Category Archive Unyakuo

KUWA MAKINI, HATUA ZA UNYAKUO ZINAENDELEA.

Nakusalimu katika jina la mwokozi wetu Yesu Kristo. Karibu tuzidi kuyatafakari maneno ya uzima.

Je! Unahabari kuwa watakaonyakuliwa wameshaanza kuandaliwa?  Je! Wewe upo katika hatua ipi?

Biblia inasema zipo hatua ambazo Bwana atatumia kushuka kabla haijaja siku ile yenyewe ya sisi kutwaliwa kwenda mbinguni. Hivyo haitakuwa tendo la kushtukiza kwa wale ambao tayari yameshaingizwa katika hatua hizo.

Angalia ni nini Bwana anasema hapa..

1Wathesalonike 4:16  “Kwa sababu Bwana mwenyewe atashuka kutoka mbinguni pamoja na MWALIKO, na SAUTI YA MALAIKA MKUU, na PARAPANDA YA MUNGU; nao waliokufa katika Kristo watafufuliwa kwanza. 17  Kisha sisi tulio hai, tuliosalia, tutanyakuliwa pamoja nao katika mawingu, ili tumlaki Bwana hewani; na hivyo tutakuwa pamoja na Bwana milele. 18  Basi, farijianeni kwa maneno hayo.”

 Tafakari kwa makini hayo maneno, Bwana hasemi atashuka na “Parapanda” nao waliokufa katika Kristo watafufuliwa kwanza. Kisha sisi tulio hai, tuliosalia, tutanyakuliwa pamoja nao katika mawingu. Hapana Bali anasema, ataanza kwanza na MWALIKO, kisha SAUTI YA MALAIKA MKUU na ndipo Parapanda ya Mungu mwisho. Tofauti na sisi tunavyofikiri, kuwa ni parapanda tu ndio tutakaoisikia ndipo tunyakuliwe.

Ndugu, tafsiri ya hayo maandiko ni kuwa huwezi kuisikia parapanda ya Mungu, kama hujaitikia hatua ya mwaliko na hatua ya sauti ya malaika mkuu. Hivyo Embu tukautazame huo mwaliko ni upi na hiyo sauti ya malaika mkuu ni ipi?

1) MWALIKO.

Awali ya yote tukumbuke kuwa lengo la kunyakuliwa sisi ni ili kwenda kula karamu ya arusi ya mwanakondoo mbinguni, aliyoiandaa Yesu Kristo kwa ajili yetu, kama alivyosema katika Yohana 14:1-4 na Ufunuo 19:9. Hivyo kama tunavyojua hakuna sherehe yoyote isiyokuwa na mwaliko. Hakuna mtu anayejikuta tu kwenye arusi ya mtu bila kualikwa, hakujawahi kuwa na utaratibu huo. Na ndivyo Yesu naye, kabla ya kutupelekea huko mbinguni alipotuandalia vinono, ni sharti kwanza atualike. Hapo ndipo akatumia mfano mmoja wa Mfalme aliyemfanyia mtoto wake karamu kubwa. Lakini katika kuwaalika watu wake, kukawa na mwitikio tofauti tofauti,

Embu tuisome habari hiyo tupate kuielewa vizuri; (Soma kwa utulivu) kwasababu hapa ndipo palipo na msingi.

Mathayo 22:1  “Yesu akajibu, akawaambia tena kwa mithali, akisema, 2  Ufalme wa mbinguni umefanana na mfalme mmoja aliyemfanyia mwanawe arusi.

3  Akawatuma watumwa wake wawaite walioalikwa kuja arusini; nao wakakataa kuja.

4  Akatuma tena watu kwa wengine, akisema, Waambieni wale walioalikwa, Tazameni, nimeandaa karamu yangu; ng’ombe zangu na vinono vimekwisha kuchinjwa, na vyote vimekuwa tayari, njoni arusini.

5  Lakini hawakujali, wakaenda zao, mmoja shambani kwake, mmoja kwenye biashara yake;

6  nao waliosalia wakawakamata watumwa wake, wakawatenda jeuri, na kuwaua.

7  Basi yule mfalme akaghadhibika; akapeleka majeshi yake, akawaangamiza wauaji wale, akauteketeza mji wao.

8  Kisha akawaambia watumwa wake, Arusi i tayari, lakini wale walioalikwa hawakustahili.

9  Basi enendeni hata njia panda za barabara, na wote mwaonao waiteni arusini.

10  Watumwa wale wakatoka wakaenda njia kuu, wakakusanya wote waliowaona, waovu kwa wema; arusi ikajaa wageni.

11  Lakini alipoingia yule mfalme ili kuwatazama wageni wake, akaona mle mtu mmoja asiyevaa vazi la arusi.

12  Akamwambia, Rafiki, uliingiaje humu nawe huna vazi la arusi? Naye akatekewa.

13  Mfalme akawaambia watumishi, Mfungeni mikono na miguu, mchukueni mkamtupe katika giza la nje; ndiko kutakuwako kilio na kusaga meno.

14  Kwa maana waitwao ni wengi, bali wateule ni wachache.

Ukitafakari hapo, utajiuliza, iweje mfalme akualike kwenye sherehe yake halafu usiende?..Ni heri angekuwa mtu wa kawaida, lakini walioalikwa hawakulijali hilo, kwamba yule ni mfalme na sio mtu wa kawaida, hawana budi kuahirisha shughuli zao waende, kwani wamepewa heshima kubwa, lakini  kwao mambo yalikuwa tofauti, wakapuuzia na kibaya zaidi wakawapiga na kuwaua baadhi ya watumwa wake.

