Category Archive Mbigu Mpya na Nchi Mpya

Tofauti kati ya mbinguni, peponi, Kuzimu, Jehanamu, na Paradiso ni ipi?

SWALI: Naomba kuelewa kwa undani Tofauti kati ya mbinguni, peponi, Kuzimu, Jehanamu, na Paradiso ni ipi?


JIBU:

Mbinguni,

Sehemu nyingi Biblia inaposema mbinguni, huwa inamaanisha moja kwa moja kule Mungu alipo Pamoja Malaika zake, Kule ambako Bwana Yesu alikwenda kutuandalia makao. Mahali ambapo sisi kama watakatifu bado hatujafika hata mmoja.

Ndio mbingu ya Tatu, ambayo Mtume Paulo alinyakuliwa kuonyeshwa baadhi ya vitu vilivyopo kule vipo kule ambavyo havielezeki kibinadamu, kwasababu upeo wetu ni mdogo. (2Wakorintho 12:1-4)

Ni juu sana, ambako, hatuna maelezo ya kutosha kupaelezea, mpaka tutakapofika.

2Nyakati 6:18 “Lakini Mungu je! Yamkini atakaa na watu duniani? Tazama, mbingu na mbingu za mbingu za mbingu hazikutoshi; siuze nyumba hii niliyoijenga!”

Peponi/Paradiso:

Ni mbingu ya mangojeo, ambayo sio makazi yetu ya kudumu. Mtakatifu anayekufa sasa hivi anakwenda mahali panapoitwa Peponi/Paradiso, akisubiria, siku ya unyakuo ifike, arudi kaburini achukue mwili wake, kisha aungane Pamoja na wale watakatifu watakaokuwa hai wakati huo, na moja kwa moja safari ya kwenda mbinguni ianze, kule Bwana Yesu alipo.

Yule mwizi pale msalabani, Bwana alimwambia maneno hayo;

Luka 23:42 “Kisha akasema, Ee Yesu, nikumbuke utakapoingia katika ufalme wako.

43 Yesu akamwambia, Amin, nakuambia, leo hivi utakuwa pamoja nami peponi”.

Wengine wanaiita mbingu ya pili, lakini vyovyote vile iitwavyo, bado ni mahali pa mangojeo pa watakatifu, Ndio kifuani pa Ibrahimu, yule maskini Lazaro alikwenda (Luka 16:19-31), ndio kule ambazo zile Roho zilizo chini ya madhahabu zilikuwa zinalia, zikiomba zilipiziwe kisasi kwa watesi wao.

Ufunuo 6:9 “Na alipoifungua muhuri ya tano, nikaona chini ya madhabahu roho zao waliochinjwa kwa ajili ya neno la Mungu, na kwa ajili ya ushuhuda waliokuwa nao.

10 Wakalia kwa sauti kuu, wakisema, Ee Mola, Mtakatifu, Mwenye kweli, hata lini kutokuhukumu, wala kuipatia haki damu yetu kwa hao wakaao juu ya nchi?

11 Nao wakapewa kila mmoja nguo ndefu, nyeupe, wakaambiwa wastarehe bado muda mchache, hata itakapotimia hesabu ya wajoli wao na ndugu zao, watakaouawa vile vile kama wao”.

Vilevile huku ndio kule wale wafu waliofufuka na Bwana Yesu walipoelekea kwa mara ya kwanza. (Mathayo 27:52-53)

Hivyo leo, hii ukifa katika Kristo, basi unakwenda katika eneo hili la mbingu, ambalo ni lizuri sana. Ukisubiri ufufuo wa mwisho.

Kuzimu:

Kuzimu kibiblia ni Neno lililomaanisha makao ya wafu  Au kaburini. Ambapo, waovu na wema walikuwa wanakwenda kabla ya Kristo kuja duniani, kuwatenganisha moja kwa moja kimakao,

 Ayubu anasema

Ayubu 14:13 “Laiti ungenificha kuzimuni, Ukanilinda kwa siri, hata ghadhabu zako zitakapopita, Na kuniandikia muda ulioamriwa, na kunikumbuka!”

Daudi pia alipazungumzia, (Zaburi 16:10), kwamba Bwana hatomwacha huko milele.

Lakini baada ya Bwana Yesu kuja, wakatifu walitoka huko  makaburini, na kwenda peponi/ Paradiso. Mahali pa raha Zaidi pa juu na si makaburini tena. Hivyo wanaobakia makaburini au kuzimu ni waovu.

Jehanamu:

Ni mahali pa mangojeo pa waovu, ni mahali pa mateso, kama vile Paradiso palivyo mahali pa raha pa mangojeo kwa watakatifu, vivyo hivyo jehanamu nako, ni mahali pa mangojeo pa watu waovu wanaokufa sasa. Wanaadhibiwa huko, wakingojea siku ile ya hukumu ya mwisho ifike. Ili wapewe hukumu yao, katika hukumu ya kile kiti cheupe cha enzi cha mwanakondoo, kisha wakatupwe kwenye lile ziwa la moto, ambalo ndio mauti ya pili ilipo.

Ni sawa na mhalifu anayekamatwa sasa hivi, kabla ya kuhukumiwa kifungo, huwa anawekwa kwanza mahabusu, akisubiria siku ya kupandishwa kizimbani ifike, ahukumiwe kisha akatumikie kifungo chake Jela, Ndivyo ilivyo kwa watu waovu wanaokufa sasa, na waliokufa zamani. Wanakwenda katika sehemu hii ya mateso, ambayo si ya kawaida.

Bwana Yesu alisema..

Marko 9:45 “Na mguu wako ukikukosesha, ukate; ni afadhali kuingia katika uzima, u kiwete, kuliko kuwa na miguu miwili, na kutupwa katika jehanum; [

46 ambamo humo funza wao hafi, wala moto hauzimiki.]”

Je! Wewe ni wa makao yapi?

Swali, la kujiuliza ni Je! Tukifa leo, au Unyakuo ukitukuta leo, mimi na wewe tutakuwa wa upande upi? Katika mambo ambayo hupaswi kuyachukulia juu juu tu, basi ni mambo ya Maisha yako ya milele. Kwasababu ukishakufa hakuna nafasi ya pili tena. Kama umestahili Jehanamu basi utaendelea kuishi humo milele.

Ni heri ukamgeukie Kristo, maadamu muda mchache bado unao. Acha kutazama, mambo ya ulimwengu, kwani huwa yanapumbaza sana, kukufanya usione kama kuna mabaya yanakuja mbele, Moja ya hizi siku utajutia Maisha yako, uliishije endapo hukumpa Kristo Maisha yako leo.

Tubu dhambi zako, maanisha kumfuata Yesu.

Bwana atusaidie, kuyafahamu haya.

Shalom.

Tafadhali washirikishe na wengine habari hizi njema,

Kwa maombezi/Ratiba za ibada/ Ushauri/ Maswali.
Piga namba hizi: +255693036618 au +255789001312

pia kama utapenda uyapate mafundisho haya kwa njia ya Whatsapp au email basi tutumie ujumbe kwenye namba hizo hizo.

Mada Nyinginezo:

SIKU YA UNYAKUO ITAKUKUTAJE?

Je! kuna maombi yoyote ya kumtoa mtu aliyekufa kwenye mateso ya kuzimu?

MILANGO YA KUZIMU.

MBINGU MPYA NA NCHI MPYA. (Sehemu ya 1)

Rudi nyumbani

Print this post

Je tutakaa mbinguni milele?

 Maandiko yanasema katika 1Wathesalonike 4:17 tutakaa na Bwana milele mbinguni, sasa iweje tushuke tena kutawala na Yesu duniani kwa miaka 1000?.. Au tutarudi tena mbinguni, baada ya utawala huo kuisha?

Jibu: Tusome..

1Wathesalonike 4:16 “Kwa sababu Bwana mwenyewe atashuka kutoka mbinguni pamoja na mwaliko, na sauti ya malaika mkuu, na parapanda ya Mungu; nao waliokufa katika Kristo watafufuliwa kwanza.

17 Kisha sisi tulio hai, tuliosalia, tutanyakuliwa pamoja nao katika mawingu, ili tumlaki Bwana hewani; NA HIVYO TUTAKUWA PAMOJA NA BWANA MILELE.

18 Basi, farijianeni kwa maneno hayo.

Kama ukitafakari maandiko hayo kwa makini yanasema “Tutakuwa pamoja na Bwana milele”. Na sio “tutaishi na Bwana mbinguni milele”.. 

Kuna tofauti ya kuwa na mtu milele na kuishi na mtu mahali fulani milele.
Kuwa na Yesu milele maana yake ni kwamba popote atakapokuwepo tutakuwepo naye, popote atakapokwenda tutakwenda naye..hatutamwacha wala yeye hatatuacha, kama alivyotuacha sasa na kwenda mbinguni.

Lakini baada ya sisi kwenda mbinguni huko alipo ,tutakuwa naye milele, hata wakati atakaporudi kwaajili ya hukumu ya vita vya harmagedon tutakuwa naye hatatuacha mbinguni..maandiko yanasema hivyo..

Yuda 1:14 “Na Henoko, mtu wa saba baada ya Adamu, alitoa maneno ya unabii juu ya hao, akisema, Angalia, Bwana alikuja na watakatifu wake, maelfu maelfu”.

Umeona hapo?..

