Katika Yakobo 1:13 Biblia inasema Mungu hamjaribu mtu, lakini tukirudi kwenye kitabu cha Mwanzo 22:1 tunaona Mungu alimjaribu Ibrahimu. Hapo naomba mwanga zaidi.

by Admin | 3 September 2019 08:46 am09

JIBU: Tunapaswa tufahamu mistari hiyo ilikuwa inalenga katika Nyanja gani, mfano kama tukisoma huo wa Yakobo1:13 Unasema  

“Mtu ajaribiwapo, asiseme, Ninajaribiwa na Mungu; maana Mungu hawezi kujaribiwa na maovu, wala yeye mwenyewe hamjaribu mtu.

14 Lakini kila mmoja hujaribiwa na tamaa yake mwenyewe huku akivutwa na kudanganywa.

15 Halafu ile tamaa ikiisha kuchukua mimba huzaa dhambi, na ile dhambi ikiisha kukomaa huzaa mauti.”  

Unaona ukiangalia hapo kwa makini utagundua kuwa analenga katika mambo maovu, kwamfano uzinzi, au ulevi, uchawi, usengenyaji, wizi,n.k. Kwamfano utakuta mtu ni mkristo, na hapo mwanzo alikuwa hazini wala hanywi pombe, lakini pengine ghafla mbele yake kikapita kichocheo kimojawapo cha zinaa labda tuseme kahaba, au picha chafu za ngono, sasa yeye badala avikatae na avikimbie hivyo vichochezi yeye kidogo kidogo anavutiwa navyo na kuanza kuvifuatilia au kudokoa na kuvitazama, huko ndiko kuvutwa na kudanganywa kwenyewe kunakozungumziwa hapo, na kama akizidi kuendelea kuviendekeza hivyo vichocheo baadaye vinazaa dhambi hapo ndipo unakuta mtu wa namna hiyo anaingia katika uzinzi moja kwa moja, na anakuwa mbaya kuliko hata wale aliowakuta huko na mwisho wa siku anazaa mauti kwasababu ile dhambi ilisha komaa hapo hawezi kugeuka tena kilichosalia ni kwenda kwenye ziwa la moto.  

Sasa mtu kama huyo hawezi kusema Mungu alikuwa anamjaribu,kumletea kahaba, kwasababu Mungu hashikamani na ouvu wa aina yoyote..bali ni tamaa ya mambo yake ndio iliyokuwa inamvuta huko. Yusufu alipojaribiwa na mke wa Potifa sio Mungu aliyekuwa anamjaribu pale, bali ni ouvu, lakini yeye aliishinda kwasababu hakuiendekeza hiyo roho.

Lakini pia ifahamike kuwa mtu yeyote anapoamua kumfuata Mungu, inamaanisha kuwa anakuwa mwanafunzi wa Kristo moja kwa moja, na tunajua kuwa hakuna mwanafunzi yeyote anayesoma tu bila kujaribiwa kwa mitihani, hiyo haipo?, Mwalimu atajuaje kuwa huyu mwanafunzi ameelewa au la, Vinginevyo shule itajikuta inaandaa watu wasiokuwa na uwezo wa kitaaluma, Vivyo hivyo kwa Mungu pia kuna mitihani,unajaribiwa kuangaliwa kama umekidhi vigezo au la!   Na kujaribiwa huko hakuna lengo la kukuangusha, bali kukuimarisha. Mwalimu yoyote mwenye akili timamu hawezi kuwajaribu wanafunzi wake kwa kuwachanganya kwenye bweni moja wanafunzi wa kike na wa kiume walale humo humo, kwa lengo la kupima kiwango chao cha elimu..huko ni kuwapoteza na sio kuwafundisha, bali atawapa mitihani kulingana na wanachofundishwa darasani,   Na ndivyo Mungu anavyofanya kwa watoto wake wote, hawajaribu kwa maovu, bali kwa yale waliyokuwa wanafundishwa na kuyapitia katika imani yao, na ndio yaliyomkuta Ibrahimu na ndiyo yaliyowakuta wana wa Israeli na ndiyo yatakayokukuta wewe ambaye unasema umeamua kumfuata Kristo..

Mwanzo 22:1 “Ikawa baada ya mambo hayo Mungu ALIMJARIBU Ibrahimu, akamwambia, Ee Ibrahimu! Naye akasema, Mimi hapa.

2 Akasema, Umchukue mwanao, mwana wako wa pekee, umpendaye, Isaka, ukaende zako mpaka nchi ya Moria, ukamtoe sadaka ya kuteketezwa huko juu ya mlima mmojawapo nitakaokuambia.”  

Ukisoma tena habari ya wana Israeli walipokuwa jangwani utaona Mungu akiwaambia hivi…  

Kumbukumbu 8:2 “Nawe utaikumbuka njia ile yote Bwana, Mungu wako aliyokuongoza miaka hii arobaini katika jangwa, ili akutweze, KUKUJARIBU kuyajua yaliyo moyoni mwako, kwamba utashika amri zake, au sivyo.

3 Akakutweza, akakuacha uone njaa, akakulisha kwa mana, usiyoijua wewe wala baba zako hawakuijua; apate kukujulisha ya kuwa mwanadamu haishi kwa mkate tu, bali huishi kwa kila litokalo katika kinywa cha Bwana.

4 Mavazi yako hayakuchakaa, wala mguu wako haukuvimba, miaka hiyo arobaini.”  

Vivyo hivyo leo hii unaweza kusema umemfuata Yesu, lakini kusema hivyo tu haitoshi, Mungu ataipima imani yako kwake,..pengine anaweza kuruhusu ukachekwa kwa ajili ya wokovu wako, aangalie je! Utauacha?, ataruhusu uchukiwe na kutengwa na ndugu, aangalie je! Kweli ulimaanisha kumfuata?, ataruhusu upitie kupungukiwa aangalie je! Unampenda wakati wa raha tu, au hadi wakati wa mateso, ataruhusu upitie hiki au kile..Huko ndio kujaribiwa na Mungu. Lakini Mungu hawezi kukuletea pombe, au kahaba, au hirizi au pesa haramu, ukasema ni Mungu anakujaribu,,ukikutana na mambo ya namna hiyo maovu fahamu kuwa unajaribiwa kwa tamaa zako mwenyewe sio kwa ajili ya IMANI yako.  

Ubarikiwe.


Mada Nyinginezo:

MAJARIBU MATATU YA YESU KRISTO.

AYUBU ALITESEKA KATIKA MAJARIBU KWA MIAKA MINGAPI?

TUTAWEZAJE KUMZALIA MUNGU MATUNDA?

FUATILIA NDOTO HII, UTAJIFUZA KITU.

KWANINI NABII ISAYA ALIAGIZWA KUHUBIRI UCHI?

MSHAHARA WA DHAMBI.


Rudi Nyumbani:

DOWNLOAD PDF
WhatsApp

Source URL: https://wingulamashahidi.org/2019/09/03/katika-yakobo-113-biblia-inasema-mungu-hamjaribu-mtu-lakini-tukirudi-kwenye-kitabu-cha-mwanzo-221-tunaona-mungu-alimjaribu-ibrahimu-hapo-naomba-mwanga-zaidi/