TAFUTA UZIMA WA MILELE NA SI UZIMA TU!.

TAFUTA UZIMA WA MILELE NA SI UZIMA TU!.

Ipo tofauti ya “Uzima” na “Uzima wa milele”.

Uzima, kila mwanadamu anao, na si wanadamu tu peke yao wenye uzima, bali hata Wanyama wanao uzima, na hata ndege na mimea. Lakini Pamoja na kwamba Uzima upo kwa viumbe vingi, lakini Uzima wa milele haupo kwa wote.

Uzima wa Milele ni kitu kingine kabisa…ambacho Mtu hana budi kukitafuta.. Na asipokitafuta na kukipata ataishia kuwa na uzima tu wa kitambo, ambao hautadumu sana, kwasababu wote wasio na uzima wa milele ndani yao, wakishakufa hawatafufuliwa na kuendelea kuishi, badala yake wataangamizwa katika ziwa la moto.

Na Uzima wa milele (ambao kwa lugha nyingine unaitwa “UZIMA TELE”), Unapatikana kwa mmoja tu ambaye ni Yesu.

Yohana 10:10 “…mimi nalikuja ili WAWE NA UZIMA, KISHA WAWE NAO TELE”.

Umeona?..Bwana Yesu amekuja ili tuwe na UZIMA, yaani tuwe na Afya, tuishi Maisha ya heri katika mwili, lakini hajaishia hapo, bali pia tuwe na UZIMA TELE, (Yaani tuwe Uzima wa Milele).

SASA SWALI NI JE TUTAUPATAJE UZIMA WA MILELE?

Jambo moja linalowachanganya wengi, ni kudhani kuwa kuwa na maadili mazuri au kuwa na dini nzuri, au KUSHIKA AMRI 10, ndio kupata Uzima wa milele, pasipo kujua kuwa kuzishika amri 10, au kuwa na dini nzuri, au dhehebu zuri, kama mtu “hajaamua kujikana nafsi ya kumfuata Bwana Yesu” ni kazi bure.. Dini yake nzuri huyo mtu, au maadili yake mazuri, au sifa yake nzuri bado, hakutampa uzima wa milele.

Hebu tusome kisa kifuatacho.. (Zingatia vipengele vilivyoanishwa kwa herufi kubwa).

Mathayo 19:16 “Na tazama, mtu mmoja akamwendea akamwambia, Mwalimu, nitende jambo gani jema, ili nipate UZIMA WA MILELE?

17 Akamwambia Kwani kuniuliza habari ya wema? Aliye mwema ni mmoja. LAKINI UKITAKA KUINGIA KATIKA UZIMA, zishike amri.

18 Akamwambia, Zipi? Yesu akasema, Ni hizi, Usiue, Usizini, Usiibe, Usishuhudie uongo,

19 Waheshimu baba yako na mama yako, na, Mpende jirani yako kama nafsi yako.

20 Yule kijana akamwambia, Haya yote nimeyashika; nimepungukiwa na nini tena?

21 Yesu akamwambia, UKITAKA KUWA MKAMILIFU, ENENDA UKAUZE ULIVYO NAVYO, UWAPE MASKINI, NAWE UTAKUWA NA HAZINA MBINGUNI; KISHA NJOO UNIFUATE”.

Hapo nataka uone maswali, huyu mtu aliyomwuliza Bwana na Majibu Bwana aliyompa.. Swali la kwanza huyu mtu alitaka kujua jinsi ya kuupata UZIMA WA MILELE. Lakini utaona Bwana Yesu alimwambia akitaka KUUPATA UZIMA, (Zingatia; sio uzima wa milele, bali Uzima tu), azishike amri.

Ikiwa na maana kuwa Kuzishika amri 10 peke yake hazimpi mtu UZIMA WA MILELE, bali zinampa tu UZIMA. (aishi Maisha marefu hapa duniani na ya heri) Sawasawa na Walawi 18:5.

Walawi 18:5 “Kwa ajili ya hayo mtazishika amri zangu na hukumu zangu; ambazo MTU AKIZITUMIA ATAISHI KWA HIZO; mimi ndimi Bwana”.

Lakini swali la pili, huyu mtu alilomwuliza Bwana Yesu ni kwamba, tayari ameshazishika hizo amri, ni kitu gani alichopungukiwa Zaidi?.

Na Bwana Yesu alipoona kuwa anauhitaji UZIMA WA MILELE na si UZIMA TU!. Ndipo akamwambia “akauze kila kitu alichonacho kisha amfuate” kwa ufupi, ajikane nafsi yake ajitwike msalaba wake na kumfuata.

Lakini kwasababu yule mtu alikuwa anautaka Uzima na si Uzima wa milele, hakutaka kufanya vile, akaondoka!.. Na akaondoka akiwa na Uzima, na heri katika Maisha, lakini hana Uzima wa milele, jambo la kuhuzunisha sana.

Ndugu unayesoma ujumbe huu, maandiko yanasema kuwa Yesu Kristo ni yeye yule, jana na leo na hata milele, habadiliki (kasome Waebrania 13:8), Maana yake ni kuwa vigezo vyake ni vile vile, kwa jinsi alivyomwambia huyu bwana, kwamba akauze vyote amfuate ndipo apate uzima wa milele, ndivyo anavyotuambia hata watu wa leo.

