Jibu: Turejee…
Matendo 7:58 “wakamtoa nje ya mji, wakampiga kwa mawe. Nao mashahidi WAKAWEKA NGUO ZAO MIGUUNI PA KIJANA MMOJA ALIYEITWA SAULI.
59 Wakampiga kwa mawe Stefano, naye akiomba, akisema, Bwana Yesu, pokea roho yangu”.
Zipo tafiti zinasema kuwa zamani za biblia, akipatikana mtu na kosa la kustahili kuuawa kwa kupigwa mawe, basi wale mashahidi waliolishuhudia kosa la huyo mtu, kabla ya kutekeleza mauaji walivua nguo zao kama ishara ya kiapo walichokitoa/ushahidi kuwa ni kweli.
Lakini dhana hiyo haina marejeo yoyote ya biblia, hivyo si ya kusadikika.
Lakini sababu pekee yenye kuleta maana ya mavazi ya mashahidi kuwekwa miguuni mwa Sauli ni ili wawe wepesi katika kutekeleza zoezi hilo la mauaji.
Ni kawaida wana michezo au wapiganaji kupunguza mavazi yao kabla ya mchezo kuanza ili wawe wepesi, ndicho walichokifanya hawa mashahidi, walipunguza mavazi yao ya nje, na kumpatia kijana Sauli awahifadhie kwa muda na baadae wazichukue baada ya kumuua Stefano.
Na tunasoma Sauli (ambaye baadaye ndiye aliyekuja kuwa Paulo), alikubali kuwatunzia..
Matendo 22:20 “Na damu ya Stefano shahidi wako ilipomwagwa, mimi nami nilikuwa nikisimama karibu, nikikubali, na kuzitunza nguo zao waliomwua”.
Sasa ni kwanini Bwana MUNGU aruhusu mavazi ya wauaji yatunzwe na Sauli?.
Sababu kuu ni kwamba Bwana MUNGU alijua Sauli atakuja kugeuka baadaye na kuwa mtumishi wake kwa watu wa Mataifa.
Hivyo kitendo cha zile nguo kuwekwa miguuni mwa Sauli ni kuweka sababu baadae ya Wayahudi pamoja na wakristo waliopo Yerusalemu kumkataa, ili aende kwa watu wa mataifa…
Kwani watakapokumbuka lile tendo la kushiriki kwake kumuua Stefano, wamkatae na kumwona hafai..
Matendo22:17 “Ikawa nilipokwisha kurudi Yerusalemu, nilipokuwa nikisali ndani ya hekalu, nikawa hali ya kuzimia roho,
18 nikamwona, naye akiniambia, Hima, utoke Yerusalemu upesi, KWA SABABU HAWATAKUBALI USHUHUDA WAKO katika habari zangu.
19 Nami nikasema, Bwana, wanajua hao ya kuwa mimi nalikuwa nikiwafunga gerezani wale wanaokuamini na kuwapiga katika kila sinagogi.
20 Na damu ya Stefano shahidi wako ilipomwagwa, mimi nami nilikuwa nikisimama karibu, nikikubali, na kuzitunza nguo zao waliomwua.
21 Naye akaniambia, Enenda zako; KWA KUWA NITAKUTUMA UENDE MBALI KWA WATU WA MATAIFA”.
Na utaona faida ya Paulo kuhubiri kwa watu wa Mataifa ndio mazao ya nyaraka zote za Paulo, ambazo mpaka leo zimekuwa msingi wa Neno la Mungu.
Tunachojifunza zaidi kuwa yapo makosa ambayo yalitokea zamani, na MUNGU aliyaruhusu yatokee kwasababu yamebeba kusudi kubwa mbeleni.
Makosa mengine yaliruhusiwa zamani ili yatuondolee viburi leo, mengine yaliruhusiwa ili tupate fursa njema leo, na mengine ni ushuhuda kwa wengine na maonyo kwa wengi e n.k
Hivyo kila jambo lina kusudi lake.
Bwana akubariki.