana 1:12 “ Bali wote waliompokea aliwapa uwezo wa kufanyika watoto wa Mungu, ndio wale waliaminio jina lake”.

Uwezo huo unatufanya tuwe watu wengine tofauti na tulivyokuwa hapo kwanza..Ndio hapo zile pombe tulizokuwa hatuwezi kuziacha ghafla tunajikuta tunaweza kuziacha, ule uasherati tuliokuwa tunaona ni mgumu kuuacha tunajikuta tunaushinda, yale matusi ambayo tulikuwa tunaona ni mepesi kuyatamka ulimini mwetu tunajikuta hatuyatoi tena vinywani mwetu n.k.

Bwana atubariki.

Maran atha!

Group la whatsapp Jiunge na magroup yetu ya whatsapp kwa kubofya hapa > Group-whatsapp

Tafadhali washirikishe na wengine habari

hizi njema,

Kwa maombezi/Ratiba za ibada/ Ushauri/ Maswali.
Piga namba hizi: +255693036618 au +255789001312

Jiunge na kundi letu la mafundisho ya Biblia whatsapp kwa kubofya hapa > Group-whatsapp


Mada Nyinginezo:

Rudi nyumbani

Print this post

TOA HUDUMA ILIYO BORA.

Shalom, Jina la Bwana wetu Yesu Kristo libarikiwe. Karibu tujifunze Biblia, Neno la Mungu ambalo ni mwanga wa njia yetu, na taa iongozayo miguu yetu..

Biblia inatuambia katikaAyubu 22:21 “Mjue sana Mungu, ili uwe na amani; Ndivyo mema yatakavyokujia”….Ikiwa na maana kuwa Mema hayawezi kuja wala Amani tusipomjua Mungu vizuri, hivyo moja ya tatizo kubwa linalotukabili sisi wanadamu hususani wakristo ni kutokumjua Mungu vizuri, Hatumjui Mungu anafanyaje kazi, na anawapatiaje watu mema.

Ni Dhahiri kuwa mema mengi tunayoyatafuta ni mema ya hapa duniani, kama vile kuwa na mali, kufanikiwa katika kazi, kupata mume mzuri au mke mzuri wa Maisha, kupata kibali na vingine vingi..Lakini Mema ya ufalme wa Mbinguni ni bora Zaidi na yenye faida mara dufu!

Kwa ufupi leo tujifunze ni kwa namna gani Mungu anawapatia mema watu wake (mema ya hapa duniani).

Biblia inasema Mungu ni Mungu mwenye haki (Zaburi 7:9-11, Zab.11:7, Isaya 45:21), ikiwa na maana kuwa huwapa haki wale wanaostahili haki. Mungu kamwe hawezi kumpa mtu kitu asichokistahili.

Hebu tujifunze kwa mifano kidogo. Inatokea mtu ana biashara yake ya kawaida tu!, na ni Mkristo ambaye ni mwombaji mzuri, na kila siku anaiombea kazi yake, na anatumia mpaka Mafuta, na maji kuiweka wakfu, na pia anayo mpaka picha ya Bwana Yesu nyuma ya ukuta WA jengo la biashara yake, na kila siku kabla ya kuanza kazi anaiombea hata lisaa limoja, lakini bado unakuta pamoja na jitihada zote hizo mambo bado hayaendi vizuri anapata hasara au anaishia kupata mapato kidogo…Sasa yapo mambo mengi yanaweza kusababisha hilo lakini leo tutaangalia jambo kubwa sana linalosababisha matokeo hayo!… Na hilo si lingine Zaidi ya KUTOKUTOA HUDUMA INAVYOSTAHILI.

Unaweza kuwa mkristo mwombaji kweli na mwaminifu katika kuisogeza kazi yako mbele za Mungu, lakini kama hutajifunza kutenda mapenzi ya Mungu katika kazi yako, maombi yako au ya mwingine juu yako hayatasaidia kitu, yatakuwa ni kazi bure, kama ndani ya kazi yako hutatoa huduma nzuri inayovutia, inayostahili wewe kupata faida, kama hutatoa huduma itakayomvutia yule anayetaka kununua kutoka kwako aweze kurudi tena, kama hutakuwa mnyenyekevu, na mtu wa kujishusha katika kazi hiyo, kama hutakuwa mtu wa kupokea ushauri na kuuchuja katika Neno na kuufanyia kazi, kamwe maombi hayatakusaidia chochote, kadhalika kama hutakuwa msafi katika kazi yako, kama hutakuwa ni mpole kwa wateja wako hata ukibandika picha 20 zenye sura zinazofanana na Bwana Yesu nyuma ya ukuta wa jengo hilo, na kuweka stika za Mistari ya biblia 100, hazitasaidia chochote..

