MAJARIBU MATATU YA YESU KRISTO

by Admin | 17 July 2018 08:46 pm07

Majaribu matatu Yesu aliyojaribiwa na shetani akiwa njikani siku 40, yanaweza yakachukuliwa kivyepesi lakini ukiyachunguza kwa undani yana tafsiri kubwa sana na maana kubwa sana katika maisha ya kila mkristo akiwapo hapa duniani, na yanahitaji uongozo wa Roho Mtakatifu kuyaelewa yale majaribu yana maana gani kama yalivyoandikwa pale. 

Wengi wetu tunafikiri kuwa Yesu alipandishwa nyikani siku 40, kujaribiwa na ibilisi, na alipomaliza kujaribiwa alirejea katika maisha yake ya kawaida halafu basi yaliishia pale. Watu pia wanafikiria kuwa shetani alimtokea Yesu kwa mfano wa nyoka au vinginevyo na kuanza kumjaribu kumpa yale majaribu matatu.

Lakini hiyo sio kweli dhumuni kuu la Yesu kupandishwa nyikani ni kwenda kukutana na Mungu wake kwa dhumuni la kupokea maagizo fulani au ufunuo fulani, Tunaona sehemu fulani kristo aliwaambia wanafunzi wake mwenyewe Mathayo 17:21  [Lakini namna hii haitoki ila kwa kusali na kufunga.] Yesu Kristo hakuongozwa na Roho na kufunga siku 40 nyikani kwenda kukutana na shetani hapana bali ni kwenda kukutana na Mungu wake.

Tunaweza tukaona mfano mwingine kama Musa alivyoitwa na Mungu mlimani kwenda kuchukua zile amri 10, alifunga siku 40 usiku na mchana, na alikuja kufunga tena siku nyingine  40 mchana na usiku kuwaombea wana wa israeli kwa makosa waliyoyafanya ya kuabudu sanamu. Kwahiyo Bwana Yesu Kristo kufunga nyikani siku 40 ilikuwa ni kwa ajili ya huduma yake iliyokuwa inakaribia kwenda kuanza, ndipo huko Mungu alipomfunulia huduma yake itakavyokuwa pamoja na yale majaribu makuu matatu atakayokutana nayo katika maisha yake ya huduma.

JARIBU LA KWANZA:

Tunasoma katika luka 4:1-4 “1 Na Yesu, hali amejaa Roho Mtakatifu, alirudi kutoka Yordani, akaongozwa na Roho muda wa siku arobaini nyikani,
2 akijaribiwa na Ibilisi. Na siku hizo alikuwa hali kitu; hata zilipotimia, aliona njaa.
3 Ibilisi akamwambia, Ukiwa ndiwe Mwana wa Mungu, liambie jiwe hili liwe mkate.
4 Yesu akamjibu, Imeandikwa ya kwamba mtu hataishi kwa mkate tu.”

Hapa tunaona Bwana Yesu baada ya siku 40 kuisha aliona njaa na alipoona njaa akiwa kama mwanadamu alitamani chakula, lakini safari yake ya nyikani ilikuwa bado haijakwisha kwahiyo shetani alipoona kuwa huyu mtu anauhitaji wa chakula alimletea ushawishi moyoni wa kugeuza  jiwe kuwa mkate kwasababu alifahamu kuwa anaweza kufanya hivyo.

Sasa hapa inadhaniwa kuwa shetani alimtokea akamwambia hivyo la! hakumtokea bali alimletea ushawishi moyoni kufanya vile, biblia inasema mtu anajaribiwa kwa tamaa zake mwenyewe,(yakobo 1:14 ). Yesu kama asingeona njaa asingejaribiwa, njaa ilipokuja shetani naye akapata nafasi lakini pamoja na hayo Bwana alishinda kwa kuwa aliyajua maneno ya Baba yake kuwa “mtu hataishi kwa mkate tu bali kwa kila neno litakalotoka katika kinywa cha Mungu”, aliona sio vema kuyakatiza mapenzi ya Mungu kwa sababu ya chakula, alitambua kuwa ni Mungu ndiye aliyempeleka kule kwa hiyo hata kama siku za kukaa kule nyikani zingeongezeka mpaka kufikia 60,au 70 au 100. angeendelea kuishi kwasababu anaishi kwa neno linalotoka katika kinywa cha baba yake na sio kwa chakula cha mwilini tu. Kwahiyo tunaweza kuona Yesu Kristo aliweza kushinda kwa namna hiyo.

