LULU YA THAMANI.

by Admin | 1 April 2019 08:46 pm04

Shalom, Mtu wa Mungu karibu tujifunze Neno la Mungu, ambapo leo kwa Neema za Bwana tutajifunza kwa sehemu juu ya ufunuo uliopo katika ufalme wa Mbinguni. Biblia inasema katika..

Mathayo 13.45 “Tena ufalme wa mbinguni umefanana na mfanya biashara, mwenye kutafuta LULU NZURI;

46 naye alipoona lulu moja ya thamani kubwa, alikwenda akauza alivyo navyo vyote, akainunua”.

Mfano huu ulitolewa na Bwana Yesu Kristo, alipokuwa anawafundisha makutano maana ya ufalme wa Mbinguni..Kama ukichunguza kwa makini utagundua kuwa Bwana Yesu alikuwa anapenda kutumia mifano ya kidunia hii kuifananisha na ufalme wa mbinguni Ikiwa na maana kuwa mambo mengi au shughuli nyingi za ulimwengu huu zimebeba kwa sehemu Fulani siri za ufalme wa Mbinguni ndani yake..Katika shughuli za haki au za uovu ndani yake kuna hekima za Kimungu..ndio maana utaona mahali pengine Bwana anatoa mfano wa Mpanzi aliyekwenda kupanda mbegu zake shambani…na mahali pengine Bwana Yesu anatoa mfano wa mwizi (kwamba atakuja kama mwivi usiku wa manane)…ikiwa na maana kuwa hata katika WIZI kuna hekima ya kiMungu ndani yake…ingawa kwa kusema hivyo sio kwamba anahalalisha wizi, sehemu nyingine anatoa mfano wa yule kadhi dhalimu..ikiwa na maana kuwa hata katika udhalimu pia ipo hekima ya Mungu ndani yake..nk

Lakini leo tutajifunza juu ya huu mfano wa Mfanyabiashara aliyekuwa akitafuta lulu ya thamani na alipoiona alikwenda kuuza kila alicho nacho ili kuinunua.

Sasa LULU ni nini?.

Lulu ni madini fulani ya thamani sana..ambayo hayachimbwi kutoka ardhini kama madini mengine yachimbwavyo bali asili yake ni baharini…Madini haya yanatengenezwa ndani ya mwili wa samaki, wanaojulikana kama “Oyster”…na samaki hawa sio kama samaki wa kawaida tunaowajua wenye mapezi na mikia na macho, hapana bali jamii ya hawa samaki hawana mapezi wala macho, wala mikia na wala hawaogelei ogelei kama viumbe wengine wa majini, bali wapo kama kokwa la embe hivi lililokauka na wanakaa katika sakafu ya bahari chini kabisa, hawaruki ruki huko na huko, wakati wote wanakuwa wametulia tu chini ya habari, …Hivyo ni ngumu kuwaona kwani unaweza ukapita ukadhani ni mawe tu yamelala kumbe ni samaki.

Sasa hayo madini yanayoitwa LULU yanaanza kujitengeneza kama chembe ndogo ya mchanga, tumboni mwa hao samaki, na kwa kadiri muda unavyozidi kuendelea..yanaongezeka ukubwa kidogo kidogo na hata kufikia ukubwa wa kama hizi gololi wanazochezea watoto wadogo..kwa jinsi inavyokuwa kubwa ndivyo thamani yake inavyozidi kuongezeka. Watu wanaokwenda kuyatafuta madini hayo baharini wanatumia gharama nyingi na muda mwingi na hatari nyingi..kwasababu inawagharimu waende mbali kwenye vilindi vya maji na wazame chini mpaka kwenye sakafu ya bahari na kuanza kuangalia angali huku na huko kama mtoto anayetafuta hela aliyoiangusha njiani..inawaachua hata siku nzima kukaa chini maji, hana hiyo inaweza kwenda kwa miezi kadhaa, Na kwa tabu nyingi wakibahatika kuwapata hao samaki wanawachukua na kwenda kuwapasua na kutoa hayo madini..

Sasa kutokana na madini hayo kuwa adimu na kuwa mazuri kupita kiasi, thamani yake nayo inakuwa kubwa zaidi…lulu moja ya ukubwa wa juu, thamani yake inaweza ikafika mpaka sh.milioni 250 za kitanzania. Hiyo ni moja tu!

