LENGO LA SHETANI KWA WATOTO WA KIZAZI HIKI.

by Admin | 11 September 2018 08:46 am09

Hekima ya dunia hii inasema “Samaki mkunje, angali mbichi”, Hii ikiwa na maana kuwa Samaki akisha kauka hawezi kukunjika tena, ukijaribu kufanya hivyo atavunjika, Na ndivyo ilivyo kwa watoto wetu, Hekima ya Neno la Mungu pia inatumbia, Mithali 22: 6 “Mlee mtoto katika njia impasayo, Naye hataiacha, hata atakapokuwa mzee”.

Neno hili kinyume chake ni kweli mtoto asipolelewa katika njia impasayo, hataiacha hiyo njia mbovu hata atakapokuwa mzee. Hivyo Mungu yupo hapo sana katika kuhakikisha hatma yake inakuwa salama kadhalika na shetani naye yupo hapo kutaka kuharibu hatma ya maisha ya mtoto yule angali ni mchanga. Hivyo nguvu ya ziada inahitajika katika kutengeneza maisha ya mtu katika utoto wake kuliko katika utu uzima.

Tunafahamu kabisa dunia ya sasa sio kama ile ya zamani, mambo maovu yaliyopo leo ni mengi kuliko yale ya zamani, ngoja nikupe kisa changu mwenyewe ambacho ni mfano hai kabisa ya mambo yanayoendelea katika ulimwengu wa watoto: 

Nakumbuka tulipokuwa watoto (mimi na ndugu yangu), ilikuwa ni kati ya umri wa miaka 4-7 hivi, kuna vitu vilikuwa tunaviona vinaendelea katika mazingira yaliyokuwa yanatuzunguka, nyumbani kulikuwa na tv, na kwa kipindi hicho cha zamani kidogo, nyimbo za Michael Jackson, na nyimbo za kikongo ndizo zilikuwa zinavuma sana, hivyo ilikuwa ni ngumu kwenda katika nyumba yoyote yenye TV na kukosa mkanda wa (VHS) wa hizo nyimbo, Cha ajabu tulikuwa tunaona watu wazima wanaangalia na kufurahia lakini sisi tulikuwa tunaogopa kwamfano kama ulishawahi kutazama video za Michael Jackson nyingi zilikuwa na maudhui ya kutisha tisha tu, mara utaona anajigeuza kuwa mchanga, mara yupo makaburini,n.k. Sasa yale mambo watu wazima walikuwa wanaona ni kawaida tu, lakini sisi ilikuwa inatuathiri ndani kwa ndani na hauwezi ukasema kwasababu wewe ni mtoto na hujui maana ya hayo mambo, mpaka ilifikia kipindi vile vitu tulivyokuwa tunaviona kwenye TV vikaanza kujidhihirisha nje, tukaanza kuviona wazi wazi.

Tulikuwa tunaviona sana sana wakati wa usiku tunashutuka, na kuona vijiwatu vidogo vidogo vinafungua milango ya jiko, wanaingia na kuanza kucheza mbele yetu kama wale wale tuliokuwa tunawaona wanaocheza kwenye TV, ni wale wale tu isipokuwa hapa tunawaona dhahiri. Na mfano mtu mzima akijaribu kuingia ndani kwa ghafla vilikuwa vinakimbia na kujificha. Vilikuwa vinajidhihirisha kwetu tu, (kumbuka hizo sio ndoto au imagination, ni vitu dhahiri kabisa tulikuwa tunaviona, kwasababu wote wawili tulikuwa tunaviona, na mpaka sasahivi na utu uzima wetu tunavikumbuka) ..sasa ilifikia kipindi ilikuwa vikitokea tunaona kawaida tu, hatuoni tena ni ajabu, wala hatuviogopi, badala yake tunacheka, kumbuka wakati mambo haya yanaendelea hakuna mtu mwingine alikuwa anajua, kadhalika na vitu vingine vingi vya ajabu ajabu tulikuwa tunaviona ambavyo vilitokana na mambo tuliokuwa tunayatazama kwenye TV. Lakini mambo haya yalianza kupotea pale mzazi wetu mmoja alimpompa Bwana maisha yake.