Lakini jaribu hili sio kwamba liliishia pale nyikani tu, ule ulikuwa kwake ni kama ufunuo wa mambo atakayokwenda kukutana nayo mbeleni katika huduma yake, Mungu alimuonyesha  ni moja ya jaribu kuu ambalo shetani atampelekea katika maisha yake ya huduma.

Maana ya kugeuza jiwe kuwa mkate ni ipi?
kugeuza jiwe kuwa mkate inatokea pale mtu anayopitia hali ya uhitaji au shida ya kitu fulani na anafahamu kuwa ni Mungu ndiye aliyempitisha katika hiyo hali, lakini yeye anatafuta njia mbadala ya kujing’amua na hiyo shida angali iko katika uwezo wako wa kufanya hivyo, mfano Yesu Kristo alitambua kuwa anapitia katika hali ya taabu na alikuwa na uwezo wa kugeuza lile jiwe kuwa mkate lakini hakufanya vile kwasababu alijua kuwa angeenda nje ya mapenzi ya Mungu sio kana kwamba hakuwa na njaa au alikuwa anajinyima au hakuweza kufanya la! bali alijinyenyekeza chini ya Mungu katika hali ngumu aliyokuwa nayo..

Tunaona jaribu kama hili liliwapata  wana wa Israeli  lakini walilishindwa pale walipopitishwa miaka 40 nyikani wakaanza kumnung’unikia Mungu wakitaka watimiziwe matakwa yao wenyewe na sio matakwa ya Mungu. Tunaona katika hali ngumu waliyokuwa nayo nyikani ukafikia wakati wakasikia njaa kama Yesu Kristo alivyosikia njaa, na kwajinsi  Yesu alivyokuwa na uwezo wa kubadilisha jiwe kuwa mkate vivyo hivyo na wao pia walikuwa na uwezo huo huo wa kubadilisha jiwe kuwa mkate mfano huu tunawaona badala ya kujinyenyekeza chini ya mapenzi ya Mungu wakaanza kumnung’unikia Mungu wakitaka nyama nyikani na Mungu aliwapa nyama, alikuwa akiwapa chochote walichokuwa wanakihitaji(huku ndio kugeuza jiwe kuwa mkate)..

Kumbuka wana wa israeli walikuwa wanajua kuwa lolote watakalomwomba Mungu atawapa kama vile Yesu alivyojua kuwa lolote atakalomwomba Baba yake atampa,  tunaona wana wa israeli walikuwa wanashushiwa mana kule jangwani kwa hiyo wakatumia kigezo hicho kwa tamaa zao kutaka vitu ambavyo sio sawasawa na mapenzi ya Mungu kwa kisingizio kuwa wanasikia njaa lakini hawajui kuwa shetani ameshawashinda kwa kutoweza kulishinda hilo jaribu.

 kumbukumbu 8:1-5″Amri hii ninayokuamuru leo mtaishika kuitenda, mpate kuishi na kuongezeka, na kuingia katika nchi ile ambayo Bwana aliwaapia baba zenu; nanyi mtaimiliki.
2 Nawe utaikumbuka njia ile yote Bwana, Mungu wako aliyokuongoza miaka hii arobaini katika jangwa, ili akutweze, kukujaribu kuyajua yaliyo moyoni mwako, kwamba utashika amri zake, au sivyo.
3 Akakutweza, akakuacha uone njaa, akakulisha kwa mana, usiyoijua wewe wala baba zako hawakuijua; apate kukujulisha ya kuwa mwanadamu haishi kwa mkate tu, bali huishi kwa kila litokalo katika kinywa cha Bwana.
4 Mavazi yako hayakuchakaa, wala mguu wako haukuvimba, miaka hiyo arobaini.
5 Nawe fikiri moyoni mwako, ya kuwa kama vile baba amrudivyo mwanawe, ndivyo Bwana, Mungu wako, akurudivyo.”

