MAOMBI YA KUFUNGULIWA KIUCHUMI.

by Admin | 11 November 2021 08:46 pm11

Kabla ya kwenda katika maombi Awali ya yote ni vizuri ukafahamu kuwa mafanikio ya kiuchumi yanaweza kuletwa na vitu vikuu vitatu

  1. Mwanadamu mwenyewe.
  2. Shetani.
  3. Mungu.

Na kila mmoja anayo kanuni yake ya kuyafikia hayo mafanikio.

Kwamfano kwa mwanadamu, ili aweze kujikomboa kiuchumi, kanuni ni moja nayo ni “kuwa na bidii katika kufanya kazi”..haijalishi kazi hiyo itakuwa ni ya kuuza pipi, maadamu unatia bidii ndani yake, utafanikiwa kwasababu  katika bidii hiyo, huko huko ndio unazalika ubunifu  na mikakati, ya kupiga hatua, na kuwekeza,n.k. na mwisho wa siku utafanikiwa, Hata kama hatofikia utajiri ule, lakini mwisho wa siku utajikomboa kiuchumi, haijalishi atafanya hivyo kwa muda gani. Na hapo atakuwa tayari kashajikomboa kiuchumi.

Lakini kanuni za ibilisi ni tofauti na zile za kibinadamu. Pengine kwake si lazima ujishughulishe sana, lakini akakupa mafanikio tu, Kwasababu ndicho alichojaribu kufanya kwa Bwana Yesu, kwa kumwambia  tu amsujudie ndipo atakapompa mali zote.

Mathayo 4:9 “akamwambia, Haya yote nitakupa, ukianguka kunisujudia.”

Unapokwenda kwa waganga watakupa mafanikio, lakini wakiwa na masharti yao kwamba ni lazima ufanye kitu fulani kwa shetani n.k..

Lakini tunaporudi kwa Mungu, napo pia kuna kanuni zake, za kufanikiwa. Ukienda nje ya hizo, na huku unahitaji mafanikio, au kukombolewa kiuchumi usijidanganye, unapoteza muda. Nenda tu kajibidiishe huko kama wanadamu wengine, utafanikiwa pia kwa njia hizo.

Lakini Kanuni za Mungu za kumkomboa mtu kiuchumi  ni zipi?;

Kabla ya kuombewa ni lazima uwe mwana wake. Na mtu anakuwa mwana wake kwa kutubu dhambi zake zote, na kubatizwa, kisha kupokea Roho Mtakatifu. Na baada ya hapo kuanzia huo wakati na kuendelea kuishi maisha yampendezayo Mungu.

Biblia inasema..

Mathayo 6:31 “Msisumbuke, basi, mkisema, Tule nini? Au Tunywe nini? Au Tuvae nini?

32 Kwa maana hayo yote Mataifa huyatafuta; kwa sababu Baba yenu wa mbinguni anajua ya kuwa mnahitaji hayo yote.

33 Bali utafuteni kwanza ufalme wake, na haki yake; na hayo yote mtazidishiwa”.

Unaona? Ukishautafuta kwanza ufalme wake na haki yake, kuanzia huo wakati unakuwa tayari sasa, kushiriki Baraka zote kutoka kwa Mungu, kiwepesi  pale unapomwomba.

Neno la Mungu linasema hivi..

2Wakorintho 8:9 “Maana mmejua neema ya Bwana wetu Yesu Kristo, jinsi alivyokuwa maskini kwa ajili yenu, ingawa alikuwa tajiri, ili kwamba ninyi mpate kuwa matajiri kwa umaskini wake”.

Na pia Yesu mwenyewe alisema..

Mathayo 19:28 “Yesu akawaambia, Amin, nawaambia ya kwamba ninyi mlionifuata mimi, katika ulimwengu mpya, atakapoketi Mwana wa Adamu katika kiti cha utukufu wake, ninyi nanyi mtaketi katika viti kumi na viwili, mkiwahukumu kabila kumi na mbili za Israeli.

