HEKIMA NI NINI? NA UFAHAMU UNAPATIKANA WAPI?

HEKIMA NI NINI? NA UFAHAMU UNAPATIKANA WAPI?


Kitabu cha Ayubu sura ya 28, kinaeleza jinsi HEKIMA ilivyojificha mbali sana kiasi kwamba mwanadamu pamoja na ujuzi wake mwingi na maarifa yake mengi hajaipata, licha ya kwamba amefanikiwa kuchimba mahandaki makubwa ili kutafuta madini ndani yake lakini pia hajaipata, licha ya kwamba anayo teknolojia kubwa ya kuwa na vyombo maalumu vya kumfanya kutua mwezini, lakini alipofika na huko hakuikuta vile vile, biblia inasema wanyama nao hawajui inapatikana wapi, kadhalika na vitu vya asili kama bahari na milima havitambui ilipo,

AYUBU sura ya 28

Mstari wa 1-15

“1 Hakika kuna shimo wachimbako fedha, Na mahali wapatapo dhahabu waisafishayo.

2 Chuma hufukuliwa katika ardhi, Na shaba huyeyushwa katika mawe.

3 Binadamu hukomesha giza; Huyatafuta-tafuta hata mpaka ulio mbali, Mawe ya giza kuu, giza tupu.

4 Hufukua shimo mbali na makao ya watu; Husahauliwa na nyayo zipitazo; Huning’inia mbali na watu, huyumba-yumba huko na huko.

5 Katika ardhi ndimo kitokeamo chakula; Na chini yake hupinduliwa kama kwa moto. 

6 Mawe yake ni mahali zipatikanapo yakuti; Nayo ina mchanga wa dhahabu.

7 Njia ile hapana ndege mkali aijuaye, Wala jicho la tai halijaiona;

8 Wanyama wakali wajivunao hawajaikanyaga, Wala simba mkali hajaipita.

9 Huunyoshea mwamba wa gumegume mkono wake; Huipindua milima hata misingi yake.

10 Hukata mifereji kati ya majabali; Na jicho lake huona kila kito cha thamani

11 Hufunga vijito visichuruzike; Na kitu kilichostirika hukifunua.

12 BALI HEKIMA ITAPATIKANA WAPI? NA MAHALI PA UFAHAMU NI WAPI?

13 MWANADAMU HAJUI THAMANI YAKE, WALA HAIONEKANI KATIKA NCHI YA WALIO.

14 Vilindi vyasema, Haimo ndani yangu; Na bahari yasema, Haiko kwangu.

15 HAIPATIKANI KWA DHAHABU, WALA FEDHA HAITAPIMWA IWE THAMANI YAKE.”

BASI HEKIMA YATOKA WAPI? NA MAHALI PA UFAHAMU NI WAPI?.  21 Kwa kuwa imefichwa mbali na macho ya wote walio hai, Na kusitirika na ndege wa angani.

Biblia inaendelea kueleza kama Hekima ingekuwa inapatikana kwa thamani ya dhahabu au fedha basi ingeshapatikana na watu siku nyingi, au ingekuwa inapatikana kwenye vilindi au baharini ingekuwa ni heri, lakini huko kote mwanadamu ameshafika na hakuikuta. Lakini je! Inapatikana wapi?.

Biblia inaendelea…

“16 Haiwezi kutiwa thamani kwa dhahabu ya Ofiri, Wala kwa shohamu ya thamani nyingi, wala kwa yakuti ya samawi.

17 Dhahabu na vioo haviwezi kulinganishwa nayo; Wala kubadili kwake hakutakuwa kwa vyombo vya dhahabu safi.

18 Havitatajwa fedhaluka wala bilauri; Naam, kima cha hekima chapita marijani.

19 Yakuti ya rangi ya manjano ya Kushi haitasawazishwa nayo, Wala haitatiwa kima kwa dhahabu safi.

20 BASI HEKIMA YATOKA WAPI? NA MAHALI PA UFAHAMU NI WAPI?.

21 Kwa kuwa imefichwa mbali na macho ya wote walio hai, Na kusitirika na ndege wa angani.

22 Uharibifu na Mauti husema, Tumesikia habari zake kwa masikio yetu.

23 Mungu ndiye aijuaye njia yake, Naye anajua mahali pake.”

Viumbe vyote vya asili na visivyo vya asili na vyenyewe pia vinasema havijui makao yake, Ni Mungu pekee ndiye anayejua makao yake. Na tunasoma baada ya wote kushindwa kufikia makao ya HEKIMA na UFAHAMU, Ndipo Mungu naye akaazimu kuingilia kati na kuchunguza makao yao yako wapi?.. Naye pia kama mwanadamu aliingia katika uchunguzi wa kina na utafiti wa hali ya juu, akapanda milimani, akashuka vilindini, akashuka zaidi mpaka kuzimu, akarudi kwenye mbingu, akapitia sayari zote akazunguka kote kote kila mahali, akaingia mpaka kwenye mioyo ya wanadamu kuitafuta hekima, hakuna mahali ambapo hakufika. Ndipo mwishoni akaipata, na alipoipata akaihakiki na kuithibitisha, na ndipo akaja KUWAAMBIA WANADAMU.

Mstari wa 24-28 inaendelea kusema..

“24 Maana anatazama hata miisho ya nchi, Na kuona chini ya mbingu nzima.

