KWANINI NDOA NYINGI ZINAVUNJIKA? (Sehemu ya 1: Upande wa wanaume)

by Admin | 25 October 2021 08:46 am10

Katika siku hizi za mwisho, migogoro ya kindoa imekuwa ni mingi sana, kiasi kwamba ndoa kudumu hata mwaka mmoja, ni jambo la kushukuru sana. Kila kukicha mikwaruzano, hakuna amani, kila mmoja amemchoka mwenzake. Mpaka wengine kudhani huyo mwenzi aliyemuoa au aliyeolewa naye halikuwa chaguo sahihi kutoka kwa Mungu, hivyo  suluhisho pekee ni kuachana.

Nataka nikuambie, kabla hujafikiria kuachana na huyo mwenzi wako, Tafuta kwanza kama kuna watu walishapitia tatizo kama hilo la kwako, na uone walilitatuaje tatuaje, au mwisho wao ulikuwaje..

Kumbuka kuvunjika kwa ndoa, ni kushindwa kwa pande zote mbili (au moja), kujua wajibu wake katika ndoa kama Neno la Mungu linavyoagiza..

Ndoa inafananishwa na safari ya Maisha/ ya wokovu, si wakati wote, itakuwa ni “HONEY MOON”, si wakati wote mtakuwa ni vijana, si wakati wote mtakuwa Pamoja, na si wakati wote mambo yataenda sawa.. Haijalishi ndoa hiyo, atakuwa ameifungishwa Mungu mwenyewe Kanisani au la.  Kushuka na kupanda kutakuwa ni sehemu ya Maisha yenu.

Leo hii tutajifunza, mfano wa ndoa moja maarufu katika biblia, na jinsi ilivyokumbana  na migogoro mikubwa sana, ambayo naamini ni Zaidi ya migogoro ya ndoa zote zilizowahi kutokea ulimwenguni, lakini Pamoja na hayo  bado iliendelea kudumu hadi dakika ya mwisho, naamini kwa kupitia hiyo itakuponya na wewe pia ambaye kwenye ndoa yako zimeshaanza kuonekana dalili za nyufa.

Na ndoa hiyo si nyingine Zaidi  ya ile ya ADAMU.

Adamu alichaguliwa mke na Mungu mwenyewe, tena aliyeumbwa kutoka katika ubavu wake kabisa,kuonyesha kuwa ni wake kweli kweli,. Lakini waliishi kwa kipindi Fulani kirefu kwa raha na furaha bila taabu wala shida yoyote,  hadi siku mambo yalipoanza kubadilika,

Na yalibadilika, kwa kukengeuka kwa mwanamke kwanza, pale ambapo aliacha kusikiliza maagizo ya mume wake(aliyopewa na Mungu), ya kutokula matunda ya mti wa ujuzi wa mema na mabaya, lakini yeye akayala kwa tamaa ya kutaka kuwa kama Mungu, ya kutaka kuwa kichwa (yaani kumzidi hata mume wake),ya kutaka kumiliki,  akayala bila kumshirikisha mume wake, lakini kinyume chake ni kuwa tamaa hiyo Mungu aliipindua na kuihamishia kwa mume wake badala yake, na ndio maana utaona leo hii  kwanini wanaume wanauchu wa kutawala, kuwa vichwa, hiyo tamaa mwanzoni haikuwepo kwao bali ilikuwa kwa mwanamke, baada ya kuasi Mungu ndio akamuadhibu mwanamke kwa kosa hilo la kumuhamishia mwanaume.

Mwanzo 3:16 “Akamwambia mwanamke, Hakika nitakuzidishia uchungu wako, na kuzaa kwako; kwa utungu utazaa watoto; na tamaa yako itakuwa kwa mumeo, naye atakutawala”.

Sasa na baadaye Adamu alipoona, mke wake kaharibu, ameasi, akakubali na yeye, kuingia katika matatizo ya mke wake kwa hiari yake yeye mwenyewe (kwasababu yeye hakudanganywa), na baada ya hapo, Mungu akamlaani naye pia.

Tangu huo wakati, Maisha yakawa magumu kweli, kwasababu dhambi imeshaingia, kulima kwa shida kukanza, magonjwa yakazuka, vifo vikaingia, kila aina ya shida ikazuka tangu huo wakati na kuendelea, kila kukicha hali ndio ilizidi kuwa mbaya, hadi kwa Watoto waliowazaa, hakuna amani katikati yao, wakawa wanauana.. Embu tengeneza picha ingekuwa wewe ni Adamu ungemfanyaje huyo mwanamke baada ya hapo?

Ni wazi kuwa ungempa talaka siku ile ile ya kwanza alipofanya kosa lile si ndio?. Tena baada ya hapo ungekuwa ni wa kulaumu Maisha yako yote, kwamba Mungu amekupa mkosi na balaa, ni heri ungebakia tu peke yako bila kuoa, lakini tangu ulipompata huyo mwanamke, mambo yako ndio yameenda kombo kabisa kabisa…

Lile kampuni amelifilisi, mali zote zimepukutika umerudia umaskini ambao ulikuwa umeshauaga zamani, amekuletea gonjwa la ukimwi kwa kutanga tanga kwake, amekufanya utengane sio tu na ndugu zako, bali hata na Mungu wako. Mwanzoni ulikuwa  ukifanya ibada vizuri, lakini tangu umuoe yule mwanamke, muda kusali haupo! Kila kitu unakipata kwa shida, tofauti na ulivyokuwa ‘Single’.