Kwahiyo mbinguni tutakwenda na vile vile tutarudi kutawala na Kristo kwa miaka elfu hapa duniani..

Kulingana na maandiko mbinguni tutakaa kwa kipindi cha miaka saba tu!..baada ya hapo tutarudi kutawala na Kristo hapa duniani kwa miaka elfu, na hatitarudi tena mbinguni..Kwani Mji wa kimbinguni Yesrusalemu mpya utashuka hapa, na hapa patageuzwa kuwa mbingu mpya na nchi mpya.

Kwa maelezo marefu kuhusu mbingu mpya na nchi mpya unaweza kufungua hapa >> Mbingu mpya na nchi mpya

Hivyo hatuna budi kupiga mbio ili tuweze kuwa miongoni mwa watakaokuwa na Bwana milele.

Maran atha!

Tafadhali washirikishe na wengine habari hizi njema,

Kwa maombezi/Ratiba za ibada/ Ushauri/ Maswali.

Piga namba hizi: +255693036618 au +255789001312

pia kama utapenda uyapate mafundisho haya kwa njia ya Whatsapp au email basi tutumie ujumbe kwenye namba hizo hizo.


Mada Nyinginezo:

Je mbinguni itakuwa ni kuimba tu wakati wote?.

Tofauti kati ya ufalme wa mbinguni na ufalme wa Mungu ni ipi?

KUJIFUNUA KWA YESU KWA PILI.

Je! Kuna malaika wangapi mbinguni?

Jeshi la Mbinguni wana wa Israeli waliloliabudu ni lipi?

Rudi nyumbani

Print this post

MBINGU MPYA NA NCHI MPYA. (Sehemu ya 3)

Sasa kumbuka kama tulivyoona katika malaka zilizotangulia, huko nyuma kote baada ya Mungu kuiumba dunia, alichokuwa anafanya ni UKARABATI TU, lakini sio uumbaji mwingine. Lakini hatua hii ambayo ndio ya mwisho Mungu atafanya uumbaji mwingine. Na uumbaji huu sio kwamba ataiondoa dunia yote, na kuitupa motoni, kama wengi wanavyodhani hapana, bali atafanya kama vile atakavyofanya kwenye miili yetu mipya ya kimbinguni.

Sasa kama bado hujasoma sehemu ya kwanza na ya pili, basi bofya hapa chini upitie kwanza, ndipo uendelee na sehemu hii ya tatu na ya mwisho>>

MBINGU MPYA NA NCHI MPYA. (Sehemu ya 1)

MBINGU MPYA NA NCHI MPYA. (Sehemu ya 2)

Siku ile tutakapoenda mbinguni, Mungu atatushushia miili mipya isiyokuwa ya udongo, bali imetengenezwa kwa matirio ya kimbinguni. Na itakaposhushwa , hii miili ya sasa tuliyonayo haitauliwa na kutupwa motoni, hapana bali itavaliwa au itamezwa na ile mipya ya kimbinguni, biblia inasema hivyo katika.

1Wakorintho 15.51 “Angalieni, nawaambia ninyi siri; hatutalala sote, lakini sote tutabadilika,

52 kwa dakika moja, kufumba na kufumbua, wakati wa parapanda ya mwisho; maana parapanda italia, na wafu watafufuliwa, wasiwe na uharibifu, nasi tutabadilika.

53 Maana sharti huu uharibikao uvae kutokuharibika, nao huu wa kufa uvae kutokufa.

54 Basi huu uharibikao utakapovaa kutokuharibika, na huu wa kufa utakapovaa kutokufa, hapo ndipo litakapokuwa lile neno lililoandikwa, Mauti imemezwa kwa kushinda.

55 Ku wapi, Ewe mauti, kushinda kwako? U wapi, Ewe mauti, uchungu wako?”.

Umeona hapo, ndivyo itakavyokuwa pia juu ya mbingu mpya na nchi mpya. Sio kwamba dunia yetu, itaangamizwa kabisa iondolewe hapana, bali ITAGEUZWA, na kuwa DUNIA ya ajabu sana, ambayo mfano wake hauwezi kuelezeka, hauwezi kulinganishwa hata kwa chembe na ulimwengu huu wa sasa. Utukufu wake, utakuwa ni wa mbali sana sana sana, tena sana.

Vivyo hivyo na hizi mbingu zilizo juu yetu yaani (sayari, nyota, magimba n.k.) Vitakuwa na mwonekano mwingine tofauti kabisa, vitaanza kuwa na uhai navyo.

Ukisoma Ufunuo 21&22 yote Biblia inatoa tabia za hiyo mbingu mpya na nchi mpya jinsi zitakavyokuwa, nazo ni hizi;

  • Hakutakuwa na Bahari
  • Hakutakuwa na kilio
  • Hakutakuwa na maombolezo
  • Hakutakuwa na laana
  • Hakutakuwa na maumivu
  • Hakutakuwa na kifo
  • Hakutakuwa na Usiku.

Pia ile Yerusalemu mpya, (mji wa kimbinguni), ndio utashuka juu ya hii nchi mpya na mbingu mpya. Mji ambao utakuwa ni kitovu cha ulimwengu, ambao ni bibi-arusi tu na Kristo ndio watakaouingia.

Zaidi ya yote, ni kuwa Mungu atahamisha maskani yake, na kuileta duniani. Kwa mara ya kwanza mwanadamu ataishi na Mungu, na kuuona uso wake.

Ufunuo 21:3 “Nikasikia sauti kubwa kutoka katika kile kiti cha enzi ikisema, Tazama, maskani ya Mungu ni pamoja na wanadamu, naye atafanya maskani yake pamoja nao, nao watakuwa watu wake. Naye Mungu mwenyewe atakuwa pamoja nao”.

Vilevile Muda utaondolewa, hakutakuwa tena na kitu kinachoitwa muda, kwani tutaishi Milele na milele na milele isiyokuwa na mwisho. Katika furaha na amani na vicheko daima.

Hakika ni mambo ambayo hayaelezeki, yaani tutamfurahia Mungu kila inapoitwa leo. Hizi sayari zote zisizohesabika mabilioni kwa mabilioni huko angani zitakuwa na kazi nyingi sana, hazikuumbwa ziwe ukiwa, hatuwezi kufahamu kila kitu lakini tukifika huko ndipo tutajua.

Bwana Yesu alimalizia na kusema maneno haya;

Ufunuo 22:12 “Tazama, naja upesi, na ujira wangu u pamoja nami, kumlipa kila mtu kama kazi yake ilivyo.

13 Mimi ni Alfa na Omega, mwanzo na mwisho, wa kwanza na wa mwisho.

14 Heri wazifuao nguo zao, wawe na amri kuuendea huo mti wa uzima, na kuingia mjini kwa milango yake”.

Ndugu yangu, kumbuka ili kufika huko, maandalizi yake yanaanza sasa. Inasikitisha kuona kuwa wapo watu ambao hawatafika huko, Ikiwa leo hii tunaishi maisha ya ukristo vuguvugu, tunasema tumeokoka lakini ulimwengu umejaa ndani yetu. Tunatazamia vipi, tuende mbinguni kwenye unyakuo?. Au tunatazamia vipi tuingie Yerusalemu mpya.

Hizi ni nyakati ambazo, si za kubembelezewa tena wokovu, ni wewe mwenyewe tu kuona, jinsi hali halisi ilivyo. Hakuna dalili ambayo haijatimia. Siku yoyote, unyakuo utapita, na dhiki kuu itaanza.

Ikiwa hujaokoka, embu leo fanya uamuzi sahihi, Tubu dhambi zako kwa kumaanisha kabisa kugeuka, kisha, nenda kabatizwe katika ubatizo sahihi wa kuzamishwa katika maji mengi na kwa jina la YESU KRISTO, sawasawa na Matendo 2:38, Kisha Bwana mwenyewe atakupa kipawa cha Roho wake Mtakatifu, 

Ukikamilisha hizo hatua zote, basi ujue tayari wewe ni mwana wa ufalme, jukumu lako litakuwa ni kuutuzwa wokovu wako kwa maisha ya utakatifu na ya kumcha Mungu na ya ibada ya kweli utakayokuwa unayaishi. Ukisubiria unyakuo, na zaidi hiyo mbingu mpya na nchi mpya itakayokuja huko mbeleni.

Lakini ikiwa utahitaji msaada wa kuokoka, au kubatizwa, au swali basi wasiliana nasi kwa namba zetu hizi kwa msaada zaidi. +255693036618/ +255789001312

Bwana akubariki sana.

Tafadhali washirikishe na wengine habari hizi njema,

Kwa maombezi/Ratiba za ibada/ Ushauri/ Maswali.
Piga namba hizi: +255693036618 au +255789001312

pia kama utapenda uyapate mafundisho haya kwa njia ya Whatsapp au email basi tutumie ujumbe kwenye namba hizo hizo.

Mada Nyinginezo:

MBINGU MPYA NA NCHI MPYA. (Sehemu ya 1)

MBINGU MPYA NA NCHI MPYA. (Sehemu ya 2)

MKESHA WA KUINGIA MWAKA MPYA KILA MWAKA NI WA KUUTHAMINI SANA.

UNYAKUO.

