VIASHIRIA VINGINE VYA ROHO MTAKATIFU KUWEPO NDANI YAKO.

by Admin | 15 July 2024 08:46 pm07

Jina la Bwana na Mwokozi wetu, (Mkuu wa Uzima na Mfalme wa wafalme), YESU KRISTO libarikiwe. Karibu tujifunze Neno la Mungu wetu lililo taa na Mwanga wa njia zetu (Zab. 119:105).

Kiashiria cha Kwanza ni UTAKATIFU:

kwamba Roho Mtakatifu yupo ndani yako (au umebatizwa na Roho Mtakatifu) ni UTAKATIFU, angalia maisha yako, je dhambi imekuwa hafifu kiasi gani, ukijilingalisha na kipindi cha nyuma.. Ukiona kuna nguvu kubwa ndani yako ya kushinda dhambi, basi tambua kuwa si wewe, bali ni uwepo wa nguvu za Roho Mtakatifu ndani yako.

Kiashairia cha Pili ni KARAMA:

Karama maana yake ni ile shauku/msukumo  wa kumtumikia Mungu katika eneo Fulani, ambao unakutofautisha na mwingine.. Ukiona una shauku kubwa ya kumtumikia Mungu, na ukiangalia shauku hiyo huioni kwa mwingine aliye karibu na wewe, au ukijaribu kumweleza mwingine ni kama hakuelewi, basi fahamu kuwa hiyo shauku si wewe, bali ni Nguvu/msukumo wa Roho Mtakatifu ndani yako. (ndio maana zinaitwa karama za roho, 1Wakorintho 12:1)

Kiashiria cha Tatu ni KUCHUKIWA/KULAUMIWA BILA SABABU:

Si kila lawama ni ishara mbaya: Ukiona kila unalolifanya la KiMungu linazua lawama, au shida mahali ulipo..basi hiyo pia ni ishara nyingine ya uwepo wa Roho Mtakatifu ndani yako..

1Petro 4:14 “MKILAUMIWA kwa ajili ya jina la Kristo ni heri yenu; kwa kuwa Roho wa utukufu na wa Mungu anawakalia”.

Kiashiria cha Nne: KUPUNGUA KWA HOFU NDANI YAKO.

Ukiona hofu imeisha ndani yako, kiasi kwamba wakati  wengine wana wasiwasi kuhusiana na mambo Fulani wewe huna wasiwasi hata kidogo, na unajihisi kabisa kuwa Mungu yupo na wewe, basi fahamu kuwa kuna uwepo wa Nguvu za Roho Mtakatifu ndani yako, na si wewe kwa akili zako (kwasababu kwa akili za kawaida, hakuna mtu mwenye akili timamu asiyetishwa na misukosuko ya maisha).

Kiashiria cha Tano: FURAHA.

Ukiona kuna furaha isiyoelekeza ndani yako kila unapofikiria habari za YESU, na wakati mwingine unatamani kumweleza mwingine, na ukijaribu ni kama haoni kama unavyoona, basi fahamu kuwa si wewe hisia zako, bali ni nguvu za Roho Mtakatifu ndani yako, Wagalatia 5:22.

Kiashiria cha Sita: MFULULIZO WA MAFUNUO.

Ukiona kila unapotembea unamwona YESU katika neno lake, au unauona uweza wa YESU, ambao unakuletea changamko Fulani, na msisimko wa kipekee, ambao huoni kwa mwingine, basi tambua kuwa ni kazi za Roho Mtakatifu hizo ndani yako.. kwani kwa kawaida macho yaliyofumbwa hayawezi kumwona YESU popote wala kuuona uweza wake.

Vile vile ishara hii inaambatana na kupata ufahamu wa maandiko kwa namna ya kipekee sana.

SASA UFANYE NINI UNAPOGUNDUA KUWA ROHO MTAKATIFU YUPO NDANI YAKO?

  1. USIMZIMISHE ROHO (1Wathesalonike 5:19)

Kumzimisha Roho Mtakatifu ni kitendo cha kumfanya Roho Mtakatifu aondoke ndani yako na kukaa mbali nawe aidha kwa muda kwa muda au moja kwa moja.. na vitu vinavyomzimisha Roho Mtakatifu ni dhambi za makusudi…kama uzinzi, wizi, ibada za sanamu na kupenda mambo ya kidunia.

Mambo haya mtu akiyafanya Roho Mtakatifu anaondoka ndani yake, na ile nguvu ya kushinda dhambi inaondoka ndani yake, vile vile ile nguvu ya kushinda hofu pia inaondoka ndani yake.