Sasa kwanini Vitu hivyo havisaidii chochote katika kukuletea faida?

Ni kwasababu hujajua kuwa Mungu ni Mungu mwenye haki. Na Watumishi wa Mungu wote wanatumika katika kuwapelekea watu huduma njema sharti walifahamu hilo, Mungu hawezi kumtumia mtu kuwapikia uchafu au sumu watu wake!..hivyo kama wewe ni mchafu katika mahali ulipo kwenye kazi yako labda ya Mgahawa, hiyo ndio sababu Mungu hawezi kuinyanyua izidi kusitawi, hapo ili utumike na Mungu kuwalisha watu wake chakula bora ni sharti uwe msafi sana, kwasababu kuna watu wameamka asubuhi kutoka majumbani mwao na huku wamemwomba Mungu awaepushe na hatari zote ikiwemo sumu na uchafu kuingia katika miili yao, sasa Mungu hawezi kuwajibu hao maombi yao kwa kuwaleta kwenye mgahawa wako ambao unapika uchafu na vyakula visivyo na ubora! Kwa kujidanganya kuwa Mungu ameifunika biashara yako..hapana Mungu ni Mungu mwenye haki! Hawezi mtu kumwomba Mkate akampa jiwe!..Mungu hayupo duniani kuwapatia watu mabaya bali mema…

Hivyo ukitaka kazi yako ya mgahawa isitawi usitegemee maombi tu peke yake…Kuwa Msafi wa viwango vya juu sana,kupita wengine..pika chakula freshi na chenye viwango… ndipo Mungu atakufanya kuwa mtumishi wake kuwapatia chakula safi wanadamu wake na utaona wateja ambao hujawahi kuwaona wakimiminika kwenye hiyo kazi yako.

Na kitu kimoja kisichojulikana na wengi, ni kwamba Mungu hatendi kazi kama shetani atendavyo, shetani ndio ana kitu kinaitwa chuma ulete, au mazingaumbwe anatumia kiini macho,kwamba mtu anaweza kupata chochote katika hali hiyo hiyo aliyopo, hata akiwa mchafu, anaweza kutumia nguvu za giza, kuleta wateja..Mungu hana hicho kitu chuma ulete, wala hatumii kiini macho kuwaletea watu wake fedha!..vinginevyo sifa yake ya kuwa Mungu mwenye haki haitakuwepo!.

Kadhalika kama ni duka, Mungu hawezi kukutumia wewe kuwalisha watu vitu vilivyoisha muda wake wa matumizi (vilivyo-expire), hata kama unakesha kwa wiki mara mbili kuiombea, hata kama unaitolea sadaka nyingi kiasi gani, haiwezekani Mungu kukunyanyua.…kwanini hawezi kufanya hivyo kwasababu, yeye sio Mungu wa kuwapa watu sumu..kama tu asivyokuwa Mungu wa watumishi wa uongo (manabii wa Uongo)..Na kadhalika wafanya biashara wa uongo Mungu hawezi kuwa nao, hata wawe waombaji kiasi gani…atawaepusha watu wake na duka lako….

Pia unapokuwa katika kazi yako unapaswa uwe mnyenyekevu, hupaswi kuwa mtu wa hasira na mtukanaji, au mkorofi. Mungu hawezi kukutumia kuwahudumia watu wake uende ukawatukane na kuwazalilisha..Pia unapaswa kuhakikisha unafanya juhudi kufikisha huduma yako mpaka mlangoni mwa wateja wako au wanaohitaji!..Kwasababu hata watumishi wa Mungu wa kweli anaowatumia hutuletea Neno la Mungu mpaka ndani ya mageti yetu kwa unyenyekevu wote, na ndivyo injili ilivyofanikiwa duniani kote…Kadhalika katika kazi yako, kama unauza mkate mfikishie mteja wako mpaka mlangoni, Mungu anapendezwa na watu wanaotua huduma njema, watu wake wahudumiwe mpaka mahali walipo, na mtu anapohudumiwa kwa njia hiyo, moyoni atafurahi na hivyo atamtukuza Mungu na kumshukuru, na akishafurahi na Mungu atafurahiwa na wewe na hivyo kuibarikia hiyo kazi yako izidi kusonga mbele Zaidi..Hapo ndipo atakapomshawishi Yule mtu kuja tena, na Yule mtu kumwambia mtu mwingine, hivyo hivyo mpaka wanakuwa wengi.