Sasa hawa wanalinganishwa na wayahudi, ambao ndio waliokuwa wa kwanza kupewa mwaliko huu ya injili, lakini waliwaangamiza, manabii wengi wa Mungu, mpaka ikafikia hatua ya Kristo akawakataa kabisa, akawakatilia mbali (Soma Mathayo 23:37-39). Hivyo Mungu akahamishia mpango wake wa wokovu kwa watu wa mataifa, ambao ndio mimi na wewe.

Ambao tunalinganishwa sasa na hao waovu, na vilema, waliookotwa huko mabarabarani wakaalikwa kwenye karamu. Maandiko yanatuambia kundi hilo halikukataa mwaliko kama lile la kwanza. Bali lilikubali lote, Lakini sasa ndani ya ukumbi, akaonekana mmoja ambaye alikuwa tofauti na wenzake, yeye hakuwa na “vazi la arusi”. Utajiuliza ni kwanini akose vazi lile? Ni kwanini asifanane na wenzake? Utagundua kuna jambo alilipuuzia, ambalo angepaswa alifanye kabla ili akidhi vigezo vya yeye kuila karamu.

Sasa kabla hatujatazama vazi hilo ni nini? Maana ya mfano huo ni mwaliko wa wokovu ambao tunahubiriwa sisi sote. Ukweli ni kwamba leo hii lipo japo kubwa la watu katika kanisa “wanaokiri wokovu”, wengi wao wamebatizwa, wanashiriki ibada kama kawaida kanisani, wanatoa zaka, wote wanakiri kuwa wanamsubiria Yesu aje kuwanyakua. Lakini je! Ni wote watakaonyakuliwa?  La! Bwana anasema..Siku ile Mmoja atanyakuliwa mmoja ataachwa!(Mathayo 24:40-41) .. Maana yake ni kwamba hupaswi kuridhika tu kuitwa mkristo, lipo jambo la ziada unapaswa ufanye ili ukidhi vigezo vya kuiila karamu ya mwanakondoo mbinguni. Usiridhike tu kusema mimi ni mshirika, mimi ni muumini, acha kabisa hayo mawazo, katika siku hizi za mwisho tunazoishi, yule mtu aliketi kabisa ukumbini, akaona vinono vyote lakini hakula hata kimoja..Sasa embu tuitazame hatua ya pili,

2) SAUTI YA MALAIKA MKUU.

Bwana anasema atashuka na..”Sauti  ya malaika mkuu”. Maana yake ni kwamba kabla ya kuisikia parapanda, ni sharti uisikie hii sauti ya malaika mkuu. Tukirudi katika hiyo habari, ni kwamba yule mtu ambaye hakuwa na mavazi ya arusi, hakuisikia/aliipuzia sauti ya mjumbe aliyesimama pale mlangoni kuwapa maelekezo ya namna ya kukubaliwa katika karamu. Wakati wenzake wanamsikiliza, walipoambiwa wakaoge, wabadili mavazi yao ya kihuni, ya ki-utupu, ya ki-zinzi, ya ki-dunia. Wavae mavazi meupe ya sherehe, yeye akaona ule ni mzigo mzito sana, anamnyima uhuru wake, akataka kwenda kipekee pekee na staili zake, maadamu ameshapewa heshima ya kualikwa na mfalme. Hawezi kuzuiliwa. Hivyo akaendelea kustarehe vilevile pale ukumbini, akimsubiria mfalme, kuja kuwapongeza wageni wake waliomtii.  Lakini alipofika kwake, akidhani, sasa ni wakati wa kupongezwa, akashangaa amebadilikiwa uso, badala ya kupongezwa, ndio kwanza anafungwa Kamba kama vile vibaka, kisha anatupwa nje!

Unajua ni kwanini mpaka biblia inasema ndipo kutakuwa na kilio na kusaga meno, maana yake ni kuwa huyu mtu ambaye alikuwa ameshaweka mawazo yake katika kusheherekea, ghafla anajikuta yupo nje, ni wazi kuwa yeye ndio atakayeumia Zaidi kuliko wale ambao hawakuwahi kualikwa kabisa.

Hivyo kundi hili linafananishwa na watu wote, wanaoitwa wakristo walio kanisani, lakini hawana mavazi ya arusi. Na vazi la Arusi ni UTAKATIFU. Maandiko yanasema hivyo.

Ufunuo 19:7  “Na tufurahi, tukashangilie, tukampe utukufu wake; kwa kuwa arusi ya Mwana-Kondoo imekuja, na mkewe amejiweka tayari.

8  Naye amepewa kuvikwa kitani nzuri, ing’arayo, safi; kwa maana kitani nzuri hiyo ni MATENDO YA HAKI YA WATAKATIFU.

9  Naye akaniambia, Andika, Heri walioalikwa karamu ya arusi ya Mwana-Kondoo. Akaniambia, Maneno haya ni maneno ya kweli ya Mungu.