  1. USIMHUZUNISHE ROHO (Waefeso 4:30)

Kumhuzunisha Roho sawasawa na Waefeso 4:30, ni kitendo cha kumfanya Roho Mtakatifu asifurahiwe na wewe, na matokeo ya kumhuzunisha Roho Mtakatifu kwa muda mrefu, ni kuondoka ndani ya mtu.

Mambo yafuatayo yanaweza kuwa sababu ya Roho Mtakatifu kuhuzunika ndani yetu..

1. Tabia ya kukosa Imani…kama vile Bwana YESU alivyohuzunishwa na wanafunzi wake mara kadhaa, pale walipokuwa wanapungukiwa na Imani, mpaka kufikia hatua ya kuwaambia mara kwa mara “Imani yenu iko wapo”

Vile vile na sisi tunapopungukiwa na Imani katika mazingira tukutanayo hiyo Roho Mtakatifu anaugua ndani yetu, hivyo hatuna budi kuwa watu wa Imani daima.

Na Imani chanzo chake ni kusikia Neno la Mungu, (ambayo tafsiri yake ni kusoma na kujifunza biblia). Neno la MUNGU linapokaa kwa wingi ndani yetu pamoja na maombi basi viwango vyetu vya Imani vinakuwa na hivyo tunakuwa katika hali ya kumpendeza Roho Mtakatifu.

2. Tabia ya uvivu wa kiroho.. Ukiwa mlegevu kutenda yakupasayo, Roho Mtakatifu anaugua kwasababu hutumii kile ulichopewa,

Kama viashiria hivyo havipo ndani yako basi huenda Roho MTAKATIFU bado hajaingia ndani yako, au amesogea pembeni, na hiyo si kwasababu wewe ni mbaya, au una kasoro, au wengine ni bora kuliko wewe mbele zake, LA!..bali ni kwasababu bado hujafungua mlango, au ulikuwa hujui jinsi ya kuufungua mlango..kwasababu yeye anatamani aingie ndani yako Zaidi hata ya wewe unavyotamani.

Sasa swali la msingi, unaufunguaje mlango ili aingie ndani yako?

Kanuni ni rahisi sana, isiyogharimu hata theluthi ya senti moja.. na kanuni  yenyewe ni kukiri tu makosa yako, kwamba wewe ni mwenye dhambi na hivyo unahitaji msaada wake (kutubu) kwa kumaanisha kabisa kuacha mambo yote mabaya.., na kwenda kubatizwa katika ubatizo sahihi wa maji mengi na kwa jina la Bwana YESU, kama bado ulikuwa hujabatizwa, baada ya hapo yeye mwenyewe ataingia ndani yako, na utaona matunda hayo na mengine Zaidi ya hayo..

Matendo 2:37 “Walipoyasikia haya wakachomwa mioyo yao, wakamwambia Petro na mitume wengine, Tutendeje, ndugu zetu?

38  Petro akawaambia, Tubuni mkabatizwe kila mmoja kwa jina lake Yesu Kristo, mpate ondoleo la dhambi zenu, nanyi mtapokea kipawa cha Roho Mtakatifu.

39  Kwa kuwa ahadi hii ni kwa ajili yenu, na kwa watoto wenu, na kwa watu wote walio mbali, na kwa wote watakaoitwa na Bwana Mungu wetu wamjie”

Kama haujabatizwa na utahitaji msaada huo, basi waweza wasiliana nasi kwa namba zilizoanishwa hapa chini na tutakusaidia juu ya hilo.

Ubarikiwe sana.

Washirikishe na wengine habari hizi njema kwa kushea

Ikiwa utapenda kupata msaada wa kumpokea Yesu maishani mwako bure, Basi wasiliana nasi kwa namba uzionazo chini ya makala hii.

Pia kwa kupokea mafundisho ya kila siku kwa njia ya WHATSAPP, jiunge na channel yetu kwa kupofya link hii >> https://whatsapp.com/channel/0029VaBVhuA3WHTbKoz8jx10

Kwa mawasiliano: +255789001312 au +255693036618

Bwana akubariki.

Mafundisho mengine:

FAHAMU VIASHIRIA VYA MTU ALIYESAMEHEWA DHAMBI ZAKE.

JINSI ROHO MTAKATIFU ANAVYOWAFUNULIA WATU MAANDIKO.

IMANI “MAMA” NI IPI?

ZIFAHAMU KAZI TATU ZA ROHO MTAKATIFU KATIKA ULIMWENGU.

UJIO WA BWANA YESU.

Rudi Nyumbani

DOWNLOAD PDF
WhatsApp

Source URL: https://wingulamashahidi.org/2024/07/15/viashiria-vingine-vya-roho-mtakatifu-kuwepo-ndani-yako/