Sasa tukirudi kwenye huo mfano Bwana Yesu alioutoa unaosema…ufalme wa Mungu umefanana na mfanya biashara aliyeona LULU ya thamani akaenda kuuza kila kitu alicho nacho ili kuinunua, alikuwa na maana kuwa, huyu mfanya biashara, alikwenda mahali akakuta LULU inauzwa kwa thamani ya chini…tuchukue mfano hiyo lulu yenye thamani ya sh.milioni 250 akaikuta inauzwa sh.milioni 100. Na alipoiona kwasababu yeye anaijua thamani yake halisi, na hana hela ya kutosha akatumia akili ya kwenda kuuza vyote alivyo navyo kama ni mashamba, kama ni nyumba kama ni mifugo yake, vyovyote vile…ili kwamba apate hela ya kutosha, akainunue hiyo lulu inayouzwa kwa bei ya chini..

Sasa kumbuka Bwana Yesu anamwita huyu mtu mfanyabiasha, na unajua mtu akiwa mfanyabiashara yupo kimaslahi zaidi, uyo kwaajili ya kupata faida.

Hivyo yeye kuuza kila kitu ili akainunue ni alijua siku atakapokwenda kuiuza kwa thamani yake halisi atapata faida kubwa na hivyo atakwenda tena kununua mashamba mazuri kuliko hata yale aliyouza, atakwenda kununua tena mifugo mingine mingi, atakwenda kujenga tena nyuma yenye thamani kama ile ya kwanza na bado atabakiwa na faida yake juu..

Kwahiyo huyu mfanyabiashara hakuwa mjinga, kwamba auze kila kitu halafu akae na lulu ndani kama urembo…hapana kumbuka yeye ni mfanya-biashara, aliinunua ili akaiuze.

Ndugu yangu Bwana Yesu Kristo ndio hiyo LULU YA THAMANI, Anapatikana BURE lakini HAPATIKANI KIRAHISI. Kama tu Lulu Baharini inavyopatikana bure lakini si kirahisi, kadhalika na Bwana Yesu, ndio maana alisema katika Luka 14.33 “Basi, kadhalika kila mmoja wenu asiyeacha vyote alivyo navyo, HAWEZI KUWA MWANAFUNZI WANGU”.

Unapousikia ujumbe huu, mimi ninayekuhubiria ni kama mfanya biashara ninayekuletea YESU KRISTO kwa bei ya chini..na wewe unayesikia ni kama mfanya-biashara mwenye kutafuta lulu hii ya thamani, hivyo unachopaswa kufanya ni kwenda kuuza kila ulicho nacho..ili upate pesa ya kutosha kumnunua huyu Yesu Kristo moyoni mwako, na kisha nenda kamwuze nawe kwa wengine ndipo utaona faida. Na gharama za kumnunua ndio hizo…”kuuza kila kitu cha ulimwengu huu unachokishikilia sasa kinachokufanya uwe mbali na Mungu wako” kuacha kila kitu kiovu, kukubali kuacha kila aina ya dhambi maishani mwako, kukubali kuingia gharama ya kuacha anasa, na mambo ya kiulimwengu, kukubali kuacha uasherati na uzinzi, kukubali kuacha utumiaji mbaya wa mitandao, kuchat mambo yasiyofaa mitandaoni, kukubali kuacha ulevi, na utazamaji wa pornography, kukubali kuacha kuvaa nguo fupi na zinazobana na suruali na vimini, kukubali kuacha kampani mbaya za watu wenye mizaha, na matusi, kukusudia kuuza muda wako wote kwa Mungu, kukusudia kumgeukia Mungu kwa moyo wako wote, na kwa akili zako zote, na kubeba msalaba wako na kuelekea Kalvari. Ndugu yangu wa thamani mtu asikudanganye kuwa utampa Bwana Yesu nje ya njia hiyo…yeye mwenyewe alisema katika..

Luka 14.25 “Makutano mengi walipokuwa wakifuatana naye, aligeuka, akawaambia,

26 Kama mtu akija kwangu naye hamchukii baba yake, na mama yake, na mke wake, na wanawe, na ndugu zake waume na wake; naam, na hata nafsi yake mwenyewe, hawezi kuwa mwanafunzi wangu.

27 Mtu ye yote asiyeuchukua msalaba wake na kuja nyuma yangu, hawezi kuwa mwanafunzi wangu”

Maneno haya ni magumu, lakini ndio ukweli wa mambo…ukitaka kwenda kununua lulu ya thamani Yule anayekuuzia atakwambia usipofikia kiwango Fulani cha fedha, huwezi kuipata..sio kwamba anataka kukuumiza hapana bali huo ndio ukweli wa mambo kwamba kitu unachokitafuta ni cha thamani ya juu, hivyo anaweza kukushauri uende ukauze hata shamba au nyumba ili upate fedha ya kutosha ya kuinunua..lakini kama usipotaka basi ni sawa uamuzi ni wakwako.