Vivyo hivyo kristo katika huduma yake ambayo Mungu alikuwa akimtuma alijifunza kutokutazama vitu vya nje kama mali,chakula, mavazi hakujali hata sehemu ya kulala japokuwa alikuwa na uwezo wa kupata mali, kula na kunywa, na sehemu za kulala kwasababu alihesabu kutenda mapenzi ya Mungu kwanza ni bora kuliko njaa ya vitu vya nje 

yohana 4:30-34 Basi wakatoka mjini, wakamwendea.
31 Huko nyuma wanafunzi wakamsihi wakisema, Rabi, ule.
32 Akawaambia, Mimi ninacho chakula msichokijua ninyi.
33 Basi wanafunzi wake wakasemezana, Je! Mtu amemletea chakula?
34 Yesu akawaambia, Chakula changu ndicho hiki, niyatende mapenzi yake aliyenipeleka, nikaimalize kazi yake.”

 Kwahiyo alifahamu eneo shetani atakalomtesea katika maisha yake ya huduma ni hapo kwenye njaa ya mambo ya nje, lakini kwa kujua ufunuo huo alikuja kuweza kuyashinda yote. Na ndio maana aliwaambia mahali fulani wanafunzi wake

 mathayo 6:26″ Kwa sababu hiyo nawaambieni, Msisumbukie maisha yenu, mle nini au mnywe nini; wala miili yenu, mvae nini. Maisha je! Si zaidi ya chakula, na mwili zaidi ya mavazi?
26 Waangalieni ndege wa angani, ya kwamba hawapandi, wala hawavuni, wala hawakusanyi ghalani; na Baba yenu wa mbinguni huwalisha hao. Ninyi je! Si bora kupita hao? ” aleluya!!

Jambo hili hili linajirudia kwa Mkristo anayesema ameamua kumtumikia Mungu, kumbuka haya majaribu matatu kila mkristo lazima ayapitie na hakuna majaribu makubwa zaidi ya hayo shetani anaweza akamjaribu mtu, vivyo hivyo kwa mkristo aliyeamua kumtumikia Mungu atambue kuwa ni lazima akutane na hili jaribu, pale shetani anapokuona upo karibu na Mungu wako sana na upo katika hali ya nyikani(kumbuka nyikani ndipo Mungu anaposhushia mana, na nyikani ni sehemu yoyote isiyokuwa na tumaini lolote,

Inawezekana katika maisha sana sana katika safari ya wokovu mtu anapoanza kumwangalia Kristo) hapo ndipo shetani analeta ushawishi kama huo alioupata Bwana ili uache njia yako, anatumia Neno kukufanya wewe utimize tamaa yako ambayo sio sawasawa na mapenzi ya Mungu, atakwambia fanya hivi au fanya vile ili uishi vizuri ndipo umtumikie Mungu, atakwambia acha hicho unachokifanya fanya kwanza hichi ujikwamue kimaisha..

Atakwambia sasa tafuta kwanza maisha ndipo uje kumtumikia Mungu baadaye, tafuta pesa kwanza maana unashida ya pesa sasa hivi halafu Mungu utamtafuta baadaye, atakwambia jiweke vizuri kiuchumi kisha utaenda baadaye kuhubiri injili, atakwambia huoni watumishi wote wanafanya hivyo,?? na atakupa sababu zote kwamba una uwezo wa kufanya hayo yote na ni kweli ukiangalia unao huo uwezo lakini nia yake yeye sio wewe kuyakidhi mahitaji yako bali ni kukufanya utoke katika kusudi la Mungu la kumtazama yeye, anakufanya usilifahamu neno la “mtu hataishi kwa mkate tu,”

kwahiyo anatumia tamaa zako kukufanya uende kinyume na mapenzi ya Mungu. kumbuku wana wa israeli walivyokuwa Mungu kuwapitisha nyikani ilikuwa sio kwenda kuwakomoa, lakini wangejuaje kama Mungu anaweza kuwalisha pasipo kazi ya mikono? wangelifahamu vipi hilo neno la MTU HATAISHI KWA MKATE TU ?? kama wasingepitishwa nyikani. unaona ni kusudi kabisa la Mungu kumpitisha mtoto wake nyikani ili ajifunze kumtegemea lakini shetani anavumbua njia mbadala kumchonganisha na Mungu haya ndiyo yaliyowakuta wana wa Israeli.

