MSHAHARA WA DHAMBI:

by Admin | 18 April 2019 08:46 am04

Warumi 6:23 “Kwa maana mshahara wa dhambi ni mauti; bali karama ya Mungu ni uzima wa milele katika Kristo Yesu Bwana wetu.”

Shalom Mtu wa Mungu karibu tujifunze Maneno ya Mungu wetu, kama wengi wetu tunavyojua hakuna maisha nje ya Yesu Kristo, yeye pekee ndio sababu ya sisi kuendelea kuishi leo hii hapa duniani kama tulivyo, tunaishi kwa ajili yake, na hata tukifa tunakufa kwa ajili yake..

Warumi 14: 7 “Kwa sababu hakuna mtu miongoni mwetu aishiye kwa nafsi yake, wala hakuna afaye kwa nafsi yake.

8 Kwa maana kama tukiishi, twaishi kwa Bwana, au kama tukifa, twafa kwa Bwana. Basi kama tukiishi au kama tukifa, tu mali ya Bwana.

9 Maana Kristo alikufa akawa hai tena kwa sababu hii, awamiliki waliokufa na walio hai pia.” 

Yesu Kristo pekee ndiye aliyepewa mamlaka yote ya vitu vya mbinguni na vya duniani..utasema mbona biblia inasema “shetani ndiye mungu wa ulimwengu huu”…Ndio! Shetani ni mungu wa ulimwengu huu, kwa ruksa maalumu..Amepewa mamlaka atawale kwa kitambo tu, na mamlaka hayo kapokea kutoka kwa Yesu Kristo, …lakini itafika wakati leseni yake itaisha muda..atafungwa kwa miaka 1000, kupisha utawala wa Amani wa Bwana wetu YESU KRISTO kufanya kazi hapa duniani, na baadaye atafunguliwa kidogo ili kutimiza kusudi fulani na kisha atatupwa katika lile ziwa la moto. Hivyo tunaposema anamaliki sasa ulimwengu haimaanishi anafanya lolote kwa kujiamulia hapana! Anayo mipaka akitaka kufanya jambo lazima apate kibali kutoka juu kama alivyokwenda kufanya kwa Ayubu..

Kwahiyo unaweza ukauona ukuu alionao Bwana wetu Yesu Kristo sasa…kwamba vitu vyote sasa vipo chini ya himaya yake..kakabidhiwa kila kitu, yaaani tunaposema kila kitu maana yake hakuna kilichosalia…hata wanyama wa porini, hata mimea, hata waovu, hata yule mbwa au paka, au bundi au yule fisi unayemwona kule porini, hata kuzimu na malaika wote…vyote kwasasa vipo chini yake (anavimiliki) ana uwezo wa kufanya chochote atakacho juu yao. Nimependa kulizungumza hili kwasababu wapo wachache ambao bado hawajapata Neema ya kulielewa hili kwa undani..yaani mamlaka Yesu Kristo aliyonayo sio ya kimlinganisha na kitu kingine chochote.

Alisema katika Mathayo 28: 18 “Yesu akaja kwao, akasema nao, akawaambia, Nimepewa mamlaka yote mbinguni na duniani”.

Lakini leo kwa Neema za Bwana..hatutaingia sana huko, bali tutajifunza juu ya MSHAHARA WA DHAMBI.

Siku moja nilikuwa napita mahali Fulani mahali walipokuwa wanauza mahindi karibu na mashine ya kusaga..sasa pembezoni mwa mtaro nikaona baadhi ya punje za mahindi zimeanguka na nyingine zilikuwa zimeshaanza kumea. Nikajiuliza kwa nini zile mbegu zimeota pale na wakati hakuna mtu aliyekusudia kuzipanda pale? Wakati natafakari hilo kitu kikaingia ndani mwangu na nijikuta ninasema…”hakika apandacho mtu ndicho atakachovuna kama watu wanavyosema”…haijalishi hiyo mbegu ilipandwa kwa makusudi au kwa bahati mbaya, kwa kujua au kwa kutokujua lakini mwisho wa siku kile kilichopandwa kitamea tu..

Wengi wetu tunafikiri mkulima ni Yule tu aliyetoka na mbegu zake nyumbani na kwenda kuzipanda shambani..lakini ni zaidi ya hapo, mkulima ni hata Yule aliyeangusha mbegu njiani pasipo yeye kujijua na ikamea…Naye pia anastahili kupata malipo ya kazi yake..Ni majibu ya Mungu kwa kile alichokipanda…hata kama alikuwa hajui..Mungu ameshamjibu! Ndio maana ile mbegu ikamea hata kama alikuwa hajui.

Hali Kadhalika na sisi katika maisha yetu..Yapo mambo mengi tunayapanda ambayo aidha kwa kujua au kwa kutokujua..hiyo haizuii chochote ni lazima yalete majibu. Ukipanda mbegu njema utavuna mema…na ukipanda mbegu mbaya utavuna hizo hizo..

Ukitenda dhambi kwa kutokujua kuwa umetenda dhambi au ukitenda dhambi kwa kujua…zote mbili zinaleta matokeo yanayofanana…na matokeo yenyewe ni mauti…kwasababu biblia inasema mshahara wa dhambi ni mauti. Ni sawa na mtu aliyepanda mbegu yake shambani na mwingine aliiangusha pasipo kujua mtaroni na kuendelea na shughuli zake…wote wawili mbegu zao zitamea tofauti ni kwamba mmoja atakuwa anaona na kufuatilia hatua za ukuaji, mwingine atakuwa haoni wala hafahamu kuwa alichokipanda kinaendelea kuota huko…lakini utakapofika msimu wa mavuno, mavuno yote yatakomaa kwa wakati mmoja.