Kadhalika mdogo wetu mmoja alituambia jambo kama hilo hilo liliwahi kumtokea alipokuwa mdogo, alikuwa anaona mtu anamtokea mwenye ngozi kama ya nyoka na kuzungumza naye usiku. Wakati huo wazazi hawaelewi chochote ni yeye tu na hilo pepo basi.

Sasa mambo hayo yalikuwa ni zamani wakati utandawazi haujawa mkubwa je! leo hii itakuwaje? Kwa watoto wa leo, siku hizi sio TV tu peke yake, kuna simu tena zenye internet, Kuna magemu, ya kila aina kwenye simu za wazazi, na kibaya zaidi magemu yenyewe ukiangalia karibu yote yanadhima za kipepo ndani yake, kwamfano, magemu kama , House of the dead, mortal combat, spiderman, Zuma, Diablo.Titan n.k.Pia Kuna magemu mengine yanakuwepo sana kwenye simu unakuta mtu analiendesha au anakimbizwa na limnyama fulani la ajabu kutoka pangoni , na yeye anajaribu kulikimbia,(Nadhani utakuwa unalifahamu) sasa vitu kama hivi watu waliovitengeneza hawajavibuni tu ilimradi hapana bali wamevitoa kama vilivyo katika ulimwengu wa roho wa kishetani (ni vikundi maalumu kabisa vya kishetani vinavyofanya hizi kazi), wanachofanya ni kuchukua taswira yenye uwezo wa kama hayo mapepo na kuyatengenezea magemu yanayofanana nao pamoja na kazi zao.

Kama vile tu wanavyotengeneza magemu ya mipira, utakuta aina ya mchezaji na uwezo wake ndani ya gemu ndio yuko hivyo hivyo katika ulimwengu wa kawaida duniani, kadhalika magemu yote yanayohusiana na viumbe na vitu vya ajabu ajabu vipo kweli katika ulimwengu wa roho,na kazi zao ndio hizo hizo, kukimbiza watu, kuua, kupaa, kutesa watu, kushusha watu kuzimu, kunywa damu za watu, n.k.

Sasa unakuta mtoto akitazama au akicheza magemu ya namna hiyo kidogo kidogo anaanza kuwa na ushirika na ile roho, mwisho wa siku kile kitu alichokuwa anakiona kwenye tv au gemu kinakuja kumtokea wazi, aidha kwa njia ya ndoto au dhahiri kabisa..Na kibaya zaidi mtoto hawezi kukwambia na wakati mwingine kinamwonya asikwambie, Kumbuka lile ni pepo kidogo kidogo linaanza kumpa maagizo, na uwezo wa kutenda kama lile pepo lilivyokuwa linafanya ndani ya gemu, ndio hapo unakuta mtoto anaanza kubadilika tabia anaanza kuwa mtundu, saa nyingine mtoto anafanya mambo yasiyoeleweka, anazungumza maneno yasiyoeleweka mara nyingine anakuwa na hisia ambazo unaona kabisa sio kawaida kwa mtoto kuwa nazo, unakutaa mtoto mdogo lakini anaonyesha tabia za kiutu uzima, tabia za kizinzi, mwingine anajithiri sehemu zake za siri,n.k. hii yote ni kutokana na hizo roho alizozipata kutoka katika ma- TV na Magemu,

Zipo shuhuda nyingi za namna hiyo, wazazi wanashuhudia baada ya watoto wao kwenda kufanyiwa mahojiano wanakiri kuwa vile vitu walivyokuwa wanaviona kwenye tv (cartoons,) na magemu vilikuwa vikiwatokea dhahiri, na kuwaendesha.

Hivyo wewe kama mzazi au dada, au kaka, una watoto wako au wadogo zako, unadhani unawapenda unapowawekea magemu kwenye simu, au unapowawekea programu za ajabu, unapowaruhusu watazame TV na miziki ya kidunia, unapowaruhusu watazame tamthilia na filamu zisizokuwa na misingi yoyote ya kikristo au kuelimisha, unadhani hapo umempenda mtoto? La! kinyume chake unamuharibu, biblia inasema mlee mtoto katika njia impasayo naye hataiacha hata atakapokuwa mtu mzima, mtoto anapolilia mambo hayo unatakiwa utumie nguvu pasipo hurumu tena akemewe kabisa aogope kuulizia vitu kama hivyo siku nyingine.

