MAPAMBO YA WANAWAKE WALIOUKIRI UCHAJI WA MUNGU.

MAPAMBO YA WANAWAKE WALIOUKIRI UCHAJI WA MUNGU.

Masomo maalumu kwa wanawake.

Jina la Bwana na Mwokozi wetu Yesu Kristo libarikiwe, karibu tujifunze biblia Neno la Mungu wetu lililo taa na Mwanga wa njia yetu (Zab.119:105).

Je wewe ni mwanamke? Na unapenda upate kibali mbele za watu?..au je wewe ni binti na unatamani upate ndoa, tena iliyo bora na ya Baraka?, au je wewe ni mwanamke uliyeolewa na unatamani ndoa yako Bwana aibariki na pia upate kibali na heshima Zaidi katika ndoa yako?. Kama ndio basi hakikisha unazingatia mapambo!!..

Katika biblia kuna wanawake waliofanya utafiti wa mapambo yaliyo bora na mazuri na yenye mvuto mkubwa, ili kwamba wawe na mvuto wa heshima mbele za watu, wengine ili wapate ndoa nzuri na kibali kwa wenzi wao..na walipoyatumia hayo mapambo wakafanyika kuwa wanawake bora kuliko wote, na wenye kukubalika kuliko wote.

Wanawake hawa hawakutumia mapambo ya kiulimwengu kama kupaka wanja machoni au kupaka rangi mdomoni ili waolewe au waheshimiwe na waume zao, vile vile hawakuvaa nusu uchi ili wavutie mbele ya wanaowatafuta kuoa, wala hawakusuka nywele ili waonekane warembo, wala hawakupaka rangi katika kucha zao, ili wavutie mbele za watu na kupata ndoa, lakini walitumia mapambo ya aina nyingine na hayo hakawapa ndoa wanazozitafuta, yakawapa heshima wanayoitafuta, yakawapa kibali wanachokitaka n.k.

Na mapambo hayo ni yapi…..?

1Petro 3:3 “Kujipamba kwenu, kusiwe kujipamba kwa nje, yaani, kusuka nywele; na kujitia dhahabu, na kuvalia mavazi;

4 bali kuwe utu wa moyoni usioonekana, katika mapambo yasiyoharibika; yaani, ROHO YA UPOLE NA UTULIVU, ILIYO YA THAMANI KUU MBELE ZA MUNGU.

5 MAANA HIVYO NDIVYO WALIVYOJIPAMBA WANAWAKE WATAKATIFU WA ZAMANI, waliomtumaini Mungu, na kuwatii waume zao.

6 Kama vile Sara alivyomtii Ibrahimu, akamwita Bwana; nanyi ni watoto wake, mfanyapo mema, wala hamkutishwa kwa hofu yo yote”.

Nataka tuuangalie huo mstari wa 5 unaosema “MAANA HIVYO NDIVYO WALIVYOJIPAMBA WANAWAKE WATAKATIFU WA ZAMANI”..

Kwahiyo kumbe zamani kulikuwa na wanawake “watakatifu” na “wasio watakatifu”. Na kila kundi lilikuwa na aina yake ya mapambo ili lipate kibali na kuvutia.

Na hapa biblia inatufundisha wanawake wa zamani waliokuwa watakatifu ijapokuwa katika masomo yao kulikuwa na vipodozi vingi, kulikuwa na rangi nyingi za kucha, na za uso na za mdomoni, lakini wao kwa ufunuo waliokuwa nao hawakuchagua mojawapo wa  hayo mapambo, badala yake waliona yana kasoro, hivyo wakachagua mapambo ya ndani ambayo ni UPOLE, HESHIMA, UTII NA UTULIVU.

Wakaona hayo ndio yatakayowafanya waolewe, ndio yatakayowafanya wapendwe na waume zao, ndio yatakayowafanya wapate kibali katika ndoa zao na jamii zao, ndiyo yatakayowafanya waonekane wa thamani, na si kupaka wanja, au kupaka rangi mdomoni, au kujichubua, au kuvaa nusu tupu.

Ndio maana sasa utaona biblia inasema kama vile Sara alivyokuwa mtii kwa Ibrahimu mumewe hata kufikia hatua ya kumwita Ibrahimu “bwana”, Roho hiyo ya unyenyekevu na utii, na utulivu, ndio iliyomfanya Sara awe “mama wa mataifa” na si “wigi kichwani” wala rangi mdomoni, wala hereni sikioni. Kulikuwa na wanawake wengi katika ile nchi, ambao walikuwa wanajiremba na pengine hata kukaribia kufanana na malaika, lakini Ibrahimu hakuwachagua hata mmoja wao!.

