BWANA SI MWEPESI WA HASIRA, LAKINI BWANA NI MWINGI WA HASIRA.

BWANA SI MWEPESI WA HASIRA, LAKINI BWANA NI MWINGI WA HASIRA.

Kuna wakati ulifika Nabii Nahumu alifunuliwa juu ya hatma ya mji mmoja ulioitwa Ninawi, Mji huu ndio uliokuwa mji mkuu waTaifa la Ashuru, ulikuwa mji wa kwanza kwa ukubwa kuliko mji yote iliyokuwa ulimwengu kwa wakati ule. Baadaye ndio ikaja kutokea miji mwingine ulioitwa Babeli ..Sasa katika mambo aliyoongozwa Nabii Nahumu kuandika ni pamoja na uvumilivu wa hasira ya Mungu, pamoja na ukali wa hasira ya Mungu. Maneno hayo utayaona mwanzoni kabisa mwa kitabu cha Nahumu..

Nahumu 1:1 “Ufunuo juu ya Ninawi. Kitabu cha maono aliyoyaona Nahumu….

2 Bwana ni Mungu mwenye wivu, naye hujilipiza kisasi; Bwana hujilipiza kisasi, NAYE NI MWINGI WA HASIRA; Bwana hujilipiza kisasi juu ya adui zake, huwawekea adui zake akiba ya hasira.

3 BWANA SI MWEPESI WA HASIRA, ana uweza mwingi….”

Unaona, sasa unaweza ukajiuliza ni kwanini Mungu azungumze maneno hayo mawili kwa wakati mmoja?

Utakumbuka kuwa mji huu wa Ninawi ndio ule mji ambao Nabii Yona alitumwa kwenda kuwahubiria juu ya dhambi zao kwamba watubu..Kama tunavyoijua ile habari, watu wale walisikia injili ya Yona, na walipotubu Mungu aliwarehemu japokuwa walikuwa sio wakamilifu ipasavyo.. hiyo ilimfanya mpaka Yona amkasirikie Mungu kwanini hajawaangamiza wale watu waovu..Ndipo Mungu akamwambia Yona maneno yafuatayo;

Yona 4:11 “na mimi, je! Haikunipasa kuuhurumia Ninawi, mji ule mkubwa; ambao ndani yake wamo watu zaidi ya mia na ishirini elfu, wasioweza kupambanua katika mkono wao wa kulia na mkono wao wa kushoto; tena wamo wanyama wa kufugwa wengi sana?”

Unaona huruma za Mungu jinsi zilivyokuwa nyingi?.. Japokuwa walikuwa ni waabudu miungu, wapagani, lakini Mungu aliwahurumia tu pale walipotubu dhambi zao na kugeuka…Lakini tunavyozidi kusoma biblia tunaona, mambo hayakuwa hivyo siku zote ulifika wakati mji huo wa Ninawi ulirudia mambo yale yale ya kale, uovu ukaendelea kama ulivyokuwa pale mwanzo kipindi Yona anatumwa, wakasahau kuwa walinusurika kuwa jivu mfano wa Sodoma na Gomora.

Matokeo yake ndio tunakuja kuona Nabii Nahumu akitokea na kutoa unabii juu ya mwisho wa Taifa hilo..Pengine wakati Nahumu anatoa unabii huu waliona kama ni utani tu, kwamba watatubu tu kama kipindi kile cha Yona?..Wakawa wanasema tunajua Mungu siku zote si mwepesi wa hasira, Mungu ni wa rehema, anaghahiri mabaya..Hata hivyo hawezi kuliangamiza Taifa kubwa kama hili duniani (Ashuru) na mji wetu huu Ninawi ulio msaada wa mataifa mengi ulimwenguni.

Ndivyo walivyodhania, wakapumbazwa, wakajisahau kabisa, tena na jinsi walivyoona wamefanikiwa kuwachukua wayahudi utumwani, (yale makabila 10), ndio wakadhani kuwa Mungu amewapendelea..

Lakini Nabii Nahumu akatoa unabii juu ya mji huo..akisema.

Nahumu 3:7 “Hata itakuwa, wote wakutazamao watakukimbia, wakisema, Ninawi umeharibika; ni nani atakayeuhurumia? Nikutafutie wapi wafariji”?

Hayo maneno aliyoyasema nabii Nahumu yalikuja kutimia kama yalivyo, ni kwa vile tu, biblia haiwezi kuandika kila kitu, na kila historia, kama ingekuwa ni hivyo vitabu visingetosha duniani vya biblia. Lakini historia ipo wazi kabisa inaonyesha, ulipofika mwaka wa 612 KK, Wababiloni pamoja na wamedi waliunganisha nguvu, na kuizunguka Ninawi mji mkuu wa Ashuru, na kuuteka na kuungamiza, na hapo ndipo ikawa mwisho wa Taifa linaloitwa ashuru na mji wa Ninawi mpaka leo hii tunavyozungumza ni miaka zaidi ya 2,500, ni vipande vya mawe tu vimesimama pale kaskazini mwa Iraq. Na taifa la Babeli ndipo lilipopatia nguvu hapo, ambalo nalo baadaye lilikuja kuangamizwa hivyo hivyo.