Kama wewe ni mwasherati, na unajua kabisa uasherati ni dhambi, au ni mlevi, au mtazamaji pornography, au mwizi, au mlawiti, au mfanyaji masturbation, au msagaji, au mtoaji mimba, au msengenyaji..na unafanya hayo kwa makusudi kabisa..kuwa na uhakika kabisa mbegu hizo Mwisho wa siku mbegu hizo zitakuzalia mauti..

Halikadhalika kama mwingine ni mwizi, au muasherati, au mfanyaji masturbation, au mtukanaji au mlevi, na hana habari kuwa mambo hayo ni mabaya na ni dhambi mbele za Mungu..huyo naye ni sawa na mtu aliyeiangusha mbegu yake kwenye mtaroni kando ya barabara pasipo kujijua..ambapo itamea na wakati ukifika kazi yake itaonekana na watu wote hata kama yeye hajui..Hivyo na yeye pia mbegu zake zitamzalia MAUTI!! Atakufa katika roho na katika mwili.

Mfano leo hii ukienda kubaka mwanafunzi, serikali haitaki kujua kuwa ulikuwa unaifahamu sheria au la, hiyo si kazi yao…Kazi yao ni moja tu kukuhukumu kulingana na sheria inavyosema ,utakwenda gerezani miaka 30.

Biblia inasema katika

Wagalatia 6: 7 “MSIDANGANYIKE, MUNGU HADHIHAKIWI; kwa kuwa cho chote apandacho mtu, ndicho atakachovuna.

8 Maana yeye apandaye kwa mwili wake, katika mwili wake atavuna uharibifu; bali yeye apandaye kwa Roho, katika Roho atavuna uzima wa milele”.

Unaona? Mungu hadhikiwi biblia inasema hivyo…uwe umepanda kwa bahati mbaya au kwa makusudi, kwa kujua au kwa kutokujua…sheria ni ile ile ni lazima uvune ulichokipanda ni sheria Mungu aliyoiweka katika mambo yote hata mambo ya asili.

Biblia inaposema mshahara wa dhambi ni mauti…haimaanishi adhabu ya dhambi ndio mauti!…hapana bali MSHAHARA! Zingatia hilo neno “mshahara”…adhabu maana yake unapewa mateso kulingana na kile kitu kibaya ulichokifanya…mshahara maana yake ni “unalipwa kulingana na kazi uliyoifanya”….Kwahiyo dhambi ni “kazi”..na ina mshahara haina adhabu bali mshahara…

Ndio maana Bwana Yesu alisema katika Ufunuo 22:12..

“Tazama, naja upesi, na ujira wangu u pamoja nami, KUMLIPA KILA MTU KAMA KAZI YAKE ILIVYO.
13 Mimi ni Alfa na Omega, mwanzo na mwisho, wa kwanza na wa mwisho”.

Kwahiyo kitakachotokea siku ya hukumu sio watu kwenda kusomewa adhabu, bali kwenda kulipwa MISHAHARA YAO. Kila mtu kama kazi yake ilivyo…waliofanya kazi ya dhambi ndio watalipwa mauti ya milele, kadhalika waliofanya haki watalipwa uzima wa milele.

Kwahiyo ndugu, unayesoma ujumbe huu ambaye bado upo nyuma ya wakati (Yaani Kristo yupo mbali na wewe), na unafanya dhambi za makusudi au pengine sio za makusudi bali kwa kutokujua…Nataka nikuambie maisha nje ya Yesu Kristo, ni sawa na kuangusha mbegu barabarani na kwenda zako pasipo kujua kuwa zinaendelea kujiotea zenyewe huko ulikoziangusha. Na ujira wako upo! Vivyo hivyo dhambi zako ziwe za kwa kujua au kwa kutokuja zitafikishwa HUKUMUNI! Na zitapewa ujira wake.

Ni maombi yangu kuwa Bwana atakujalia kuliona hilo na kuweka mambo yako sawa sasa na kujitengenezea mshahara ulio bora wa uzima wa milele, kumchagua Yesu Kristo kuwa fungu lako lilolo bora, mkuu wa uzima, Biblia inasema mkumbuke muumba wako siku za ujana wako, kabla haijakaribia miaka utakaposema sina furaha katika hiyo. Hii ikiwa na maana kuwa utafikia miaka fulani hutaweza tena kumkumbuka muumba wako, kama unamsikia sasa na kumkataa.

Bwana akubariki katika Jina la Yesu, naye akupe kila haja ya moyo wako wewe uliyemchagua yeye.

Amina.

Tafadhali shiriki ujumbe huu kwa wengine na Bwana atakubariki. Pia unaweza ukapata mafundisho haya Kwa njia ya Whatsapp yako, jiunge na channel yetu Kwa kubofya hapa >> WHATSAPP


Mada Zinazoendana:

MADHARA YA DHAMBI YA UASHERATI.

JE! SISI KAMA WAKRISTO NI DHAMBI KUSHEHEREKEA KRISMASI?

KUNA TOFAUTI GANI KATI YA DHAMBI, UOVU NA KOSA KIBIBLIA!


Rudi Nyumbani

DOWNLOAD PDF
WhatsApp

Source URL: https://wingulamashahidi.org/2019/04/18/mshahara-wa-dhambi/