25 Apate kuufanyia upepo uzito wake; Naam, anayapima maji kwa kipimo.

26 Hapo alipoiwekea mvua amri, Na njia kwa umeme wa radi.

27 Ndipo alipoiona na kuitangaza; Aliithibitisha, naam, na kuichunguza.

28 Kisha akamwambia mwanadamu, TAZAMA, KUMCHA BWANA NDIYO HEKIMA, NA KUJITENGA NA UOVU NDIO UFAHAMU.”

Maneno hayo ndiyo aliyomalizia Bwana, baada ya utafiti na uchunguzi wa hali ya juu, Na sisi tunajua hakuna mwanadamu mwenye Akili zaidi ya Mungu, Utafiti wa Mungu ni bora mara nyingi zaidi kuliko utafiti wa wanasayansi au wanajimu, na wanafalsafa. Kama wanasema HEKIMA ni kusoma sana, au kuwa na akili nyingi za kimasomo au ujasiriamali, au kuwa tajiri sana, kama wao wanasema hekima ni kuwa maarufu, kama wao wanasema ufahamu ni kuwa na ujuzi wa kufanya jambo fulani, lakini sisi tunajua Bwana katuonyesha HEKIMA ni nini, na ufahamu unapatikana wapi?.. NI KUMCHA YEYE, NA KUEPUKANA NA UOVU. Hilo tu.! Tukizingatia hayo mbele za Mungu tutakuwa ni watu wenye hekima sana na Ufahamu mkubwa.

Sulemani ingawa alikuwa ni mtu mwenye maarifa mengi na ufahari mkubwa ambao hakuna mtu aliyekuwa mfano wake, tangu wakati ule hata sasa, Ni mtu aliyekuwa na elimu pamoja na ujuzi wa viumbe vyote, ikiwepo miti, samaki, wanyama, alikuwa na ujuzi wa hali ya juu kiasi cha kutunga nyimbo na mashairi kwa hekima nyingi sana, alikuwa na uwezo wa kutenganisha hukumu ambapo vitu kama hivyo vilihitaji watu wenye akili nyingi kama mahakimu. Ilifika wakati yeye mwenyewe alikiri kuwa hakukosa lolote, wala hakujinyima nafsi yake kwa chochote. Lakini pamoja ya kwamba aliipata hekima yote ya kidunia, aliisahau HEKIMA MOJA YA MUNGU.

Kwa Kupuuzia amri za Mungu, na kuanza kwenda kuoa wake wageni, na kuabudu miungu migeni, akalitangua lile NENO walilopewa wafalme kwa amri ya Musa kwamba mtu yeyote atakayekuja kuwa mfalme kati yao, asijiongezee wake, wala mali kupita kiasi, wala asiabudu miungu mingine, zaidi ya yote anapaswa aandike amri za Mungu katika chuo ajifunze huko siku zote za maisha yake namna ya kumcha Mungu katika ufalme wake.(Kumbukumbu 17:14-20). Lakini yeye hakufanya hivyo akakaidi. 

Na alipogundua makosa yake kuwa aliiacha hekima hasaa inayopatikana katika kumcha Mungu, akaishia kusema UBATILI MTUPU, KILA KITU NI UBATILI.!

Sulemani alisema katika..

 Mhubiri 2: 10 “Wala sikuyanyima macho yangu cho chote yalichokitamani; wala sikuuzuia moyo wangu katika furaha yo yote; maana moyo wangu ulifurahi kwa sababu ya kazi yangu yote, na hii ilikuwa sehemu yangu katika kazi yangu yote.

11 Kisha nikaziangalia kazi zote zilizofanywa kwa mikono yangu, na taabu yote niliyotaabika katika kuzitenda; na tazama, YOTE NI UBATILI na kujilisha upepo, wala faida hakuna chini ya jua.”

Na mwisho wa siku Sulemani alimalizia na kusema….”

Mhubiri 12:13-14

“13 HII NDIYO JUMLA YA MANENO; yote yamekwisha sikiwa; MCHE MUNGU, NAWE UZISHIKE AMRI ZAKE, MAANA KWA JUMLA NDIYO IMPASAYO MTU.

14 Kwa maana Mungu ataleta hukumuni kila kazi, pamoja na kila neno la siri, likiwa jema au likiwa baya.”

Hivyo ndugu, kweli zipo hekima nyingi duniani na sio kwamba ni mbaya ni nzuri na nyingine zinahitajika sana katika jamii zetu lakini usisahau, Mungu mbele zake HEKIMA NI MOJA TU!. Anayoitambua yeye, nayo ni KUMCHA BWANA , NA KUEPUKANA NA UOVU. Ni heri ukakosa hizo nyingine lakini usiikose hiyo. Ichukie dhambi mpe Bwana maisha yako, mche yeye, Elimu yako, ujuzi wako, mali zako ni vizuri kuwa nazo lakini zisije zikakufikisha mahali ukasema ni ubatili mtupu kama alivyofanya Sulemani, kwa jambo moja tu, ya kupuuzia amri za Mungu sasa. Kwasababu Bwana alishasema mwenyewe..Hekima ya ulimwengu huu ni upuuzi mbele zake (1Wakoritho 3:19). Hivyo kuwa makini unavyoenenda katika ulimwengu huu. Kumbuka YESU KRISTO ndiye HEKIMA YA MUNGU.(1wakoritho 2:6-9)

Mungu akubariki.

Pia unaweza ukapata mafundisho haya Kwa njia ya Whatsapp yako, jiunge na channel yetu Kwa kubofya hapa >> WHATSAPP


Mada Nyinginezo:

MUNGU AKIKUPITA LEO, HAIMAANISHI KUWA HAJAKUCHAGUA.

HUDUMA YA (ELIFAZI, BILDADI, NA SOFARI).

CHUKIZO LA UHARIBIFU

TOA SADAKA ISIYO NA KASORO KWA BWANA.

https://wingulamashahidi.org/2020/01/25/kwanini-mungu-alimtumia-musa-kwa-viwango-vile/


Rudi Nyumbani

Print this post

About the author

Admin administrator

Subscribe
Notify of
guest
0 Comments
Inline Feedbacks
View all comments