Sio kwamba huyu ndugu, alikuwa na bahati mbaya mpaka aambiwe vile na Bwana Yesu. Hapana!. Maneno hayo hayo aliwaambia pia wanafunzi wake kabla ya kumfuata..

Luka 14:33 “Basi, kadhalika kila mmoja wenu asiyeacha vyote alivyo navyo, hawezi kuwa mwanafunzi wangu”.

Sasa kuacha vyote kunakozungumziwa hapo ni kukitoa kitu katika moyo wako moja kwa moja, kama ni mali, Rafiki, ndugu, au chochote kile, unakitoa moyoni mwako na kuwa tayari kuyafanya mapenzi ya Mungu..Kama kimeondoka kweli moyoni mwako, basi hata ukiwa nacho kimwili hakina madhara yoyote, kwasababu kiwepo au kisiwepo, hakikusumbui kwasababu huna muunganiko nacho kiroho.. Lakini kama umekiondoa kimwili lakini moyoni mwako bado kipo, bado utakuwa hujafanya chochote..

Hivyo hiyo ni kanuni KUU sana, ambayo sote tunapaswa tujifunze. Gharama za kuupata uzima wa milele si ndogo. Zinahitaji kujikana nafsi kweli kweli, na kubeba msalaba na kumfuata Yesu.

Hebu kwa kumalizia tuisome faida hiyo ya kujikana nafsi na kumfuata Yesu kwa kumalizia mistari ya chini..

Mathayo 19:22 “Yule kijana alipolisikia neno lile, akaenda zake kwa huzuni; kwa sababu alikuwa na mali nyingi.

23 Yesu akawaambia wanafunzi wake, Amin, nawaambieni, ya kwamba itakuwa shida tajiri kuingia katika ufalme wa mbinguni.

24 Nawaambia tena, Ni rahisi zaidi ngamia kupenya tundu ya sindano, kuliko tajiri kuingia katika ufalme wa Mungu.

25 Wanafunzi waliposikia, walishangaa mno, wakisema, Ni nani basi awezaye kuokoka?

26 Yesu akawakazia macho, akawaambia, Kwa wanadamu hilo haliwezekani; bali kwa Mungu yote yawezekana.

27 Ndipo Petro akajibu, akamwambia, Tazama, sisi tumeacha vyote tukakufuata; tutapata nini basi?

28 Yesu akawaambia, Amin, nawaambia ya kwamba ninyi mlionifuata mimi, katika ulimwengu mpya, atakapoketi Mwana wa Adamu katika kiti cha utukufu wake, ninyi nanyi mtaketi katika viti kumi na viwili, mkiwahukumu kabila kumi na mbili za Israeli.

29 Na kila mtu aliyeacha nyumba, au ndugu wa kiume au wa kike, au baba, au mama, au watoto, au mashamba, kwa ajili ya jina langu, atapokea mara mia, na kuurithi uzima wa milele”.

Je! Umejikana nafsi na kumfuata Yesu? Au unajitumainia dini yako?, huyu kijana alikuwa na dini na ameshika amri zote lakini hakuwa na uzima wa milele ndani yake?, unadhani wewe na dhehebu lako utautolea wapi?..

Maadili yako yatakupa Uzima tu!, ni kweli utabarikiwa kwa kuishi vizuri duniani, kwa kuwa na moyo mzuri, lakini kama Yesu hajaingia ndani yako, huna uzima wa milele.

Ukitaka uzima wa milele weka dhehebu lako pembeni, weka dini yako pembeni, weka mali zako pembeni, weka uzuri wako pembeni, weka umaarufu wako pembeni,  weka sifa zako pembeni, na kila kitu chako, weka kando nenda kama mshamba mbele zake Bwana Yesu, kama asiyejua chochote, kama mtu aliyezaliwa leo, kama vile kondoo aliyetayari kuchungwa…Bwana Yesu anataka moyo uliojiachia kwake, moyo wa unyenyekevu..hapo ndipo atakapokuonyesha njia na kukupa uzima wa milele?.

Kama hujaokoka basi hakikisha siku ya leo haipiti bila kuokoka, kwasababu hujui ni nini kitatokea kesho, tafuta mtu aliye mkristo, aombe Pamoja na wewe katika sala fupi ya kumkaribisha Bwana Yesu maishani mwako, au wasaliana nasi kwa namba zilizopo chini ya somo, tutakusaidia kwa hilo.

Bwana akubariki.

Maran atha!

Tafadhali shea na wengine ujumbe huu;

Pia Kwa maombezi/ Ushauri/ Maswali/ Whatsapp:
Tuandikie katika BOXI la Maoni hapo chini au
Piga namba hizi: +255693036618 au +255789001312 Jiunge na kundi letu la mafundisho ya Biblia whatsapp kwa kubofya hapa > Group-whatsapp


Mada Nyinginezo:

NUNUA MAJI YA UZIMA.

NUNUA MAJI YA UZIMA.

MFALME ANAKUJA.

OLE WAO WANAOJITAHIDI KUMFICHA BWANA MASHAURI YAO.

FANYIKA SIPORA WA KRISTO, UNYAKUO UPO KARIBU.

Rudi nyumbani

Print this post

About the author

Admin administrator

Subscribe
Notify of
guest
2 Comments
Newest
Oldest Most Voted
Inline Feedbacks
View all comments
Samari
Samari
1 year ago

Bwana azidi kuwa pamoja nanyi na azidi kuwatia nguvu daima siku zote amina