Jambo hili hili linawatokea wakristo wengi wanapopitishwa nyikani(kumbuka kila mkristo lazima apitishwe nyikani) wanashindwa na hili jaribu la shetani wanashindwa kufahamu kuwa mtu hataishi kwa mkate tu bali kwa kila neno litakalotoka katika kinywa cha Mungu, mtu hataishi kwa pesa tu, mtu hataishi kwa kazi tu, mtu hataishi kwa mifumo tuliyoizoea tu, mtu hataishi kwa gari na nyumba tu, mtu hataishi kwa umaarufu wala chochote cha ulimwengu huu, bali mtu ataishi kwa neno la Mungu tu!! Mungu ni zaidi ya mali na kila kitu Kristo anasema .

(Mathayo16:25-26..”Kwa kuwa mtu atakaye kuiokoa nafsi yake, ataipoteza; na mtu atakayepoteza nafsi yake kwa ajili yangu, ataiona.

26 Kwani atafaidiwa nini mtu akiupata ulimwengu wote, na kupata hasara ya nafsi yake? Au mtu atatoa nini badala ya nafsi yake? ).

kila siku unasema ngoja nisubirie kidogo, nisubirie kwanza nifanye kitu fulani nikishakipata ndipo nianze kumtafuta Mungu, mwingine yupo katika taabu anasema ngoja kwanza nitafute pesa nitoke katika hii tabu ndipo nianze kumtafuta Mungu huko ndiko kugeuza jiwe kuwa mkate, unadhania kuwa mtu ataishi kwa pesa tu pasipo pesa huwezi kuishi(wana wa israel hawakuwa na fedha lakini walilishwa miaka 40 jangwani), unasema pasipo nyumba huwezi kuishi(yesu alilala milimani ambaye ndiye tunayemwita Bwana wetu na mfalme wetu),

 Yesu alisema

mathayo 6:31-34″ Msisumbuke, basi, mkisema, Tule nini? Au Tunywe nini? Au Tuvae nini?

32 Kwa maana hayo yote Mataifa huyatafuta; kwa sababu Baba yenu wa mbinguni anajua ya kuwa mnahitaji hayo yote.

33 Bali utafuteni kwanza ufalme wake, na haki yake; na hayo yote mtazidishiwa.

34 Basi msisumbukie ya kesho; kwa kuwa kesho itajisumbukia yenyewe. Yatosha kwa siku maovu yake.” 

Na pia Yesu alisema chakula changu ni kuyatenda mapenzi ya baba yangu (yohana 4:34) vivyo hivyo na sisi tuseme hivyo chakula chetu ni kuyatenda mapenzi ya baba yetu na kuyamaliza. Tusigeuze jiwe(vitu visivyo na uhai)  kuwa mkate. Mungu anapotuita tuwe tayari kutii na kusema ndio pasipo kuangalia mambo mengine ya kando kando, kwa kufanya hivyo ndivyo tutakavyoshinda hilo jaribu la mkate vinginevyo hatutaweza.

JARIBU LA PILI:

Luka 4:5-6″  Akampandisha juu, akamwonyesha milki zote za ulimwengu kwa dakika moja.
6 Ibilisi akamwambia, Nitakupa wewe enzi hii yote, na fahari yake, kwa kuwa imo mikononi mwangu, nami humpa ye yote kama nipendavyo.

7 Yesu akajibu akamwambia, Imeandikwa, Msujudie Bwana Mungu wako, umwabudu yeye peke yake. “

Kwenye Jaribu hili tunaona Kristo akihamishwa kutoka nyikani mpaka kwenye milki zote za ulimwengu akaonyeshwa fahari zote za ulimwengu. Hapa sio shetani alimchukua katika mwili bali ni alichukuliwa na Mungu katika maono kuonyeshwa lile jaribu la shetani litakavyokuwa katika maisha yake ya huduma”. Kwa namna ya kawaida ni vigumu adui yako akuambie nisujudie halafu nitakupa vitu vyote, unafahamu kabisa huwezi kumsujudia kwasababu unajua kabisa anakujaribu kwahiyo ni wazi kabisa shetani hakumtokea Yesu bali ni Mungu ndiye aliyemwonyesha yale maono, na hili jambo lilikuja kutimia katika maisha yake kule mbeleni pale huduma yake ilipoanza kuwa kubwa, alipojulikana kila mahali na watu wote mfano huu tunaona alipokwenda Samaria wale watu wa ule mji walitaka kumshika na kumfanya mfalme

(Yohana 6:14-15 “Basi watu wale, walipoiona ishara aliyoifanya, walisema, Hakika huyu ni nabii yule ajaye ulimwenguni.

