UKITAKA KUFANIKIWA, FANANA NA MWANAMKE WA SAREPTA

UKITAKA KUFANIKIWA, FANANA NA MWANAMKE WA SAREPTA

Jina kuu la Bwana na Mwokozi wetu Yesu KRISTO libarikiwe, karibu tujifunze biblia.

Sarepta ulikuwa ni mji mdogo uliokuwepo nje kidogo mwa nchi ya Israeli, katika Taifa la Lebanoni.

Katika biblia tunasoma kipindi Nabii Eliya amefunga Mbingu miaka mitatu na nusu kwa Neno la Bwana,  aliongozwa aende mpaka mji huu wa Sarepta ambapo kulikuwepo na Mwanamke ambaye Bwana alikuwa amemwandaa ili amlishe.

Mungu angeweza kumshushia Nabii Eliya mana kutoka mbinguni na akala akashiba, lakini hakufanya hivyo, bali alitumia watu na viumbe kumlisha wakati dunia nzima inapitia njaa. Mara ya kwanza alitumia kunguru (1Wafalme 17:4), na mara ya pili akatumia Mtu (ambaye ndiye huyu mwanamke wa Sarepta).

Sasa huyu mwanamke wa Sarepta alikuwa na tabia ya kipekee ambayo kupitia hiyo tunaweza kuvuna hekima ya mafanikio ya kimwili na kiroho.

Inawezekana mambo yako hayaendi sawa, inawezekana unapitia kipindi kigumu sana cha mbingu kufungwa juu yako, kila mahali unapogusa hapaendi, kila unalojaribu halifanikiwi, kila mahali ni ukame!!

Kama unapitia hii hali, basi usiende kutafuta kuombewa! Bali fanya kama alivyofanya huyu mwanamke wa Sarepta.

Ukifanya kama alivyofanya huyu mwanamke wa Sarepta, basi kipindi ambacho wengine watakuwa wanalia matatizo na dhiki, wewe hutakuwa katika hayo matatizo wala hizo dhiki..

Sasa ni kitu gani alichokifanya huyu mwanamke mpaka kufikia hatua ya yeye kuishi vizuri katikati ya vipindi vya shida na njaa na mauti?

Hebu tusome habari yake kwa ufupi kisha tujifunze tabia aliyokuwa nayo.

1Wafalme 17:7 “Ikawa, baada ya siku kupita, kile kijito kikakatika, kwa sababu mvua haikunyesha katika nchi. 

8 Neno la Bwana likamjia, kusema,

9 Ondoka, uende Sarepta, ulio mji wa Sidoni, ukae huko. Tazama, nimemwagiza mwanamke mjane wa huko akulishe

10 Basi, akaondoka, akaenda Sarepta; hata alipofika langoni pa mji, kumbe! Mwanamke mjane alikuwako akiokota kuni; akamwita, akamwambia, Niletee, nakuomba, maji kidogo chomboni nipate kunywa.

11 Alipokuwa akienda kuleta, akamwita akasema, Niletee, nakuomba, kipande cha mkate mkononi mwako.

12 Naye akasema, Kama Bwana, Mungu wako, aishivyo, sina mkate, ila konzi ya unga katika pipa, na mafuta kidogo katika chupa; nami ninaokota kuni mbili ili niingie nijipikie nafsi yangu na mwanangu, tuule tukafe.

13 Eliya akamwambia, Usiogope; enenda ukafanye kama ulivyosema; lakini unifanyie kwanza mkate mdogo ukaniletee; kisha ujifanyie nafsi yako na mwanao. 

14 Kwa kuwa Bwana, Mungu wa Israeli, asema hivi, Lile pipa la unga halitapunguka, wala ile chupa ya mafuta haitaisha, hata siku ile Bwana atakapoleta mvua juu ya nchi.

15 Basi akaenda, akafanya kama alivyosema Eliya; na yeye mwenyewe, na Eliya, na nyumba yake, wakala siku nyingi. 

16 Lile pipa la unga halikupunguka, wala ile chupa ya mafuta haikuisha, sawasawa na neno la Bwana alilolinena kwa kinywa cha Eliya”.

Umeona tabia ya huyu mwanamke?.. alikubali kutoa chakula chake kipindi ambacho amebakiwa nacho kidogo!!.. kipindi ambacho hajui kesho itakuwaje.. Alikubali kuweka sababu zake kando ilimradi tu aone Neno la Mungu linazidi kusambaa kupitia mtumishi wake,  aliona mtu wa Mungu,au kazi ya Mungu ina thamani mara nyingi zaidi ya kazi zake yeye au uwepo wake yeye na mwanae.  

Hivyo akajitoa sadaka maisha yake.. akijua kuwa hata kama atakufa na njaa yeye na mwanae lakini atakuwa na thawabu kubwa mbinguni, atakuwa hajaifanya kazi ya Mungu isimame… Hicho ndicho kilichomfanya Mungu ayaangalie matatizo yake, na kumfungulia Mbingu wakati wengine bado mbingu zimefungwa.

Na Mungu ni yeye Yule jana, leo na hata milele hajabadilika (Waebrania 13:8)..  Ukitaka Bwana ayaangalie mambo yako, basi wewe weka kando mambo yako na shida zako, na anza kujishughulisha na mambo yake..

Hii ndio shida kubwa inayowakabili wakristo wengi, huwa wanatanguliza matatizo yao mbele za Mungu na huku hawataki kumjali Mungu katika maisha yao.. wanatafuta kuombewa mambo yao yakae sawa, lakini kutafuta kuyaweka sawa mambo ya Mungu hawataki..