UFUNUO: Mlango wa 1

Rudi nyumbani

Print this post

MBINGU MPYA NA NCHI MPYA. (Sehemu ya 2)

Sasa kama tulivyotangulia kuona katika sehemu ya kwanza kuwa hii dunia yetu ilipoumbwa, ilipitia uharibifu wa mara kwa mara, na baadaye kukarabatiwa  tena na sasa imesaliwa na uharibifu mmoja wa mwisho ambao  utakuja ulimwenguni hivi karibuni, na uharibifu wenyewe hautakuwa wa maji tena, bali wa moto. (2Petro 3:6-7)

Kwahiyo Mungu atakapomaliza kuuharibifu huu ulimwengu na kuwaondoa waovu wote, ataikarabati hii dunia na kuirejeshea utukufu wake kwa ilivyokuwa pale Edeni.  Na sababu ya Mungu kufanya hivyo, ili kuruhusu YESU KRISTO kuja kutawala hapa duniani pamoja na watakatifu wake, kama Mfalme wa Wafalme, na Bwana wa Mabwana kwa kipindi cha  miaka elfu moja (1000).

Wakati huo dunia itakuwa yenye amani tele, watu wataanza kuishi umri mrefu kama mwanzo, biblia inasema, mtu atakayekuwa na umri wa miaka 100 ataitwa bado mtoto mchanga,

Isaya 65:20 “Hatakuwapo tena mtoto wa siku chache, wala mzee asiyetimia siku zake; kwa maana mtoto atakufa mwenye umri wa miaka mia; bali mtenda dhambi mwenye umri wa miaka mia atalaaniwa”.

Watu watakuwa wakipanda na kujengwa wala hakuna atakayekuja kuharibu, au kuong’oa mazao yao. Wanyama wote watakuwa wapole, simba atakula majani, na mtoto atacheza kwenye tundu la nyoka na asidhuriwe kwa lolote (Isaya 65:21:25).

Lakini pamoja na hayo, biblia inarekodi pia watu waovu watakuwepo, ila dhambi haitatawala kwasababu shetani wakati huo atakuwa amefungwa, mtu akiasi kwa namna yoyote ile atauliwa,

Hivyo kwa ujumla ni kuwa utakuwa ni utawala wa amani nyingi sana, ni kipindi ambacho Mungu amewahifadhia watakatifu wake kuwafurahisha na kuwapa raha. Mimi na wewe tusikose hiyo sabato kuu ya Mungu ya utawala huo wa miaka 1000.

kwa urefu wa somo hilo la utawala wa miaka elfu, fungua hii link >>https://wingulamashahidi.org/2019/05/30/utawala-wa-miaka-1000/ 

Sasa mara baada ya utawala huo kupita, biblia inasema tena, shetani atafunguliwa kwa kipindi kifupi sana, kuwajaribifu wale waovu waliokuwa ndani ya dunia hiyo. Watakapo jaribu kuizunguka kambi ya watakatifu, wakati huo huo moto utashuka na kuwaangamiza wote. Kisha watahukumiwa na kutupwa katika lile ziwa la moto

Ufunuo 20:7 “Na hiyo miaka elfu itakapokwisha, Shetani atafunguliwa, atoke kifungoni mwake;

8 naye atatoka kuwadanganya mataifa walio katika pembe nne za nchi, Gogu na Magogu, kuwakusanya kwa vita, ambao hesabu yao ni kama mchanga wa bahari.

9 Wakapanda juu ya upana wa nchi, wakaizingira kambi ya watakatifu, na mji huo uliopendwa. Moto ukashuka kutoka mbinguni, ukawala.

10 Na yule Ibilisi, mwenye kuwadanganya, akatupwa katika ziwa la moto na kiberiti, alimo yule mnyama na yule nabii wa uongo. Nao watateswa mchana na usiku hata milele na milele”.

Baada ya hapo, mpango wote wa ukarabatiji wa ulimwengu utakuwa umeisha, kinachofuata sasa hiyo ni mbingu mpya na nchi mpya, ambayo Mungu aliikusudia tangu zamani wanadamu waishi ndani yake.

Jambo ambalo ndio shabaha yetu kuu sisi watakatifu. Hiyo mbingu mpya na nchi mpya. Kama vile mtume Petro alivyosema katika.

2Petro 3:13 “Lakini, kama ilivyo ahadi yake, mnatazamia mbingu mpya na nchi mpya, ambayo haki yakaa ndani yake.

14 Kwa hiyo, wapenzi, kwa kuwa mnatazamia mambo hayo, fanyeni bidii ili mwonekane katika amani kuwa hamna mawaa wala aibu mbele yake”.

Mpaka hapo utakuwa umeona jinsi Mungu alivyoiumba dunia yake, na kila ilipoharibiwa, baadaye aliiponya kwa sehemu au aliikarabati na kuirudisha kama mwanzo. Lakini hakuwahi kufanya uumbaji mwingine mpya, wa ulimwengu.

Hivyo fuatana nami katika sehemu ya Tatu na ya mwisho, ambayo inaelezea sasa, jinsi hiyo mbingu mpya na nchi mpya itakavyokuja kuwa.

Bofya chini kwa sehemu ya kwanza na ya tatu >>>

MBINGU MPYA NA NCHI MPYA. (Sehemu ya 1)

MBINGU MPYA NA NCHI MPYA. (Sehemu ya 3)

Tafadhali washirikishe na wengine habari hizi njema,

Kwa maombezi/Ratiba za ibada/ Ushauri/ Maswali.
Piga namba hizi: +255693036618 au +255789001312

pia kama utapenda uyapate mafundisho haya kwa njia ya Whatsapp au email basi tutumie ujumbe kwenye namba hizo hizo.

Mada Nyinginezo:

MBINGU MPYA NA NCHI MPYA. (Sehemu ya 1)

YANAYOENDELEA SASA KATIKA MADHABAHU YA MUNGU ROHONI.

NITAFANYA YERUSALEMU KUWA JIWE LA KUWALEMEA .

UTAWALA WA MIAKA 1000.

Rudi nyumbani

Print this post

MBINGU MPYA NA NCHI MPYA. (Sehemu ya 1)

Nakusalimu katika jina kuu sana lipitalo majina yote la Bwana wetu Yesu Kristo, Nakukaribisha katika kujifunza maneno ya uzima.  Na leo tutajifunza juu ya mbingu mpya na nchi mpya.

Hili ni moja ya maswali yanayoulizwa na watu wengi, Je! Hiyo mbingu mpya na Nchi mpya inayozungumziwa katika maandiko itakuwa wapi? Je ni mbinguni au duniani?. Na Je! Itakuwa ni hii hii dunia yetu au italetwa dunia nyingine na Mungu?. Ili kufahamu fuatana nami mpaka mwisho wa makala hizi.

Historia ya mbingu na nchi:

Sasa kabla hatujaenda kutazama juu ya mbingu mpya na nchi mpya, ni vizuri tukafahamu historia ya “mbingu na nchi” ilianzia wapi. Tukisoma kile kitabu cha Mwanzo, biblia inasema

Hapo mwanzo Mungu aliziumba mbingu na nchi ..(Mwanzo 1:1)

Inaposema “mbingu” inamaanisha anga lote, yaani sayari, na nyota na magimba yote yanayoonekana juu. Na “Nchi” inamaanisha hii dunia yetu tunayoishi sisi wanadamu na viumbe vyote.

Sasa Mungu alipoiumba, ilikuwa ni kamilifu sana, yenye kupendeza, lakini baada ya muda Fulani kupita,ambao biblia haijaeleza ni kipindi cha muda gani, ilikuja kuharibiwa na kuwa UKIWA.  Ikiwa na maana hakukuwa na kiumbe chochote kinachoishi, au uhai wowote unaoendelea, ikabakia kuwa kama mojawapo ya sayari nyingine, isipokuwa tu, hii yetu ilisalia na maji.

Mwanzo 1:2 “Nayo nchi ilikuwa ukiwa, tena utupu, na giza lilikuwa juu ya uso wa vilindi vya maji; Roho ya Mungu ikatulia juu ya uso wa maji”.

Najua pengine unaweza ukawa na swali, Je! Umejuaje, kuwa dunia yetu, hapo mwanzo ilikuwa ni nzuri na kamilifu kabla ya Mungu kuanza kutuumba sisi. Jibu ni kuwa maandiko yanatuambia Mungu hajawahi kuiumba nchi na kuiacha katika hali ya ukiwa. Soma.

Isaya 45:18 “Maana Bwana, aliyeziumba mbingu, asema hivi; Yeye ni Mungu; ndiye aliyeiumba dunia na kuifanya; ndiye aliyeifanya imara; HAKUIUMBA UKIWA, aliiumba ili ikaliwe na watu; Mimi ni Bwana, wala hapana mwingine”.

Unaona hapo? Anasema, hakuiumba ukiwa, ikiwa na maana kuwa Mungu haachi kazi nusu nusu anaumba kikamilifu. Hivyo hiyo inatuonyesha kuwa kabla ya sisi wanadamu kuumbwa, Mungu alikuwa tayari kashaiumba dunia kamilifu na yenye uhai ndani yake, Lakini kukatokea jambo Fulani la uharibifu, ikapelekea Mungu kuiharibu dunia ile, Na hatuwezi kushangaa jambo kama hilo kusababishwa na shetani, na mapepo yake, kwasababu hao ndio waliokuwepo kabla ya sisi wanadamu kuumbwa. Lakini siri hiyo Mungu kaificha ni yeye mwenyewe ndiye anayejua yaliyokuwa yanaendelea huko nyuma.