Ndio maana malaika wa kanisani letu la Mwisho lijulikanalo kama Laodikia. Alipewa ujumbe, unaotuhusu sisi. Ambao hautaki tuwe vuguvugu. Kwasababu tukiwa vuguvugu tutatapikwa. Kumbuka kila kipindi cha Kanisa kilikuwa na malaika wake, mtoa ujumbe, na huyo malaika, alisema kigezo cha kila mmojawao kukubaliwa na Kristo. Tangu kanisa la kwanza, hadi sasa tupo kanisa la mwisho la saba, lijulikanalo kama Laodikia.

Huyo ndio malaika wetu mkuu, ambaye kaachiliwa kutushushia ujumbe huo, hatuna budi kuisikia sauti yake. Kwamba tuwe moto tusiwe vuguvugu, vilevile tununue mavazi meupe, kwa Kristo. Yaani  tuishi maisha matakatifu wasiokuwa na madoa, ili tukidhi vigezo vya kunyakuliwa kwasababu tukikosa maisha hayo, kamwe tusijidanganye sisi ni wakristo.

Tuusome ujumbe wetu;

Ufunuo 3:14  “Na kwa malaika wa kanisa lililoko Laodikia andika; Haya ndiyo anenayo yeye aliye Amina, Shahidi aliye mwaminifu na wa kweli, mwanzo wa kuumba kwa Mungu.

15  Nayajua matendo yako, ya kuwa hu baridi wala hu moto; ingekuwa heri kama ungekuwa baridi au moto. 16  Basi, kwa sababu una uvuguvugu, wala hu baridi wala moto, nitakutapika utoke katika kinywa changu.

17  Kwa kuwa wasema, Mimi ni tajiri, nimejitajirisha, wala sina haja ya kitu; nawe hujui ya kuwa wewe u mnyonge, na mwenye mashaka, na maskini, na kipofu, na uchi.

18  Nakupa shauri, ununue kwangu dhahabu iliyosafishwa kwa moto, upate kuwa tajiri, NA MAVAZI MEUPE UPATE KUVAA, AIBU YA UCHI WAKO ISIONEKANE, na dawa ya macho ya kujipaka macho yako, upate kuona.

19  Wote niwapendao mimi nawakemea, na kuwarudi; basi uwe na bidii, ukatubu.

20  Tazama, nasimama mlangoni, nabisha; mtu akiisikia sauti yangu, na kuufungua mlango, nitaingia kwake, nami nitakula pamoja naye, na yeye pamoja nami.

21  Yeye ashindaye, nitampa kuketi pamoja nami katika kiti changu cha enzi, kama mimi nilivyoshinda nikaketi pamoja na Baba yangu katika kiti chake cha enzi.

22  Yeye aliye na sikio, na alisikie neno hili ambalo Roho ayaambia makanisa”

Hivyo wewe kama mkristo, Epuka maisha ya uvuguvugu. Sababu ya wale wanawali watano wapumbavu kutoingia karamuni, ilikuwa ni hiyo hiyo ya uvuguvugu, hawana mafuta ya kutosha kuziwasha taa zao (Mathayo 25). Mungu anajua tabia ya kanisa la sasa, halipendi kukemewa dhambi linapenda mwonekano wa nje tu, lakini ndani ya uchafu. Bwana atusaidie roho hii isituvae.

3) PARAPANDA YA MUNGU.

Sasa ukishakidhi vigezo hivyo, maana yake unakuwa umepita kigezo cha “walioitwa” mpaka kuwa “mteule”. Unachongoja wewe ni unyakuo tu, parapanda itakapolia, utapaa mawinguni, na hata ukifa kabla Yesu hajarudi, utafufuliwa siku ile, kwasababu ulitii mwaliko na Sauti ya Malaika wako mkuu.

Lakini ukifa katika ukristo vuguvugu, kisha ukafa leo, siku ile ya unyakuo hutafufuliwa na watakatifu wengine, utaendelea kubaki makaburini mpaka siku ya hukumu. Ndugu, unasubiri nini, usiokoke? Na ikiwa umeokoka, maisha ya uvuguvugu utaendelea nayo mpaka lini? Leo upo kanisani, kesho disco, leo unamsifu Mungu, kesho unasikiliza nyimbo za kidunia, leo unatoa sadaka, kesho unakula rushwa, hayo maisha yatakufikisha wapi? Hujui kuwa tunaishi katika kizazi ambacho yamkini kinaweza shuhudia tukio la Unyakuo, kutokana na kutimia kwa dalili zote za siku za mwisho?

Embu tubu sasa umaanishe kumfuata Yesu, mambo aliyotuandalia Yesu ni mazuri yasiyoelekeza, mambo ambayo jicho haliwahi kuona wala sikio kusikia. Tusiyakose hayo. Kosa kila kitu, Usikose Unyakuo. Ikiwa upo tayari kutubu leo dhambi zako kwa kumaanisha kuziacha.

Wasiliana nasi kwa namba hizi bure +255693036618/ +255789001312, tukupe mwongozo wa sala ya toba.. Fanya uamuzi wa haraka sasa, kwani kesho si yao.

Shalom.

Tafadhali shea na wengine ujumbe huu;

Pia Kwa maombezi/ Ushauri/ Maswali/ Whatsapp:
Tuandikie katika BOXI la Maoni hapo chini au
Piga namba hizi: +255693036618 au +255789001312

Jiunge na kundi letu la mafundisho ya Biblia whatsapp kwa kubofya hapa > Group-whatsapp

Mada Nyinginezo:

KWANINI KUWE NA UTAWALA WA MIAKA 1000

MAPIGO YA VITASA SABA, NA SIKU YA BWANA.

