MBINGU MPYA NA NCHI MPYA. (Sehemu ya 1)

by Admin | 27 August 2021 08:46 am08

Nakusalimu katika jina kuu sana lipitalo majina yote la Bwana wetu Yesu Kristo, Nakukaribisha katika kujifunza maneno ya uzima.  Na leo tutajifunza juu ya mbingu mpya na nchi mpya.

Hili ni moja ya maswali yanayoulizwa na watu wengi, Je! Hiyo mbingu mpya na Nchi mpya inayozungumziwa katika maandiko itakuwa wapi? Je ni mbinguni au duniani?. Na Je! Itakuwa ni hii hii dunia yetu au italetwa dunia nyingine na Mungu?. Ili kufahamu fuatana nami mpaka mwisho wa makala hizi.

Historia ya mbingu na nchi:

Sasa kabla hatujaenda kutazama juu ya mbingu mpya na nchi mpya, ni vizuri tukafahamu historia ya “mbingu na nchi” ilianzia wapi. Tukisoma kile kitabu cha Mwanzo, biblia inasema

Hapo mwanzo Mungu aliziumba mbingu na nchi ..(Mwanzo 1:1)

Inaposema “mbingu” inamaanisha anga lote, yaani sayari, na nyota na magimba yote yanayoonekana juu. Na “Nchi” inamaanisha hii dunia yetu tunayoishi sisi wanadamu na viumbe vyote.

Sasa Mungu alipoiumba, ilikuwa ni kamilifu sana, yenye kupendeza, lakini baada ya muda Fulani kupita,ambao biblia haijaeleza ni kipindi cha muda gani, ilikuja kuharibiwa na kuwa UKIWA.  Ikiwa na maana hakukuwa na kiumbe chochote kinachoishi, au uhai wowote unaoendelea, ikabakia kuwa kama mojawapo ya sayari nyingine, isipokuwa tu, hii yetu ilisalia na maji.

Mwanzo 1:2 “Nayo nchi ilikuwa ukiwa, tena utupu, na giza lilikuwa juu ya uso wa vilindi vya maji; Roho ya Mungu ikatulia juu ya uso wa maji”.

Najua pengine unaweza ukawa na swali, Je! Umejuaje, kuwa dunia yetu, hapo mwanzo ilikuwa ni nzuri na kamilifu kabla ya Mungu kuanza kutuumba sisi. Jibu ni kuwa maandiko yanatuambia Mungu hajawahi kuiumba nchi na kuiacha katika hali ya ukiwa. Soma.

Isaya 45:18 “Maana Bwana, aliyeziumba mbingu, asema hivi; Yeye ni Mungu; ndiye aliyeiumba dunia na kuifanya; ndiye aliyeifanya imara; HAKUIUMBA UKIWA, aliiumba ili ikaliwe na watu; Mimi ni Bwana, wala hapana mwingine”.

Unaona hapo? Anasema, hakuiumba ukiwa, ikiwa na maana kuwa Mungu haachi kazi nusu nusu anaumba kikamilifu. Hivyo hiyo inatuonyesha kuwa kabla ya sisi wanadamu kuumbwa, Mungu alikuwa tayari kashaiumba dunia kamilifu na yenye uhai ndani yake, Lakini kukatokea jambo Fulani la uharibifu, ikapelekea Mungu kuiharibu dunia ile, Na hatuwezi kushangaa jambo kama hilo kusababishwa na shetani, na mapepo yake, kwasababu hao ndio waliokuwepo kabla ya sisi wanadamu kuumbwa. Lakini siri hiyo Mungu kaificha ni yeye mwenyewe ndiye anayejua yaliyokuwa yanaendelea huko nyuma.

Sasa wakati ulipofika wa sisi kuumbwa Mungu akaanza kuikarabati dunia tena. ndipo hapo  tunaona akasema na iwe mwanga ikawa mwanga, n.k. Mpaka ikiwa sehemu nzuri sana tena ya kutuvutia, lakini tunajua maisha yalipokuja kuendelea mbele Adamu akaasi, dhambi ikaingia, baadaye hali ikaendelea kuwa mbaya kupitiliza, hadi Mungu akaghahiri kuwaumba wanadamu, baadaye akasema nitawaangamiza wanadamu wote, watoke katika uso wa nchi.

Ndipo hapo akaleta kitu kinachoitwa gharika duniani, akaigharikisha dunia nzima. Akasalia Nuhu tu, na familia yake, jumla watu 8, dunia ikabakia ukiwa kama ilivyokuwa pale mwanzo.

Isaya 24:1 “Tazama, Bwana ameifanya dunia kuwa tupu, aifanya ukiwa, aipindua, na kuwatawanya wakaao ndani yake”.

Hivyo, dunia ya wakati ule ilipogharikishwa, haikukarabatiwa tena na Mungu kama alivyofanya pale mwanzo, badala yake aliyakausha maji tu, lakini uzuri mwingi wa mbingu na nchi ulipotea, jua likawa kali kuliko pale mwanzo, kwasababu maji yaliyokuwa juu ya anga yalipunguzwa, umri wa watu kuishi ukapungua sana, kutoka miaka elfu hadi miaka 120, Kama Mungu alivyosema.

Basi, baada ya hapo maisha yakaendelea tena kama kawaida, watu wakaongezeka , wakaijaza dunia, maasi yakarudi na kuongeza, tena hata zaidi ya kipindi kile cha Nuhu, Mungu akaanza kuwaonya wanadamu kwa vinywa vya manabii wake, akawaambia huu ulimwengu utakwenda kuangamizwa , kama ilivyokuwa kipindi kile cha gharika, lakini kuangamziwa kwake hakutakuwa kwa maji tena, bali kwa moto, ili kuifanya kuwa UKIWA tena.

