KUTII NI BORA KULIKO DHABIHU.

by Admin | 4 August 2022 08:46 am08

Jina la Bwana wetu Yesu Kristo libarikiwe karibu tuyatafakari maneno ya uzima.

Neno la Mungu linasema…

1Samweli 15:22 “Naye Samweli akasema, je! Bwana huzipenda sadaka za kuteketezwa na dhabihu Sawasawa na kuitii sauti ya Bwana? Angalia, KUTII ni bora kuliko dhabihu, Na KUSIKIA kuliko mafuta ya beberu.

23 Kwani kuasi ni kama dhambi ya uchawi, Na ukaidi ni kama ukafiri na vinyago; KWA KUWA UMELIKATAA NENO LA BWANA, Yeye naye amekukataa wewe usiwe mfalme”.

Ni vizuri kumtolea Bwana, tena ni moja ya maagizo yake ambayo tukiyatenda kwa hiari yetu wenyewe basi tutapata thawabu nyingi. Lakini ni vizuri pia kujua jambo moja kuwa Mungu wa Mbingu na nchi si mkusanya mapato kutoka kwetu, na wala hahitaji kitu kutoka kwetu.

 Zaidi sana vyote tunavyomtolea yeye kama sadaka, vinaenda kutumika kwaajili ya watumishi wake na huduma alizowapa.. lakini yeye mwenyewe hakuna chochote anachokipokea.  Kwasababu yeye hahitaji kupokea chochote kutoka kwetu, kwamaana vitu vyote vinatoka kwake.

Kwahiyo kama fedha zetu haziendi mbinguni aliko yeye, wala matoleo yetu mengine hayapai mbinguni kumfikia, maana yake ni kwamba lipo jambo lingine ambalo ni muhimu sana kwake kupokea kutoka kwetu, Zaidi ya sadaka na matoleo tunayomtolea. Na jambo lenyewe si lingine Zaidi ya KULITII NENO LAKE.

Bwana anataka mioyo ya kutii tunapolisikia NENO LAKE.. Hiyo ndiyo dhabihu na sadaka anayoikubali kuliko zote..

Isaya 66:1 “Bwana asema hivi, Mbingu ni kiti changu cha enzi, na dunia ni mahali pa kuweka miguu yangu; mtanijengea nyumba ya namna gani? Na mahali pangu pa kupumzikia ni mahali gani?

2 Maana mkono wangu ndio uliofanya hivi vyote, vitu hivi vyote vikapata kutokea, asema Bwana; lakini mtu huyu ndiye nitakayemwangalia, mtu aliye mnyonge, mwenye roho iliyopondeka, ATETEMEKAYE ASIKIAPO NENO LANGU”.

Unaona?..Unaposoma kwenye biblia kuwa “waasherati na wazinzi hawataurithi ufalme wa Mbinguni (Wagalatia 5:20)”.. na ukaacha kulitii hili NENO, na kinyume chake ukaendelea na uzinzi wako, huku ukijitumainisha kwa sadaka zako nyingi unazoendelea kuzitoa.. fahamu kuwa UNAFANYA MACHUKIZO MBELE ZA MUNGU!!..Kwasababu maandiko yanasema…

Mithali 15:8 “SADAKA YA MTU MBAYA NI CHUKIZO KWA BWANA…..”.

Unaposoma kuwa Wenye dhambi sehemu yao itakuwa ni katika lile ziwa la Moto, kwasababu wamekataa kutubu dhambi zao, na wewe unajijua kabisa bado hujatubu dhambi zako kwa kumaanisha kuziacha, bado ukawa unaendelea na kulipa zaka zako, bado ukawa unaendelea na kuchangia kazi ya Mungu..nataka nikukumbushe kuwa UNAFANYA MACHUKIZO!!.. Mungu wetu si mkusanya mapato kutoka kwetu, na wala hahitaji fedha zetu… Yeye mwenyewe(Yesu Kristo) alisema maneno yafuatayo..

Mathayo 9:13 “Lakini nendeni, mkajifunze maana yake maneno haya, NATAKA REHEMA, WALA SI SADAKA”.

Bwana Yesu anachotaka kuona kutoka kwetu, MIOYO YA TOBA, iliyosikia Neno lake na kutetemeka na kuamua KUGEUKA!..Kumbuka kutii ni bora kuliko dhabihu. Kamwe usijitumainishe katika matoleo unayoyatoa na ukasahau kulitii NENO LA MUNGU. Bwana amelitukuza Neno lake kuliko kitu kingine chochote.

Kabla ya kufikiria kumtolea Mungu, fikiria kujitakasa kwanza, fikiria kuacha uzinzi na ukahaba kwanza, fikiria kuacha kuacha ulevi, fikiria kuacha wizi, fikiria kuacha Ugomvi na baada ya kuacha hayo yote, ndipo ufikirie kumtolea Bwana matoleo yako, lakini kamwe usitangulize dhambi zako mbele ndipo sadaka zako zifuate, kwasababu ukifanya hivyo utakuwa unajitafutia laana badala ya baraka..

Mithali 15:8 “SADAKA YA MTU MBAYA NI CHUKIZO KWA BWANA; Bali maombi ya mtu mnyofu ni furaha yake”.

Kumbukumbu 23:7 “Pasiwe na kahaba katika binti za Israeli, wala pasiwe na hanithi katika wana wa Israeli wanaume.

18 Usilete ujira wa kahaba, wala mshahara wa mbwa, katika nyumba ya Bwana, Mungu wako, kwa ajili ya nadhiri yo yote; kwani haya ni machukizo kwa Bwana, Mungu wako, yote mawili”

Siku zote Litii Neno la Bwana, kwasababu hilo ndilo MWANGA WA NJIA YETU, YA KWENDA MBINGUNI.

Bwana akubariki,

Maran atha!!

Tafadhali shea na wengine ujumbe huu;

Pia Kwa maombezi/ Ushauri/ Maswali/ Whatsapp:
Tuandikie katika BOXI la Maoni hapo chini au
Piga namba hizi: +255693036618 au +255789001312

Mada Nyinginezo:

Dhabihu ni nini?

CHAMBO ILIYO BORA.

Mahali pa juu palikuwa ni wapi kama tunavyosoma katika biblia?

NINI MAANA YA KUTUBU

FUNDISHO KUU LA NEEMA YA MUNGU KWETU.

Rudi nyumbani

DOWNLOAD PDF
WhatsApp

Source URL: https://wingulamashahidi.org/2022/08/04/kutii-ni-bora-kuliko-dhabihu/