BONDE LA KUKATA MANENO.

Kutekewa maana yake nini?(Mathayo 22:12)

JIPE MOYO MKUU.

Kati ya Unyakuo,dhiki kuu, utawala wa miaka 1000 kipi kinaanza

Rudi nyumbani

Print this post

Nini tofauti ya Majira na Wakati?

Wakati ni “kipindi cha Muda” kwa kusudi Fulani, Kwamfano ukipanga kesho saa 7 mchana uende sokoni kununua bidhaa.. sasa huo muda wa “Saa 7 mchana” ndio unaoitwa “wakati wa kwenda kununua bidhaa”

Lakini “Majira” ni kipindi cha Muda ambacho ni cha “Msimu” Kwamfano Msimu wa mvua za masika hayo ni “majira ya masika”..msimu wa matunda ya maembe “hayo ni majira ya maembe”.. Msimu wa baridi, unaitwa “Majira ya baridi”.. Msimu wa joto huo unaitwa “majira ya joto”.

Mwanzo 8:22 “Muda nchi idumupo, MAJIRA YA KUPANDA, na mavuno, wakati wa baridi na wakati wa hari, wakati wa kaskazi na wakati wa kusi, mchana na usiku, havitakoma”

Sulemani alizidi kuliweka hili vizuri kitabu cha Mhubiri..

Mhubiri 3:1 “Kwa kila jambo kuna MAJIRA YAKE, Na WAKATI kwa kila kusudi chini ya mbingu. 

2 Wakati wa kuzaliwa, na wakati wa kufa; Wakati wa kupanda, na wakati wa kung’oa yaliyopandwa;

3 Wakati wa kuua, na wakati wa kupoza; Wakati wa kubomoa, na wakati wa kujenga; 

4 Wakati wa kulia, na wakati wa kucheka; Wakati wa kuomboleza, na wakati wa kucheza”

Unaweza kusoma zaidi juu ya Majira na Nyakati katika Mwanzo 7:21, Zaburi 1:3, Walawi 15:25,  na Ayubu 39:1.

Lakini pia yapo majira na nyakati katika makusudi ya Mungu. Na kusudi kuu ambalo ni muhimu kulijua majira yake ya kurudi kwa BWANA YESU MARA YA PILI!.. Hatuwezi kujua “Wakati” lakini “majira” ya kurudi kwake, tunaweza kuyajua… Ni kama vile hatuwezi kujua siku au wakati mvua itanyesha, lakini tunajua msimu, kuwa tukishaufikia huo msimu basi tunajua  siku yoyote mvua itaanza kunyesha.

Vile vile Bwana Yesu hakutoa wakati wa kurudi kwake, lakini alitoa “MAJIRA” Kwamba tuyafikiapo hayo majira basi tutajua kuwa WAKATI wowote atatokea mawinguni.

Marko 13:32 “Walakini habari ya siku ile na saa ile hakuna aijuaye, hata malaika walio mbinguni, wala Mwana, ila Baba.

33  Angalieni, kesheni, [ombeni], kwa kuwa hamjui WAKATI ule utakapokuwapo”

Sasa Majira ya kurudi kwake ni yapi, ambayo tukiyatazama tutajua kuwa yupo mlangoni?.

Si mengine zaidi ya yale tunayoyasoma katika Mathayo 24, Luka 21 na Marko 13... kwamba kutatokea “Tauni” mahali na mahali, kutasikika tetesi za vita mahali na mahali, kutatokea na magonjwa mfano wa Tauni mahali na mahali, vile vile kutatokea na manabii wengi wa uongo ambao watawadanganya wengi na upendo wa wengi utapoa na maasi yataongezeka.

Hivyo tukishaona hizo dalili basi tunajua kuwa tayari tumeingia katika MAJIRA YA KURUDI KWAKE…na kwamba wakati wowote atatokea mawinguni, na hivyo tunapaswa tuchukue tahadhari… Na majira yenyewe ndio haya tuliyopo mimi na wewe..

Ndugu yangu Yesu anarudi wakati wowote!!, na yeye mwenyewe alituonya tuwe macho!, tukeshe katika roho kila siku, ili siku ile isije ikatujia ghafla..

Lakini tukifumba macho yetu na kukataa kuyatazama haya majira na kuchukua tahadhari.. basi tutaangukia katika like kundi la wanafiki Bwana Yesu alilolitaja katika Luka 12:54-56 na siku ile itatujia ghafla na hatutapona.

Luka 12:54  “Akawaambia makutano pia, Kila mwonapo wingu likizuka pande za magharibi mara husema, Mvua inakuja; ikawa hivyo.

55  Na kila ivumapo kaskazi, husema, Kutakuwa na joto; na ndivyo ilivyo.

56  Enyi wanafiki, mwajua kuutambua uso wa nchi na mbingu; imekuwaje, BASI, KUWA HAMJUI KUTAMBUA MAJIRA HAYA?”

Bwana akubariki.