Watamwambia Mungu, tazama mwanangu hajala, mwanangu hana ada ya shule, mwanangu yuko hivi yuko vile, mimi sina chakula, mimi sina kazi, mimi sina hiki au kile..(wanakuwa ni watu wa kujijali wao) na hawana habari na mambo ya Mungu au kazi ya Mungu, wakidhani kuwa kwasababu Mungu ni muweza wa mambo yote, hivyo hahitaji kupewa chochote au kufanyiwa chochote.

Ni kweli yeye ni mweza wa yote, na hahitaji kufanyiwa chochote, lakini wakati mwingine anafanya hivyo kutujaribu upendo wetu kwake,.. angeweza kumshushia Eliya Mana kama alivyowashushiwa wana wa Israeli jangwani lakini hakufanya hivyo kwa Eliya, bali alimpeleka Eliya kwa huyu mwanamke, ili aujaribu upendo wake kwake.

Wengi wetu hatujui kuwa Mungu anafurahiwa sana na matoleo yetu kipindi ambacho hatuna kitu zaidi ya kipindi ambacho tuna kila kitu. Utasema hilo tunalithibitisha vipi kimaandiko?… Rejea ile habari ya Yule mwanamke mjane aliyetoa riziki yake yote katika sanduku la hazina…Utaona baada ya kutoa Bwana Yesu anamsifia, na tena anasema katoa zaidi ya wote, kwasababu hao wengine walitoa katika sehemu zilizowazidi…

Marko 12:41  “Naye akaketi kulielekea sanduku la hazina, akatazama jinsi mkutano watiavyo mapesa katika sanduku. Matajiri wengi wakatia mengi.

42  Akaja mwanamke mmoja, mjane, maskini, akatia senti mbili, kiasi cha nusu pesa.

43  Akawaita wanafunzi wake, akawaambia, Amin, nawaambia, Huyu mjane maskini ametia zaidi kuliko wote wanaotia katika sanduku la hazina;

44  maana hao wote walitia baadhi ya mali iliyowazidi; bali huyu katika umaskini wake ametia vyote alivyokuwa navyo, ndiyo riziki yake yote pia”

Kwaufupi huyu mjane, hakubakiwa na kitu, huenda alijua baada ya kutoa vile atakaa siku kadhaa na njaa… lakini akiwa katika hiyo hali, Bwana Yesu alimsifia.. huenda baada ya pale, alishangaa kwa milango ya Baraka iliyofululiza mbele yake.

Na wewe ukitaka Mbingu zifunguke juu yako, usianze kutoa visababu katika kumtolea Mungu, usianze kusema sijalipa kodi, usianze kusema sina chakula, sijalipa ada, sijafanya hiki, sijafanya kile, ngoja nikusanye kidogo nitakapopata nitatoa.. Ni kweli siku ukipata na kutoa basi Bwana atakubariki, hataacha kukubariki!!!… lakini  hujui tarehe wala siku mambo yako yatakapokuwa sawa..

Walikuwepo wanawake wengi sana kipindi cha Eliya wenye matatizo ya chakula kama huyu wa Sarepta, ambao na wenyewe pengine walikuwa wanafunga na kuomba Mungu awape riziki kwasababu ya ukame…lakini Eliya hakutumwa kwao kwasababu hizo hizo, huenda angeenda kwao na kuwaambia wampe yeye kwanza mkate, wangemfukuza kwa mawe, tena wangemtukana…

Wangesema hatuwezi kuona watoto wetu wanakufa njaa halafu tukupe wewe mzee chakula chao, wangetumia hata na maandiko kuthibitisha hilo.. Kwaufupi kila mmoja angeeleza shida zake na sababu zake kwanini asingempa Eliya mkate.. Ndicho Bwana Yesu alichokisema katika Luka 4:25.

Luka 4:25 “Lakini, kwa hakika nawaambia, Palikuwa na wajane wengi katika nchi ya Israeli zamani za Eliya, wakati mbingu zilipofungwa miaka mitatu na miezi sita, njaa kuu ikaingia nchi nzima;

26  wala Eliya hakutumwa kwa mmojawapo, ila kwa mjane mmoja wa Sarepta katika nchi ya Sidoni”.

Na sisi pia tukitaka mbingu zifunguke juu yetu kabla ya wakati wake, hatuna budi kumjali Mungu zaidi ya kujijali sisi, hatuna budi kuyatazama mambo ya Mungu zaidi kuliko mambo yetu. Hii ni moja ya kanuni za Mafanikio.

Bwana Yesu atubariki.

Maran atha.

Tafadhali shea na wengine ujumbe huu;

Pia Kwa maombezi/ Ushauri/ Maswali/ Whatsapp:
Tuandikie katika BOXI la Maoni hapo chini au
Piga namba hizi: +255693036618 au +255789001312

Mada Nyinginezo:

Je Eliya aliandika waraka baada ya kupaa mbinguni?

Kwanini wajane vijana hawakupaswa kuandikwa?

NYAKATI SABA ZA KANISA NA WAJUMBE WAKE.

MWANAMKE, BINTI, MAMA. (Sehemu ya 3)

Nini maana ya kumpenda Bwana kwa moyo,roho, akili na nguvu zetu zote?

Rudi nyumbani

Print this post

About the author

Admin administrator

Subscribe
Notify of
guest
1 Comment
Newest
Oldest Most Voted
Inline Feedbacks
View all comments
Elinuru Ifande
Elinuru Ifande
1 year ago

Asante I sana kwa masomo mazuri mno. Mmenisaidia kunijenga kiroho