Nahumu 3:19 “Jeraha yako haipunguziki; jeraha yako ni nzito sana; wote wasikiao habari zako wapiga makofi juu yako; kwa maana ni nani ambaye uovu wako haukupita juu yake daima”?

Biblia inasema Ninawi ni mji uliokuwa umekaa pasipo kufiri, upo upo tu, ukidhani wenyewe ndio wenyewe, ulipokuwa unashinda vita vingi, na unafanikiwa kuchukua mateka mataifa mengi, lakini siku yao ilipofika, yalikuwa ni majuto yasiyoelezeka..

Sefania 2:13 “Naye atanyosha mkono wake juu ya upande wa kaskazini, na kuiangamiza Ashuru; naye ataufanya Ninawi kuwa ukiwa, kuwa mahali pakavu kama jangwa…..

15 HUU NDIO MJI ULE WA FURAHA, ULIOKAA PASIPO KUFIKIRI, ULIOSEMA MOYONI MWAKE, MIMI NIKO, Wala hapana mwingine ila mimi. Jinsi ulivyokuwa ukiwa, Mahali pa kulala pa wanyama wa bara! Kila mtu apitaye atazomea, Na kutikisa mkono wake”.

Ezekieli 32:22 “Ashuru yuko huko, na watu wake wote jamii; makaburi yake yamzunguka; wote pia wameuawa, wameanguka kwa upanga”

Ni nini Bwana anataka tujue?

Hiyo ni kuonyesha kuwa japokuwa Mungu si mwepesi wa Hasira, lakini hasira yake inapofika kilele basi ni MWINGI WA HASIRA..yaani haipoi kwa haraka, inadumu milele kama sio kwa kipindi kirefu sana..

Na ndio maana leo hii watu wengi wanaposoma yale mapigo yaliyoandikwa kwenye kitabu cha ufunuo wanaona kama hayafikirikiki kwa akili za kibinadamu, ni kweli unaweza kudhani hivyo lakini ndugu yale mapigo unavyoyaona pale ndivyo yatakavyokuwa.. Ziwa la moto unavyolisikia ndivyo lilivyo. Ukienda kule, hutatamani hata adui yako afike huko kwa mateso yaliyo kule yasiyoelezeka.. “Mungu si mwepesi wa hasira, lakini ni mwingi wa hasira”

Kama leo unalikataa Neno lake, na unaona hakuna chochote kinachotokea au kitakachoweza kutokea juu yako, pengine Mungu amekuambia utubu mara nyingi, lakini unafanya hivyo leo, kesho unarudia mambo yale yale ya kidunia.. Upo wakati utafananishwa na Ninawi..Utakatwa na kupotea moja kwa moja, wakati huo ukifika hata uombeje, hata ulieje, hakuna rehema tena juu yako.

Mambo haya sio uongo!..yaliwatokea watu wa Ninawi kama yalivyo..kasome katika Historia baada ya kukataa maonyo, na pia yaliwatokea wana wa Israeli vile vile kwa kukataa maonyo, na hata kusababisha Mungu kukataa kuwasamehe. Soma mistari ifuatayo utathibitisha..

2Nyakati 36: 15 “Naye Bwana, Mungu wa baba zao, akatuma kwao kwa mikono ya wajumbe wake, akiondoka mapema, na kutuma; kwa sababu aliwahurumia watu wake, na makao yake;

16 lakini waliwadhihaki wajumbe wa Mungu, na kuyadharau maneno yake, na kuwacheka manabii wake, hata ilipozidi ghadhabu ya Bwana juu ya watu wake, hata kusiwe na kuponya.

17 Kwa hiyo akaleta juu yao mfalme wa Wakaldayo, aliyewaua vijana wao kwa upanga nyumbani mwa patakatifu pao, asiwahurumie kijana wala mwanamwali, mzee wala mkongwe; akawatia wote mkononi mwake”.

Mathayo 3:10 “Na shoka limekwisha kuwekwa penye mashina ya miti; basi kila mti usiozaa matunda mazuri hukatwa na kutupwa motoni”.

Kama hujampokea Yesu, fanya hivyo sasa..

Bwana akubariki.

Maran Atha.

Tafadhali washirikishe na wengine habari hizi njema, na pia kama utapenda tuwe tunakutumia masomo haya kwa njia ya email yako au Whatsapp tutumie ujumbe kwenye box la maoni chini au piga namba hii +255 789001312


Mada Nyinginezo:

AMELAANIWA AANGIKWAYE MSALABANI.

YONA: Mlango wa 4

JE KUVAA PETE NI DHAMBI?

JE! KUBET NI DHAMBI?

HAPANA HATA MMOJA ATAKAYEIONJA KARAMU YANGU.

Rudi Nyumbani:

Print this post

About the author

Admin administrator

Subscribe
Notify of
guest
0 Comments
Inline Feedbacks
View all comments