Kupiga ramli ni nini katika biblia?

by Admin | 17 June 2022 08:46 am06

Ramli ni elimu ya ufalme wa giza, wanayotumia waganga na wenye mapepo ya utambuzi katika kutabiri mambo yajayo, hivyo mtu yeyote anayetumia elimu hiyo kutabiri mambo yajayo, mtu huyo anapiga ramli.

Na watu walipiga ramli aidha kwa njia ya kutumia viganja vya mikono, au kwa kutumia viungo vya Wanyama.

Katika agano la kale, Bwana Mungu aliwakataza wana wa Israeli wasipige ramli ya aina yoyote ile, baadhi walitii na wengi hawakutii, bali waliendelea kupiga ramli na kufanya mambo mengine mabaya…jambo lililowafanya watolewe kutoka katika nchi yao na kupelekwa Babeli na Ashuru utumwani.

2Wafalme 17:16 “Wakaziacha amri zote za Bwana, Mungu wao, wakajifanyizia sanamu za kusubu, yaani, ndama mbili, wakafanya na Ashera, wakaliabudu jeshi lote la mbinguni, wakamtumikia Baali.

17 Wakawapitisha watoto wao, waume na wake, motoni, WAKAPIGA RAMLI, wakafanya uchawi, wakajiuza nafsi zao wapate kufanya yaliyo maovu machoni pa Bwana, hata kumkasirisha.

18 Kwa hiyo Bwana akawaghadhibikia Israeli sana, akawahamisha mbali na uso wake; wala hapana aliyesalia ila kabila ya Yuda peke yake

19 Hata na watu wa Yuda hawakuyashika maagizo ya Bwana, Mungu wao, lakini walikwenda katika amri za Israeli walizokuwa wamezifanya wenyewe.

20 BASI BWANA AKAKIKATAA KIZAZI CHOTE CHA ISRAELI, AKAWATESA, NA KUWATIA KATIKA MIKONO YA WATU WENYE KUWATEKA NYARA, HATA ALIPOKWISHA KUWATUPA, WATOKE MACHONI PAKE”.

Lakini swali la kujiuliza, je ni kweli Ramli ina matokeo yoyote??..Kwamba mtu akienda kwa mganga na kupiga ramli ili ajue kesho yake itakuwaje, ni kweli atatabiriwa sahihi mambo yajayo?.

Jibu ni la!.. Shetani kamwe hajui kesho kutatokea nini, kama vile mwanadamu asivyojua kesho ni nini kitatokea. Mwenye uwezo wa kujua kesho ni Mungu peke yake!, kwasababu yeye ndio MWANZO na MWISHO, fahamu zake hazina mipaka.

Lakini shetani anachoweza kufanya ni kupanga jambo leo ambalo anatumaini kuwa kesho litatokea. Kwahiyo mtu anayekwenda kwa mganga, akitaka kujua kesho yake itakuwaje..shetani atakachokifanya ni kumpangia huyo mtu kesho yake, jinsi itakavyokuwa.

Kwamfano mtu anakwenda kwa mganga kutaka kujua kama kesho atatembelewa na wageni au la!.. na yule mganga akamtabiria na kumwambia kwamba kesho atatembelewa na wageni, na tena akawataja na majina, na muda watakaokuja.. Na kweli kufikia hiyo kesho, hao wageni wakaja kama alivyotabiriwa jana.

Sasa hapo sio kwamba huyo mganga, kimiujiza kapelekwa kesho na kuona matukio yake. Bali anachokifanya ni kutuma mapepo, ambayo yatakwenda kuwaingia hao watu aliowataja na kuwashawishi wamtembelee huyo mtu katika huo muda aliopanga yeye siku ya kesho.

Kwahiyo hao wageni na wenyewe kama hali zao za kiroho zipo chini, basi wataingiliwa na hayo mapepo na kesho kwa kujua au kutokujua wanajikuta wanakwenda safari ambayo hawajaitegemea, ili kutimiza ubashiri wa huyo mganga!.

Kwahiyo wote wanaopiga ramli, ndio kitu wanachofanyiwa na shetani (wanatengenezewa matukio) pasipo wao kujua, wakidhani wanaambia mambo yajayo. Hiyo ndio sababu Bwana aliwakataza na anatukataza Watoto wake hata leo, tujiepushe na Ramli na aina yoyote ile pamoja na ushirikina, kwasababu zinaasisiwa na shetani, baba wa Uongo. (Yohana 8:44).

Shetani angekuwa anajua mambo yajayo (future), basi angejua hata siku ya unyakuo ni lini, lakini hajui chochote!. Anachojua kiufasaha ni mambo yaliyopita tu!, kwasababu tayari ni matukio ambayo yameshatokea, jambo ambalo pia lipo ndani ya uwezo wetu sisi wanadamu kujua mambo yaliyopita, lakini si kujua mambo yajayo.

Kwahiyo unapokwenda kwa mganga kupiga ramli kutaka kujua kesho yako, fahamu kuwa ni umeenda kwa shetani kutengenezewa kesho yako na si kuambiwa kesho yako, Utatengenezewa vifo na shetani, utatengenezewa mikosi, na shida, na vile vile utatengenezewa baraka bandia ambazo mwisho wake ni laana.

Ukitaka kuijua kesho yako itakuwaje soma Neno la Mungu..Hilo ndio litakupa unabii kamili na wa uhakika wa kesho yako jinsi itakavyokuwa.

Maran atha!

Tafadhali shea na wengine ujumbe huu;

Pia Kwa maombezi/ Ushauri/ Maswali/ Whatsapp:
Tuandikie katika BOXI la Maoni hapo chini au
Piga namba hizi: +255693036618 au +255789001312


Mada Nyinginezo:

Kwanini Mungu aliwaagiza wana wa Israeli wasikisaze chakula?

Je shetani ana uwezo wa kujua mawazo ya mtu?

Nini maana ya kupiga Kite! Katika biblia.

Je ni halali kupiga kura kanisani kuchagua viongozi?

Rudi nyumbani

DOWNLOAD PDF
WhatsApp

Source URL: https://wingulamashahidi.org/2022/06/17/kupiga-ramli-ni-nini-katika-biblia/