Tofauti kati ya mbinguni, peponi, Kuzimu, Jehanamu, na Paradiso ni ipi?

by Admin | 13 March 2022 08:46 pm03

SWALI: Naomba kuelewa kwa undani Tofauti kati ya mbinguni, peponi, Kuzimu, Jehanamu, na Paradiso ni ipi?


JIBU:

Mbinguni,

Sehemu nyingi Biblia inaposema mbinguni, huwa inamaanisha moja kwa moja kule Mungu alipo Pamoja Malaika zake, Kule ambako Bwana Yesu alikwenda kutuandalia makao. Mahali ambapo sisi kama watakatifu bado hatujafika hata mmoja.

Ndio mbingu ya Tatu, ambayo Mtume Paulo alinyakuliwa kuonyeshwa baadhi ya vitu vilivyopo kule vipo kule ambavyo havielezeki kibinadamu, kwasababu upeo wetu ni mdogo. (2Wakorintho 12:1-4)

Ni juu sana, ambako, hatuna maelezo ya kutosha kupaelezea, mpaka tutakapofika.

2Nyakati 6:18 “Lakini Mungu je! Yamkini atakaa na watu duniani? Tazama, mbingu na mbingu za mbingu za mbingu hazikutoshi; siuze nyumba hii niliyoijenga!”

Peponi/Paradiso:

Ni mbingu ya mangojeo, ambayo sio makazi yetu ya kudumu. Mtakatifu anayekufa sasa hivi anakwenda mahali panapoitwa Peponi/Paradiso, akisubiria, siku ya unyakuo ifike, arudi kaburini achukue mwili wake, kisha aungane Pamoja na wale watakatifu watakaokuwa hai wakati huo, na moja kwa moja safari ya kwenda mbinguni ianze, kule Bwana Yesu alipo.

Yule mwizi pale msalabani, Bwana alimwambia maneno hayo;

Luka 23:42 “Kisha akasema, Ee Yesu, nikumbuke utakapoingia katika ufalme wako.

43 Yesu akamwambia, Amin, nakuambia, leo hivi utakuwa pamoja nami peponi”.

Wengine wanaiita mbingu ya pili, lakini vyovyote vile iitwavyo, bado ni mahali pa mangojeo pa watakatifu, Ndio kifuani pa Ibrahimu, yule maskini Lazaro alikwenda (Luka 16:19-31), ndio kule ambazo zile Roho zilizo chini ya madhahabu zilikuwa zinalia, zikiomba zilipiziwe kisasi kwa watesi wao.

Ufunuo 6:9 “Na alipoifungua muhuri ya tano, nikaona chini ya madhabahu roho zao waliochinjwa kwa ajili ya neno la Mungu, na kwa ajili ya ushuhuda waliokuwa nao.

10 Wakalia kwa sauti kuu, wakisema, Ee Mola, Mtakatifu, Mwenye kweli, hata lini kutokuhukumu, wala kuipatia haki damu yetu kwa hao wakaao juu ya nchi?

11 Nao wakapewa kila mmoja nguo ndefu, nyeupe, wakaambiwa wastarehe bado muda mchache, hata itakapotimia hesabu ya wajoli wao na ndugu zao, watakaouawa vile vile kama wao”.

Vilevile huku ndio kule wale wafu waliofufuka na Bwana Yesu walipoelekea kwa mara ya kwanza. (Mathayo 27:52-53)

Hivyo leo, hii ukifa katika Kristo, basi unakwenda katika eneo hili la mbingu, ambalo ni lizuri sana. Ukisubiri ufufuo wa mwisho.

Kuzimu:

Kuzimu kibiblia ni Neno lililomaanisha makao ya wafu  Au kaburini. Ambapo, waovu na wema walikuwa wanakwenda kabla ya Kristo kuja duniani, kuwatenganisha moja kwa moja kimakao,

 Ayubu anasema

Ayubu 14:13 “Laiti ungenificha kuzimuni, Ukanilinda kwa siri, hata ghadhabu zako zitakapopita, Na kuniandikia muda ulioamriwa, na kunikumbuka!”

