Je! kuna mwanamke mwingine aliyempaka Bwana marhamu (manukato) zaidi ya Mariamu ndugu yake Lazaro?

by Admin | 3 May 2023 08:46 am05

Jibu: Kulikuwa na tukio zaidi ya moja la Bwana Yesu kupakwa mafuta…Tukio la kwanza ni hilo tunalolisoma katika injili tatu,  (Mathayo 26:6-13 na Marko 14:3-8  na Yohana 12:1-3), ambapo  biblia inaonyesha moja kwa moja kuwa ni Mariamu ndugu yake Lazaro, ndiye aliyempaka Bwana Marhamu siku sita kabla ya pasaka.

Tusome,

Yohana 12:1 “Basi, siku sita kabla ya Pasaka, Yesu alifika Bethania, alipokuwapo Lazaro, yeye ambaye Yesu alimfufua katika wafu.

2  Basi wakamwandalia karamu huko; naye Martha akatumikia; na Lazaro alikuwa mmojawapo wa wale walioketi chakulani pamoja naye.

3  Basi Mariamu akatwaa ratli ya marhamu ya nardo safi yenye thamani nyingi, akampaka Yesu miguu, akamfuta miguu kwa nywele zake. Nayo nyumba pia ikajaa harufu ya marhamu”.

Lakini tukirudi katika Injili ya Luka, tunasoma tukio lingine ambalo linakaribia sana kufanana na hili la Bethania, ambapo biblia inasema alitokea mwanamke mmoja mwenye dhambi na kuanguka miguuni pake na kulia huku akimpaka mafuta.

Jibu: Turejee..

Luka 7:36 “Mtu mmoja katika Mafarisayo alimwalika ale chakula kwake; akaingia katika nyumba yake yule Farisayo, akaketi chakulani.

37  Na tazama, mwanamke MMOJA WA MJI ULE, ALIYEKUWA MWENYE DHAMBI, alipopata habari ya kuwa ameketi chakulani katika nyumba ya yule Farisayo, alileta chupa ya marimari yenye marhamu.

38  Akasimama nyuma karibu na miguu yake, akilia, akaanza kumdondoshea miguu machozi yake, na kuipangusa kwa nywele za kichwa chake, akiibusu-busu miguu yake na kuipaka yale marhamu.”

Sasa ni viashiria gani vinatuthibitishia kuwa yale yalikuwa ni matukio mawili tofauti?

  1. Katika Mlango wa 7 wa kitabu cha Luka tunaona Bwana Yesu alikuwa akihubiri Miji ya Galilaya (Naini na Kapernaumu), ambayo ipo kaskazini mwa Israeli, mbali kabisa na mji wa Bethania ambao upo kusini mwa Israeli, Na Mariamu dada yake Lazaro alikuwa anaishi huko Bethania mbali kabisa na Galilaya na Biblia inaonyesha tukio hili lilitokea huko katika mojawapo wa miji ya Galilaya.. ikimaanisha kuwa lilikuwa ni tukio lingine tofauti na lile lililotokea la Mariamu wa Bethania, na lilikuwa ni tukio lililowahi kutoka kabla ya hili la mwisho la Bethania.

Hivyo kwa hitimisho ni kuwa haya ni matukio mawili tofauti, yaliyotokea kukaribiana na biblia haikumtaja Yule mwanamke wa Galilaya alikuwa ni nani?.. labda huenda alikuwa ni Yule Yule Mariamu alimpaka mara mbili, au ni mwanamke mwingine ambaye biblia haijamtaja jina lake.

Lakini hayo yote si ya muhimu sana kuyajua, (kwamba ni nani, au ni matukio mangapi) lililo la muhimu kulijua ni tendo hilo la kiimani wanawake hawa waliloyoyafanya.. sasa kujua kwa undani Siri iliyokuwepo katika kumpaka Bwana mafuta fungua hapa >>> AKAKIVUNJA KIBWETA AKAIMIMINA KICHWANI PAKE.

Bwana atubariki.

Tafadhali shea na wengine ujumbe huu;

Pia Kwa maombezi/ Ushauri/ Maswali/ Whatsapp:
Tuandikie katika BOXI la Maoni hapo chini au
Piga namba hizi: +255693036618 au +255789001312

Mada Nyinginezo:

Rudi nyumbani

DOWNLOAD PDF
WhatsApp

Source URL: https://wingulamashahidi.org/2023/05/03/je-kuna-mwanamke-mwingine-aliyempaka-bwana-marhamu-manukato-zaidi-ya-mariamu-ndugu-yake-lazaro/