Tafadhali shea na wengine ujumbe huu;

Pia Kwa maombezi/ Ushauri/ Maswali/ Whatsapp:
Tuandikie katika BOXI la Maoni hapo chini au
Piga namba hizi: +255693036618 au +255789001312

Mada Nyinginezo:

WAKATI ULIOKUBALIKA NALIKUSIKIA

Mtu wa kwanza kufa alikuwa nani?

KUNA NGUVU YA ZIADA KATIKA KULING’ANG’ANIA KUSUDI LA MUNGU.

KUOTA UNAENDESHA GARI.

TAZAMA, MWISRAELI KWELI KWELI, HAMNA HILA NDANI YAKE!

Rudi nyumbani

Print this post

SIKU YA UNYAKUO ITAKUKUTAJE?

Siku ya unyakuo itakukutaje?


Shalom.Jina la Bwana wetu Yesu Krito libarikiwe.

Karibu tujifunze Biblia..Je unajua kuwa kuna siku Kristo atakuja kuwachukua wateule wake? Na kwenda nao mbinguni?..Je unajua watakaokwenda mbinguni ni wachache sana?…Biblia inasema njia ile imesonga na mlango ni mwembamba?..

Mathayo 7:14 “ Bali mlango ni mwembamba, na njia imesonga iendayo uzimani, nao waionao ni wachache”.

Je unajua…baada ya unyakuo kupita…watu watakaoachwa watajuta sana?..Wengi watatamani muda urudishwe dakika 5 tu nyuma angalau watubu…lakini watakuwa wameshachelewa…Je unajua karibia kila mtu duniani tayari kashaonyeshwa aidha kwa ndoto au kwa maono siku ya unyakuo? awe mwenye dhambi au asiye mwenye dhambi…tayari kashaota ndoto angalau moja inayohusiana na kurudi kwa Kristo mara ya pili?. Na wengi wao wanaoonyeshwa hayo wanakuwa wameachwa?..Na wanapata hisia kali sana baada ya kuamka na wanashukuru Mungu imekuwa ni ndoto na wala si kitu cha kweli?.

Binafsi nilishawahi kuota ndoto kama hizo mara kadhaa zamani sana…na zote nilikuwa najiona nimeachwa ni chache sana nilijiona nimekwenda na Bwana lakini nyingi nimeachwa.…na nikiwa ndani ya ndoto nilikuwa nalia na kuomboleza na kumwomba Mungu anirudishe muda angalau dakika 5 nyuma kabla ya unyakuo nirekebishe mambo yangu!…na nikishtuka kutoka usingizini nashukuru Mungu kwamba ni ndoto na si kitu halisi..Hivyo nakwenda kutubu na kumuahidi Mungu kuzidi kujitakasa ili nisije nikaachwa kwenye unyakuo halisi utakapofika…

Lakini yote hayo ni tisa..kumi ni siku tutakayokutana na tukio lenyewe la kuachwa kwenye unyakuo!!…

Siku moja, muda mrefu kidogo umepita, tulikuwa ndani ya nyumba nyakati za jioni kama saa moja na nusu hivi usiku…Umeme ulikatika mtaa mzima..Kukawa na giza lile tororo kabisa..tukaamua kutoka ndani kukaa nje…Na Mahali tulipokuwa tunaishi sio mahali penye watu wengi wanaojichanganya na wengine ni mahali ambapo ikifika jioni tu ni kimyaa na kila mtu kajifungia kwake..Sasa wakati tumekaa nje kidogo tulikuwa wawili mimi na ndugu yangu…tukasema hebu tutazame juu kidogo tuangalie nyota utukufu wa Mungu mbinguni…

Siku hiyo haikuwa na mawingu hivyo nyota zilikuwa zinaonekana vizuri hata zile zinazotembea….….Sasa wakati tunatazama juu ulitokea mwanga fulani wa ajabu wenye rangi unaokaribiana na blue hivi unaong’aa sana, kama mita 5 hivi juu yetu..ukimulika kutokea upande wa magharibi kuelekea upande wa mashariki..na ulikuwa kama unasogea hivi…. Haukuwa na sauti hata kidogo lakini ulikuwa na mwangaza mkali na ulidumu kwa muda kama wa sekunde 3 hivi au Zaidi kidogo..halafu ukatoweka!..ulimulika pale tulipokuwepo kote kukawa kama mchana hivi…

Haukuwa mwanga wa radi kwasababu kipindi hicho kilikuwa ni kipindi cha kiangazi, na wala haikuwa ile mianga inayotokea inamulika bila sauti yoyote wakati wa vipindi vya mvua. Siku hiyo juu hakukuwa na wingu hata moja ni nyota tuu zilikuwa zimetanda anga zima..tokea kaskazini, kusini mashariki mpaka magharibi..hakukuwa na dalili ya wingu…Na mwanga huo hakuja na sauti yoyote…Nakumbuka siku chache tu nyuma tulikuwa tunazungumzia masuala ya unyakuo..Na tulikuwa tunaufahamu ule mstari unaosema…

Luka 17:24 “kwa kuwa, kama vile umeme umulikavyo toka upande huu chini ya mbingu hata upande huu chini ya mbingu, ndivyo atakavyokuwa Mwana wa Adamu katika siku yake.”

