Sala ya Toba na Rehema.

by Admin | 14 July 2020 08:46 am07

Ni jambo jema kutafuta sala ya toba na rehema, angali muda upo.

Inawezekana umemkosea Mungu sana, na leo unatamani kujua kama ipo njia ya kumrudia yeye tena, inawezekana, umeua, au umetoka nje ya ndoa, au umetoa mimba, umemtukana Mungu, umeiba, umeenda kwa waganga, umewavunjia heshima wazazi wako, umeaudhi watu wengine n.k.

Inawezekana pia wewe ni mmojawapo wa ambao wameona kuendelea kuishi Maisha bila Mungu ni kupotea tu, na umeamua sasa uutafute uso wake. Basi kama wewe ni mmojawapo, uamuzi ulioufikiria ni mzuri sana, Na yapo makusudi makubwa sana Mungu kukufikisha mahali hapa,

Bwana Yesu alisema..

Yohana 6:37  “Wote anipao Baba watakuja kwangu; wala ye yote ajaye kwangu sitamtupa nje kamwe”.

Kama leo umeamua kudhamiria kweli kutubu dhambi zako, basi ni ahadi yake kuwa hatakutupa nje kamwe! Kuanzia huu wakati na kuendelea utaona maajabu makubwa sana katika Maisha yako kama ilivyokuwa hata kwetu.

Kinachohitajika ni wewe tu, kumaanisha kabisa kutoka katika moyo wako kwamba kuanzia leo, wewe na dhambi basi! Ulimwengu nyuma Yesu mbele, hilo tu, pekee linatosha wewe kuupokea wokovu wa Bwana..Anataka kukusamehe lakini ni mpaka pale wewe utakapojutia na kusema mimi ninauaga ulimwengu kwa miguu yote miwili.

Wengi wanadhani ni sala Fulani tu, ndio inayompa mtu wokovu, hapana, nitakuonyesha sehemu kwenye biblia mwanamke mmoja mwenye dhambi nyingi (kahaba) kwa kujutia tu makosa yake, mpaka kulia machozi mengi sana mbele za Yesu..Hilo peke yake lilitosha kwa Yesu kuuona moyo wake uliomaanisha kutubu  na saa ile ile Yesu akamwambia, UMESAMEHEWA DHAMBI ZAKO. Soma (Luka 7:36-48), utathibitisha hilo.

Hivyo hata na wewe leo ukitia Nia kweli kweli, basi sala fupi nitakayokuambia uiombe  hapo mbele kidogo, italeta mabadiliko makubwa sana katika Maisha yako ya rohoni. Kwasababu moja kwa moja Kristo anakwenda kuingia ndani  yako kukubadilisha, na kuanzia huu wakati na kuendelea ataendelea kuwa na wewe kukusaidia kushinda na baadhi ya yale mambo ambayo ulikuwa huwezi.

Hivyo kama upo tayari kutubu leo dhambi zako, basi

Basi uamuzi unaoufanya ni wa busara sana ambao hautakaa uujutie maisha yako yote kama ilivyokuwa hata kwetu sisi. Sasa unachopaswa kufanya, hapo ulipo, chukua muda mchache ujitenge peke yako. Kisha piga magoti, kisha fuatisha sala hii kwa Imani, ukijua kuwa Yesu mwokozi yupo hapo karibu na wewe pembeni yako kukusikia..Kisha ukiwa sasa katika utulivu Sema sala hii kwa sauti.

EE MUNGU BABA, NAJA MBELE ZAKO, NIKIWA NINAJITAMBUA KUWA MIMI NI MKOSAJI NA NIMEKUTENDA DHAMBI NYINGI, NA KWAMBA NIMESTAHILI HUKUMU. LAKINI WEWE MUNGU WANGU ULISEMA KATIKA NENO LAKO KUWA WEWE NI MUNGU WA REHEMA UNAYEWAREHEMU  MAELFU ELFU YA WATU WANAOKUPENDA WEWE. NA LEO HII NINAKUJA MBELE ZAKO NAHITAJI MSAMAHA WAKO NA MSAADA WAKO MUNGU WANGU, NINATUBU DHAMBI ZANGU ZOTE KWA KUMAANISHA NA KWA MOYO WANGU WOTE, NINAKIRI KUWA YESU KRISTO NI BWANA, NA YEYE NDIYE MWOKOZI WA HUU ULIMWENGUNI. HIVYO NAOMBA DAMU YA MWANAO TAKATIFU INISAFISHE UOVU WANGU WOTE SASA NIFANYIKE KUWA KIUMBE KIPYA KUANZIA LEO NA HATA MILELE.

ASANTE BWANA YESU KWA KUNIPOKEA NA KUNISAMEHE.

AMEN.

Sasa ikiwa umefuatisha sala hiyo kwa Imani ..Hatua iliyobakia kwako ni kuithitisha toba yako kwa Vitendo ikiwa ulikuwa unafanya mambo yote ambayo hayampendezi Mungu unayaacha na kujitenga nayo, Sasa Mungu akishaona umegeuka kwa vitendo basi toba yako anaipokea na atakuja ndani yako wakati huo huo na kufanya makao ya milele kwako.

Vile vile unahitaji, kutafuta kanisa la kiroho ambalo utajumuika na wakristo wengine katika kumwambudu Mungu, na kujifunza biblia ili uukulie wokovu. Na vilevile ili upate ubatizo sahihi wa kuzamishwa katika maji mengi na kwa jina la YESU KRISTO kwa ajili ya ondoleo la dhambi zako.

Pia unaweza kuihifadhi tovuti yetu hii , katika kumbukumbu zako (www.wingulamashahidi.org), ili wakati mwingine ikusaidie, kwani yapo mafundisho mengi Zaidi ya 1000  na maswali mengi ya biblia yaliyojibiwa, ambayo unaweza ukajifunza na kuimarika kiroho sana, ukiwa hata hapo hapo nyumbani kwako kwenye simu yako.

Ubarikiwe sana

Mada Nyinginezo:

TOBA IGUSAYO MOYO WA BWANA.

YESU MPONYAJI.

WAKAKAA KWAKE SIKU ILE. NAYO ILIKUWA YAPATA SAA KUMI.

UMEFUMBULIWA MACHO YAKO YA KIROHO?

NINI KINATOKEA BAADA YA KIFO?

MKATAE SHETANI NA MAWAZO YAKE YA KIBINADAMU.

Rudi Nyumbani:

DOWNLOAD PDF
WhatsApp

Source URL: https://wingulamashahidi.org/2020/07/14/sala-ya-toba-na-rehema/