Sasa wakati ulipofika wa sisi kuumbwa Mungu akaanza kuikarabati dunia tena. ndipo hapo  tunaona akasema na iwe mwanga ikawa mwanga, n.k. Mpaka ikiwa sehemu nzuri sana tena ya kutuvutia, lakini tunajua maisha yalipokuja kuendelea mbele Adamu akaasi, dhambi ikaingia, baadaye hali ikaendelea kuwa mbaya kupitiliza, hadi Mungu akaghahiri kuwaumba wanadamu, baadaye akasema nitawaangamiza wanadamu wote, watoke katika uso wa nchi.

Ndipo hapo akaleta kitu kinachoitwa gharika duniani, akaigharikisha dunia nzima. Akasalia Nuhu tu, na familia yake, jumla watu 8, dunia ikabakia ukiwa kama ilivyokuwa pale mwanzo.

Isaya 24:1 “Tazama, Bwana ameifanya dunia kuwa tupu, aifanya ukiwa, aipindua, na kuwatawanya wakaao ndani yake”.

Hivyo, dunia ya wakati ule ilipogharikishwa, haikukarabatiwa tena na Mungu kama alivyofanya pale mwanzo, badala yake aliyakausha maji tu, lakini uzuri mwingi wa mbingu na nchi ulipotea, jua likawa kali kuliko pale mwanzo, kwasababu maji yaliyokuwa juu ya anga yalipunguzwa, umri wa watu kuishi ukapungua sana, kutoka miaka elfu hadi miaka 120, Kama Mungu alivyosema.

Basi, baada ya hapo maisha yakaendelea tena kama kawaida, watu wakaongezeka , wakaijaza dunia, maasi yakarudi na kuongeza, tena hata zaidi ya kipindi kile cha Nuhu, Mungu akaanza kuwaonya wanadamu kwa vinywa vya manabii wake, akawaambia huu ulimwengu utakwenda kuangamizwa , kama ilivyokuwa kipindi kile cha gharika, lakini kuangamziwa kwake hakutakuwa kwa maji tena, bali kwa moto, ili kuifanya kuwa UKIWA tena.

Unaweza kusoma hilo katika vifungu hivyo katika mistari hii;

Isaya 13:9 “Tazama, siku ya Bwana inakuja, siku kali, ya hasira na ghadhabu kuu, ILI IIFANYE NCHI KUWA UKIWA, na kuwaharibu watu wake, wenye dhambi, wasikae ndani yake.

10 Maana nyota za mbinguni na matangamano havitatoa nuru yake; jua litatiwa giza wakati wa kucha kwake, na mwezi utaacha nuru yake isiangaze.

11 Nami nitaadhibu ulimwengu kwa sababu ya ubaya wake, na wenye dhambi kwa sababu ya hatia yao; nami nitaikomesha fahari yao wenye kiburi; nami nitayaangusha chini majivuno yao walio wakali;

12 nitafanya wanadamu kuadimika kuliko dhahabu safi, na watu kuliko dhahabu ya Ofiri.

13 Kwa hiyo nitazitetemesha mbingu, na dunia itatikiswa itoke katika mahali pake, kwa sababu ya ghadhabu ya Bwana wa majeshi, na kwa sababu ya siku ya hasira yake kali”.

Soma pia,

2Petro 3:6 “kwa hayo dunia ile ya wakati ule iligharikishwa na maji, ikaangamia.

7 Lakini MBINGU ZA SASA NA NCHI zimewekwa akiba kwa moto, kwa neno lilo hilo, zikilindwa hata siku ya hukumu, na ya kuangamia kwao wanadamu wasiomcha Mungu”.

Unaona? Zoezi lile lile la Mungu kuiharibu nchi, linaendelea, lilianza kabla ya sisi kuumbwa, likatokea tena wakati wa Nuhu, na litamalizia, na wakati wetu sisi tunaoishi. Kwahiyo kinachongojewa sasa ni Mungu kuwanyakua tu watakatifu wake, baada ya hapo, kitakachofuata ni uharibifu mkubwa sana wa huu ulimwengu.Ambao utakuwa ni wa kutisha sana, kwasababu, dunia itatikiswa kwa namna ambayo haijawahi kutokea, jua litatiwa giza, visiwa vitahama, waovu wote watakufa, watakaosalia watakawa ni wachache sana pengine watu 10 tu, katika dunia nzima, kwasababu moto usiokuwa wa kawaida utaipika hii dunia tena, ili kuifanya kuwa ukiwa kama pale mwanzo.

Ufunuo 16:17 “Na huyo wa saba akakimimina kitasa chake juu ya anga. Sauti kuu ikatoka katika hekalu, katika kile kiti cha enzi, ikisema, Imekwisha kuwa.

18 Pakawa na umeme na sauti na radi; na palikuwa na tetemeko la nchi kubwa, ambalo tangu wanadamu kuwako juu ya nchi hapakuwa namna ile, jinsi lilivyokuwa kubwa tetemeko hilo. Hii ndio siku ya kiama inayofamika na wengi.

19 Na mji ule mkuu ukagawanyikana mafungu matatu, na miji ya mataifa ikaanguka; na Babeli ule mkuu ukakumbukwa mbele za Mungu, kupewa kikombe cha mvinyo ya ghadhabu ya hasira yake.

20 Kila kisiwa kikakimbia, wala milima haikuonekana tena.

21 Na mvua ya mawe kubwa sana, ya mawe mazito kama talanta, ikashuka kutoka mbinguni juu ya wanadamu. Wanadamu wakamtukana Mungu kwa sababu ya lile pigo la mvua ya mawe; kwa maana pigo lake ni kubwa mno”.

Huu wakati unatisha sana, hatuwezi kueleza mambo yote, lakini kama utataka somo linalohusiana na hii siku ya Bwana itakavyokuwa basi bofya link hii>>>> https://wingulamashahidi.org/2018/07/17/siku-ya-bwana-inayotisha-yaja/

Msingi huu utatusaidia kufahamu agenda ya Mungu juu ya hii dunia yetu, na mpaka mwisho wake utakavyokuja kuwa.

Mpaka hapo tunaweza kuendelea  katika sehemu ya pili ya mbingu mpya na nchi mpya.. Hivyo kwa mwendelezo unaweza kubofya chini>>

MBINGU MPYA NA NCHI MPYA. (Sehemu ya 2)

MBINGU MPYA NA NCHI MPYA. (Sehemu ya 3)

Tafadhali washirikishe na wengine habari hizi njema,

Kwa maombezi/Ratiba za ibada/ Ushauri/ Maswali.
Piga namba hizi: +255693036618 au +255789001312

pia kama utapenda uyapate mafundisho haya kwa njia ya Whatsapp au email basi tutumie ujumbe kwenye namba hizo hizo.

Mada Nyinginezo:

MAPIGO YA VITASA SABA, NA SIKU YA BWANA.

Je ni kweli siku ya mwisho dunia itakunjwa kama karatasi na kutupwa motoni?

Je! tunapaswa kukiamini Kitabu cha Henoko?

UFUNUO: Mlango wa 17

Rudi nyumbani

Print this post

Nifanye nini ili niwe na uhakika nikifa naenda mbinguni?

SWALI: Nifanye nini ili niwe nina uhakika kuwa hata nikifa ghafla leo hii, nina uhakika wa kwenda mbinguni kwa asilimia zote?


JIBU: Moja ya swali ambalo ukiwauliza wakristo wengi watakujibu kirahisi ni kuhusu kuokoka..Ukimuuliza Je! Umeokoka atakuambia ndio nimeokoka, lakini ukimuuliza, Ikitokea mfano umekufa ghafla leo Je! unao uhakika wa kwenda mbinguni?..Hapo ndipo utakapopata majibu tofauti tofauti, wengine watasema, siwezi kusema hilo Mungu ndio anayejua, wengine watasema kwa kweli hapo sijui, wengine watasema mimi sio Mungu na wengine watesema “natumaini” nitakwenda mbinguni, wengine watasema “ninaamini” itakuwa hivyo..Na wachache sana watasema ninao uhakika nitakwenda mbinguni..

Na katikati ya hao wachache wanaosema ninaohakika, ukiwauliza swali ni kipi kinakupa uhakika huo wa kwenda mbinguni, wengine wanatasema kwasababu ninaishi katika Maisha ya toba kila siku.

Lakini biblia inatuambia kila aliyemwamini mwana wa Mungu ni lazima awe na uhakika ya kuwa anao uzima wa milele ndani yake, na kwamba hata akifa leo atakuwa anaishi..

1Yohana 5:13 “Nimewaandikia ninyi mambo hayo, ili mjue ya kuwa mna uzima wa milele, ninyi mnaoliamini Jina la Mwana wa Mungu”.