Ibrahimu alimchagua Sara kwasababu alikuwa ni mtii, na mtulivu..(alikuwa na mapambo ya ndani)

“5 MAANA HIVYO NDIVYO WALIVYOJIPAMBA WANAWAKE WATAKATIFU WA ZAMANI, waliomtumaini Mungu, na kuwatii waume zao.

6 Kama vile Sara alivyomtii Ibrahimu, akamwita Bwana…”

Vile vile roho ya upole na ya kujisitiri iliyokuwa juu ya Rebeka, ndio iliyomfanya apate kibali kwa Isaka, kiasi kwamba alipofikishwa kwa Isaka, alifunika kichwa chake kwa shela (Mwanzo 24:62-67), ndio iliyomfanya awe mama wa Taifa kuu la Israeli (Yakobo), na si mavazi ya vimini, au ya mgongo wazi,…Na vivyo hivyo wanawake wengine wote watakatifu walitumia mapambo hayo ili kujipatia kibali.

Lakini wale wengine wa kidunia, walitumia mapambo ya nje, yaani.. vipodozi vyote walivyovitaka, waliweka pini katika pua zao, waliweka rangi kwenye kucha na kwenye kope, na midomoni, walipaka wanja machoni, na kupaka hina mwilini na kuweka nywele bandia n.k lakini wengi wa hao waliishia kutamaniwa tu na si kupendwa kama walivyotafuta,

Na wengine waliishia kuonekana kama makahaba, kama Yezebeli, (maana biblia inaonyesha Yezebeli alikuwa ni mwanamke mwenye kupaka uwanja machoni na kupamba kichwa, maana yake kusokota rasta, na kuweka nywele bandia, na ndio maana biblia ikamtaja kama mwanamke kahaba na mchawi soma 2Wafalme 9:22,30, Ufunuo 2:20-22).

Na siku zote mapambo haya mawili hayawezi kwenda pamoja!, ukitumia moja lazima lingine utalikosa…

Ukiwa unapaka uso rangi, unajichubua, unatoboa pua  huwezi kuwa na unyenyekevu, utii, utulivu, au mapambo mengine yote ya ndani huwezi kuwa nayo… ni lazima tu utakuwa na kiburi, tamaa, wivu,.  

Na vile vile huwezi kuwa mtii, mnyenyekevu, mpole (mapambo yote ya ndani) halafu ukavaa nusu uchi, vimini au nguo za kubana…

Ingekuwa mapambo haya mawili yanaweza kwenda pamoja (yaani ya ndani na ya nje) basi biblia isingesema wanawake wasijipambe kwa “mapambo ya nje”, badala yake ingesema “wasijipambe  kwa mavazi ya nje tu pake yake bali pia wajipambe kwa mapambo ya ndani”. Lakini utaona imekosoa moja na kulihakiki lingine, ikiwa na maana kuwa mapambo haya hayawezi kwenda pamoja.

Mama, dada, binti unayetaka kwenda mbinguni?, na unayetaka kupendeza na kupata kibali.. basi zingatia kujipamba kwa mapambo ya ndani na nje jiweke katika hali yako ya asili, uone kama hutapata kazi unayoitafuta, au ndoa, au kibali popote pale uendapo kama ilivyokuwa kwa akina Sara, na wanawake wengine wa kwenye biblia, na Zaidi ya yote pia utaenda mbinguni kwasababu miili yetu ni hekalu la Roho Mtakatifu, na si midoli ya matangazo ya nguo masokoni.

1Timotheo 2:9  “Vivyo hivyo wanawake na wajipambe kwa mavazi ya kujisitiri, pamoja na adabu nzuri, na moyo wa kiasi; si kwa kusuka nywele, wala kwa dhahabu na lulu, wala kwa nguo za thamani;

10  bali kwa matendo mema, kama iwapasavyo wanawake wanaoukiri uchaji wa Mungu”

Bwana akubariki.

Tafadhali shea na wengine ujumbe huu;

Pia Kwa maombezi/ Ushauri/ Maswali/ Whatsapp:
Tuandikie katika BOXI la Maoni hapo chini au
Piga namba hizi: +255789001312 au +255693036618 . jiunge na channel yetu Kwa kubofya hapa >> WHATSAPP

Mada Nyinginezo:

NJIA NYINGINE YA KUPATA REHEMA NA KIBALI KUTOKA KWA MUNGU.

NAFASI YA MWANAMKE KATIKA KANISA

Kwanini wanawake wengi huwa wanalipuka mapepo?

MWANAMKE, BINTI, MAMA. (Sehemu ya 3)

LAKINI SISI HATUKUIPOKEA ROHO YA DUNIA.

Rudi nyumbani

Print this post

About the author

Admin administrator

Subscribe
Notify of
guest
0 Comments
Inline Feedbacks
View all comments