Daudi pia alipazungumzia, (Zaburi 16:10), kwamba Bwana hatomwacha huko milele.

Lakini baada ya Bwana Yesu kuja, wakatifu walitoka huko  makaburini, na kwenda peponi/ Paradiso. Mahali pa raha Zaidi pa juu na si makaburini tena. Hivyo wanaobakia makaburini au kuzimu ni waovu.

Jehanamu:

Ni mahali pa mangojeo pa waovu, ni mahali pa mateso, kama vile Paradiso palivyo mahali pa raha pa mangojeo kwa watakatifu, vivyo hivyo jehanamu nako, ni mahali pa mangojeo pa watu waovu wanaokufa sasa. Wanaadhibiwa huko, wakingojea siku ile ya hukumu ya mwisho ifike. Ili wapewe hukumu yao, katika hukumu ya kile kiti cheupe cha enzi cha mwanakondoo, kisha wakatupwe kwenye lile ziwa la moto, ambalo ndio mauti ya pili ilipo.

Ni sawa na mhalifu anayekamatwa sasa hivi, kabla ya kuhukumiwa kifungo, huwa anawekwa kwanza mahabusu, akisubiria siku ya kupandishwa kizimbani ifike, ahukumiwe kisha akatumikie kifungo chake Jela, Ndivyo ilivyo kwa watu waovu wanaokufa sasa, na waliokufa zamani. Wanakwenda katika sehemu hii ya mateso, ambayo si ya kawaida.

Bwana Yesu alisema..

Marko 9:45 “Na mguu wako ukikukosesha, ukate; ni afadhali kuingia katika uzima, u kiwete, kuliko kuwa na miguu miwili, na kutupwa katika jehanum; [

46 ambamo humo funza wao hafi, wala moto hauzimiki.]”

Je! Wewe ni wa makao yapi?

Swali, la kujiuliza ni Je! Tukifa leo, au Unyakuo ukitukuta leo, mimi na wewe tutakuwa wa upande upi? Katika mambo ambayo hupaswi kuyachukulia juu juu tu, basi ni mambo ya Maisha yako ya milele. Kwasababu ukishakufa hakuna nafasi ya pili tena. Kama umestahili Jehanamu basi utaendelea kuishi humo milele.

Ni heri ukamgeukie Kristo, maadamu muda mchache bado unao. Acha kutazama, mambo ya ulimwengu, kwani huwa yanapumbaza sana, kukufanya usione kama kuna mabaya yanakuja mbele, Moja ya hizi siku utajutia Maisha yako, uliishije endapo hukumpa Kristo Maisha yako leo.

Tubu dhambi zako, maanisha kumfuata Yesu.

Bwana atusaidie, kuyafahamu haya.

Shalom.

Tafadhali washirikishe na wengine habari hizi njema,

Kwa maombezi/Ratiba za ibada/ Ushauri/ Maswali.
Piga namba hizi: +255693036618 au +255789001312

pia kama utapenda uyapate mafundisho haya kwa njia ya Whatsapp au email basi tutumie ujumbe kwenye namba hizo hizo.

Mada Nyinginezo:

SIKU YA UNYAKUO ITAKUKUTAJE?

Je! kuna maombi yoyote ya kumtoa mtu aliyekufa kwenye mateso ya kuzimu?

MILANGO YA KUZIMU.

MBINGU MPYA NA NCHI MPYA. (Sehemu ya 1)

Rudi nyumbani

DOWNLOAD PDF
WhatsApp

Source URL: https://wingulamashahidi.org/2022/03/13/tofauti-kati-ya-mbinguni-peponi-kuzimu-jehanamu-na-paradiso-ni-ipi/