Bwana alimaanisha nini kusema “Na kondoo wengine ninao ambao si wa zizi hili” Hao kondoo wengine ni akina nani?

by Admin | 6 September 2019 08:46 pm09

JIBU: Tukisoma Yohana 10:16 Inasema…

“Na kondoo wengine ninao, ambao si wa zizi hili; na hao nao imenipasa kuwaleta; na sauti yangu wataisikia; kisha kutakuwako kundi moja na mchungaji mmoja”.

Katika Mstari huo tunaona imeweka wazi kabisa kuwa Mchungaji ni Bwana Yesu mwenyewe…na Bila shaka kondoo ni watu wake…..Na kama kondoo ni watu wake ni Dhahiri kuwa ni lazima Mahali wanapoishi ndipo patakuwa zizi lao. Sasa katika Biblia Nchi ya Israeli inafananishwa na zizi la Mungu, ikiwa na maana kuwa wayahudi ni kondoo wa Mungu waliopo katika zizi linaloitwa Israeli. Tunalithibitisha hilo katika..

Ezekieli 34:13 “Nami nitawatoa katika watu wa mataifa, na kuwakusanya katika nchi zote, nami nitawarudisha katika nchi yao wenyewe; nami nitawalisha juu ya milima ya Israeli, kando ya mifereji ya maji; na katika mahali pote pa nchi panapokaliwa na watu.

14 Nami nitawalisha malisho mema, pa juu ya milima ya mahali PALIPOINUKA PA ISRAELI LITAKUWA ZIZI LAO; huko watalala katika zizi jema; nao watakula malisho mema, juu ya milima ya Israeli.

15 Mimi mwenyewe nitawalisha kondoo zangu, nami nitawalaza, asema Bwana MUNGU”.

Vivyo hivyo kinyume chake, watu wote ambao si wa Israeli ndio wapo zizi lingine ambalo Bwana alilolizungumzia pale, Yaani sisi watu wa Mataifa ndio Bwana aliokuwa ana maanisha kondoo wa Zizi lingine, ambao nasi pia ulifika wakati, tuliingizwa na kuwa miongoni mwa kondoo wake Bwana, kwasababu injili ilianza kwanza kwa wayahudi ndipo ikaja kwetu…..na kwa kupitia msalaba sisi pamoja na wayahudi wote tumekuwa kundi moja, na Bwana wetu amekuwa ni mmoja (Yesu Kristo).

Waefeso 2:11 “Kwa ajili ya hayo kumbukeni ya kwamba zamani ninyi, mlio watu wa Mataifa kwa jinsi ya mwili, mnaoitwa Wasiotahiriwa na wale wanaoitwa Waliotahiriwa, yaani, tohara ya mwilini iliyofanyika kwa mikono;

12 kwamba zamani zile mlikuwa hamna Kristo, mmefarakana na jamii ya Israeli, wageni wasio wa maagano ya ahadi ile. Mlikuwa hamna tumaini, hamna Mungu duniani.

13 Lakini sasa, katika Kristo Yesu, ninyi mliokuwa mbali hapo kwanza mmekuwa karibu kwa damu yake Kristo.

14 Kwa maana yeye ndiye amani yetu, ALIYETUFANYA SISI SOTE TULIOKUWA WAWILI KUWA MMOJA; akakibomoa kiambaza cha kati kilichotutenga”

Unaona hapo? Alitufanya sisi wawili (yaani sisi watu wa mataifa na wayahudi) kuwa mmoja…yaani kwa kundi moja.

Wagalatia 3:27 “Maana ninyi nyote mliobatizwa katika Kristo mmemvaa Kristo.

28 Hapana Myahudi wala Myunani. Hapana mtumwa wala huru. Hapana mtu mume wala mtu mke. Maana ninyi nyote mmekuwa mmoja katika Kristo Yesu”.

Je! Na wewe ni miongoni mwa kondoo wake?..Umeingizwa ndani ya kundi la Kristo, Kumbuka hatufanyiki kondoo wa Kristo kwa kujiunga na Kanisa bali kwa kutubu na kubatizwa na kupokea Roho? Na kuishi Maisha matakatifu?.

Ubarikiwe.


Mada zinazoendana:

MAANA YA HUU MSTARI NI IPI? MITHALI 14:4 ‘ZIZI NI SAFI AMBAPO HAPANA NGOMBE;BALI NGUVU ZA NGOMBE ZALETA FAIDA NYINGI’.

MAMBO YATAKAYOTOKEA ISRAELI SIKU ZA HIVI KARIBUNI.

AMIN! NAWAAMBIA KIZAZI HIKI HAKITAPITA!

CHUKIZO LA UHARIBIFU

JE! MABALASI BWANA YESU ALIYOYATUMIA KUGEUZIA MAJI KUWA DIVAI, YALITUMIKA TU KWA KAZI HIYO?

WAFALME WATOKAO MAWIO YA JUA.

 


Rudi Nyumbani:

DOWNLOAD PDF
WhatsApp

Source URL: https://wingulamashahidi.org/2019/09/06/bwana-alimaanisha-nini-kusema-na-kondoo-wengine-ninao-ambao-si-wa-zizi-hili-hao-kondoo-wengine-ni-akina-nani/