Kadhalika Kama ni mjenzi Mungu hawezi kukutumia wewe kuwajengea watu nyumba ambazo zipo chini ya viwango, kwasababu kuna watu wamemwomba Mungu awapatie nyumba zilizobora na fundi aliyemwaminifu na mwenye ujuzi wa kutosha, hivyo ili Ukidhi hiyo nafasi ya kuwa Mtumishi wa Mungu katika eneo hilo, ni sharti ujitahidi kuielewa vyema hiyo kazi kwa kwenda kutafiti mbinu mpya za ujenzi, kuongeza ujuzi wako na kuongeza ustadi…ili Mungu achague kukutumia wewe na si mwingine katika nafasi hiyo, hapo ndipo utakapoona mafanikio makubwa, usikimbilie kutafuta faida ya haraka haraka, …lakini kama hutataka kutafuta kutoa huduma bora yenye viwango, Bwana Mungu atatafuta mtu mwingine hata kama asiye mkristo aliyekidhi hivyo viwango, kuifanya kazi hiyo…..kwahiyo maombi peke yake hayatoshi!. Matendo ndio yenye nguvu zaidi..Inakupasa ujitahidi uwe bora Zaidi ya wengine ili ukawafanyie watu kilicho bora wamtukuze yeye…

Kadhalika na mambo mengine yote yaliyosalia…jambo ni lile lile…. “JITAHIDI KUTOA HUDUMA ILIYO YA VIWANGO VYA KIMBINGUNI ”

Hata unapotafuta kuoa au kuolewa!! Formula ni hiyo hiyo, NI lazima uwe mtakatifu, usipofanya hivyo na kutegemea maombi peke yake, nakuhakikishia hutaolewa wala hutaoa!…au kama utaoa au kuolewa basi utaoa mtu asiyesahihi au kuolewa na mtu asiyesahihi.

Kwanini?

Kwasababu wewe ni mwenye kiburi na mwasherati halafu unamwomba Mungu akupe mume mwenye hofu ya Mungu, mpole, mnyenyekevu, atakayekujali na kukupenda na kukuheshimu, na asiyekuwa mwasherati….Hujui kwamba huyo mume unayemwomba aliye na vigezo hivyo vya hofu ya Mungu, naye pia anamwomba Mungu ampe mke aliye kama yeye alivyo, mwenye hofu ya Mungu kama yeye, msikivu kama yeye alivyo, asiye mwasherati kama yeye, asiye mwenye kiburi na aliye mnyenyekevu…. Sasa Mungu hawezi kumpa mtoto wake nyoka aliyemwomba samaki!…Kwahiyo Mungu atahakikisha anamtafutia Mke mwema yule mwanamume mwenye hofu ya Mungu kama yeye…Na huyo mke atakuwa sio wewe kwasababu wewe huna vigezo hivyo…..Wewe utaishia kupata mwenye vigezo kama vya kwako vya uasherati, kiburi, na kahaba..Lakini ukiwa mtakatifu Mungu atakupatia Mtakatifu mwenzako na wala haitachukua Muda!…Na pia utakatifu ni wajibu!..hatuwi watakatifu tu kwasababu tunatafuta wachumba!..Ni wajibu wetu kuwa watakatifu maadamu tunaitwa wakristo!

Ndio maana Kuna umuhimu wa kumjua sana Mungu, ili mema yakujie…Mungu anataka tufanye kazi ya haki, tupate haki, anataka tuwe watakatifu tuwapate watakatifu, anataka tuwe wakujitoa ndipo na wengine wajitoe kwa ajili yetu…anataka tuwe watu wa kutoa huduma njema ndipo atubariki. Anataka tumjue kwa mapana hayo….Maombi yanafaa sana endapo tutaomba na kutenda!

Zaburi 18:25 “Kwa mtu mwenye fadhili utakuwa mwenye fadhili; Kwa mkamilifu utajionyesha kuwa mkamilifu;

26 Kwake ajitakasaye utajionyesha kuwa mtakatifu; Na kwa mpotovu utajionyesha kuwa mkaidi.”

Bwana akubariki sana!. jiunge na channel yetu Kwa kubofya hapa >> WHATSAPP


Mada Zinazoendana:

UNAWAFAHAMU MANABII WA UONGO?

MJUE SANA YESU KRISTO.

ITAFAKARI VEMA KAZI YA MUNGU


Rudi Nyumbani

Print this post