Unaweza kusoma hilo katika vifungu hivyo katika mistari hii;

Isaya 13:9 “Tazama, siku ya Bwana inakuja, siku kali, ya hasira na ghadhabu kuu, ILI IIFANYE NCHI KUWA UKIWA, na kuwaharibu watu wake, wenye dhambi, wasikae ndani yake.

10 Maana nyota za mbinguni na matangamano havitatoa nuru yake; jua litatiwa giza wakati wa kucha kwake, na mwezi utaacha nuru yake isiangaze.

11 Nami nitaadhibu ulimwengu kwa sababu ya ubaya wake, na wenye dhambi kwa sababu ya hatia yao; nami nitaikomesha fahari yao wenye kiburi; nami nitayaangusha chini majivuno yao walio wakali;

12 nitafanya wanadamu kuadimika kuliko dhahabu safi, na watu kuliko dhahabu ya Ofiri.

13 Kwa hiyo nitazitetemesha mbingu, na dunia itatikiswa itoke katika mahali pake, kwa sababu ya ghadhabu ya Bwana wa majeshi, na kwa sababu ya siku ya hasira yake kali”.

Soma pia,

2Petro 3:6 “kwa hayo dunia ile ya wakati ule iligharikishwa na maji, ikaangamia.

7 Lakini MBINGU ZA SASA NA NCHI zimewekwa akiba kwa moto, kwa neno lilo hilo, zikilindwa hata siku ya hukumu, na ya kuangamia kwao wanadamu wasiomcha Mungu”.

Unaona? Zoezi lile lile la Mungu kuiharibu nchi, linaendelea, lilianza kabla ya sisi kuumbwa, likatokea tena wakati wa Nuhu, na litamalizia, na wakati wetu sisi tunaoishi. Kwahiyo kinachongojewa sasa ni Mungu kuwanyakua tu watakatifu wake, baada ya hapo, kitakachofuata ni uharibifu mkubwa sana wa huu ulimwengu.Ambao utakuwa ni wa kutisha sana, kwasababu, dunia itatikiswa kwa namna ambayo haijawahi kutokea, jua litatiwa giza, visiwa vitahama, waovu wote watakufa, watakaosalia watakawa ni wachache sana pengine watu 10 tu, katika dunia nzima, kwasababu moto usiokuwa wa kawaida utaipika hii dunia tena, ili kuifanya kuwa ukiwa kama pale mwanzo.

Ufunuo 16:17 “Na huyo wa saba akakimimina kitasa chake juu ya anga. Sauti kuu ikatoka katika hekalu, katika kile kiti cha enzi, ikisema, Imekwisha kuwa.

18 Pakawa na umeme na sauti na radi; na palikuwa na tetemeko la nchi kubwa, ambalo tangu wanadamu kuwako juu ya nchi hapakuwa namna ile, jinsi lilivyokuwa kubwa tetemeko hilo. Hii ndio siku ya kiama inayofamika na wengi.

19 Na mji ule mkuu ukagawanyikana mafungu matatu, na miji ya mataifa ikaanguka; na Babeli ule mkuu ukakumbukwa mbele za Mungu, kupewa kikombe cha mvinyo ya ghadhabu ya hasira yake.

20 Kila kisiwa kikakimbia, wala milima haikuonekana tena.

21 Na mvua ya mawe kubwa sana, ya mawe mazito kama talanta, ikashuka kutoka mbinguni juu ya wanadamu. Wanadamu wakamtukana Mungu kwa sababu ya lile pigo la mvua ya mawe; kwa maana pigo lake ni kubwa mno”.

Huu wakati unatisha sana, hatuwezi kueleza mambo yote, lakini kama utataka somo linalohusiana na hii siku ya Bwana itakavyokuwa basi bofya link hii>>>> https://wingulamashahidi.org/2018/07/17/siku-ya-bwana-inayotisha-yaja/

Msingi huu utatusaidia kufahamu agenda ya Mungu juu ya hii dunia yetu, na mpaka mwisho wake utakavyokuja kuwa.

Mpaka hapo tunaweza kuendelea  katika sehemu ya pili ya mbingu mpya na nchi mpya.. Hivyo kwa mwendelezo unaweza kubofya chini>>

MBINGU MPYA NA NCHI MPYA. (Sehemu ya 2)

MBINGU MPYA NA NCHI MPYA. (Sehemu ya 3)

Tafadhali washirikishe na wengine habari hizi njema,

Kwa maombezi/Ratiba za ibada/ Ushauri/ Maswali.
Piga namba hizi: +255693036618 au +255789001312

pia kama utapenda uyapate mafundisho haya kwa njia ya Whatsapp au email basi tutumie ujumbe kwenye namba hizo hizo.

Mada Nyinginezo:

MAPIGO YA VITASA SABA, NA SIKU YA BWANA.

Je ni kweli siku ya mwisho dunia itakunjwa kama karatasi na kutupwa motoni?

Je! tunapaswa kukiamini Kitabu cha Henoko?

UFUNUO: Mlango wa 17

Rudi nyumbani

DOWNLOAD PDF
WhatsApp

Source URL: https://wingulamashahidi.org/2021/08/27/mbingu-mpya-na-nchi-mpya-sehemu-ya-1/