SI KWA MATENDO BALI NEEMA.

by Admin | 15 March 2023 08:46 am03

Ikiwa unafanya matendo mazuri yanayompendeza Mungu, basi mshukuru Mungu kwa hayo lakini USIJISIFU wala kujigamba hata kidogo kwa hayo. Kwasababu wakati unadhani kuwa umefanya 100 yanayompendeza Mungu kwa siku moja, yapo mengine 200 uliyoyafanya yasiyompendeza Mungu, kwa kutokujua.

Laiti tukifunguliwa macho na kuona makosa yetu yote tunayoyafanya bila sisi wenyewe kujua, tusingeendelea kujitamani hata kidogo, tusingeendelea kujivuna, tusingeendelea kujisifia vimema vichache vichache tunavyovitenda kwa siku!!!…Kwaufupi maisha yetu yamejaa makosa mengi kuliko mema!, hata kama tutajiona kama tuna mema mengi kuliko kasoro.. Lakini uhalisia utabakia pale pale kwamba makosa yetu yamezidi mema yetu..

Kwahiyo kama Mungu ni wa haki, basi ni haki yake atulipe mabaya mengi kuliko mema.

Kama ukimlazimisha Mungu akuhesabie haki ya kukubariki kwa sadaka yako uliyotoa  jumapili, vile vile anapaswa akuhesabie haki ya kuadhibiwa kwa mawazo yako ya kutamani na kwa hasira uliyomwonea ndugu yako siku hiyo hiyo ya jumapili. Na maandiko yanasema mtu amwoneaye ndugu yake hasira ni mwuaji, kwahiyo unapaswa uhukumiwe kama mwuaji..

Lakini kama hutaki Mungu atazame udhaifu wako huo na hutaki akuadhibu kwa makosa yako basi usilazimishe akulipe kwa matendo yako mazuri unayomfanyia. Bali kinyume chake nyenyekea!!!.. Fanya tu yakupasayo kufanya sawasawa na Luka 17:10.

Luka 17:10  “Vivyo hivyo nanyi, mtakapokwisha kuyafanya yote mliyoagizwa, semeni, Sisi tu watumwa wasio na faida; tumefanya tu yaliyotupasa kufanya”.

Na kama tukiingia mkataba huo na Mungu wa kupokea haki yetu kwa matendo yetu, basi tunazo sababu nyingi za kulipwa mabaya kuliko mema. Kwasababu Mungu siku zote ni  wa haki.

Lakini kama mara nyingi Mungu anatuvumilia kwa mabaya yetu tunayoyafanya sawasawa na Zaburi 130:3  “Bwana, kama Wewe ungehesabu maovu, Ee Bwana, nani angesimama? Lakini kwako kuna msamaha, Ili Wewe uogopwe”…basi na sisi hatuna budi kutoyatumainia mema yetu tunayoyafanya!.

Ndio hapa sasa panazaliwa kitu kinachoitwa NEEMA!... Neema tafsiri yake ni upendeleo maalumu usiokuwa na sababu. Kwamba unapokea tu kitu kutoka kwa Mungu pasipo matendo yako.. Yaani Mungu anapenda tu kukupa si kwasababu wewe ni mtenda mema, au ni mwombaji sana, au ni mfungaji sana, au ni mhubiri mzuri… La!, bali anakutendea tu mema bila kwa upendo wake tu!, na huruma zake na kupenda kwake.

Ndio maana hatuna budi kila siku KUOMBA NEEMA YA MUNGU ije juu yetu. Kwasababu tukiipata hiyo tumepata kila kitu.

Usijivune, bali omba neema kwasababu Mungu huwapinga wenye kiburi na kuwapa wanyenyekevu Neema yake (1Petro 5:5).

Afya uliyonayo ni kwa neema tu, Uzima ulio nao ni kwa Neema tu, karama uliyo nayo ni kwa neema tu, zaidi sana hata Wokovu ulio nao ni kwa Neema tu na wala si kwa matendo yako.

Waefeso 2:8 “Kwa maana mmeokolewa kwa neema, kwa njia ya imani; ambayo hiyo haikutokana na nafsi zenu, ni kipawa cha Mungu;

9  wala si kwa matendo, mtu awaye yote asije akajisifu”

Na zaidi ya yote pia Roho Mtakatifu tunampokea kwa Neema..

Wagalatia 3:2 “Nataka kujifunza neno hili moja kwenu. Je! Mlipokea Roho kwa matendo ya sheria, au kwa kusikia kunakotokana na imani”

Omba Neema!!.. omba Neema!, Omba Neema…usitumainie matendo yako..

Bwana akubariki.

Tafadhali shea na wengine ujumbe huu;

Pia Kwa maombezi/ Ushauri/ Maswali/ Whatsapp:
Tuandikie katika BOXI la Maoni hapo chini au
Piga namba hizi: +255693036618 au +255789001312

Mada Nyinginezo:

NINI TOFAUTI KATI YA MATENDO YA SHERIA NA MATENDO YA IMANI?

NEEMA YA MUNGU KWA MARIAMU.

FUNDISHO KUU LA NEEMA YA MUNGU KWETU.

Kama tunaokolewa kwa neema kwanini wokovu tuupate kwa nguvu?

Nini tofauti ya Uwezo na Uweza kibiblia?

Rudi nyumbani

DOWNLOAD PDF
WhatsApp

Source URL: https://wingulamashahidi.org/2023/03/15/si-kwa-matendo-bali-neema/