Mhubiri 7:9 “Usifanye haraka kukasirika rohoni mwako,
Maana yake Mpumbavu ndiye anayeihifadhi hasira, lakini mwenye hekima anashughulika na hasira yake na kuishinda…
Mithali 29:11 ”Mpumbavu hudhihirisha hasira yake yote; Bali mwenye hekima huizuia na kuituliza”
Mithali 14:29 “Asiye mwepesi wa hasira ana fahamu nyingi; Bali mwenye roho ya hamaki hutukuza upumbavu”.
MADHARA YA HASIRA INAYOKAAA KIFUANI.
1. MAUTI.
Biblia inasema Hasira inamwua mtu mpumbavu…
Ayubu 5:2 “Kwani hasira humwua mtu mpumbavu…”
Inaanza kuua heshima ya mtu, utu wa mtu na mwisho inamaliza mwili…
2. HASIRA HAIBADILISHI JAMBO.
Hasira inayokaa kifuani haibadilishi chochote bali inaongeza matatizo kwa mtu..
Ayubu 18:4 “Wewe ujiraruaye mwenyewe katika hasira yako, Je! Dunia itaachwa kwa ajili yako wewe? Au jabali litaondolewa mahali pake?”
3.HASIRA INAZAA MAAMUZI YA MABAYA.
Mithali 14:17 “Yeye aonaye hasira upesi atatenda kwa ujinga; Na mtu mwenye hila mbaya huzirwa”.
4. HASIRA INACHOCHEA MAGOMVI.
Mtu mwenye hasira hawezi kukosa ugomvi…
Mithali 15:18 “Mtu wa hasira huchochea ugomvi; Bali asiye mwepesi wa hasira hutuliza mashindano”.
CHANZO CHA HASIRA.
Hivi ni vyanzo vitatu vikuu vya hasira inayokaa kifuani.
1. MAISHA YA DHAMBI.
Ukiwa nje na wokovu, huwezi kuiepuka roho ya hasira, utakuwa daima mtu wa hasira, yaweza isijidhihirishe kila wakati lakini itakuwa ipo ndani yako tu.
2. KUJIAMINISHA KUWA UNA HASIRA.
Upo usemi uliozoelekea vinywani mwa wengi kuwa “mimi huwa na hasira sana”… kauli hiyo inatia muhuri na uhalali wa hasira kukaa kifuani mwako, ifute hiyo kauli kinywani mwako, kwani unavyojiwazi na kujinenea ndivyo utakavyokuwa..
3. KUAMBATANA NA WATU WENYE HASIRA.
Angalia watu unaotembea nao au unaoishirikiana nao ni watu wa namna gani, watu unaojiunganisha nao wanaweza kuathiri tabia yako njema.
Mithali 22: 24 “Usifanye urafiki na mtu mwenye hasira nyingi; Wala usiende na mtu wa ghadhabu nyingi
25 Usije ukajifunza njia zake; Na kujipatia nafsi yako mtego”.
NAMNA YA KUKOMESHA HASIRA.
Komesha hasira yako kwa kumwamini Bwana Yesu na kutubu…maana hasira mwisho wake ni hukumu..
Zaburi 37:8 “Ukomeshe hasira, uache ghadhabu, Usikasirike, mwisho wake ni kutenda mabaya.
9 Maana watenda mabaya wataharibiwa, Bali wamngojao BWANA ndio watakaoirithi nchi”.
Ukimpokea Bwana YESU kwa kumaanisha kabisa na ukaamua kubadilisha mtindo wa maisha ikiwemo makundi ya watu wasio wa imani, Bwana Yesu kupitia Roho wake mtakatifu atakutakasa utu wako wa ndani na atakupa busara ambayo itaishinda hasira mbaya ya ibilisi..
Mithali 19:11”Busara ya mtu huiahirisha hasira yake; Nayo ni fahari yake kusamehe makosa”.
Bwana atusaidie.