29 Na kila mtu aliyeacha nyumba, au ndugu wa kiume au wa kike, au baba, au mama, au watoto, au mashamba, kwa ajili ya jina langu, atapokea mara mia, na kuurithi uzima wa milele.

30 Lakini wengi walio wa kwanza watakuwa wa mwisho, na walio wa mwisho watakuwa wa kwanza”.

Hivyo kabla ya kwenda kukuombea Baraka zako kutoka kwa Mungu.. ni sharti kwanza uwe  tayari leo kumkabidhi Bwana Yesu maisha yako, kwa kumaanisha kabisa. Kama upo tayari basi hapo ulipo tafuta sehemu yenye utulivu, kisha piga magoti, kisha sema sala hii kwa imani, kwa kumaanisha kabisa, na Mungu atakuokoa siku ya leo.

EE MUNGU BABA, NAJA MBELE ZAKO, NIKIWA NINAJITAMBUA KUWA MIMI NI MKOSAJI NA NIMEKUTENDA DHAMBI NYINGI, NA KWAMBA NIMESTAHILI HUKUMU. LAKINI WEWE MUNGU WANGU ULISEMA KATIKA NENO LAKO KUWA WEWE NI MUNGU WA REHEMA UNAYEWAREHEMU  MAELFU ELFU YA WATU WANAOKUPENDA WEWE. NA LEO HII NINAKUJA MBELE ZAKO NAHITAJI MSAMAHA WAKO NA MSAADA WAKO MUNGU WANGU, NINATUBU DHAMBI ZANGU ZOTE KWA KUMAANISHA NA KWA MOYO WANGU WOTE, NINAKIRI KUWA YESU KRISTO NI BWANA, NA YEYE NDIYE MWOKOZI WA HUU ULIMWENGUNI. HIVYO NAOMBA DAMU YA MWANAO TAKATIFU INISAFISHE UOVU WANGU WOTE SASA NIFANYIKE KUWA KIUMBE KIPYA KUANZIA LEO NA HATA MILELE.

ASANTE BWANA YESU KWA KUNIPOKEA NA KUNISAMEHE.

AMEN.

Sasa kwa sala hiyo fupi, amini kuwa Bwana Yesu ameshakusamehe, Na kuanzia sasa unakuwa tayari kushiriki, Baraka zote kutoka kwa Mungu.

Yeye mwenyewe alisema maneno haya;

Kumbukumbu: MLANGO 28

1 Itakuwa utakaposikia sauti ya Bwana, Mungu wako, kwa bidii, kutunza kuyafanya maagizo yake yote nikuagizayo leo, ndipo Bwana, Mungu wako, atakapokutukuza juu ya mataifa yote ya duniani;

2 na baraka hizi zote zitakujilia na kukupata usikiapo sauti ya Bwana, Mungu wako.

3 Utabarikiwa mjini, utabarikiwa na mashambani.

4 Utabarikiwa uzao wa tumbo lako, na uzao wa nchi yako, na uzao wa wanyama wako wa mifugo, maongeo ya ng’ombe wako, na wadogo wa kondoo zako.

5 Litabarikiwa kapu lako, na chombo chako cha kukandia unga.

6 Utabarikiwa uingiapo, utabarikiwa na utokapo.

7 Bwana atawafanya adui zako wainukao juu yako kupigwa mbele yako; watakutokea kwa njia moja, lakini watakimbia mbele yako kwa njia saba.

8 Bwana ataiamuru baraka ije juu yako katika ghala zako, na mambo yote utakayotia mkono wako; naye atakubarikia katika nchi akupayo Bwana, Mungu wako.

9 Bwana atakuweka uwe taifa takatifu kwake, kama alivyokuapia; utakaposhika maagizo ya Bwana, Mungu wako, na kutembea katika njia zake.