Kuna wazazi au walezi wengine wanaogopa na wengine hawataki kabisa kuwaadhibu watoto wao, kwa kisingizio eti tunaishi kazazi kipya kile ni cha zamani kimeshapita, watoto wa siku hizi hawapigwi wanaelekezwa tu…Huo ni uongo wa shetani, ndio inafikia hatua mpaka mtoto anamtukana mtu mzima na mzazi anamwangalia tu, anaiba na mzazi anamwangalia tu, akidhani kuwa akimwadhibu mwanaye atajisikia vibaya au atapata matatizo fulani ya kiafya,..Au ataona kama haonyeshi upendo kwa familia yake..Hivyo anaepuka kabisa kumudhi mwanae.. Lakini biblia inasema..

Mithali 22: 15 “Ujinga umefungwa ndani ya moyo wa mtoto; Lakini fimbo ya adhabu itaufukuzia mbali”.

Na pia inasema …

Mithali 23: 13 “Usimnyime mtoto wako mapigo; MAANA UKIMPIGA KWA FIMBO HATAKUFA.

14 Utampiga kwa fimbo, NA KUMWOKOA NAFSI YAKE NA KUZIMU”. .

Unaona hapo siku ile wazazi wengi watawajibika kujibu ni kwanini watoto wao wapo kuzimu, angali wasingepaswa kuwepo huko. Tunasema watoto wa siku hizi wamebadilika, lakini ki-ukweli wazazi wa siku hizi ndio waliobadiliaka, watoto ni wale wale.

Unaweza ukadhani ukimwadhibu mwanao, atakuja kukuchukia baadaye, lakini akizoeshwa hivyo atakapokuja kuwa mtu mzima, na yeye kupata akili kama wewe atakushukuru sana kwa kumlea vizuri, kwasababu ndivyo hivyo Neno la Mungu linavyosema:

Waebrania 12: 11 “Kila adhabu wakati wake haionekani kuwa kitu cha furaha, bali cha huzuni; lakini baadaye huwaletea wao waliozoezwa nayo matunda ya haki yenye amani”

Na matunda ya kumlea vizuri mwanao utakuja kuyaona mwishoni…Biblia inasema hivyo pia..Mithali 29: 17 “Mrudi mwanao naye atakustarehesha; Naam, atakufurahisha nafsi yako”

Wewe kama mzazi/mlezi anza kumjenga mwanao/mdogo wako leo katika misingi ya Kikristo, badala ya kumwacha asikilize miziki ya kidunia katika TV, anza kumfundisha kuimba tenzi za rohoni, mapambio na nyimbo za kumsifu Mungu, badala ya kumwacha aangalie Tamthilia zisizokuwa na maana anza kumfundisha hadithi za biblia (kama safari ya wana wa Israeli, hadithi za Eliya, wafalme, Yona, Danieli n.k.) kuliko kubaki kujazwa hadithi mbovu za watu wasioamini katika TV, Anza kumfundisha jinsi ya kutumia jina la YESU, mzoeshe kutumia jina la YESU kila mahali alipo, anza kumfundisha kusali, mfundishe umuhimu na madhara ya kuwa na tabia zisizofaa, mpeleke katika madarasa ya biblia ya watoto jumapili kanisani, kama watu wa dini nyingine wanafanya hivyo wewe kwanini usifanye.??..Kadhalika jenga desturi ya kuwaombea na kuwawekea mikono watoto wako mara kwa mara wewe mwenyewe na kuwatamkia maneno ya baraka.. Kwa kufanya hivyo utakuwa umeiokoa roho ya mwanao katika kizazi hiki kibaya kilichopotoka na dhidi ya roho chafu zinazozunguka kuwanasa watoto.

Ubarikiwe sana.

Pia unaweza ukapata mafundisho haya Kwa njia ya Whatsapp yako, jiunge na channel yetu Kwa kubofya hapa >> WHATSAPP

DOWNLOAD PDF
WhatsApp

Source URL: https://wingulamashahidi.org/2018/09/11/lengo-la-shetani-kwa-watoto-wa-kizazi-hiki/