KUFUKIZA UVUMBA NDIO KUFANYAJE?

by Admin | 2 September 2019 08:46 am09

SWALI: KUFUKIZA UVUMBA ndio kufanyaje? Na tena wana wa Israel walimfukizia uvumba Malkia wa mbinguni, ndio yupi huyo?


JIBU: Uvumba ni aina Fulani ya manukato, yanayotengenezwa kwa viungo mbalimbali ambavyo baada ya kutengenezwa pamoja, huwa yanachomwa na kutoa harufu Fulani iliyo nzuri. Sasa katika biblia (Agano la Kale) wana wa Israeli walipokuwa jangwani kabla ya kufika nchi ya Ahadi, walipewa maagizo na Mungu mwenyewe watengeneze UVUMBA, na makuhani watakuwa wanauchoma huo kila siku ndani ya ile Hema waliyoambiwa waitengeneze..

Na ni makuhani peke yao ndio waliokuwa wanaruhusiwa kufanya hiyo kazi ya kuvukiza uvumba. Hivyo Makuhani waliuchukua huo uvumba na kuuchoma kila siku ndani ya ile hema ya kukutania katika madhabahu ndogo iliyokuwemo kule ndani, Na ilikuwa ni amri ya daima ni lazima wafanye hivyo kila siku..Na Bwana aliwaagiza wana wa Israeli wasitengeneze uvumba wowote kwa viungo hivyo kwa ajili ya mambo yao..Fomula ya kutengeneza huo uvumba ni kwa ajili ya Bwana tu!

 Kutoka 30:34 “Bwana akamwambia Musa, Jitwalie MANUKATO MAZURI, yaani, natafi, na shekelethi, na kelbena; viungo vya manukato vizuri pamoja na ubani safi; vitu hivyo vyote na viwe vya kipimo kimoja;

35 nawe UTAFANYA UVUMBA WA VITU HIVYO, manukato ya kazi ya ustadi wa mtengenazaji manukato, yatakuwa yamekolea, safi, matakatifu;

36 nawe baadhi yake utayaponda sana, na kuyaweka mbele ya ushuhuda ndani ya hema ya kukutania, hapo nitakapokutana nawe; nayo yatakuwa kwenu matakatifu sana.

37 Na uvumba utakaofanya, hamtajifanyia uvumba wenye viungo sawasawa na uvumba huo; utakuwa kwenu mtakatifu kwa ajili ya Bwana”.

Sasa swali ni kwanini Bwana aliwapa hayo maagizo ya kuchoma uvumba ndani ya nyumba yake??

 Jibu ni kwamba kila kitu kilichokuwemo ndani ya ile Hema ya kukutania kilikuwa ni lugha ya picha ya jambo linaloendelea rohoni….kwamfano kile kinara cha taa saba ndani ya nyumba ya Mungu kiliwakilisha makanisa saba katika ufunuo sura ya 2 na ya 3, kadhalika Yule kuhani mkuu anayeingia patakatifu pa patakatifu na Damu ya mwanakondoo ili kufanya upatanisho, anamwakilisha Yesu Kristo, ambaye ndiye kuhani wetu mkuu aliyeingia patakatifu pa patakatifu kwa damu yake mwenyewe mara moja tu! 

Kadhalika na ule UVUMBA, kwa jinsi ulivyokuwa unachomwa ndani ya Nyumba ya Mungu, na moshi wake kukijaza kile chumba, na kupaa juu mbinguni..Jambo lile lilikuwa linafunua jinsi gani maombi ya watakatifu yanavyomfikia Mungu, kwanza yanakuwa yameandaliwa kulingana na Neno lake, pili yanapaa juu kama moshi na kumfikia Mungu mbinguni, kwani tunajua kitu pekee kinachopaa juu chenyewe ni moshi..Hivyo kwasababu yametengenezwa na viungo vinavyoendana na Neno la Mungu, maombi ya watakatifu yanakuwa ni harufu nzuri ya kuvutia mbele za Mungu, yanakuwa kama perfume mbele zake. Na ndio maana Daudi alisema maneno haya..