10 Na mataifa yote ya duniani watakuona umeitwa kwa jina la Bwana, nao watakuwa na hofu kwako.

11 Bwana atakufanya uwe na wingi wa uheri, katika uzao wa tumbo lako, na uzao wa wanyama wako wa mifugo, na uzao wa nchi yako, katika nchi Bwana aliyowaapia baba zako kwamba atakupa.

12 Atakufunulia Bwana hazina yake nzuri, nayo ni mbingu, kwa kutoa mvua ya nchi yako kwa wakati wake, na kwa kubarikia kazi yote ya mkono wako; nawe utakopesha mataifa mengi, wala hutakopa wewe.

13 Bwana atakufanya kuwa kichwa, wala si mkia; nawe utakuwa juu tu, wala huwi chini; utakapoyasikiza maagizo ya Bwana, Mungu wako, nikuagizayo hivi leo, kuyaangalia na kufanya;

14 msipokengeuka katika maneno niwaamuruyo leo kwa lo lote, kwenda mkono wa kuume wala wa kushoto, kwa kuifuata miungu mingine na kuitumikia.

Baraka hizo zote, zitakufuata endapo utadumu tu katika WOKOVU.

Basi sasa, nitakuombea, ili milango hii ifunguke, katika maisha yako. Hapo ulipo Piga tena magoti, niombe kwa ajili yako. Fuatisha kwa sauti sala hii;

Baba Mwenyezi, Mungu wa milele, ahsante kwa kutupa zawadi ya kutuletea mkombozi duniani, Bwana wetu Yesu Kristo. Asante kwa kuwa alikuja kutukomboa kutoka katika dhambi zetu na laana zetu. Lakini hakuishia hapo tu, bali alitukomboa, mpaka na UCHUMI wetu.

Nami leo hii nimempokea na kumkiri kwa kumaanisha kabisa kumfuata tangu sasa hadi milele. Naomba Mungu wako zile Baraka zote ulizoziahidi katika Kumbukumbu la Torati 28:1-14, zinijilie juu yangu. Nami nikawe Baraka kwa jamii na kwa kanisa lako. Kuanzia sasa ikiwa kuna kazi zozote za ibilisi zilizotangulia nyuma yangu kunizuilia Baraka zangu, ninazikataa kwa jina la Yesu Kristo. Naiita Damu ya Yesu ikasafishe kapu langu, na mfuko wangu.

Asante Mungu wangu kwa kunikomboa.

Amen.

Basi, ikiwa umeyafuatilisha maombi hayo, ujue kuanzia sasa, Mungu atatembea na wewe katika uchumi wako, kwa kile unachokifanya, tenda mapenzi ya Mungu, utaona akikupigania. Lakini kumbuka Kama tulivyotangulia kusema, inahitaji Kutembea na Mungu ili akukamilishie ahadi hizo, sio tu kukiri kwa mdogo, unakwenda kuendelea na mambo yako..nikuambie ukweli tu, inahitaji maisha.

Mungu akubariki sana.

Ikiwa utahitaji msaada zaidi wa kumjua Mungu, au ubatizo, au unaswali lolote kuhusu biblia,  basi wasiliana nasi kwa namba zetu hizi Simu/Whatsapp: +255693036618 /  +255789001312

Mada Nyinginezo:

REKEBISHA YAFUATAYO ILI UCHUMI WAKO UKAE SAWA.

TWEKA MPAKA VILINDINI.

NI YESU YUPI UMEMPOKEA?, NI ROHO IPI UMEIPOKEA? NA INJILI IPI UMEIPOKEA?

HUTATAMBUA LOLOTE, SIKU YA UNYAKUO IKIFIKA.

Rudi nyumbani

DOWNLOAD PDF
WhatsApp

Source URL: https://wingulamashahidi.org/2021/11/11/maombi-ya-kufunguliwa-kiuchumi/