15 Kisha Yesu, hali akitambua ya kuwa walitaka kuja kumshika ili wamfanye mfalme, akajitenga, akaenda tena mlimani yeye peke yake. “)

 Jaribu kufikiria leo hii kama Bwana Yesu angekuwa mfalme wa wasamaria msalaba tungeujulia wapi, kwahiyo tunaliona hilo ni jaribu shetani alilomletea lakini alikumbuka alionyeshwa na baba yake akiwa jangwani, ya kwamba utamsujudia Bwana Mungu wako yeye peke yake, sasa kusujudia pale sio kwenda kumpigia magoti shetani bali ni kukubaliana na jambo lolote shetani atakalokuletea mbele yako kinyume cha mapenzi ya Mungu, tunaona hata leo hii watu wanamsujudia shetani pasipo hata wao kujua pale wanapotenda dhambi, unadhani shetani angemtokea mtu na kumwambia nisujudie nani angekubali?? yeye siku zote anatumia hila kuabudiwa anamfanya mtu adhani kuwa anamwabudu Mungu kumbe anamwabudu shetani.

Vivyo hivyo shetani alivyokuwa anajaribu kufanya kwa Bwana Yesu Kristo kwa kutaka kusujudiwa kwa kupitia ufahari,lakini Kristo alishinda, aliona ni vyema kuiendea njia ya msalaba aliyowekewa na baba yake kuliko kukubali sifa na heshima na vyeo na ukuu na ufalme kutoka kwa watu.Lakini leo hii angeonekana ni mtu anayechezea bahati.

Vivyo hivyo jaribu hili pia linawakuta wakristo sana sana watumishi wa Mungu walio katika huduma, mwanzoni wataanza vizuri katika huduma na Mungu atatembea nao lakini shetani anapoona hivyo ili kumwaribu anamletea jaribu kama hili lililomkuta Bwana Yesu, anaanza kwa kumpa umaarufu wa ghafla, watu watakuja kumwambia njoo uwe kiongozi wetu tutakupa pesa, nyumba, magari, tutakufanya kuwa maarufu kushinda hapo ulipo, tutaikuza huduma yako zaidi ya hapo ilipo, ila acha tu huo mtindo wako wa kale wa kuhubiri, punguza ukali wa maneno tutakupa kila kitu, we hubiri tu kama sisi tunavyohubiri, wengine wanaitwa na wanasiasa wawasaidie katika siasa zao na wanaahidiwa kupewa pesa nyingi.

Kwahiyo mtu huyu badala ya kukaa chini na kutafakari kama huduma yake itaathirika au la! yeye anakubali bila kufahamu kuwa hizo ni hadaa za shetani kutaka asujudiwe. Na watumishi wengi wa Mungu wameshindwa hili jaribu wameacha kusudi lao la kufundisha, na kuiendea njia ya msalaba, wakaiendea njia ya watu wa mataifa ili kupata umaarufu na heshima. luka 6:26″  Ole wenu ninyi watu wote watakapowasifu, kwa kuwa baba zao waliwatenda manabii wa uongo mambo kama hayo. “

JARIBU LA TATU:

Luka 4:9-12″ Akamwongoza mpaka Yerusalemu, akamweka juu ya kinara cha hekalu, akamwambia, Ukiwa ndiwe Mwana wa Mungu, jitupe chini;
10 kwa maana imeandikwa, Atakuagizia malaika zake wakulinde;
11 na ya kwamba,mikononi mwao watakuchukua, Usije ukajikwaa mguu wako katika jiwe.
12 Yesu akajibu akamwambia, Imenenwa, Usimjaribu Bwana Mungu wako. “

Katika jaribu la tatu tunaona Yesu Kristo akipelekwa katika kinara cha hekalu, unaweza ukajiuliza kwa nini alipelekwa Yerusalemu, na ni kwanini kwenye kinara cha hekalu na sio penginepo?