Hivyo ndugu unayesoma ujumbe huu ambaye hujampa Bwana Yesu maisha yako, au upo mguu mmoja nje, mguu mmoja ndani na unataka kuwa na maisha mazuri ya hapa duniani na huko mbinguni, unataka kupata faida hapa duniani na mbinguni, basi fahamu kuwa NJIA YA MSALABA haikwepeki. Ni lazima ujikane nafsi tu! Ni lazima uache KILA KITU CHA ULIMWENGU HUU, Ni lazima umgeuke yeye kikweli kweli, hakuna njia ya mkato..wengi wanapenda kufarijiwa kwamba kwa Bwana Yesu ni mteremko tu! Usidanganyike..Kristo ni LULU YA THAMANI. Kama alitoka mbinguni mahali penye utukufu atakuwaje wa bei rahisi huyo??..hebu chukua muda mtafakari huyu MFALME WA WAFALME!!.

Kwahiyo Bwana Yesu anatupenda na ataka tupate faida ndio maana, alitupa mfano huo wa mfanyabiashara, anataka na sisi tuwe wafanya biashara werevu tunaotafuta faida na si hasara, anataka tuingie gharama kupoteza vitu vidogo vya muda vya kitambo visivyo na maana ili tupate vitu vikubwa vya muda mrefu vyenye faida..huoni kama hiyo ni fursa nzuri kwetu??..Ndio ni fursa nzuri sana na ya faraja…ndio maana wanafunzi walipopata mashaka ya kupoteza mambo yao yote kwa ajili ya Kristo, yeye mwenyewe aliwapa faraja akawaambia watapata mara 100 hapa duniani na katika ulimwengu ujao uzima wa milele.. Tunayasoma hayo katika…

Marko 10:28 “Petro akaanza kumwambia, Tazama, sisi tumeacha vyote tukakufuata wewe.

29 Yesu akasema, Amin, nawaambieni, Hakuna mtu aliyeacha nyumba, au ndugu waume, au ndugu wake, au mama, au baba, au watoto, au mashamba, kwa ajili yangu, na kwa ajili ya Injili,

30 ila atapewa mara mia sasa wakati huu, nyumba, na ndugu waume, na ndugu wake, na mama, na watoto, na mashamba, pamoja na udhia; NA KATIKA ULIMWENGU UJAO UZIMA WA MILELE”.

Hivyo Kama hujampa Bwana Yesu maisha yako, ni wakati wako sasa wa kufanya hivyo, unachopaswa kufanya ni kutubu kwa kumaanisha na kudhamiria kuziacha dhambi zako zote, na kumaanisha kutokuzifanya tena, (UNAZIACHA KABISA) Kama ulikuwa mlevi, unaacha ulevi, kama ulikuwa unatanga tanga kwa uasherati, unauacha uasherati, kama ulikuwa unavaa vibaya unaacha, na kisha baada ya kufanya hivyo nenda katafute ubatizo sahihi popote pale kwa ajili ya ondoleo la dhambi zako, kulingana na matendo 2:38 na ubatizo sahihi ni wa kuzamishwa katika maji mengi na kwa jina la YESU KRISTO, baada ya kufanya hivyo Bwana mwenyewe atakupa kipawa cha Roho wake Mtakatifu atakayekusaidia kushinda dhambi na kukuongoza katika kuijua kweli yote ya Biblia.Na hapo utakuwa umezaliwa mara ya pili.

Bwana akubariki sana.

Tafadhali “share” ujumbe huu na wengine na Bwana akubariki. Pia unaweza ukapata mafundisho haya Kwa njia ya Whatsapp yako, jiunge na channel yetu Kwa kubofya hapa >> WHATSAPP


Mada Zinazoendana:

BEI YA UFALME WA MBINGUNI:

UFALME WA MUNGU HAUPATIKANI KIRAHISI

JIKANE NAFSI MTEULE WA MUNGU

SHETANI ANATOLEA WAPI FEDHA, ANGALI TUNAJUA FEDHA NA DHAHABU NI MALI YA BWANA?


Rudi Nyumbani

DOWNLOAD PDF
WhatsApp

Source URL: https://wingulamashahidi.org/2019/04/01/ulu-ya-thamani/