Maana ya Mithali 17:22 Moyo uliochangamka ni dawa nzuri;

by Admin | 9 May 2024 08:46 am05

SWALI: Nini maana ya

Mithali 17:22 Moyo uliochangamka ni dawa nzuri; Bali roho iliyopondeka huikausha mifupa.


JIBU: Mstari huu unatuonyesha jinsi gani hali ya moyo inavyoweza kuathiri hali za nje za mwili. Si kila wakati dawa itatibu, ikiwa moyo umepondeka afya inaweza kuathiriwa pia. Kwamfano labda mtu yupo katika nyumba au makazi ambayo hana amani, anateswa, anaudhiwa, anaabishwa, muda wote anakuwa mnyonge, utaona pia kwa namna Fulani afya yake itaathirika, labda atasumbuliwa na ugonjwa Fulani ambao hauna sababu wala chanzo.

Lakini moyo ukichangamka, hata kama huyo mtu yupo katika hali/mazingira magumu kiasi gani, mwili wake pia baada ya mda utaitikia hali ya roho yake. Na hivyo atakuwa na afya yake.

Sasa Nitaufanyaje moyo wangu uchangamke?

1)    Kwa kutembea ndani ya ahadi za Mungu katika Neno lake. Mara kadhaa katika maandiko Bwana Yesu alisema” jipeni moyo”. Unapojipa moyo katika ahadi za Mungu ukijua kabisa, ni hakika atatenda,hasemi uongo, Fahamu kuwa utakuwa ni mwanzo wa kuchangamka kwako. Kwamfano ukikumbuka kuwa alisema hatatuacha wala kutupungukia, unakuwa na amani wakati wote, nyakati zote, ukiwa na vingi ukiwa umepungukiwa yote yatakuwa sawa tu, kwasababu sikuzote yupo pamoja na wewe. Furaha inakutawala.

Hata upitiapo magonjwa, ukikumbuka ahadi zake kuwa atakuponya, ukaendelea kuzishika kwa imani, afya yako hurejea.

Yeremia 30:17 Maana nitakurudishia afya, nami nitakuponya jeraha zako, asema Bwana, kwa sababu wamekuita, mwenye kutupwa, wakisema, Ni Sayuni, ambao hapana mtu autakaye. 

18 Bwana asema hivi, Tazama, nitarudisha tena hema za Yakobo zilizohamishwa, na kuyahurumia makao yake; nao mji huo utajengwa juu ya magofu yake wenyewe, nalo jumba litakaliwa, kama ilivyokuwa desturi yake. 

19 Tena kwao itasikiwa shukrani, na sauti yao WACHANGAMKAO; nami nitawazidisha, wala hawatakuwa wachache; tena nitawatukuza, wala hawatakuwa wanyonge.

Hivyo ishi kwa kushikilia ahadi za Mungu kwenye Neno lake, zipo nyingi sana, na zimefika katika kila Nyanja ya maisha yetu. Hakuna sababu ya kutochangamka, wakati Neno la ahadi lipo. Aliyekuahidia ni Mungu wa miungu muumba wa mbingu na nchi hakuna lolote linalomshinda, kwanini uogope?

2) Pili, kwa kupenda ushirika na wengine. Kamwe usiishushe wala kuipuuzia  nguvu iliyopo ndani ya ndugu katika Kristo. Zipo nyakati utahitaji kutiwa nguvu na wenzako, hata kukaa pamoja tu, kutafakari Neno la Mungu na kumwimbia Mungu ni tiba nzuri sana, itakayochangamsha moyo wako, tofauti na kama ungekuwa mwenyewe mwenyewe tu wakati wote.

Ndivyo ilivyokuwa hata kwa Paulo, wakati ule..

Matendo 28:15  Na kutoka huko ndugu, waliposikia habari zetu, wakaja kutulaki mpaka Soko la Apio na Mikahawa Mitatu. Paulo alipowaona alimshukuru Mungu, AKACHANGAMKA.

Chuma hunoa chuma, tuwapo pamoja, tunajengana nafsi, na matokeo ya kufanya hivyo yataonekana mpaka nje.

Bwana akubariki.

Washirikishe na wengine habari hizi njema kwa kushea

Ikiwa utapenda kupata msaada wa kumpokea Yesu maishani mwako bure, Basi wasiliana nasi kwa namba uzionazo chini ya makala hii.

Pia kwa kupokea mafundisho ya kila siku kwa njia ya WHATSAPP, jiunge na channel yetu kwa kupofya link hii >> https://whatsapp.com/channel/0029VaBVhuA3WHTbKoz8jx1

Kwa mawasiliano: +255789001312 au +255693036618

Bwana akubariki.

Mafundisho mengine:

PALE AHADI ZA MUNGU ZINAPOKUJARIBU.

JE! UNAIONA ILE NCHI NZURI YA KUMETA-META MBELE YAKO?

Je sisi wakristo tunaruhusiwa kufanya 40 za marehemu?

Rudi Nyumbani

DOWNLOAD PDF
WhatsApp

Source URL: https://wingulamashahidi.org/2024/05/09/maana-ya-mithali-1722-moyo-uliochangamka-ni-dawa-nzuri/