Sasa wengi wanakosa Uhakika huu kwasababu hawajakamilishwa katika IMANI ya YESU KRISTO. Na ndio hapo utaona mtu anasema nimeokoka lakini bado anayo hofu akifa leo hajui atakwenda wapi, motoni au mbinguni? Maisha ya kubahatisha. Wengi hawafahamu kuwa Kuokoka ni Neno lenye maana pana sana, na hivyo sio suala la kuongozwa sala ya toba tu na kubaki kama ulivyo. Kuokoka ni jambo linaloleta badiliko ndani ya Maisha ya mtu. Bwana Yesu anafanya kazi ya kuyageuza Maisha ya mtu mpaka mtu huyo anafikia kiwango cha kupata uhakika wa uzima wa milele mwenyewe ndani yake bila hata ya kujilazimisha, au kihisihisi kama anao au hana..Ndani yake kunabubujika uzima wa milele.(Yohana 4:14)

Ni hatua (process)..sio tu kuongozwa sala Fulani ya toba halafu unaendelea kuishi Maisha ambayo ni kinyume na Kristo, halafu ukadhani uhakika huo utakuja wenyewe ndani yako.

Na hiyo inakuja kwa kuyatii maagizo yote Bwana anayompa mtu baada ya kutubu kwake. Akikuambua unapaswa ukabatizwe katika ubatizo sahihi mara baada ya kuokoka kwako, unatii kwa kufanya hivyo, akisema tena..

Yohana 2:15 “Msiipende dunia, wala mambo yaliyomo katika dunia. Mtu akiipenda dunia, kumpenda Baba hakumo ndani yake.

16 Maana kila kilichomo duniani, yaani, tamaa ya mwili, na tamaa ya macho, na kiburi cha uzima, havitokani na Baba, bali vyatokana na dunia.

17 Na dunia inapita, pamoja na tamaa zake, bali yeye afanyaye mapenzi ya Mungu adumu hata milele”.

Unafanya hivyo kwa kujitenga na mambo yote mabaya ya kidunia hii, kama vile ulevi, sigara,disko, anasa, matusi, miziki ya kidunia, rushwa, visasi, chuki, uasherati, utoaji mimba, vimini, mahereni, mawigi, suruali, lipsticks, wanja, n.k. unajitwika msalaba wako na kumfuata Yesu.

Na ukishafanya hivyo kwa kutii maagizo yote aliyokupa sasa hapo ndipo kuna amani Fulani inayotoka kwake na kuingia ndani yako, na hiyo ndiyo inajenga uhakika huo na kukushuhudia kuwa wewe ni mwana wa Mungu. Na hata ikitokea umekufa kwa ghafla haijalishi ni katika hali gani, huna wasiwasi kwasababu mbinguni utakwenda, kwasababu unashuhudiwa moyoni.

Lakini tukisema sisi tunaishi katika Maisha ya toba huwa tunatubu kila siku, na kila dakika na huku nyuma bado Yesu hajaleta badiliko lolote ndani yetu, hapo bado

tunajidanganya..Na mbinguni hatutakwenda. Hatubaatishi kwenda mbinguni, kwamba tunaotea saa atakayokuja atukute tumetubu.. Hivyo kumwamini Yesu na kuwa na uhakika wa uzima wa milele ni Zaidi ya kuongozwa sala ya toba, au kutubu mara kwa mara.. ni pamoja na kuyatii na kuyaishi yale yote anayokuagiza tangu siku ile uliposema nimeamua kumfuata Yesu.

Yohana 5:24 ‘Amin, amin, nawaambia, Yeye alisikiaye neno langu na kumwamini yeye aliyenipeleka yuna uzima wa milele; wala haingii hukumuni, bali amepita kutoka mautini kuingia uzimani’.

Natumai kuanzia leo wewe uliyeokoka ambaye umekuwa huna uhakika kuwa utakwenda mbinguni au la, naamini utaanza kuchukua uamuzi huo mpya wa kumfuata Yesu kwa moyo wako wote na kuyatii yote anayokuambia.., ili na wewe akupe uhakika huo wa kwenda mbinguni, lakini ukibakia katika hali hiyo hiyo ni uthibitisho kuwa huwezi kwenda mbinguni,..

Na kama Bado utakuwa bado hujamwamini Bwana Yesu na wewe unataka leo hii kuokoka, Yesu aanze kuyatengeneza Maisha yako upya, Basi uamuzi unaoufanya ni wa busara sana ambao hautakaa uujutie kama ilivyokuwa hata kwetu sisi. Unachopaswa kufanya, hapo ulipo, chukua muda mchache ujitenge peke yako. Kisha piga magoti, kisha fuatisha sala hii kwa Imani, ukijua kuwa Mungu yupo hapo karibu na wewe pembeni yako kukusikia..Kisha ukiwa sasa katika utulivu Sema sala hii kwa sauti.

EE MUNGU BABA, NAJA MBELE ZAKO, NIKIWA NINAJITAMBUA KUWA MIMI NI MKOSAJI NA NIMEKUTENDA DHAMBI NYINGI, NA KWAMBA NIMESTAHILI HUKUMU. LAKINI WEWE MUNGU WANGU ULISEMA KATIKA NENO LAKO KUWA WEWE NI MUNGU WA REHEMA UNAYEWAREHEMU MAELFU ELFU YA WATU WANAOKUPENDA WEWE. NA LEO HII NINAKUJA MBELE ZAKO NAHITAJI MSAMAHA WAKO NA MSAADA WAKO MUNGU WANGU, NINATUBU DHAMBI ZANGU ZOTE KWA KUMAANISHA NA KWA MOYO WANGU WOTE, NINAKIRI KUWA YESU KRISTO NI BWANA, NA YEYE NDIYE MWOKOZI WA HUU ULIMWENGUNI. HIVYO NAOMBA DAMU YA MWANAO TAKATIFU INISAFISHE UOVU WANGU WOTE SASA NIFANYIKE KUWA KIUMBE KIPYA KUANZIA LEO NA HATA MILELE.

ASANTE BWANA YESU KWA KUNIPOKEA NA KUNISAMEHE.

AMEN.

Sasa ikiwa umefuatisha sala hiyo kwa Imani ..Hatua iliyobakia kwako ni kuithibitisha toba yako kwa Vitendo ikiwa ulikuwa unafanya mambo yote ambayo hayampendezi Mungu unayaacha na kujitenga nayo, Sasa Mungu akishaona umegeuka kwa vitendo basi toba yako anaipokea na atakuja ndani yako wakati huo huo na kufanya makao ya milele kwako. Vile vile unahitaji, kutafuta kanisa la kiroho ambalo utajumuika na wakristo wengine katika kumwambudu Mungu, na kujifunza biblia ili uukulie wokovu. Na vilevile ili upate ubatizo sahihi wa kuzamishwa katika maji mengi na kwa jina la YESU KRISTO kwa ajili ya ondoleo la dhambi zako.

Fanya hivyo na Bwana atakusaidia

Kwa mawasiliano/mafundisho zaidi kwa njia ya whatsapp, tutumie ujumbe kwenye namba hizi: +255789001312/ +255693036618

  Au Jiunge na magroup yetu ya whatsapp kwa kubofya hapa > Group-whatsapp

Ubarikiwe sana.

Tafadhali share ujumbe huu na kwa wengine. Vilevile ikiwa utapenda tuwe tunakutumia masomo haya katika inbox yako ya facebook au whatsapp utatumia ujumbe,

Mada Nyinginezo:

BIBLIA INAITAJA NJIA KUU YA MFALME, NJIA HII NI IPI?

TUMAINI NI NINI?

Waoga ambao hawataurithi uzima wa milele ni watu wa namna gani?(Ufunuo 21:8).

NIFANYE NINI ILI MUNGU AYAJIBU MAOMBI YANGU?

TAFUTA UZIMA WA MILELE NA SI UZIMA TU!.

Biblia inasema tusiwe kwazo kwa yeyote, je! inawezekanikaje kwa dunia hii ya sasa?(2Wakorintho 6:3).

Zeri ya Gileadi ni nini?

Rudi Nyumbani:

Print this post

Kuna Mbingu ngapi?

Je kuna mbingu ngapi? Mbingu saba ni nini?..na kama zipo 7 je mbingu ya kwanza ni ipi, mbingu ya pili ni ipi, mbingu tatu pia ni ipi? na hatimaye zote saba?..

JIBU:  Katika biblia tunasoma kumetajwa uwepo wa mbingu tatu tu.

2Wakorintho 12:2 ‘Namjua mtu mmoja katika Kristo, yapata sasa miaka kumi na minne, (kwamba alikuwa katika mwili sijui; kwamba alikuwa nje ya mwili sijui; Mungu ajua). Mtu huyo alinyakuliwa juu mpaka mbingu ya tatu’.

Huyu ni Paulo aliyenyakuliwa mpaka mbingu ya tatu. Sasa biblia haijataja uwepo wa mbingu nyingine zaidi ya hizi tatu. Na pia haijazitaja mbingu hizo tatu ni zipi..Lakini kwa Neema za Bwana na kwa kuyachunguza maandiko tunaweza kuzijua ni zipi.

Ipo mitazamo kadhaa juu ya hizi mbingu tatu zilizotajwa hapo juu…Lakini inayojulikana na wengi ni kwamba Mbingu ya kwanza ni hili anga tulionalo ambalo lina hewa yetu ya oksijeni tunayoivuta, kadhalika lenye mawingu na ambalo linanyunyiza mvua..

Na mbingu ya pili ni ile ya juu zaidi yenye magimba ya vimondo, nyota na sayari

Na mbingu ya tatu ni ile ambayo Malaika watakatifu wapo.

Huu ndio mtazamo unaojulikana na wengi. Lakini upo pia mwingine ambao ndio tunaamini ni wa ukweli na huo ni kama ufuatao.

