Je! mtu kuhisi kitu fulani au kusikia sauti za watu wengine walio mbali, kunaweza tokana na Mungu?

by Admin | 2 September 2019 08:46 pm09

Baba mmoja Ananisimulia akisema, “Mimi hapa huwa ninasikia watu wanaosema wanakuja kunikamata.akaniuliza je! Na wewe unawasikia? Nikamwambia hapana mimi siwaskii[saa hiyo ni yeye tu anawasikia]. Akanichukua akanishika mkono Akaniambia” Unasikia hiyo nyimbo yangu wanaimba? (Mimi siisikii yeye peke yake anasikia)” Nikamwambia hapana” ANAOGOPA SANA.

Sasa Juzi juzi Usiku nikamkuta amesimama hapa nje nyumbani kwetu Akiwa ameshika panga mkononi mwake akaniambia “Unamsikia bibi mmoja kule ng’ambo anasema nimebaka mjukuu wake[Kwa bibi huyo ni mbali na hapa kwetu]?” Nikamwambia hapana.Akarudi nyumbani na panga lake.[Wakati huo anaongea yuko siriazi kabisa].Wakati mwingine ananiambia aliowaona watu wamesimama mlangoni kwake. Sasa Swali:Ndugu kwa nyinyi Muonavyo Hicho ni kitu gani?? KARIBUNI [Nilijaribu kumueleza habari ya kumpa Bwana maisha akasema ATAPAMBANA KIJESHI[Nilijuwa anamaanisha kwa waganga],Lakini namuona sasa hawezi kupambana kijeshi alivyosema].Hali yake inazidi kuongezeka Ikifika mahali Si ajabu akawa kichaa kabisa.

JIBU: Shalom, Mambo yanayoendelea katika roho ni mengi, na shetani naye kila kukicha anaongeza mapana ya maarifa yake…mtu akizama katika maarifa ya shetani (mfano uchawi)..anakuwa anauwezo wa kufanya vitu ambavyo kwa namna ya kawaida haviwezekani kufanyika…sasa kwa mtu kama huyo aliyekuja kukusimulia kuwa anasikia sauti za nyimbo, na ana uwezo wa kusikia mtu akizungumza akiwa mbali, ni wazi kuwa kuna roho ipo ndani yake na hiyo ni roho ya yule adui. Kwanini ni roho ya adui, na si ya Mungu? kwasababu matunda ya hiyo roho ni ya yule adui, kumpeleka kwenye uovu na kumweka katika vifungo vya uoga,wasiwasi na mkandamizo… Kwasababu matunda ya Roho Mtakatifu sio hayo ingekuwa ni Roho Mtakatifu yupo ndani ya huyo mtu ungeona matunda ya Roho ndani yake kama yalivyoandikwa kwenye kitabu cha Wagalatia

Wagalatia 5:22 “Lakini tunda la Roho ni upendo, furaha, amani, uvumilivu, utu wema, fadhili, uaminifu, upole, kiasi; juu ya mambo kama hayo hakuna sheria.”

 Umeona hapo? Roho Mtakatifu akiwa ndani ya mtu hivyo vitu hapo juu lazima vionekane, amani, furaha,upendo n.k…Lakini roho iliyopo ndani ya huyo mtu haijamsukuma kwenye upole, wala haimpeleki kwenye furaha, wala uvumilivu, wala amani…zaidi ya yote umempeleka kwenye hofu, mashaka na ghadhabu…hivyo hiyo ni moja kwa moja roho ya yule mwovu ipo ndani yake. Sasa Roho Mtakatifu akiwa ndani ya mtu huwa ni lazima atoe na kipawa fulani juu ya huyo mtu, ndio hapo anawapa wengine vipawa vya unabii, wengine lugha, wengine miujiza,ishara,uchungaji, ualimu,uinjilisti n.k [kumbuka vipawa vya Roho ni tofauti na matunda ya Roho].

 kadhalika na roho za mashetani ni hivyo hivyo, mtu akiwa na pepo fulani la utambuzi, ni lazima litampa uwezo fulani,(ni kama karama yake fulani hivi) watu wengine shetani anawapa uwezo wa kufanya utambuzi, wanakuwa na uwezo wa kutambua siri za watu, au kuona vitu vinavyoendelea sehemu nyingine mbali na mahali walipo, hata wakati mwingine wanakuwa na uwezo wa kusikia sauti na mazungumzo ya watu waliopo mbali kama huyo mzee, wengine wanakuwa na uwezo wa kufanya viishara ishara fulani (mazingaumbe mazingambwe) wengine wanakuwa hawana huo uwezo lakini wanakuwa wanauwezo mwingine mkubwa wa ushawishi…wanaweza kumshawishi mtu au jamii na wakafanikiwa kuleta vitu vyenye madhara kwa kutumia hivyo vipawa walivyonavyo vya nguvu za giza.

 Kwahiyo kwa habari ya huyo mzee ni kwamba kafungwa na nguvu za giza, aidha kwa kujua au kwa kutokujua, na kwasababu hamjui Yesu Kristo, inawezekana yeye akajihisi anakipawa kutoka kwa Mungu cha uwezo wa kujua na kuwasikia maadui zake mahali walipo, lakini ni roho ya adui ipo ndani yake, pasipo yeye kujijua,hivyo nakushauri, tenga muda umhubirie injili, ili macho yake ya rohoni yafumbuke,umweleze uwezo uliopo katika Yesu Kristo, na tumaini lililopo ndani ya Yesu Kristo, na Bwana akimpa Neema ya kuamini injili na kuipokea, mwekee mikono na kumwombea kwa Jina la Yesu na hizo roho zitamwacha atakuwa huru kabisa.

Na akizingatia kutubu kwa kuacha dhambi zake kabisa na kwenda kubatizwa katika ubatizo sahihi, basi Bwana atampa kipawa cha Roho wake Mtakatifu kwasababu yeye mwenyewe alisema ahadi hiyo ni kwa watu wote waliompokea..Na akiisha pokea Roho Mtakatifu basi yale matunda ya Roho yataambata naye..atapata amani isiyokuwa ya kawaida, furaha ya ajabu, upendo wa ajabu, uvumilivu usioelezeka, upendo usiokuwa na mipaka na fadhili nyingi. 

Bwana akubariki.


Mada nyinginezo:

JE! UMECHAGULIWA KABLA YA KUWEKWA MISINGI YA ULIMWENGU?

NI JAMBO GANI LINALOMTAMANISHA SANA BWANA TUMWOMBE BILA KUKATA TAMAA?

VITA DHIDI YA MAADUI

“WOKOVU WETU U KARIBU NASI KULIKO TULIPOANZA KUAMINI”

NITAIFAHAMU VIPI KARAMA YANGU?

NATAKA REHEMA, WALA SI SADAKA!


 

Rudi Nyumbani:

DOWNLOAD PDF
WhatsApp

Source URL: https://wingulamashahidi.org/2019/09/02/je-mtu-kuhisi-kitu-fulani-au-kusikia-sauti-za-watu-wengine-walio-mbali-kunaweza-tokana-na-mungu/