Lawama kama hizo Adamu angestahili kuwa nazo kwa mke wake, Lakini hatuoni mahali popote Adamu alimwacha mke wake, na kutamani kuishi na wanyama kama hapo mwanzo, bali alimkumbatia, akakubaliana na hali, akamsamehe, akayapanga tena upya. Akijua kuwa ule tayari ni ubavu wake. Na Mungu hakukosea kumpa, lilikuwa ni chaguo sahihi.

Mwanaume,

Kumbuka kuwa, mpaka umefikia hatua ya kumwoa huyo binti/ mwanamke, ujue kuwa ndio UBAVU wako huo Mungu aliokupa, usidhani kumtambua mke mwema ni mpaka uishi naye bila migogoro, sikuzote za Maisha yako, si kweli. Huyo ambaye upo naye katika migogoro, ni wako, na atabakia kuwa wako mpaka kifo kitakapowatenganisha.

Unachopaswa kufanya ni wewe kusimama katika nafasi yako kama ADAMU.

Suluhisho sio kumwacha, kumbuka ukimwacha huyo maana yake, unataka kurudia kuishi na Wanyama, Mpende mke wako, kwasababu hakuna kitu kinachojenga Zaidi ya upendo, mkumbatie, msamehe, mjenge upya, mvumilie, pale anapokosa, hata kama alikuletea balaa kubwa namna gani, mkumbuke Adamu, alivyoweza kuwa mvumilivu, kwa kunyang’anywa kila kitu na Mungu lakini hakumwacha Hawa. Kwani biblia inasema aliishi miaka 930, na unajua mara nyingi wanawake huwa wanakuwa na umri mrefu kuliko wanaume, kwahiyo si ajabu kuona Adamu aliishi na mke wake kwa Zaidi ya miaka hata 800, lakini sisi miaka 3 tu tumeshachokana.

Biblia inasema..

Waefeso 5:25 “Enyi waume, WAPENDENI WAKE ZENU, kama Kristo naye alivyolipenda Kanisa, akajitoa kwa ajili yake;

26 ili makusudi alitakase na kulisafisha kwa maji katika neno;

27 apate kujiletea Kanisa tukufu, lisilo na ila wala kunyanzi wala lo lote kama hayo; bali liwe takatifu lisilo na mawaa.

28 Vivyo hivyo imewapasa waume nao kuwapenda wake zao kama miili yao wenyewe. Ampendaye mkewe hujipenda mwenyewe.

29 Maana hakuna mtu anayeuchukia mwili wake po pote; bali huulisha na kuutunza, kama Kristo naye anavyolitendea Kanisa.

30 Kwa kuwa tu viungo vya mwili wake.

31 Kwa sababu hiyo mtu atamwacha baba yake na mama yake, ataambatana na mkewe na hao wawili watakuwa mwili mmoja”.

UPENDO KWA MKE wako, ni agizo kutoka kwa Mungu, na sio ihari yako tu mwenyewe. Ukiwa mwanaume wa namna hii, nataka nikuambie utaiponya ndoa yako, na itadumu sana. Wanawake kukengeuka haraka, ni jambo la kawaida, lakini wakisharudi, wanakuwa ni lulu nzuri kwako. Jifunze kusamehe, na vilevile kumpenda.

Lakini hayo yote huwezi kuyafikia kama upo nje ya Kristo. Hivyo Okoka, mkaribishe Yesu katika Maisha yako, tubu dhambi zako, kwa kumaanisha kabisa, kisha ubatizwe, upokee Roho Mtakatifu, na Kristo atakupa uwezo huo, wa kumpenda mkeo kama alivyokuwa Adamu.

Bwana akubariki.

Usikose, sehemu ya pili ya Makala hii.. Ambayo inamlenga mwanamke, kama chanzo cha migogoro ndani ya ndoa, na afanye nini ili aweze kuiponya ndoa yake.

Tafadhali washirikishe na wengine habari hizi njema,

Kwa maombezi/Ratiba za ibada/ Ushauri/ Maswali.
Piga namba hizi: +255693036618 au +255789001312

pia kama utapenda uyapate mafundisho haya kwa njia ya Whatsapp au email basi tutumie ujumbe kwenye namba hizo hizo.

Mada Nyinginezo:

Je! “Mke wa ujana wako” ni yupi kibiblia?

Ndoa ya serikali ni halali?

NDOA NA HARUSI TAKATIFU.

MISTARI YA BIBLIA KUHUSU NDOA.

Rudi nyumbani

DOWNLOAD PDF
WhatsApp

Source URL: https://wingulamashahidi.org/2021/10/25/kwanini-ndoa-nyingi-zinavunjika-sehemu-ya-1-upande-wa-wanaume/