1. Mbingu ya Kwanza: inahusisha anga lote tunaloliona kwa macho…yaani sayari, nyota, jua, mwezi, mawingu, vimondo n.k

2.Mbingu ya Pili: Ni mbingu isiyoonekana kwa macho ijulikanayo kama PARADISO au PEPONI. Ni mahali ambapo roho za watakatifu waliokufa katika Imani ya Yesu Kristo zinahifadhiwa. Mtakatifu anapokufa mwili wake unakwenda kuzikwa kaburini, unaoza lakini roho yake inachukuliwa na malaika watakatifu na kupelekwa paradiso au peponi mahali ambapo pana raha na pumziko, ambapo atakutana na roho nyingine za watakatifu waliokufa katika Imani.

Kwa pamoja watakaa huko paradiso wakingojea siku ya unyakuo ifike ambapo, siku hiyo itakapofika watarudi kuichukua miili yao ya asili na kisha kufumba na kufumbua watabadilishwa pamoja na wale watakatifu walio hai na kwa pamoja watapaa kwenda kumlaki Bwana Yesu mawinguni kwenda kuingia katika mbingu ya Tatu.

Yule mhalifu aliyesulubiwa na Bwana Yesu pale msalabani alipelekwa mahali huko ambako Bwana Yesu alimwambia atakuwa naye. (peponi).

3.Mbingu ya Tatu: Ni mahali ambapo Bwana Yesu Kristo yupo pamoja na malaika watakatifu, huko ndiko Bwana alikosema amekwenda kutuandalia makao. Huko hawaingii watu wasio kuwa na miili ya utukufu. Ni sehemu ya raha isiyo na kifani…Mambo yaliyomo humo biblia inasema jicho halijawahi kuona wala sikio kusikia, mambo ambayo Mungu kawaandalia wale wamchao.(1Wakorintho 2:9).

Hivyo jibu jepesi ya kwamba kuna mbingu ngapi kibiblia? Jibu ni tatu tu kama tulivyoziona hapo juu. Na wala hakuna mbingu saba.

Hivyo tujitahidi tuingie katika mbingu hiyo ya tatu kwa kuuvua utu wa kale wa dhambi na kuvaa utu mpya.

Waefeso 4:22 “mvue kwa habari ya mwenendo wa kwanza utu wa zamani, unaoharibika kwa kuzifuata tamaa zenye kudanganya;

23 na mfanywe wapya katika roho ya nia zenu;

24 mkavae utu mpya, ulioumbwa kwa namna ya Mungu katika haki na utakatifu wa kweli.

25 Basi uvueni uongo, mkaseme kweli kila mtu na jirani yake; kwa maana tu viungo, kila mmoja kiungo cha wenzake”

Na pia biblia inasema katika..

Waebrania 12:14 “Tafuteni kwa bidii kuwa na amani na watu wote, na huo utakatifu, ambao hapana mtu atakayemwona Bwana asipokuwa nao;”

Bwana akubariki.

Tafadhali share na wengine. Maran atha


Mada Nyinginezo:

JE! UNAYO NAFASI MBINGUNI?

Je! Mbinguni Kutakuwa na kula na kunywa?.

Je! mbinguni kuna malaika wa kike?. Na je! tukifika mbinguni tutafanana wote?

MBINGUNI YUPO NANI SASA?

Je! Bikira Maria ni MALKIA WA MBINGUNI?

MBINGUNI NI WAPI?

URIMU NA THUMIMU NI NINI KATIKA BIBLIA?

Rudi Nyumbani:

Print this post

Mbinguni ni sehemu gani?

JIBU: Ili tusichanganyikiwe jambo la muhimu  tulinalopaswa kujua ni kuwa Katika biblia Neno “mbinguni” limetumika kuwakilisha sehemu tofauti tofauti tatu.

Sehemu ya kwanza ni anga hili ambalo lipo juu yetu: Ambalo ndilo hili tunaloliona lenye nyota, mawingu, mwezi jua na sayari, ambalo ndege wote wa angani wanaruka na kufurahia, biblia imelitaja kama mbingu..Tunasoma..

Isaya 55:10 “Maana kama vile mvua ishukavyo, na theluji, kutoka mbinguni, wala hairudi huko; bali huinywesha ardhi, na kuizalisha na kuichipuza, ikampa mtu apandaye mbegu, na mtu alaye chakula;

11 ndivyo litakavyokuwa neno langu, litokalo katika kinywa changu; halitanirudia bure, bali litatimiza mapenzi yangu, nalo litafanikiwa katika mambo yale niliyolituma.”

Luka 17:24 “kwa kuwa, kama vile umeme umulikavyo toka upande huu chini ya mbingu hata upande huu chini ya mbingu, ndivyo atakavyokuwa Mwana wa Adamu katika siku yake”.

Sehemu ya Pili ya mbingu ni makao ya Mungu yalipo: Na hii ipo katika Roho, sehemu ambayo Mungu na malaika zake wanaishi, hatuwezi kuiona kwa jicho la kibinadamu wala hatuwezi kufika huko kwa kifaa chochote cha kibinadamu, lakini ni mahali halisi kabisa. Tiketi ya pekee ya kufika huko biblia inatuambia ni Yesu Kristo tu, Na hii mbingu ni pana sana ndio imejumuisha ile mbingu mpya na nchi mpya ambayo itakuja kuwa ni makao ya watakatifu baadaye, pamoja na ile paradiso (peponi) kule ambapo wale wote waliokufa zamani na wanaokufa sasa hivi katika Kristo wanahifadhiwa kwa muda wakisubiria ufufuo siku ile ya Unyakuo ili kwa pamoja waingie katika makao ya Mungu mwenyewe yaliyo juu sana na ndio maana utaona mtume Paulo alinyakuliwa mpaka mbingu ya Tatu, mbingu hii ya tatu ni hiyo ya makao ya Mungu mwenyewe,  akaonyeshwa sehemu ya maono ya huko, na kusema mambo yaliyo huko hayajuzu hata mwanadamu kuyatamka,(2Wakorintho 12:2-4). na ndiko watakatifu waliokombolewa watakapokwenda siku ile ya Unyakuo itakapofika, ni mahali patakatifu na pasafi ambapo mtu yeyote mchafu hataingia..

1Wafalme 8:27 “Lakini Mungu je? Atakaa kweli kweli juu ya nchi? Tazama, mbingu hazikutoshi, wala mbingu za mbingu; sembuse nyumba hii niliyoijenga!”

1Timotheo 6:16 “ambaye yeye peke yake hapatikani na mauti, amekaa katika nuru isiyoweza kukaribiwa; wala hakuna mwanadamu aliyemwona, wala awezaye kumwona. Heshima na uweza una yeye hata milele. Amina.”

Na sehemu ya tatu biblia inapataja kama mbinguni ni mahali pa juu sana, makao ya juu sana: Mahali ambapo Mungu pekee ndiye anayestahili kuwepo, jambo ambalo hata hapa duniani linaweza kufikiwa,

Watu walio ndani ya Yesu, ambao wameokoka kikamilifu kwa kumwamini Yesu na kubatizwa, katika ulimwengu wa roho, ni sawa na wameketi pamoja na Kristo mbinguni..

Waefeso 2:5 “hata wakati ule tulipokuwa wafu kwa sababu ya makosa yetu; alituhuisha pamoja na Kristo; yaani, tumeokolewa kwa neema.

6  Akatufufua pamoja naye, akatuketisha pamoja naye katika ulimwengu wa roho, katika Kristo Yesu;”

Kadhalika pia, Ufalme wowote au mtu yeyote anayetafuta kuinuliwa ziadi ya vitu vingine vyote huyo katika roho anaonekana anakipandia cheo cha Mungu kilipo, na Mungu yupo mbinguni, hivyo anaonekana kama amefika mbinguni.

Danieli 4:19 “Ndipo Danieli, aliyeitwa jina lake Belteshaza, akashangaa kwa muda, na fikira zake zikamfadhaisha. Mfalme akajibu akasema, Ee Belteshaza, ndoto ile isikufadhaishe wala tafsiri yake. Belteshaza akajibu, akasema, Bwana wangu, ndoto hii iwapate wao wakuchukiao, na tafsiri yake iwapate adui zako.

20 Ule mti uliouona, uliokua, ukawa na nguvu, urefu wake ukafika mpaka mbinguni, na kuonekana kwake mpaka dunia yote;

21 ambao majani yake yalikuwa mazuri, na matunda yake mengi, na ndani yake chakula cha kuwatosha wote; ambao chini yake wanyama wa kondeni walikaa, na ndege wa angani walikuwa na makao yao katika matawi yake;

22 ni wewe, Ee mfalme, uliyekua, na kupata nguvu; maana ukuu wako umekua na kufika mpaka mbinguni, na mamlaka yako yamefika mpaka mwisho wa dunia.

Mathayo 11:23 “Nawe Kapernaumu, je! Utakuzwa mpaka mbinguni? Utashushwa mpaka kuzimu; kwa kuwa kama miujiza iliyofanyika kwako ingalifanyika katika Sodoma, ungalikuwapo mji huo hata leo.”

Isaya 14:12 “Jinsi ulivyoanguka kutoka mbinguni, Ewe nyota ya alfajiri, mwana wa asubuhi! Jinsi ulivyokatwa kabisa, Ewe uliyewaangusha mataifa!

