LIPO LA KUJIFUNZA KWA WALE MASHUJAA 37 WA DAUDI.

by Admin | 27 November 2020 08:46 pm11

Kama vile Daudi alivyokuwa shujaa, vivyo hivyo yeye naye alikuwa na mashujaa wake wengine 37 waliokuwa chini yake wakimzunguka wakati wote,walipokuwa vitani kushindana na maadui zao .

Kwa ufupi mashujaa hao waligawanyika katika makundi makuu matatu (3), Kundi la kwanza lilikuwa na mashujaa watatu wa juu, kundi la pili lilikuwa na mashujaa wawili, na kundi la tatu lilikuwa na mashujaa wengine thelathini na mbili.

Hilo kundi la kwanza la juu lenye mashujaa watatu,.mtu wa kwanza aliitwa Yashobeamu Mhakmoni, mwingine ni Eleazari na wa mwisho ni Shama.. Hawa walikuwa mashujaa kweli kweli, na kundi la chini yake kidogo alikuwepo mtu mmoja aliyeitwa Abishai na mwingine ni Benaya, hawa nao walikuwa ni mashujaa sana, halafu lile kundi la mwisho, ndio alikuwepo Uria Mhiti, na wengine, yule ambaye Daudi alimtamani mke wake, hivyo akamweka kwenye vita vikali ili auwe kisha amchukue mke wake.. Huyu alikuwa mmojawapo wa wale wengine..

Sasa embu tuwatazame baadhi ya matendo ya mashujaa hawa kwa ufupi mambo waliyoyafanya, kisha mwishoni tutapata somo la kujifunza..

1) Yashobeamu Mhakmoni:

Huyu ndio Yule shujaa wa juu zaidi ya wote, katika vita alifanikiwa kuwaua wanajeshi 800 kwa mkuki wake mmoja, Jaribu kutengeneza picha mtu mmoja anaua watu 800, huyo ni shujaa kweli kweli mfano wa Samsoni,(2Samweli 23:8)

2) Eleazari, mwana wa Dodai.

Huyu naye alifanya mambo ya kustaajabisha, walipokuwa wamekusanyika ili kupigana na wafilisti kule kondeni, Israeli wote wakakimbia akabaki yeye peke yake na Daudi tu, lakini alinyanyuka na kuwapiga wafilisti, wengi kiasi kwamba hadi mkono wake ukachoka kuua, hata alipojaribu kuuachia upanga mkono wake bado umeshikamana na upanga, tu, (1Nyakati 11:12)

2Samweli 23:9 Na baada yake kulikuwa na Eleazari, mwana wa Dodai, Mwahohi, mmojawapo wa wale mashujaa watatu waliokuwa pamoja na Daudi; walipowatukana Wafilisti waliokuwa wamekusanyika huko ili kupigana, na watu wa Israeli walikuwa wamekwenda zao;

10 huyo aliinuka, akawapiga Wafilisti hata mkono wake ukachoka, na mkono wake ukaambatana na upanga; naye Bwana akafanya wokovu mkuu siku ile; nao watu wakarudi nyuma yake ili kuteka nyara tu.

3) Shama, mwana wa Agee.

Huyu naye alikuwa kwenye mashamba ya midengu pamoja na waisraeli wengine, lakini wafilisti walipotokea wakakimbia, akabaki yeye tu peke yake kondeni, akapigana na wafilisti wengi sana akawaua yeye peke yake, hivyo akafanikiwa kulilinda lile shamba la midengu lisichukuliwe na wafilisti.(2Samweli 23:11-12)

  1. Mwingine aliitwa Abishai, nduguye Yoabu,

Aliwaua kwa wakati mmoja watu 300 kwa mkuki wake,(2Samweli 23:18)

II. Benaya, mwana wa Yehoyada:

Aliwaua majitu mawili wa Kimoabu, pia alimuua simba katikati ya pango, vilevile alimuua Mmisri ambaye alikuwa mrefu sana mfano wa Goliathi, kwa kutumia silaha ya adui yake.

2Samweli 23:20…..”aliwaua simba wakali wawili wa Moabu, pia akashuka akamwua simba katikati ya shimo wakati wa theruji.

21 huyo naye akamwua Mmisri, mtu mrefu; naye huyo Mmisri alikuwa na mkuki mkononi; lakini yeye alimshukia na gongo, akamnyakulia Mmisri mkuki mkononi mwake, akamwua kwa mkuki wake mwenyewe”.