Kwahiyo baada ya tukio hilo..Mstari huo ukaja kichwani haraka sana!…tukajua kwamba kuna uwezekanano tayari unyakuo umeshapita na tumeachwa…Baada ya hapo ilikuja hisia moja ambayo siwezi kuilezea, ambayo tangu huo wakati ndio ikanifanya nisichukulie tena kiwepesi suala la kubaki kwenye unyakuo…

Nilihisi kuvunjika moyo na kujuta majuto ambayo sijawahi kuyajuta…Nilianza siku zote nilikuwa nafanya nini mpaka siku hii imenikuta kama mjinga…Nikaanza kuwaza siku chache tu mbeleni nakwenda kumshuhudia mpinga-Kristo kwa macho yangu..siku chache mbeleni nakwenda kupokea chapa…siku chache mbeleni nakwenda kukutana na dhiki kuu, kama sitakufa basi nitashuhudia mapigo yote yale yaliyoandikwa kwenye kitabu cha Ufunuo sura ya 16, maji kuwa damu, jua kutiwa giza, mvua ya mawe n.k..Nikawaza siku chache tu mbeleni hakutakuwa tena na ndugu, wala mama, wala marafiki…wala hakutakuwa tena na kitu kinachoitwa nyumbani…wala hakutakuwa tena na kufanya kazi..Mwisho wa mambo yote umeshafika!.

Nikawaza tena wakati huu sasa hivi watakatifu, waliojitakasa na kuyachukia Maisha yao kwaajili ya Kristo wanafarijiwa mbinguni..sasa hivi Paulo, anafutwa machozi na tabu zake zote zinageuzwa kuwa furaha…Nikarudi kuwaza tena..Nikifa katika dhiki kuu ninakwenda kusimama mbele ya kiti cha hukumu..kuonana uso kwa uso na Yesu Kristo… na mwishowe kuhukumiwa nakwenda kutupwa kwenye ziwa la moto.. Nikakumbuka tena hakuna kutubu katika hii hali tuliyopo sasa..Wakati tunatafakari hayo wote wawili tulijua unyakuo umepita na tumeachwa….Tukawaza tutajibu nini mbele ya kiti cha hukumu.

Usiku ulizidi kuingia nikitamani hata mvua inyeshe ili tujifariji kwamba angalau ulikuwa ni mwanga wa radi ya mvua lakini wapi hakuna chochote…Nikatazama tena ujirudie juu ili pengine tuseme ni kawaida mianga mianga kupiga wakati wa mvua lakini wapi…..hakuna kilichotokea!…palikuwa pakame na juu kulikuwa kweupe vile vile, nyota zimetanda kote na hakuna hata dalili ya wingu …Zile hisia kali za kutazamia mambo yatakayoikumba dunia zilikuwa tayari zimeshafunika hisia za wakati tuliopo…nilitamani siku hiyo iwe ndoto..nizinduke usingizini nitubu kwa kumaanisha kubadilika kabisa..lakini wapi! Ilikuwa ni hali halisi kabisa..

Ndipo asubuhi Bwana akaanza kutufundisha…kwamba haukuwa unyakuo, bali Bwana alikuwa anataka kutufundisha hali itakayotukuta endapo tukiukosa unyakuo..(Na pia kuhusu jambo lingine ambalo halihusiani na hii mada ya leo alituambia kuhusu tukio hilo). Lakini kikubwa ni kuhusu siku ile itakavyokuwa. Na hisia zitakazowapata watu siki hiyo.

Hisia hizo ndizo zitakazowakuta wengi watakaoukosa unyakuo..na siku hiyo watakaoumia sana ni wale ambao tayari kwa namna moja au nyingine walishawahi kuisikia injili huko nyuma lakini hawakutubu au walipuuzia…ambao jana tu walitoka kuhubiriwa lakini wakaikataa injili au wakaipuuzia, ambao juzi tu wametoka kusikia au kusoma habari za kuja kwa Yesu mara ya pili lakini walipuuzia…Hao ndio watakaoomboleza sana na kulia..wengine wote wataona kawaida.

Hiyo kwetu ilikuwa ni ishara kubwa sana ambayo Mungu alizungumza na sisi..Kwa kweli ilitubadilisha Maisha yetu tangu huo wakati…Mpaka leo hii siwezi kuisahau hiyo hisia…nasema nikose chochote lakini sio UNYAKUO..Na namshukuru Mungu kwa kuzungumza na mimi kwa ishara ya nje kabisa kwani angesema nami kwa ndoto tu kama siku zote pengine nisingechukulia kwa uzito kwa kiwango hicho na mpaka leo ningebaki kuchukulia kuachwa ni jambo la kawaida.

Ndugu Kuna uchungu wa ajabu na hisia mbaya sana kwa watu watakaoukosa unyakuo…Hebu jiweke kwenye mazingira leo hii ndio unyakuo umepita na umeachwa?..utajisikiaje! labda unaweza usielewe sasa mpaka siku hali hiyo itakapokukuta…Lakini usitamani uwepo..Siku hiyo utasikia unyakuo umepita masaa machache tu umepishana na mahubiri ya kukuonya utubu.

Je! Umejiweka tayari?..Biblia inasema katika Waebrani 10:37 “Kwa kuwa bado kitambo kidogo sana, Yeye ajaye atakuja, wala hatakawia”.

Leo hii unasema unyakuo bado sana..siku hiyo ikifika utatamani urudishwe dakika 5 nyuma urekebishe mambo yako lakini utakuwa umeshachelewa.