13 Nawe ulisema moyoni mwako, Nitapanda mpaka mbinguni, Nitakiinua kiti changu juu kuliko nyota za Mungu; Nami nitaketi juu ya mlima wa mkutano, Katika pande za mwisho za kaskazini.

14 Nitapaa kupita vimo vya mawingu, Nitafanana na yeye Aliye juu.

15 Lakini utashushwa mpaka kuzimu; Mpaka pande za mwisho za shimo”.

Hivyo kwa vyovyote vile, tunapaswa tujitahidi ili tufike huko, si kwa kujiinua tukiyatumainia haya Maisha, bali kwa kupitia Yesu Kristo, kwasababu biblia inasema mambo tuliyoandaliwa huko, jicho halijawahi kuona wala sikio kusikia.

Ubarikiwe.


Mada Nyinginezo:

JE! NI KWELI DUNIA ILIUMBWA TAKRIBANI MIAKA 6000 ILIYOPITA? NA JE! SHETANI ALIKUWEPO DUNIANI WAKATI DUNIA INAUMBWA?

TUMEAMBIWA TUNAPOSALI TUSIPAYUKE-PAYUKE, JE! HUKO KUPAYUKA PAYAUKA NDIO KUPI?

JE! KUNA DHAMBI KUBWA NA NDOGO?

NI NANI ANAYETAWALA DUNIA KATI YA MUNGU NA SHETANI?.


Rudi Nyumbani:

Print this post

Je! Mbinguni Kutakuwa na kula na kunywa?.

JIBU: Biblia haijaeleza kwa mapana na marefu mambo yatakayokuwa yanaendelea mbinguni baada ya unyakuo kupita, na ndio maana mtume Paulo anasema katika 1Wakorintho 13:9 “Kwa maana tunafahamu kwa sehemu; na tunafanya unabii kwa sehemu;..”

Hivyo kuhusu kama watakatifu watakula au hawatakula na kunywa biblia haijatoa jibu la moja kwa moja lakini tunaweza kutazama baadhi ya mistari inaweza kutusaidia kupata picha fulani. Tukisoma:

Marko 14.23 “Akatwaa kikombe, akashukuru, akawapa; wakakinywea wote.

24 Akawaambia, Hii ndiyo damu yangu ya agano, imwagikayo kwa ajili ya wengi.

25 Amin, nawaambia ninyi, Sitakunywa tena kabisa uzao wa mzabibu, hata siku ile nitakapounywa mpya katika ufalme wa Mungu.

26 Nao walipokwisha kuimba walitoka kwenda mlima wa Mizeituni”. 

Tunaona katika habari hiyo hapo, Yesu akiwaagiza mitume wake kwa habari ya kunywa katika ufalme wa mbinguni, Lakini pia tukimtazama Bwana baada ya kufufuka kwake alikuwa na mwili wa umilele wa utukufu usioweza kufa tena, wala kuugua, mwili ambao uliweza kufanya mambo makubwa zaidi yasiyoweza kufanywa na mwili wowote wa asili, ule mwili uliweza kupotea na kutokea mahali popote, uliweza kuchukua sura tofauti tofauti, uliweza kupaa, na mpaka sasa unaishi n.k. Na kumbuka pia biblia inatuambia “siku atakapodhihirishwa tutafanana naye (1Yohana 3:2)”..Sasa jambo ambalo utaliona pale alipowatokea mitume wake baada ya kufufuka kwake aliwaambia wampe chakula chochote ale.

Luka 24.41 “Basi walipokuwa hawajaamini kwa furaha, huku wakistaajabu, aliwaambia, Mna chakula cho chote hapa?

42 Wakampa kipande cha samaki wa kuokwa.43 Akakitwaa, akala mbele yao”. 

Hiyo inatupa picha kwa sehemu jinsi miili hii ya utukufu itakavyokuwa, haitakuwa na mipaka Fulani kwamba kwasababu ni ya umilele haitaweza kula wala kunywa. Ni kweli kabisa uzima wa hiyo miili hautakuwa tena katika vyakula, inaweza kuendelea kuishi bila ya njaa wala chakula wala kutegemea chochote kile,kwasababu asili yake ni ya kimbinguni lakini hiyo haimaanishi kuwa haitaweza kunywa wala kula. Pia kumbuka Adamu kwa asili kabla ya kuasi alikuwa mtu wa umilele, asiyeweza kufa, wala kuugua, wala kuzeeka, lakini pamoja na ukamilifu wake Mungu bado alimuumbia ndani yake kula na kunywa katika ile bustani ya Edeni. Hivyo tusubiri tuone, tukifika huko tutajua zaidi, kikubwa tu tunachopaswa kufanya sasahivi ni kujitahidi kuishi maisha ya ushindi yampendezayo Mungu ili siku ile itakapofika tusikose kuyaonja hayo mambo mazuri Mungu aliyotuandalia ambayo jicho halijawahi kuona wala sikio kusikia.

Ubarikiwe.

Mada Nyinginezo:

JE! MBINGUNI KUNA MALAIKA WA KIKE?

CHAGUA NI JIWE LIPI LITAKALO KUFAA KWA UJENZI.

ALAMA KATIKA VIPAJI VYA NYUSO.

USIONDOE ALAMA YA MPAKA ILIYOWEKWA NA MABABA.

JIHADHARI NA ROHO ZIDANGANYAZO.

UMUHIMU WA KUISHI MAISHA YAMPENDEZAYO MUNGU SASA.

MPENDE JIRANI YAKO KAMA NAFSI YAKO.


Rudi Nyumbani:

Print this post

MBINGUNI YUPO NANI SASA?

Jina la Bwana wetu Yesu Kristo libarikiwe, karibu tujifunze Biblia, ambapo leo tutajifunza kwa ufupi juu ya upeo wa kimbinguni.

Mungu alipomuumba mwanadamu, alimwumba na vitu vitatu NAFSI, MWILI na ROHO…kwasababu Mungu naye ndio yupo hivyo hivyo, anayo nafsi, mwili na Roho, maana alituumba kwa mfano wake…Nafsi yake ndio yeye mwenyewe, roho yake ndio Roho Mtakatifu, na mwili wake ndio ule Uliokuwepo Pale Kalvari, ukafufuka na kupaa mbinguni…Kwahiyo uhai uliokuwa ndani ya Mwili unaoitwa Yesu ndio Mungu mwenyewe(nafsi yake) ukisoma Wabrania 1:3 utaliona hilo…Na Roho iliyokuwepo ndani ya ule mwili wa Yesu ndiye Roho Mtakatifu mwenyewe. Hilo linatuthibitishia kuwa Mungu ni mmoja, na nafsi yake ni moja na Roho yake ni moja, na mwili wake ni mmoja.

1 Timotheo 3:16 “Na bila shaka siri ya utauwa ni kuu. Mungu alidhihirishwa katika mwili, Akajulika kuwa na haki katika roho, Akaonekana na malaika, Akahubiriwa katika mataifa, Akaaminiwa katika ulimwengu, Akachukuliwa juu katika utukufu”.

Huyo ni Bwana Yesu anazungumziwa hapo, Mungu katika mwili, aliyehubiriwa katika mataifa na akapaa juu mbinguni…kwasababu hakuna mwingine aliyepaa Mbinguni mpaka kwenye kiti cha enzi zaidi yake yeye..

Yohana 3:13 “Wala hakuna mtu aliyepaa mbinguni, ila yeye aliyeshuka kutoka mbinguni, yaani, Mwana wa Adamu”.

Utauliza mbona Biblia inasema Nabii Eliya na Henoko walipaa na kuchukuliwa mbinguni…Ndugu Nabii Eliya hakupelekwa mbinguni Bwana alipo sasa, bali alipelekwa mahali panapoitwa Peponi (paradiso), ndio maana sehemu nyingine biblia inasema Henoko alihamishwa, sio alipaa (Waebrania 11:5)….wakati mwingine biblia inapataja paradiso kama mbinguni, kwasababu ya uzuri uliopo huko…Lakini hao watu hawakupelekwa mbinguni Bwana aliko sasa, kule hakuna mwanadamu ambaye ameshafika, ni makao mapya yanaandaliwa kule kwa watu wote waliookolewa kufika siku moja kwa pamoja…hakuna mwanadamu aliyetutangulia kufika kule…Ni Bwana Yesu tu! Peke yake ndio yupo kule akituandalia makao na malaika watakatifu..Sasa kama Eliya kashafika huko kutakuwaje tena… “sehemu ambayo jicho halijawahi kuona wala sikio kusikia”? unaona?.