Zaburi 141: 2 “SALA YANGU IPAE MBELE ZAKO KAMA UVUMBA, Kuinuliwa mikono yangu kama dhabihu ya jioni.”

Kwasababu hiyo basi katika agano jipya hatuchomi ubani tena, wala hatuvukizi uvumba kwasababu hayo yalikuwa ni mambo ya mwilini yanayofunua mambo ya rohoni, HIVYO UVUMBA WETU NI MAOMBI YETU TUNAYOMWOMBA MUNGU KILA SIKU YANAYOENDANA NA NENO LAKE.Ndio maana pia tunasoma hayo katika kitabu cha Ufunuo..

Ufunuo 5:8 “ Hata alipokitwaa kile kitabu, hao wenye uhai wanne na wale wazee ishirini na wanne wakaanguka mbele za Mwana-Kondoo, kila mmoja wao ana kinubi, NA VITASA VYA DHAHABU VILIVYOJAA MANUKATO, AMBAYO NI MAOMBI YA WATAKATIFU.”

Ufunuo 8:4 “NA MOSHI WA ULE UVUMBA UKAPANDA MBELE ZA MUNGU PAMOJA NA MAOMBI YA WATAKATIFU, kutoka mkononi mwa malaika.” 

Lakini pamoja na hayo shetani naye huwa anapenda kuiga na kugeuza mambo, na kuwadanganya watu kuwa mambo hayo kwasasa yanapaswa yaendelee kufanyika, kama anavyowadanganya watu kuwa kwasababu agano la kale kondoo na mbuzi walikuwa wanachichwa kwa ajili ya upatanisho, vivyo hivyo na sasa kondoo na mbuzi wanapaswa wachichwe kwa ajili ya kuondoa mikosi katika mtu, au jamii au ukoo, hivyo watu badala wapone ndio wanajiongezea roho juu ya roho..

Vivyo hivyo leo hii Bado shetani anawadanganya watu juu ya kuvukiza uvumba, ndio utasikia watu wanaambiwa wakachome ubani manyumbani mwao kufukuza mapepo, na zaidi hata makanisani watu wanavukiza uvumba, jambo ambalo ni machukizo kwa Mungu wa mbinguni…. Na kuhusu MALKIA WA MBUNGUNI. Hakuna mahali popote biblia imesema kuna malkia mbinguni, isipokuwa imeeleza miungu ya kipagani, inayojulikana kama malkia wa Mbinguni, hivyo biblia ilipotaja malkia wa mbinguni mahali popote ilikuwa inamaanisha miungu ya kipagani inayojulikana na watu kama malkia wa mbinguni, Ni sawa na leo atokee mtu atengeneze kinyago chake halafu akiite Malkia wa mbinguni, kiuhalisia sio kweli kwamba ni malkia wa mbinguni, mbinguni Mungu aliko hapana bali kimeitwa vile kutokana na watu wanakiita chenyewe malkia wa mbinguni. 

Ubarikiwe!


Mada zinazoendana:

ZILE TUNU (DHAHABU, UVUMBA NA MANEMANE) MAMAJUSI WALIZOZITOA KWA BWANA ZILIWAKILISHA NINI?

HUYU AZAZELI NI NANI TUNAYEMSOMA KATIKA(WALAWI 16:8)

JE! SISI NI WAFALME NA MAKUHANI KWA NAMNA GANI?

NADHIRI.

MWANA WA MUNGU.

MCHE MWORORO.

 

Rudi Nyumbani:

DOWNLOAD PDF
WhatsApp

Source URL: https://wingulamashahidi.org/2019/09/02/kufukiza-uvumba-ndio-kufanyaje-na-tena-wana-wa-israel-walimfukizia-uvumba-malkia-wa-mbinguni-ndio-yupi-huyo/