Kama hujaokoka leo mlango wa Neema upo wazi..Hivyo pale ulipo jinyenyekeze kwa Mungu..Mwombe akusamehe dhambi zako zote ulizokuwa unazifanya za makusudi na ambazo sio za makusudi..Kisha baada ya kutubu fanya kama ulivyotubu..acha kufanya dhambi ulizokuwa unazifanya…kama ulikuwa mwasherati..acha uasherati, ulikuwa mwizi vivyo hivyo unaacha, ulikuwa unavaa nusu uchi..unaacha..ulikuwa mtazamaji wa picha chafu mitandaoni unazifuta na kuanza maisha mapya..

Ukishafanya hivyo Kristo atakupa amani ya ajabu moyoni mwako.Amani hiyo utakayoipata ndio itakuwa uthibitisho wa msamaha wako..Baada ya kufanya hivyo nenda kabatizwe kama hujabatizwa, ubatizo sahihi ni ule wa kuzamishwa katika maji mengi na kwa jina la Yesu Kristo. Na Roho Mtakatifu ndani yako atakuongoza katika mambo mengine yaliyosalia ikiwemo kukupa uwezo wa kushinda dhambi na ufahamu wa kuyaelewa maandiko. Ukiishi katika hali hiyo biblia imetupa uhakika wa kunyakuliwa Kristo atakaporudi..Hakuna namna yoyote ambayo unaweza usinyakuliwe.

Bwana azidi kutupa Neema yake tushinde ulimwengu huu kama yeye alivyoshinda. Ili siku ile tuifarahie karamu aliyotuandalia mbinguni milele.

Maran atha!

jiunge na channel yetu Kwa kubofya hapa >> WHATSAPP

Mada Nyinginezo:

UNYAKUO.

Ule mfano wa wanawali 10 (Mathayo 25), wale watano hawakuwa na mafuta ya ziada katika chupa zao je yale mafuta ya ziada yanawakilisha nini?

SIKU YA TAABU YA YAKOBO.

MAPIGO YA VITASA SABA, NA SIKU YA BWANA.

DHAMBI ILIYOMKOSESHA SHETANI:

Rudi Nyumbani:

Print this post

Kati ya Unyakuo,dhiki kuu, utawala wa miaka 1000 kipi kinaanza

SWALI:Naomba kuuliza kati ya Unyakuo wa watakatifu, Dhiki kuu, Vita vya har-magedoni, Utawala wa miaka 1000, Vita ya gogu na magogu, hukumu ya kiti cha enzi cheupe. Je, ni nini kinaanza na kingine kufuata kwa mpangilio wa matukio hayo?


JIBU

HATUA YA UNYAKUO.

Kwa ufupi kulingana na kalenda ya Ki-Mungu, kwasasa tunasubiria unyakuo wa watakatifu ambao huo upo karibuni sana kutokea. Wakati wowote katika kizazi chetu hichi tunachoishi jambo hilo tunaweza tukalishuhudia kwa macho yetu, Hivyo huo ndio utakoanza kwanza… Sasa baada ya unyakuo wa watakatifu kupita ambao ni watu wachache sana watakaokwenda mbinguni . Kwasababu Bwana mwenyewe alishatuonya akasema “kama ilivyokuwa katika siku za Nuhu na Lutu, ndivyo itakavyokuwa katika siku zake mwana wa Adamu, wakati ule watu wachache sana waliokoka (yaani nane kwa watatu kati ya mamilioni ya watu waliokuwepo duniani) ndivyo itakavyokuwa katika siku za unyakuo..Na sehemu nyingine alisema  

Mathayo 22:14 Kwa maana waitwao ni wengi, bali wateule ni wachache.

  Hivyo anazidi kusema…  

Luka 13:24 “Jitahidini kuingia katika mlango ulio mwembamba, kwa maana nawaambia ya kwamba wengi watataka kuingia, wasiweze”.

Unaona hapo kwahiyo hili kundi litakalonyakuliwa ambalo lilishakwisha jiweka tayari tangu zamani kwenda na Bwana litakuwa dogo sana tofauti na wengi wanavyodhani kwamba watu watatoweka mabarabarani,na dunia nzima kutaharuki kwa tukio hilo n.k. Hilo jambo halipo. Kundi hili litakapoondoka hakuna mtu asiyemjua Mungu atakayejua, dunia nzima itaendelea na shughuli zake kama kawaida…watakuja kufahamu baadaye mambo ya mambo kubadilika ndipo watakapojua kuwa kumbe unyakuo wa watakatifu ulishapita.  

HATUA YA DHIKI KUU.

Hivyo ukishapita unyakuo wa watakatifu, sasa ndio Dhiki kuu itaanza, hii itakuwa ndani ya kile kipindi cha miaka 7 ya mwisho, wakati huo mpinga-kristo atanyanyuka ili kuihimiza ile chapa ya mnyama ianze kutenda kazi haraka, kutakuwa na dhiki isiyokuwako kwa wale wote(wanawali wapumbavu) watakaokosa unyakuo.

