WAKATI ULIOKUBALIKA NALIKUSIKIA

WAKATI ULIOKUBALIKA NALIKUSIKIA

Maandiko yanasema kila jambo lina majira yake..

Mhubiri 3:1 “Kwa kila jambo kuna majira yake, Na wakati kwa kila kusudi chini ya mbingu”.

Maana yake ni kwamba kuna mambo ambayo unaweza kuyatamani yatokee lakini kama si majira yake hayawezi kutokea.

Kama muembe haujafika majira yake ya kuzaa maembe, haijalishi utaumwagia maji kiasi gani, au utauwekea mbolea kiasi gani, kamwe hautazaa..

Kwanini?

Kwasaababu sio msimu wa maembe, sio majira yake ya kuzaa..Lakini utakapofika wakati wake hata usipomwagiwa maji wala kuwekewa mbolea bado utazaa tu!!.

Kadhalika pia katika mambo ya rohoni, kuna vitu vinavyopatikana kwa msimu tu!. Sio kila wakati vipo, Na moja wapo ya hivyo ni NEEMA YA WOKOVU.

Tofauti na inavyofikiriwa na wengi kuwa Neema ya wokovu ni ya milele na ya wakati wote!.. Lakini kiuhalisia! Sio ya Milele, ni ya kupindi fulani tu!.

Kabla ya Bwana Yesu kuja duniani, neema hii ilikuwa haipatikani, hakukuwa na kitu kinaitwa msamaha wa dhambi, (Dhambi zote zilikuwa zinafunikwa tu).

Daudi, Musa, Eliya, na manabii wengine wote hawajawahi kuondolewa dhambi zao, badala yake zilikuwa zinafunikwa tu!, Na kila mwaka kunakuwa na kumbukumbu la dhambi.

Na hiyo si kwasababu walikuwa hawaombi sana, au hawakuwa na bidii..la! Walikuwa na bidii kuliko hata sisi (Maandiko yanasema Eliya alikuwa ni mtu wa kuomba sana kwa bidii, Yakobo 5:17).

Sasa kama ni hivyo kwanini, Hawakupewa hii Neema?.

Jibu ni kwasababu haukuwa Wakati wa Neema kuachiliwa duniani, haukuwa msimu wa Neema ya Mungu kudhihirika duniani, haijalishi wangeomba kiasi gani, bado hii Neema tuliyonayo sisi wasingeipata, kwasababu haukuwa wakati uliokubalika.

Lakini baada ya Bwana kuja duniani, ndipo majira mapya yakaanza.. Ukawa ni wakati uliokubalika wa Neema ya Mungu kumwagwa duniani.

Luka 4:18 “Roho wa Bwana yu juu yangu, Kwa maana amenitia mafuta kuwahubiri maskini habari njema.

Amenituma kuwatangazia wafungwa kufunguliwa kwao, Na vipofu kupata kuona tena, Kuwaacha huru waliosetwa,

19 Na kutangaza mwaka wa Bwana uliokubaliwa”.

Hapo mstari wa 19, anasema “Kutangaza mwaka wa Bwana uliokubaliwa”.

Hajaishia kusema tu “Mwaka wa Bwana”..bali pia “uliokubaliwa”.

Maana upo wakati uliokubalika na wakati ambao sio wa kukubalika.

Sasa tukishayajua hayo tunapaswa tufanye nini?

Biblia imetupa ushauri..

2 Wakorintho 6:1 “Nasi tukitenda kazi pamoja naye twawasihi msiipokee neema ya Mungu bure.

2 (Kwa maana asema,Wakati uliokubalika nalikusikia,Siku ya wokovu nalikusaidia; tazama, wakati uliokubalika ndio sasa; tazama, siku ya wokovu ndiyo sasa.)

Hapo anasema “wakati uliokubalika nalikusikia”..na “siku ya Wokovu nalikusaidia”

Kwa lugha rahisi ni kwamba “msimu wa neema nitakusikia” “Na msimu wa kuokolewa nitakusaidia”. Maana yake msimu tofauti na huo hakuna wokovu. Kama vile misimu ya matunda ilivyo.

Ndugu hii Neema ipo ukingoni sana kuisha, na itaisha siku ile Unyakuo utakapotokea duniani, baada ya hapo hata ulieje, hakuna wokovu kwasababu sio saa ya wokovu, siku hiyo hata ufungeje kwa maombi na dua na sala hutasikiwa kwasababu sio wakati uliokubalika.

Je umeichukuliaje hii Neema leo?

Manabii wa zamani walitamani kukiona hichi kipindi tulichopo lakini hawakukiona.
Huu ndio wakati wa kusikiwa maombi yetu na sala zetu na Mungu, wakati unakuja mbingu zitafungwa.

Je umeingia ndani ya Neema leo?

Unaingiaje ndani ya neema?Unaingia kwa kumkiri Yesu na kutubu dhambi zako zote na kubatizwa kwa Jina la Yesu.

Kanuni rahisi tu hiyo, inakusogeza karibu sana na Mungu kwa viwango vingine.

Maran atha!

Tafadhali washirikishe na wengine habari hizi njema,

Kwa maombezi/Ratiba za ibada/ Ushauri/ Maswali.
Piga namba hizi: +255693036618 au +255789001312

pia kama utapenda uyapate mafundisho haya kwa njia ya Whatsapp au email basi tutumie ujumbe kwenye namba hizo hizo.


Mada Nyinginezo:

WALA MSIUANGALIE MWILI, HATA KUWASHA TAMAA ZAKE.

Neema ni nini?

FUMBO ZA SHETANI.

MFANYE BWANA YESU MWENYEJI MAISHANI MWAKO.

Rudi nyumbani

Print this post

About the author

Admin administrator

Subscribe
Notify of
guest
0 Comments
Inline Feedbacks
View all comments