Ono hili alipewa kuonyeshwa mwisho wa safari yake ya huduma, kwamba mwishoni atawekwa kwenye kinara cha hekalu ambacho ni msalaba, Yesu Kristo safari yake ya mwisho ilikuwa ni msalabani(hata sio ajabu kuyaona makanisa yakiwa na msalaba juu, hii inaleta picha kuwa pale juu ya kinara cha hekalu alipowekwa Yesu ni msalabani) na kumbuka hata pale msalabani shetani alikuwa akimjaribu kwa maneno hayohayo kama tunayoyaona hapo juu, shetani alimwambia kipitia vinywa vya wale watu

 Mathayo 27: 39-44″ Nao waliokuwa wakipita njiani wakamtukana, wakitikisa-tikisa vichwa vyao, wakisema,
40 Ewe mwenye kulivunja hekalu na kulijenga kwa siku tatu, jiokoe nafsi yako; ukiwa ndiwe Mwana wa Mungu, shuka msalabani.
41 Kadhalika na wale wakuu wa makuhani wakamdhihaki pamoja na waandishi na wazee, wakisema, Aliokoa wengine, hawezi kujiokoa mwenyewe.
42 Yeye ni mfalme wa Israeli; na ashuke sasa msalabani, nasi tutamwamini.
43 Amemtegemea Mungu; na amwokoe sasa, kama anamtaka; kwa maana alisema, Mimi ni Mwana wa Mungu.
44 Pia wale wanyang’anyi waliosulibiwa pamoja naye walimshutumu vile vile. “

 Lakini kama Bwana Yesu Kristo asingetambua hayo majaribu ambayo alionyeshwa na baba yake akiwa nyikani angejishusha chini msalabani na watu wote wangeamini kwasababu alikuwa anao huo uwezo, picha hii hii tunaiona pale usiku ule walipokuja kumshika Yesu na petro alipotaka kumwokoa Bwana  alimwambia (mathayo 26:52-54 ”

Ndipo Yesu akamwambia, Rudisha upanga wako mahali pake, maana wote waushikao upanga, wataangamia kwa upanga. Ama wadhani ya kuwa mimi siwezi kumsihi Baba yangu, naye ataniletea sasa hivi zaidi ya majeshi kumi na mawili ya malaika? Yatatimizwaje basi maandiko, ya kwamba hivyo ndivyo vilivyopasa kujiri?” ) Kwahiyo tunaona Yesu Kristo alikuwa ana huo uwezo wa kujishusha msalabani lakini je! angejishusha msalabani mapenzi ya baba yangetimizwaje? na sisi tungepataje wokovu?.

Vivyo hivyo na kwa mkristo yeyote anayeipenda njia ya msalaba(japo sio wote watakayoipitia ) jaribu kama hili atakutana nalo ndilo la mwisho kumbuka shetani hatakuacha hata katika dakika ya mwisho ya wewe kukata roho atakuwa karibu yako kukufanya uanguke. Msalaba ndio hatua yetu ya mwisho, Yesu alisema mimi ndimi njia na kweli na uzima mtu haji kwa baba isipokuwa kwa njia ya mimi, njia hapo anayoizungumzia ni maisha yake yeye sasa tunayaamishia kwetu, na alisema pia mtumwa sio mkuu kuliko Bwana wake, kama yeye walimwita belzebuli, mwenye pepo, alienda msalabani kufa kifo cha aibu je! inatupasaje sisi? hatupaswi kuionea haya njia ya msalaba, watazame mitume na manabii na wakristo wa kale kwa kuitetea kweli na kuisimamia kweli hawakupenda maisha yao hata kufa, walihesabu kuwa utukufu wa Mungu ni bora kuliko utukufu wa wanadamu, Kristo alisema mtu yeyote akitaka kunifuata ajikane nafsi yake, ajitwike msalaba wake anifuatae kila siku (mathayo 16:24),na unajua msalaba ni nini?, mwisho wake ni golgotha. 

Kwahiyo utakapofikia katika jaribu la tatu na la mwisho ambalo shetani atakuacha ni pale utakapoona unaenda kutiwa mikononi mwa shetani kama Yesu Kristo na  mitume na manabii. walivyofanyiwa, angali una uwezo wa kujiepusha nalo kama Yesu tunaweza kuona shetani alimvaa hata Petro akijaribu kumshawishi Yesu asiipitie njia ya msalaba, lakini Yesu alimwambia nenda nyuma yangu shetani huyawazi ya Mungu bali ya wanadamu, lakini Yesu alijinyenyekeza kama kondoo aendaye kuchinjwa na ndivyo walivyofanya mitume watu wa Mungu kama stephano, yohana n.k huko ndiko kulishinda hilo jaribu( na kumalizia kusema Baba wasamehe kwa kuwa hawajui watendalo).