Ndugu Wakati huo sio wa kutamani kuwepo, kwasababu mfano wa mateso yatakayokuwepo huko Bwana anasema hayakuwahi kutokea katika kipindi chochote katika historia na wala hayatakaa yatokee mengine mfano wa hayo baada ya hapo.   Na pia kumbuka dhiki hiyo vile vile haitamuhusu kila mtu duniani, hapana bali nalo litakuwa ni kundi dogo tu, tena wale watakaogundua kuwa ule ni mfumo wa shetani, wakati huo dunia nzima itaifurahia mfumo wa mpinga-kristo. kwasababu wakati huo mpinga-kristo atakuwa mwerevu ili awapate wengi hivyo Utaonekana kama ni ustaharabu mzuri sana wa amani aliouleta, na utapendwa na wengi. Na wale wote watakaojaribu kuufichua uovu wake wao ndio wataonekana kama wenyewe ndio wapinga-kristo badala yake. Sasa baada ya hawa watu (bikiria wapumbavu) kuuliwa. Kitakachofuata kitakuwa ni ile siku kuu ya Bwana ya kutisha. Ambayo Bwana aliiweka mahususi kwa ajili ya watu wote waovu.  

Amosi 5:18 “Ole wenu! Ninyi mnaoitamani siku ya Bwana; kwani kuitamani siku ya Bwana? Ni giza, wala si nuru. 19 Ni kama mtu aliyemkimbia simba, akakutana na dubu; au aliingia katika nyumba akauegemeza mkono wake ukutani, nyoka akamwuma. 20 Je! Siku ya Bwana haitakuwa giza, wala si nuru? Naam, yenye giza sana, wala haina mwanga. ”

Sasa Hapo ndipo Bwana atajilipizia mwenyewe kisasi juu ya mataifa yote yaliyosalia ulimwenguni yaliyopokea ile chapa ya mnyama, na watu wote yasiyomcha Mungu, hii itaambatana na yale mapigo ya vitasa 7 (Ufunuo 16).   Na ndio humo humo katikati vile vita vya Har-magedoni vitapangwa, pale mataifa yote duniani yatakusanyika ili kufanya vita na mwanakondoo, Hii haitakuwa kabisa vita kwasababu Mungu hapigani na wanadamu,.Bwana anasema ule upanga(Neno lake) utokao katika kinywa chake ndio utakaowaua.

(Ufunuo 19:11-21) Hao waliokusanyika. Hivyo Bwana atawaua wote, na mizoga yao itakuwa chakula cha ndege wa angani.   Hapa ndipo mataifa yote ulimwenguni yataomboleza wakitamani milima iwaangukie wajisitiri na ghadhabu ya Mungu mwenyezi, (Ufunuo 6:12).  

HATUA YA UTAWALA WA MIAKA 1000. 

Hivyo Mungu akishayahukumu mataifa kitakachofuata ni utawala wa amani wa Bwana wetu Yesu Kristo wa miaka1000. Huko dunia itarejezwa tena katika hali yake nzuri ya mwanzo kama Edeni au zaidi ya hapo, dhambi haitatawala tena (kwasababu shetani atakuwa amefungwa wakati huo),

VITA YA GOGU NA MAGOGU

japo waovu biblia inarekodi watakuwepo na ndio hao baada ya ule utawala kuisha, shetani atakapofunguliwa tena kwa kipindi kifupi akawadanganye ili walete madhara, Biblia inasema moto utashuka kutoka mbinguni na kuwameza..Hiyo ndio hiyo vita ya Gogu na Magogu inayozungumziwa kwenye(Ufunuo 20:8),

Hivyo hiyo nayo hakutakuwa vita kabisa kwasababu pindi watakapotaka kujaribu kufanya hivyo moto utashuka kutoka mbinguni na kuwameza wote.  

HUKUMU YA KITI CHEUPE CHA ENZI.

Kisha baada ya hapo YESU KRISTO Bwana wetu atakaa katika kiti chake cha enzi CHEUPE, na wafu wote watafufuliwa wale ambao hawakuwepo katika ufufuo wa kwanza pamoja na hao waliokuwa wanataka kufanya vita na watakatifu wa Mungu ndani ya ule utawala wa miaka 1000. Wote kwa pamoja watahukumiwa kulingana na matendo yao.  

HATUA YA ZIWA LA MOTO.

Kisha baada ya hapo watatupwa katika lile ziwa la moto alipo shetani na malaika zake. Na ndipo mbingu mpya na nchi mpya zitakapokuja…Kuanzia huo wakati na kuendelea muda utaondolewa, na umilele utaanza, mambo ya kwanza yatakuwa yamekwisha pita tazama yamekuwa mpya…

Haleluya..Huko tutazidi kumjua Mungu kwa namna isiyo ya kawaida.Tuombe tusikose kuwepo huko,.Biblia inasema mambo ambayo jicho halijawahi kuona wala sikio kusikia, wala kuingia katika moyo wa mwanadamu, mambo ambayo Mungu amewaandalia wale wampendao (1Wakorintho 2:9).   Mungu wetu ni mwema. Libarikiwe jina lake. Milele na milele. Amina.  

Ubarikiwe sana. jiunge na channel yetu Kwa kubofya hapa >> WHATSAPP


Mada zinazoendana:

SIKU YA BWANA INAYOTISHA YAJA!

SIKU YA TAABU YA YAKOBO.

DANIELI: Mlango wa 1

UFUNUO: Mlango wa 16.

TUJIFUNZE JAMBO KWA WANAWAKE HAWA WAWILI:

UDHAIFU WA SADAKA!


Rudi Nyumbani:

 

 

Print this post