III. Mwingine ni Elhanani ambaye alimwangusha Goliathi, mfano wa yule aliyeangushwa na Daudi.

2Samweli 21:19 “Kulikuwa na vita tena na Wafilisti huko Gobu; na Elhanani, mwana wa Yairi, Mbethlehemi, alimwua Goliathi, Mgiti, ambaye mti wa mkuki wake ulikuwa kama mti wa mfumaji.

20 Kulikuwa na vita tena huko Gathi; ambako kulikuwa na mtu mrefu sana, mwenye vidole sita katika kila mkono, na vidole sita katika kila mguu, jumla yake ishirini na vinne; yeye naye alizaliwa kwa Mrefai.

21 Naye huyo alipowatukana Israeli, ndipo Yonathani, mwana wa Shama, nduguye Daudi, akamwua.

22 Hao wanne walizaliwa kwake huyo Mrefai wa Gathi; wakaanguka kwa mkono wa Daudi, na kwa mikono ya watumishi wake.

IV. Na mashujaa wengine ambao walifanya matendo ya kishujaa unaweza kuwasoma katika..2Samweli 23:14-17..

Lakini tunavyousoma ushujaa wao watu hawa, tunaweza kujiuliza Daudi aliwatolea wapi? Je aliwaiba katikati ya jeshi la Sauli?, au alienda kuwatafuta miongoni mwa watu waliokuwa na nguvu sana Israeli? Jibu ni la!

Mashujaa hawa 37, Daudi aliokuwa nao, hakuwatoa katikati ya kambi za kivita, bali walikuwa ni watu wa kawaida sana wasiokuwa na uelekeo wowote wa ki maisha, watu hohe-hahe tu, watu waliokuwa katika umaskini, wenye dhiki nyingi, wenye madeni, watu dhaifu, watu wasio na raha moyoni, ndio waliokusanyika wakawa pamoja na Daudi, na kati ya hao ndio likanyanyuka wimbi kubwa la mashujaa namna ile ambao waliogopeka na majeshi makubwa yaliyokuwepo wakati ule.

1Samweli 22:1 “Basi Daudi akaondoka huko, akakimbilia pango la Adulamu; na ndugu zake na watu wote wa mbari ya baba yake waliposikia habari hiyo, wakamwendea huko.

2 Na kila mtu aliyekuwa katika hali ya dhiki, na kila mtu aliyekuwa na deni, na watu wote wenye uchungu mioyoni mwao, wakakusanyika kwake; naye akawa jemadari wao; nao waliokuwa pamoja naye walipata kama watu mia nne”.

Sasa Daudi ni mfano wa Kristo, hata sasa Bwana anao mashujaa wake wa Injili, na bado anaendelea kuwatafuta, lakini maandiko yanatuambia mashujaa hao hawatafuti katikati ya watu wenye vyeo, watu matajiri, watu wenye ujuzi mwingi, badala yake anawatafuta katikati ya watu wasiokuwa na uelekeo wowote, watu wa kawaida sana…

1Wakoritho 1:26 “Maana, ndugu zangu, angalieni mwito wenu, ya kwamba si wengi wenye hekima ya mwilini, si wengi wenye nguvu, si wengi wenye cheo walioitwa;

27 bali Mungu aliyachagua mambo mapumbavu ya dunia awaaibishe wenye hekima; tena Mungu alivichagua vitu dhaifu vya dunia ili aviaibishe vyenye nguvu;

28 tena Mungu alivichagua vitu vinyonge vya dunia na vilivyodharauliwa, naam, vitu ambavyo haviko, ili avibatilishe vile vilivyoko;

29 mwenye mwili awaye yote asije akajisifu mbele za Mungu”.

Unaona, hivyo ndugu.. Mimi na wewe tunayo nafasi sana kubwa ya kuwa mashujaa wa Kristo ikiwa tu tutakubali kuambatana naye, hilo tu, umaskini wako sio kigezo, madeni yako sio sababu, dhiki zako sio sababu za wewe kutokuwa shujaa wa Bwana. Usije ukasema ooh! Mimi nilikuwa sina pesa ndio maana nikashindwa kukutumikia..Siku ile mashujaa kama hao watatuhukumu.

Maran Atha.

Tafadhali washirikishe na wengine habari hizi njema, na pia kama utapenda tuwe tunakutumia mafundisho ya Neno la Mungu ya mara kwa mara kwa njia ya email yako au Whatsapp basi tutumie ujumbe kwenye namba hii +255 789001312

Mada Nyinginezo:

Rudi Nyumbani:

DOWNLOAD PDF
WhatsApp

Source URL: https://wingulamashahidi.org/2020/11/27/lipo-la-kujifunza-kwa-wale-mashujaa-37-wa-daudi/