MBINGU MPYA NA NCHI MPYA. (Sehemu ya 2)

by Admin | 27 August 2021 08:46 am08

Sasa kama tulivyotangulia kuona katika sehemu ya kwanza kuwa hii dunia yetu ilipoumbwa, ilipitia uharibifu wa mara kwa mara, na baadaye kukarabatiwa  tena na sasa imesaliwa na uharibifu mmoja wa mwisho ambao  utakuja ulimwenguni hivi karibuni, na uharibifu wenyewe hautakuwa wa maji tena, bali wa moto. (2Petro 3:6-7)

Kwahiyo Mungu atakapomaliza kuuharibifu huu ulimwengu na kuwaondoa waovu wote, ataikarabati hii dunia na kuirejeshea utukufu wake kwa ilivyokuwa pale Edeni.  Na sababu ya Mungu kufanya hivyo, ili kuruhusu YESU KRISTO kuja kutawala hapa duniani pamoja na watakatifu wake, kama Mfalme wa Wafalme, na Bwana wa Mabwana kwa kipindi cha  miaka elfu moja (1000).

Wakati huo dunia itakuwa yenye amani tele, watu wataanza kuishi umri mrefu kama mwanzo, biblia inasema, mtu atakayekuwa na umri wa miaka 100 ataitwa bado mtoto mchanga,

Isaya 65:20 “Hatakuwapo tena mtoto wa siku chache, wala mzee asiyetimia siku zake; kwa maana mtoto atakufa mwenye umri wa miaka mia; bali mtenda dhambi mwenye umri wa miaka mia atalaaniwa”.

Watu watakuwa wakipanda na kujengwa wala hakuna atakayekuja kuharibu, au kuong’oa mazao yao. Wanyama wote watakuwa wapole, simba atakula majani, na mtoto atacheza kwenye tundu la nyoka na asidhuriwe kwa lolote (Isaya 65:21:25).

Lakini pamoja na hayo, biblia inarekodi pia watu waovu watakuwepo, ila dhambi haitatawala kwasababu shetani wakati huo atakuwa amefungwa, mtu akiasi kwa namna yoyote ile atauliwa,

Hivyo kwa ujumla ni kuwa utakuwa ni utawala wa amani nyingi sana, ni kipindi ambacho Mungu amewahifadhia watakatifu wake kuwafurahisha na kuwapa raha. Mimi na wewe tusikose hiyo sabato kuu ya Mungu ya utawala huo wa miaka 1000.

kwa urefu wa somo hilo la utawala wa miaka elfu, fungua hii link >>https://wingulamashahidi.org/2019/05/30/utawala-wa-miaka-1000/ 

Sasa mara baada ya utawala huo kupita, biblia inasema tena, shetani atafunguliwa kwa kipindi kifupi sana, kuwajaribifu wale waovu waliokuwa ndani ya dunia hiyo. Watakapo jaribu kuizunguka kambi ya watakatifu, wakati huo huo moto utashuka na kuwaangamiza wote. Kisha watahukumiwa na kutupwa katika lile ziwa la moto

Ufunuo 20:7 “Na hiyo miaka elfu itakapokwisha, Shetani atafunguliwa, atoke kifungoni mwake;

8 naye atatoka kuwadanganya mataifa walio katika pembe nne za nchi, Gogu na Magogu, kuwakusanya kwa vita, ambao hesabu yao ni kama mchanga wa bahari.

9 Wakapanda juu ya upana wa nchi, wakaizingira kambi ya watakatifu, na mji huo uliopendwa. Moto ukashuka kutoka mbinguni, ukawala.

10 Na yule Ibilisi, mwenye kuwadanganya, akatupwa katika ziwa la moto na kiberiti, alimo yule mnyama na yule nabii wa uongo. Nao watateswa mchana na usiku hata milele na milele”.

Baada ya hapo, mpango wote wa ukarabatiji wa ulimwengu utakuwa umeisha, kinachofuata sasa hiyo ni mbingu mpya na nchi mpya, ambayo Mungu aliikusudia tangu zamani wanadamu waishi ndani yake.

Jambo ambalo ndio shabaha yetu kuu sisi watakatifu. Hiyo mbingu mpya na nchi mpya. Kama vile mtume Petro alivyosema katika.

2Petro 3:13 “Lakini, kama ilivyo ahadi yake, mnatazamia mbingu mpya na nchi mpya, ambayo haki yakaa ndani yake.

14 Kwa hiyo, wapenzi, kwa kuwa mnatazamia mambo hayo, fanyeni bidii ili mwonekane katika amani kuwa hamna mawaa wala aibu mbele yake”.

Mpaka hapo utakuwa umeona jinsi Mungu alivyoiumba dunia yake, na kila ilipoharibiwa, baadaye aliiponya kwa sehemu au aliikarabati na kuirudisha kama mwanzo. Lakini hakuwahi kufanya uumbaji mwingine mpya, wa ulimwengu.

Hivyo fuatana nami katika sehemu ya Tatu na ya mwisho, ambayo inaelezea sasa, jinsi hiyo mbingu mpya na nchi mpya itakavyokuja kuwa.

Bofya chini kwa sehemu ya kwanza na ya tatu >>>

MBINGU MPYA NA NCHI MPYA. (Sehemu ya 1)

MBINGU MPYA NA NCHI MPYA. (Sehemu ya 3)

Tafadhali washirikishe na wengine habari hizi njema,

Kwa maombezi/Ratiba za ibada/ Ushauri/ Maswali.
Piga namba hizi: +255693036618 au +255789001312

pia kama utapenda uyapate mafundisho haya kwa njia ya Whatsapp au email basi tutumie ujumbe kwenye namba hizo hizo.

Mada Nyinginezo:

MBINGU MPYA NA NCHI MPYA. (Sehemu ya 1)

YANAYOENDELEA SASA KATIKA MADHABAHU YA MUNGU ROHONI.

NITAFANYA YERUSALEMU KUWA JIWE LA KUWALEMEA .

UTAWALA WA MIAKA 1000.

Rudi nyumbani

DOWNLOAD PDF
WhatsApp

Source URL: https://wingulamashahidi.org/2021/08/27/mbingu-mpya-na-nchi-mpya-sehemu-ya-2/