Utauliza tena, na hao wanaoona maono wakipelekwa mbinguni, ina maana maono yao ni batili?..Wengi wao wanaosema wamepelekwa mbinguni kiuhalisia hawajapelekwa mbinguni kwasababu huko hakuna mtu ambaye ameshafika…wanachokiona ni Maono ya mbinguni…Bwana anawaonyesha maono ya jinsi mbinguni kunavyofanana fanana, lakini sio kwamba wamefika,..Sasa Bwana anaweza kuwapa maono ambayo wakati mwingine ni dhahiri kabisa mtu anaweza akahisi yupo mahali pengine katika mwili kabisa…lakini yakawa ni maono tu sio sehemu halisi…

Hata katika namna za kawaida mtu anaweza kuota ndoto ambayo ni kama dhahiri kabisa, katika ndoto akahisi kabisa vile vitu kama vile haoti, akasikia harufu, akachoka, akahisi baridi ndani ya ndoto, akahisi jua linampiga, akahisi njaa, wakati mwingine akahisi mpaka maumivu katika ndoto, Lakini si kweli kwamba huyo mtu saa hiyo yupo katika huo ulimwengu…Hizo zinaitwa njozi. Na ndivyo Bwana anavyozungumza na watu, anaweza kuwapa watu wake maono kama vile wapo Mbinguni kabisa, wakaona pengine barabara za dhahabu, au almasi, wakaona bustani nzuri, wakaona Malaika watakatifu, wakaona uzuri usioelezeka wa huko, hisia ambazo wanaweza wakadhani ni kweli wamefika kule..Hapana kule hawajafika isipokuwa wamepewa tu maono ya kule.

Lengo la Bwana kuwaonyesha vile ni kutaka kuwaonjesha watu wake uzuri watakaokwenda kukutana nao kule, na wawafikishie wengine ujumbe. Na Bwana anaweza kumpa mtu yeyote maono hayo. Sasa ukikosa maarifa ya kuyaelewa haya, unaweza ukajipiga kifua mbele na kufikiri kwamba umeshawahi kufika mbinguni kabla ya wengine…Mambo yaliyopo kule wala hatuwezi kuyafikiria wala kuyastahimili katika hii miili yetu na akili zetu, mpaka tubadilishwe ndipo tutakapoweza kuyaelezea.

Na maono haya Bwana anayowapa watu, yanatofautiana mwingine ataonyeshwa hivi mwingine vile…mwingine kwenye maono hayo ataonyeshwa barabara za dhahabu, mwingine almasi, mwingine marumaru, mwingine ataonyeshwa makasri, mwingine mahekalu, mwingine ataonyeshwa tunu za kipekee, mwingine ataonyweshwa malaika wamevaa kanzu nyeupe wameshikilia upanga, mwingine ataonyeshwa wamevaa nyeupe zenye mshipi wa dhahabu na wameshikilia matarumbeta, mwingine ataonyeshwa wamevaa blue n.k Nk kwa jinsi Bwana atakavyopenda kumwonesha mtu. Ndio maana utaona kila mmoja anakuja na ushuhuda wake tofauti na mwingine wa mambo aliyoyaona…

Sasa kama wangekuwa wamepelekwa mahali halisi, wasingekuja kila mmoja na ushuhuda wake? Unaona? Wote wangekuja na ushuhuda unaofanana…Lakini kwasababu ni maono, maono hayawezi kufanana…ndio maana utaona Hata kwenye Biblia Yohana wa Patmo alipewa maono yenye maudhui sawa na yale ya Nabii Danieli lakini yalikuwa hayafanani…utaona Danieli anaonyeshwa wanyama wanne wanatoka baharini, mmoja alikuwa mfano wa simba, mwingine chui, mwingine Dubu na mwingine kiumbe kisichojulikana (Danieli 7:3-7)…Lakini Yohana anaonyeshwa mnyama mmoja akitoka baharini aliye mfano wa chui, miguu yake kama ya dubu na kinywa kama kinywa cha simba..(Ufunuo 13:2). Sasa alichoonyeshwa Yohana wa Patmo na Danieli ni kitu kimoja isipokuwa katika maono tofauti..ndio maana utaona kuna utofauti kidogo huyu kaonyeshwa wanyama wanne, lakini huyu kaonyeshwa mnyama mmoja mwenye maumbile ya wanyama wote wanne.

Utaona tena jambo hilo katika Kitabu cha Ezekieli, yeye alionyeshwa makerubi wana nyuso nne kila upande, uso wa mwanadamu, tai, Ndama, pamoja na simba, yaani kerubi mmoja ana nyuso nne..kwenye maono ndivyo alivyoonyeshwa..

Ezekieli 1: 5 “Kukatokea katikati yake mfano wa viumbe hai vinne. Kuonekana kwao kulikuwa hivi; walikuwa na sura ya mwanadamu.

6 Na kila mmoja alikuwa na nyuso nne, na kila mmoja alikuwa na mabawa manne.

7 Na miguu yao ilikuwa miguu iliyonyoka; na nyayo za miguu yao zilikuwa kama nyayo za miguu ya ndama; zikimetameta kama rangi ya shaba iliyosuguliwa sana.

8 Nao walikuwa na mikono ya mwanadamu chini ya mabawa yao, pande zote nne; na wote wanne walikuwa na nyuso zao na mabawa yao hivi;

9 mabawa yao yaliungana, hili na hili; nao hawakugeuka walipokwenda, walikwenda kila mmoja kuelekea mbele.

10 Kwa habari za mfano wa nyuso zao; walikuwa na uso wa mwanadamu; na hao wanne walikuwa na uso wa simba upande wa kuume; na hao wanne walikuwa na uso wa ng’ombe upande wa kushoto; na hao wanne walikuwa na uso wa tai pia”.

Lakini Yohana wa Patmo yeye alionyeshwa Kila Kerubi na uso mmoja, yupo aliyekuwa na uso wa Tai, mwingine Uso wa Ndama, mwingine wa Mwanadamu na mwingine wa Simba, lakini hakuoneshwa kuwa kerubi mmoja ana nyuso nne kama alivyooneshwa Nabii Ezekieli.

Ufunuo 4: 6 “Na mbele ya kile kiti cha enzi kulikuwa na mfano wa bahari ya kioo, kama bilauri; na katikati ya kile kiti cha enzi, na pande zote za kile kiti, walikuwako wenye uhai wanne, wamejaa macho mbele na nyuma.

7 Na huyo mwenye uhai wa kwanza alikuwa mfano wa simba; na mwenye uhai wa pili alikuwa mfano wa ndama; na mwenye uhai wa tatu alikuwa na uso kama uso wa mwanadamu; na mwenye uhai wa nne alikuwa mfano wa tai arukaye.

8 Na hawa wenye uhai wanne, kila mmoja alikuwa na mabawa sita; na pande zote na ndani wamejaa macho, wala hawapumziki mchana wala usiku, wakisema, Mtakatifu, Mtakatifu, Mtakatifu, Bwana Mungu Mwenyezi, aliyekuwako na aliyeko na atakayekuja”.

Sasa Yohana na Ezekieli sio kwamba wameonyeshwa vitu tofauti, hapana..ni kitu kimoja isipokuwa katika maono mawili tofauti.

Kwahiyo Mbinguni hakuna aliyefika sasa, ni sehemu mpya Bwana anayowaandalia watu wake, na watakaofika ni wale tu waliooshwa dhambi zao kwa damu yake, yaani wale waliomwamini yeye na kutubu na kubatizwa, na kuishi maisha ya utakatifu (Waebr 12:14)..Wapendwa wetu waliokufa katika Kristo sasa wapo mahali pa mangojeo panapoitwa Paradiso au peponi (Ni mahali wamehifadhiwa pa raha sana, lakini ni pa muda tu, wakingoja siku ile ifike)..Na sisi tutakapokufa kabla ile siku haijafika tutakwenda kuungana nao kule, ni sehemu nzuri sana, wote tutakuwa tunaingoja ile siku kwa pamoja.

Biblia inasema siku ile itakapofika wafu wote (yaani wale waliokufa katika haki, waliohifadhiwa paradiso sehemu ya raha na mangojeo)..watafufuka (yaani watarudi katika miili hii ya asili kwanza)..na watakatifu walio hai watawaona na kuungana nao, na kwa pamoja kufumba na kufumbua tutabadilishwa miili yetu na kuvaa ya miili ya utukufu..itakayoweza kustahimili hayo mambo mazuri na mapya tutakayokwenda kuyakuta huko juu…Na ghafla tutavutwa juu mbali sana na hii ardhi (Itakuwa ni shangwe kubwa sana siku hiyo) tutaiingia mbingu ya mbingu….(na mambo tutakayoyakuta huko hakuna awezaye kuyasimulia kwasababu hakuna mtu alishawahi kufika huko kabla)…Lakini kwa walio nje ya Kristo itakuwa ni kilio na kusaga meno na maombolezo makubwa…

Siku ya mwisho yaja! Maran atha maana yake “BWANA WETU ANAKUJA” Na watakatifu waliopo paradiso wanaitamani hiyo siku ifike haraka…siku ya kufutwa machozi yao, na taabu zao na kuingizwa katika umilele.

Ufunuo 22: 20 “Yeye mwenye kuyashuhudia haya asema, Naam; naja upesi. Amina; na uje, Bwana Yesu”.

Mpe Kristo maisha yako leo, ili uwe na uhakika wa kuwepo miongoni mwa watakaokwenda kuyaona mambo mazuri Bwana aliyowaandalia watu wake..

Bwana akubariki sana.

Pia unaweza ukapata mafundisho haya Kwa njia ya Whatsapp yako, jiunge na channel yetu Kwa kubofya hapa >> WHATSAPP


Mada Zinazoendana:


Mada Zinazoendana:


TOFAUTI KATI YA NDOTO NA MAONO NI IPI?

BASI MUNGU AKAMUADHIMISHA SANA..

UNYAKUO NI NINI?

 SIKU YA BWANA NI NINI?

 NINI HUDUMA YA MALAIKA WATAKATIFU SASA?


Rudi Nyumbani

Home

Print this post