“Si watu wa kutumia mvinyo sana”, je tunaruhusiwa kutumia mvingo kidogo?(1Timotheo 3:8).

by Admin | 15 June 2022 08:46 pm06

Jibu: Tusome..

1 Timotheo 3:8 “Vivyo hivyo mashemasi na wawe wastahivu; si wenye kauli mbili, SI WATU WA KUTUMIA MVINYO SANA, si watu wanaotamani fedha ya aibu”.

Kufuatia mstari huu  wengi wamejikuta wamezama katika ulevi. Pasipo kujua msingi wa andiko hili kwa undani.

Tukisoma maandiko pasipo msaada wa Roho Mtakatifu tutajikuta tunaangamia badala ya kuponyeka..

2 Wakorintho 3:6 “Naye ndiye aliyetutosheleza kuwa wahudumu wa agano jipya; si wa andiko, bali wa roho; KWA MAANA ANDIKO HUUA, BALI ROHO HUHUISHA”.

Umeona?..andiko linaweza KUUA!!, shetani alijaribu kulitumia Andiko kumwangamiza Bwana Yesu kule jangwani wakati anajaribiwa.. “Alimwambia, jitupe chini kwakuwa imeandikwa (Mathayo 4:6-7)”..Lakini kwasababu Bwana alikuwa amejaa Roho Mtakatifu aliweza kutambua hila za shetani, na kumshinda.

Kwahiyo tukirudi katika hilo andiko linalosema kuwa Mashemasi wasiwe watu wa kutumia mvinyo sana, ni vizuri kujua muktadha wa andiko hilo, ili tusije tukafanya makosa katika kupambanua maandiko.

Sasa ili tuelewe vizuri andiko hilo maana yake ni nini, hebu twende mbele kidogo mpaka mlango wa 5, wa kitabu hicho hicho cha 1Timotheo. (Tafadhali zingatia maneno yaliyoainishwa kwa herufi kubwa).

1 Timotheo 5:23 “Tokea sasa usinywe maji tu lakini tumia mvinyo KIDOGO, kwa ajili ya TUMBO lako, na MAGONJWA yakupatayo mara kwa mara”.

Hapa tunaona Mtume Paulo kwa kuongozwa na Roho anamwambia Timotheo asitumie maji tu, bali na Mvinyo, (Na mvinyo wenyewe si mwingi bali KIDOGO).

Na ni kwasababu gani atumie mvinyo?..je! ni kwasababu ya burudani, au kujisisimua?? au kujiliwaza??, au kupunguza mawazo???…jibu ni la!..Bali ni kwasababu ya TUMBO na MAGONJWA, yampatayo mara mwa mara.

Maana yake mvinyo huo ulitumika kwa ajili la Matibabu ya magonjwa..na si kwaajili ya ulevi au kujisisimua..ndio maana hapo Paulo anamalizia kwa kusema KIDOGO..kiasi ambacho hakiwesi kumlewesha mtu, kwasababu ukitumika mwingi, utavuka lengo la matibabu, na kumfanya mtu alewe.

Na mvinyo uliokuwa unatumika, kwa matumizi ya matibabu, haukuwa kila aina ya mvinyo tu!..bali uliokuwa unatumika ni DIVAI tu!. Zamani Divai ilitumika kwa matumizi mengi, ikiwemo matibabu ya tumbo na sio tumbo tu bali hata majeraha.. Tunaweza kulithibitisha hilo katika ile Habari ya msamaria mwema.

Luka 10:33 “Lakini, Msamaria mmoja katika kusafiri kwake alifika hapo alipo; na alipomwona alimhurumia,

34 akakaribia, akamfunga jeraha zake, akizitia MAFUTA NA DIVAI; akampandisha juu ya mnyama wake, akampeleka mpaka nyumba ya wageni, akamtunza”.

Sasa Paulo kama alivyomuasa hapo Timotheo (ambaye ni askofu wa makanisa )kwamba ATUMIE MVINYO KIDOGO (Zingatia hili neno KIDOGO!!) kwa ajili ya tumbo na magonjwa ya mara kwa mara, na si burudani, ndio hivyo hivyo anawaasa mashemasi na maaskofu wengine kwamba na wao wasiwe watu wa kutumia mvinyo nyingi (maana yake watumie kidogo)..kwaajili ya magonjwa ambayo yatakuwa yanawapata mara kwa mara.

1 Timotheo 3:8 “Vivyo hivyo mashemasi na wawe wastahivu; si wenye kauli mbili, SI WATU WA KUTUMIA MVINYO SANA, si watu wanaotamani fedha ya aibu”.

Kwasababu madhara ya kutumia mvinyo nyingi ni kulewa. Na maandiko yanasema ulevi ni dhambi.

Waefeso 5:18 “Tena msilewe kwa mvinyo, ambamo mna ufisadi; bali mjazwe Roho”.

Sasa swali la kujiuliza ni je, hata leo tunapopatwa na magonjwa ya tumbo, au majeraha ya mwili tutumie Divai kujitibu?.

Jibu ni la!.. Sasahivi tunayo madawa mengi, yanayotibu tumbo na majeraha kwa ukamilifu wote. Ni sehemu chache sana za dunia zilizosalia zinazotumia njia hiyo ya matumizi ya divai kidogo kwaajili ya tiba ya tumbo au vidonda.

Kwahiyo kwa hitimisho ni kwamba ULEVI NI DHAMBI, na walevi wote hawataurithi uzima wa milele.

Wagalatia 5:19 “Basi matendo ya mwili ni dhahiri, ndiyo haya, uasherati, uchafu, ufisadi,

20 ibada ya sanamu, uchawi, uadui, ugomvi, wivu, hasira, fitina, faraka, uzushi,

21 husuda, ULEVI, ulafi, na mambo yanayofanana na hayo, katika hayo nawaambia mapema, kama nilivyokwisha kuwaambia, ya kwamba watu watendao mambo ya jinsi hiyo hawataurithi ufalme wa Mungu”.

Kama bado hujampokea Yesu, kumbuka hizi ni siku za Mwisho, kama bado ni mzinzi, au MLEVI, au mtukanaji, au mwizi, au muuaji, tambua kuwa upo hatarini!..hivyo suluhisho ni kumpokea Yesu ili akuoshe dhambi zako na kukusafisha.

Maran atha!

Tafadhali shea na wengine ujumbe huu;

Pia Kwa maombezi/ Ushauri/ Maswali/ Whatsapp:
Tuandikie katika BOXI la Maoni hapo chini au
Piga namba hizi: +255693036618 au +255789001312


Mada Nyinginezo:

Je! ni halali kwa mtu wa Mungu kutumia njia za uzazi wa mpango,ikiwamo mipira?

Je tunaruhusiwa kutumia vidonge wakati wa kufunga?

Nini maana ya “Andiko huua, bali Roho huhuisha (2Wakorintho 3:6)

Kula uzao wa tumbo lako maana yake nini? (Kumbukumbu 28:53)

Je! mabalasi Bwana Yesu aliyoyatumia kugeuzia maji kuwa divai, yalitumika tu kwa kazi hiyo?

Rudi nyumbani

DOWNLOAD PDF
WhatsApp

Source URL: https://wingulamashahidi.org/2022/06/15/si-watu-wa-kutumia-mvinyo-sana-je-tunaruhusiwa-kutumia-mvingo-kidogo1timotheo-38/