Yesu Kristo anasema

(ufunuo 3:20-22″ Tazama, nasimama mlangoni, nabisha; mtu akiisikia sauti yangu, na kuufungua mlango, nitaingia kwake, nami nitakula pamoja naye, na yeye pamoja nami.
21 Yeye ashindaye, nitampa kuketi pamoja nami katika kiti changu cha enzi, kama mimi nilivyoshinda nikaketi pamoja na Baba yangu katika kiti chake cha enzi.
22 Yeye aliye na sikio, na alisikie neno hili ambalo Roho ayaambia makanisa. ). kwahiyo kushinda ni nini?? kushinda ni kule kushinda yale majaribu matatu kama Bwana Yesu alivyoyashinda.”

Sio kwamba usipopitia hiyo njia itakufanya usiende mbinguni la! Labda utaenda lakini utakuwa hujashinda kwasababu hujapigana kikamilifu, thawabu yako itapunguzwa kama utashindwa na majaribu hayo ya shetani, 

1wakorintho 9:24″ Je! Hamjui, ya kuwa wale washindanao kwa kupiga mbio, hupiga mbio wote, lakini apokeaye tuzo ni mmoja? Pigeni mbio namna hiyo, ili mpate.

25 Na kila ashindanaye katika michezo hujizuia katika yote; basi hao hufanya hivyo kusudi wapokee taji iharibikayo; bali sisi tupokee taji isiyoharibika.

26 Hata mimi napiga mbio vivyo hivyo, si kama asitaye; napigana ngumi vivyo hivyo, si kama apigaye hewa;

27 bali nautesa mwili wangu na kuutumikisha; isiwe, nikiisha kuwahubiri wengine, mwenyewe niwe mtu wa kukataliwa.

Na pia mtume Paulo anasema,

 2timotheo 2:5″4 Hakuna apigaye vita ajitiaye katika shughuli za dunia, ili ampendeze yeye aliyemwandika awe askari.

5 Hata mtu akishindana katika machezo hapewi taji, asiposhindana kwa halali. “

mtume Paulo pia aliandika..

wafilipi 3:10-14″10 ili nimjue yeye, na uweza wa kufufuka kwake, na ushirika wa mateso yake, nikifananishwa na kufa kwake;

11 ili nipate kwa njia yo yote kuifikia kiyama ya wafu.

12 Si kwamba nimekwisha kufika, au nimekwisha kuwa mkamilifu; la! Bali nakaza mwendo ili nipate kulishika lile ambalo kwa ajili yake nimeshikwa na Kristo Yesu.

13 Ndugu, sijidhanii nafsi yangu kwamba nimekwisha kushika; ila natenda neno moja tu; nikiyasahau yaliyo nyuma, nikiyachuchumilia yaliyo mbele;

14 nakaza mwendo, niifikilie mede ya thawabu ya mwito mkuu wa Mungu katika Kristo Yesu. “

mwisho mtume Paulo aliandika 

2timotheo 4:6-8″ Kwa maana, mimi sasa namiminwa, na wakati wa kufariki kwangu umefika.

7 Nimevipiga vita vilivyo vizuri, mwendo nimeumaliza, Imani nimeilinda;

8 baada ya hayo nimewekewa taji ya haki, ambayo Bwana, mhukumu mwenye haki, atanipa siku ile; wala si mimi tu, bali na watu wote pia waliopenda kufunuliwa kwake. “

Mungu akubariki sana ndugu yetu mpendwa.

Pia unaweza ukapata mafundisho haya Kwa njia ya Whatsapp yako, jiunge na channel yetu Kwa kubofya hapa >> WHATSAPP


Mada Nyinginezo:

NI KWA NAMNA GANI TUTASHINDA MAJARIBU?

JE! DAMU INA UMUHIMU WOWOTE KATIKA MAISHA??

ZIFAHAMU NYAKATI SABA ZA KANISA NA WAJUMBE WAKE SABA

KWANINI KUNA WATU WANAFANYIWA DELIVERANCE (MAOMBI YA KUFUNGULIWA), LAKINI BAADA YA MUDA WANARUDIWA TENA NA HALI ILE ILE SABABU NI NINI?


Rudi Nyumbani

DOWNLOAD PDF
WhatsApp

Source URL: https://wingulamashahidi.org/2018/07/17/majaribu-matatu-ya-yesu-kristo/